Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unaweza Kufanya Ulimwengu Uwe Mahali Bora?

Je, Unaweza Kufanya Ulimwengu Uwe Mahali Bora?

Je, Unaweza Kufanya Ulimwengu Uwe Mahali Bora?

‘Siasa zimeshindwa kuleta hali zinazounganisha jamii. Haziwezi kurudisha maadili kama yalivyokuwa hapo kale. Hata sera zilizo bora haziwezi kuboresha uchumba au ndoa, haziwezi kufanya akina baba wawajibike kwa watoto wao, haziwezi kufanya watu waaibike kama ilivyokuwa zamani. Sheria haiwezi kuondoa matatizo mengi ya kiadili yanayotusumbua.’

JE, UNAKUBALIANA na maneno hayo yaliyosemwa na aliyekuwa msaidizi katika serikali ya Marekani? Ikiwa ndivyo, basi kuna suluhisho gani kwa matatizo mengi leo yanayotokana na pupa, ukosefu wa upendo katika familia, maadili yaliyopotoka, kutokuwa na ujuzi, na hali nyingine zinazodhoofisha jamii? Watu wengine wanahisi kwamba hakuna suluhisho lolote, kwa hiyo wanaendelea na shughuli zao za kila siku kadiri wawezavyo. Wengine wanatumaini kwamba siku moja kiongozi fulani mwenye akili na kipawa, au labda kiongozi wa kidini, atatokea na kuwaongoza ifaavyo.

Kwa kweli, miaka elfu mbili iliyopita, watu walitaka kumfanya Yesu Kristo awe mfalme wao kwa kuwa walitambua kwamba ametumwa na Mungu na hivyo angekuwa mtawala anayestahili zaidi. Hata hivyo, Yesu alipotambua makusudio yao, aliondoka mahali hapo upesi. (Yohana 6:14, 15) Baadaye alimweleza gavana Mroma kwamba ‘ufalme wake si sehemu ya ulimwengu huu.’ (Yohana 18:36) Hata hivyo, leo, ni watu wachache wanaochukua msimamo kama wa Yesu, hata viongozi wa kidini wanaodai kuwa wafuasi wake wameshindwa kufanya hivyo. Baadhi ya viongozi hao wamejaribu kufanya ulimwengu huu uwe mahali bora—ama kwa kujaribu kushawishi viongozi wa kisiasa au kwa kushikilia vyeo vya kisiasa. Tunaweza kuona jinsi walivyofanya hivyo kwa kutazama matukio ya miaka ya 1960 na 1970.

Jitihada za Dini za Kuboresha Ulimwengu

Mwishoni mwa miaka ya 1960, wanatheolojia fulani katika nchi za Amerika Kusini walianza kuwapigania maskini na watu waliodhulumiwa. Ili kutimiza lengo lao, walianzisha harakati ya kidini ya ukombozi, ambapo walionyesha kwamba Kristo si mkombozi tu wa wanadamu kama isemavyo Biblia, bali pia ni mkombozi wa kisiasa na kiuchumi. Nchini Marekani, viongozi kadhaa wa kanisa waliohangaishwa sana na kuzorota kwa maadili walianzisha shirika fulani lililoitwa Moral Majority. Shirika hilo lilikuwa na lengo la kupigania watu fulani wapate vyeo vya kisiasa ili watunge sheria zinazofaa za maadili ya familia. Vivyo hivyo, katika nchi nyingi za Kiislamu, vikundi kadhaa vimejaribu kuzuia ufisadi na mwenendo usio wa adili kwa kuchochea watu waitii sana Koran.

Je, unaamini kwamba ulimwengu umekuwa mahali bora kwa sababu ya jitihada hizo? Ukweli ni kwamba, kwa ujumla, maadili yanazidi kuzorota na matajiri wanazidi kutajirika huku maskini wakizidi kuwa mafukara, hata katika nchi ambazo harakati ya kidini ya ukombozi ilikuwa imepamba moto.

Jerry Falwell, mwanzilishi wa shirika la Moral Majority, alilivunja shirika hilo mwaka wa 1989 baada ya kushindwa kutimiza malengo yake makuu nchini Marekani. Mashirika mengine yameanzishwa baada ya shirika hilo kuvunjwa. Hata hivyo, Paul Weyrich, aliyetunga maneno “moral majority,” aliandika hivi katika gazeti Christianity Today: ‘Hata tunaposhinda katika siasa, bado ushindi huo hautokezi sera zinazofaa.’ Pia aliandika hivi: ‘Utamaduni unaleta ufukara unaoongezeka daima. Tumepatwa na matatizo ya utamaduni unaozorota, nao umezorota kwa kadiri kubwa sana hivi kwamba siasa haziwezi kusaidia.’

Mtungaji na mwandishi-habari wa makala maalumu, Cal Thomas, alitaja kile alichohisi kuwa kiini cha tatizo katika jitihada za kuboresha jamii kupitia siasa: “Badiliko la kweli hufanywa na mtu mmoja-mmoja, si kwa kupata vyeo vya kisiasa, kwa sababu matatizo yetu ya msingi ni ya kiadili na kiroho wala si ya kiuchumi na kisiasa.”

Lakini unawezaje kutatua matatizo ya kiadili na ya kiroho katika ulimwengu ambao hauna viwango, na ambapo watu hujiamulia yaliyo mema na yaliyo mabaya? Ikiwa watu mashuhuri na wenye makusudio mema—wawe ni wa dini au la—wameshindwa kufanya ulimwengu huu uwe mahali bora kwelikweli, ni nani anayeweza kufaulu? Makala inayofuata itatupa jibu. Kwa kweli, jibu hilo ndiyo sababu ya msingi iliyofanya Yesu aseme kwamba Ufalme wake haukuwa sehemu ya ulimwengu huu.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 2]

COVER: Dirty water: WHO/UNICEF photo; globe: Mountain High Maps® Copyright © 1997 Digital Wisdom, Inc.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 3]

Watoto: UN photo; dunia: Mountain High Maps® Copyright © 1997 Digital Wisdom, Inc.