Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi Ulimwengu Wenye Furaha Utakavyotokea

Jinsi Ulimwengu Wenye Furaha Utakavyotokea

Jinsi Ulimwengu Wenye Furaha Utakavyotokea

“YESU wa Nazareti ndiye aliyekuwa mwanadamu mwenye uwezo mkubwa zaidi si katika milenia hizi mbili zilizopita, bali katika muda wote ambao mwanadamu amekuwepo,” likasema gazeti Time. Alipokuwa duniani, maelfu ya watu wenye mioyo minyofu waliona ukuu wake na pia jinsi alivyowahangaikia wengine. Kwa hiyo, haishangazi kwamba walitaka kumfanya mfalme. (Yohana 6:10, 14, 15) Hata hivyo, kama ilivyotajwa katika makala iliyotangulia, Yesu alikataa kujihusisha na siasa.

ITIKIO la Yesu lilitegemea angalau mambo matatu: maoni ya Baba yake kuhusu uhuru wa wanadamu wa kujiamulia mambo, unaotia ndani utawala wa wanadamu; utambuzi wa Yesu kwamba kuna roho waovu wasioonekana ambao hupinga jitihada bora za wanadamu za kutawala; na kusudi la Mungu la kuanzisha serikali ya kimbingu itakayotawala dunia nzima. Tunapochunguza kwa makini mambo hayo matatu, tutaelewa ni kwa nini wanadamu wameshindwa kufanya ulimwengu uwe mahali bora. Pia tutaona jinsi ulimwengu bora utakavyotokea.

Je, Wanadamu Wanaweza Kujitawala?

Mungu alipowaumba wanadamu, aliwapa mamlaka ya kutawala wanyama. (Mwanzo 1:26) Lakini wanadamu walikuwa chini ya utawala wa Mungu. Mwanamume na mwanamke wa kwanza walipaswa kuthibitisha kwamba wanamtii Mungu kwa kutokula tunda la mti mmoja tu, “mti wa ujuzi wa mema na mabaya.” (Mwanzo 2:17) Kwa kusikitisha, Adamu na Hawa walitumia vibaya hiari yao na wakakosa kumtii Mungu. Kula tunda lililokatazwa hakukuwa wizi tu. Huo ulikuwa uasi dhidi ya enzi kuu ya Mungu. Kielezi-chini katika andiko la Mwanzo 2:17 katika The New Jerusalem Bible chasema kwamba Adamu na Hawa “walitaka kujitegemea kabisa, jambo linalomfanya mwanadamu asitambue kwamba aliumbwa . . . Dhambi ya kwanza ilikuwa uasi dhidi ya enzi kuu ya Mungu.”

Kwa sababu ya masuala muhimu ya adili yaliyohusika, Mungu aliruhusu Adamu na Hawa na wazao wao waamue jinsi watakavyoishi, nao wakajiwekea viwango vya mema na mabaya. (Zaburi 147:19, 20; Waroma 2:14) Kwa kweli, wanadamu walianza kujiamulia mambo tangu wakati huo. Je, wamefaulu? Baada ya kuchunguza mambo ambayo yametokea miaka mingi iliyopita twaweza kusema hawajafaulu! Andiko la Mhubiri 8:9, chapa ya 1989 lasema: “Mtu mmoja anayo mamlaka juu ya mwenziwe kwa hasara yake.” Historia yenye kusikitisha ya utawala wa mwanadamu yathibitisha ukweli wa andiko la Yeremia 10:23: “Ee BWANA, najua ya kuwa njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” Historia imethibitisha kwamba wanadamu hawawezi kufanikiwa kujitawala pasipo Muumba wao.

Yesu alikubali kabisa jambo hilo. Alichukizwa sana na wazo la kujitawala pasipo Mungu. Alisema hivi: “Sifanyi jambo lolote kwa uanzisho wangu mwenyewe. . . . Sikuzote mimi hufanya mambo yale yanayompendeza [Mungu].” (Yohana 4:34; 8:28, 29) Kwa hiyo, Yesu alikataa kabisa kukubali kupokea utawala kutoka kwa wanadamu bila idhini ya Mungu. Hata hivyo, hii haimaanishi kwamba Yesu hakutaka kusaidia wanadamu wenzake. Kinyume cha hilo, alitumia uwezo wake wote kusaidia watu wapate furaha wakati huo na pia wakati ujao. Hata alitoa uhai wake kwa ajili ya wanadamu. (Mathayo 5:3-11; 7:24-27; Yohana 3:16) Lakini Yesu alijua kwamba “kwa kila jambo kuna majira yake,” kutia ndani wakati Mungu atakapoanza kutawala wanadamu. (Mhubiri 3:1; Mathayo 24:14, 21, 22, 36-39) Hata hivyo, kumbuka kwamba katika bustani ya Edeni, wazazi wetu wa kwanza walikubali kufanya mapenzi ya roho mwovu aliyezungumza kwa kutumia nyoka halisi. Sasa tutazungumzia sababu ya pili iliyomfanya Yesu asijihusishe na siasa.

Mtawala wa Ulimwengu Asiyejulikana

Biblia yatuambia kwamba Shetani alimtolea Yesu “falme zote za ulimwengu na utukufu wazo” ili amwabudu. (Mathayo 4:8-10) Kwa kweli, Yesu alitolewa utawala wa ulimwengu—lakini kwa masharti ya Ibilisi. Yesu hakushindwa na kishawishi hicho. Lakini je, hicho kilikuwa kishawishi kweli? Je, kwa kweli Shetani angeweza kumpa Yesu falme hizo zote? Ndiyo, kwa sababu Yesu alimwita Ibilisi “mtawala wa ulimwengu,” naye mtume Paulo akamtaja kuwa “mungu wa huu mfumo wa mambo.”—Yohana 14:30; 2 Wakorintho 4:4; Waefeso 6:12.

Bila shaka, Yesu alijua kwamba Shetani hapendezwi kikweli na masilahi ya wanadamu. Alisema kwamba Shetani ni “muuaji” na “baba ya uwongo na udanganyifu wote.” (Yohana 8:44, The Amplified Bible) Bila shaka, ulimwengu ‘unaokaa katika nguvu’ za roho huyo mwovu hauwezi kuwa na furaha ya kweli. (1 Yohana 5:19) Lakini Ibilisi hatakuwa na mamlaka hayo milele. Hivi karibuni,Yesu, ambaye sasa ni kiumbe wa roho mwenye nguvu, atamwondoa Shetani na kuondoa kabisa uvutano wake.—Waebrania 2:14; Ufunuo 20:1-3.

Shetani anajua kwamba siku zake akiwa mtawala wa ulimwengu zinamalizika upesi sana. Kwa hiyo, ameazimia kuwapotosha wanadamu kabisa wasiweze kurekebika tena, kama vile alivyofanya kabla ya Furiko la siku za Noa. (Mwanzo 6:1-5; Yuda 6) Andiko la Ufunuo 12:12 lasema, “Ole wa dunia na wa bahari, kwa sababu Ibilisi ameteremka kwenu, akiwa na hasira kubwa, akijua ana kipindi kifupi cha wakati.” Unabii wa Biblia na matukio ya ulimwengu yanaonyesha kwamba tunakaribia umalizio wa “kipindi [hiki] kifupi cha wakati.” (2 Timotheo 3:1-5) Tutapata kitulizo hivi karibuni.

Serikali Itakayoleta Furaha

Sababu ya tatu iliyomfanya Yesu asijihusishe na siasa ni kwamba alijua kuwa wakati ujao hususa, Mungu angesimamisha serikali ya kimbingu itakayotawala dunia. Biblia inaita serikali hiyo Ufalme wa Mungu, nayo ilikuwa kichwa kikuu cha mafundisho ya Yesu. (Luka 4:43; Ufunuo 11:15) Yesu aliwafundisha wafuasi wake waombe Ufalme huo uje, kwa kuwa ni chini ya utawala huo tu ndipo ‘mapenzi ya Mungu yatakapotendeka duniani kama ilivyo katika mbingu.’ (Mathayo 6:9, 10) Huenda ukajiuliza, ‘Ikiwa Ufalme huo utatawala dunia nzima, ni nini kitakachozipata serikali za wanadamu?’

Jibu linapatikana katika andiko la Danieli 2:44: “Katika siku za wafalme hao [wanaotawala mwishoni mwa mfumo wa sasa] Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele, wala watu wengine hawataachiwa enzi yake; bali utavunja falme hizi [falme za wanadamu] zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.” (Italiki ni zetu.) Kwa nini itakuwa lazima Ufalme wa Mungu ‘uvunje’ tawala za kidunia? Kwa sababu tawala hizo zinaendeleza mtazamo wa kumkaidi Mungu na wa kujiamulia mambo ambao ulianzishwa na Shetani katika bustani ya Edeni. Mbali na kutowanufaisha wanadamu, wale wanaojaribu kuendeleza mtazamo huo watapambana na Muumba. (Zaburi 2:6-12; Ufunuo 16:14, 16) Kwa hiyo, twapaswa kujiuliza hivi, ‘Je, tunaunga mkono au tunapinga utawala wa Mungu?’

Utachagua Utawala wa Nani?

Ili kuwasaidia watu wafanye uamuzi unaotegemea ujuzi sahihi kuhusu utawala, Yesu aliwaagiza wanafunzi wake wahubiri “habari njema ya ufalme . . . katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya kuwa ushahidi kwa mataifa yote” kabla mfumo huu wa sasa haujakoma. (Mathayo 24:14) Ni nani leo wanaojulikana ulimwenguni pote kwa kuhubiri Ufalme wa Mungu? Ni Mashahidi wa Yehova. Kwa kweli, kwa muda mrefu gazeti hili limekuwa na maneno haya kwenye jalada yake, “Unaotangaza Ufalme wa Yehova.” Leo, Mashahidi wapatao milioni sita katika nchi zaidi ya 230 wanasaidia watu wapate ujuzi sahihi kuhusu Ufalme huo. *

Baraka kwa Raia wa Ufalme

Sikuzote Yesu alifanya mambo namna Mungu alivyotaka. Kwa hiyo, badala ya kujitegemea au kujaribu kuunga mkono au kuboresha mfumo wa mambo uliokuwako kwa kutumia mbinu za kisiasa, alijitahidi sana kuendeleza masilahi ya Ufalme wa Mungu, ambao ndio suluhisho pekee la matatizo ya ulimwengu. Kwa sababu ya uaminifu wake, alithawabishwa kwa kupewa kiti chenye utukufu mbinguni, akawa Mfalme wa Ufalme huo. Hiyo ni thawabu iliyoje kwa sababu ya kumtii Mungu!—Danieli 7:13, 14.

Mamilioni ya watu leo wanaomwiga Yesu kwa kutanguliza Ufalme na kutii mapenzi ya Mungu watapewa pia thawabu nzuri sana—pendeleo la kuwa raia wa kidunia wa Ufalme wa Mungu. (Mathayo 6:33) Chini ya utawala wake wenye upendo, watafanywa kuwa wakamilifu, na kuwa na taraja la uhai udumuo milele. (Ufunuo 21:3, 4) Andiko la 1 Yohana 2:17 lasema: “Ulimwengu unapitilia mbali na ndivyo na tamaa yao, lakini yeye ambaye hufanya mapenzi ya Mungu hudumu milele.” Itakuwa shangwe iliyoje kuishi hapa milele baada ya Shetani na wafuasi wake kuondolewa na dunia nzima kugeuzwa kuwa paradiso isiyo na utukuzo wa taifa unaosababisha migawanyiko, mifumo ya kibiashara yenye ufisadi, na dini isiyo ya kweli!— Zaburi 37:29; 72:16.

Naam, Ufalme wa Mungu ndio suluhisho halisi litakalotokeza ulimwengu wenye furaha ya kweli, na ujumbe unaotangaza ufalme huo unatajwa kwa kufaa kuwa habari njema. Ikiwa bado hujafanya hivyo, kwa nini usiwasikilize Mashahidi wa Yehova watakapokuletea habari njema nyumbani kwako?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 16 Wanapotetea Ufalme wa Mungu, Mashahidi wa Yehova hawajihusishi na siasa au kuchochea uasi dhidi ya serikali, hata katika nchi ambapo wamepigwa marufuku au wananyanyaswa. (Tito 3:1) Badala yake, wanajitahidi kusaidia watu kiroho bila kujihusisha na siasa kama vile Yesu na wanafunzi wake wa karne ya kwanza walivyofanya. Mashahidi hujitahidi kusaidia watu wanaopenda uadilifu katika jumuiya zao mbalimbali wafuate kanuni zinazofaa za Biblia, kama vile upendo wa kifamilia, unyofu, usafi wa kiadili, na mazoea mazuri ya kazi. Wao hujitahidi hasa kuwafundisha watu watii kanuni za Biblia na kutegemea Ufalme wa Mungu ambao ndio tumaini halisi la wanadamu.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Historia yathibitisha kwamba wanadamu hawawezi kufanikiwa kujitawala pasipo Mungu

[Picha katika ukurasa wa 5]

Kwa kuwa anatawala ‘mfumo wa sasa wa mambo,’ Shetani angeweza kumtolea Yesu “falme zote za ulimwengu”

[Picha katika ukurasa wa 7]

Yesu alifundisha kwamba chini ya Ufalme wa Mungu, ulimwengu utakuwa mahali pazuri sana