Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jipatie Moyo Unaompendeza Yehova

Jipatie Moyo Unaompendeza Yehova

Jipatie Moyo Unaompendeza Yehova

“Uniumbie moyo safi, ee Mungu, uweke ndani yangu roho mpya na thabiti.”—ZABURI 51:10, Biblia Habari Njema.

1, 2. Kwa nini tupendezwe na moyo wetu?

ALIKUWA mrefu na mwenye sura nzuri. Alipomwona, nabii Samweli alivutiwa sana na mwana huyu wa kwanza wa Yese hivi kwamba aliamua yeye ndiye aliyekuwa amechaguliwa na Mungu awe mfalme baada ya Sauli. Lakini Yehova akasema: “Usimtazame uso wake, wala urefu wa kimo chake; kwa maana mimi nimemkataa. . . . Wanadamu huitazama sura ya nje, bali BWANA huutazama moyo.” Yehova alimchagua Daudi, mwana wa Yese aliyekuwa na umri mdogo zaidi, ambaye ‘aliupendeza moyo wake.’—1 Samweli 13:14; 16:7.

2 Kama alivyodhihirisha baadaye, Mungu anaweza kusoma moyo wa mwanadamu: “Mimi, BWANA, nauchunguza moyo, navijaribu viuno, hata kumpa kila mtu kiasi cha njia zake, kiasi cha matunda ya matendo yake.” (Yeremia 17:10) Naam, “BWANA huijaribu [“huichunguza,” NW] mioyo.” (Mithali 17:3) Hivyo basi, ni moyo gani wa mwanadamu ambao Yehova huchunguza? Nasi tunaweza kufanya nini ili tujipatie moyo unaompendeza?

“Yule Mtu wa Siri wa Moyoni”

3, 4. Neno “moyo” hutumiwa kwenye Biblia katika maana gani hasa? Toa mifano.

3 Neno “moyo” lapatikana karibu mara elfu moja katika Maandiko Matakatifu. Mara nyingi limetumiwa kwa njia ya mfano. Kwa mfano, Yehova alimwambia hivi nabii Musa: “Waambie wana wa Israeli kwamba wanitwalie sadaka; kila mtu ambaye moyo wake wampa kupenda mtatwaa kwake sadaka yangu.” Nao wale waliotoa sadaka “wakaja kila mtu ambaye moyo wake ulimhimiza.” (Kutoka 25:2; 35:21) Ni wazi kwamba, mojawapo ya sifa ya moyo wa mfano ni kichocheo—ile nguvu ya ndani ambayo hutusukuma tutende mambo. Moyo wetu wa mfano pia hudhihirisha hisia zetu, tamaa, na mapendezi yetu. Moyo unaweza kujaa hasira au hofu, unaweza kulemewa na majonzi au kuchachawa kwa furaha. (Zaburi 27:3; 39:3; Yohana 16:22; Waroma 9:2) Moyo unaweza kuwa na kiburi au kuwa mnyenyekevu, wenye upendo au wenye chuki.—Mithali 16:5; Mathayo 11:29; 1 Petro 1:22.

4 Hivyo, mara nyingi “moyo” huhusianishwa na kichocheo na hisia, nayo “akili” huhusianishwa hasa na ufahamu. Maneno hayo yanapaswa kueleweka hivyo yanapotumiwa katika muktadha uleule katika Maandiko. (Mathayo 22:37; Wafilipi 4:7) Lakini maneno moyo na akili yanaweza kumaanisha jambo lilelile. Kwa mfano, Musa aliwahimiza Waisraeli hivi: “Ukaweke moyoni mwako [au, “akilini mwako,” NW, kielezi-chini], ya kuwa BWANA ndiye Mungu.” (Kumbukumbu la Torati 4:39) Yesu alisema hivi kuhusu waandishi waliopanga njama dhidi yake: “Kwa nini mnafikiri mambo maovu katika mioyo yenu?” (Mathayo 9:4) Maneno “uelewevu,” “ujuzi,” na ‘kuwazawaza’ yanaweza pia kuhusianishwa na moyo. (1 Wafalme 3:12, NW; Mithali 15:14, NW; Marko 2:6) Kwa hiyo, moyo wa mfano pia unaweza kuhusisha akili yetu, yaani, mawazo au ufahamu wetu.

5. Moyo wa mfano humaanisha nini?

5 Kulingana na kitabu kimoja cha marejezo, moyo wa mfano humaanisha “zile hisia za ndani kwa ujumla, kwa hiyo moyo wa mfano humaanisha mtu wa ndani kama anavyojidhihirisha kwa matendo yake mbalimbali, tamaa, mapendezi, hisia, hamu, makusudi, mawazo, ufahamu, fikira, hekima, ujuzi, ustadi, imani, kuwazawaza, kumbukumbu, na utambuzi wake.” Moyo hudhihirisha hasa hisia zetu za ndani, “mtu wa siri wa moyoni.” (1 Petro 3:4) Huo ndio moyo ambao Yehova huona na kuchunguza. Hivyo, Daudi angeweza kusali: “Uniumbie moyo safi, ee Mungu, uweke ndani yangu roho mpya na thabiti.” (Zaburi 51:10, BHN) Tunaweza kujipatia moyo safi jinsi gani?

‘Liwekeni Mioyoni Mwenu’ Neno la Mungu

6. Musa aliwapa Waisraeli ushauri gani walipokuwa wamepiga kambi kwenye Nyanda za Moabu?

6 Musa aliwashauri hivi wana wa Israeli waliokuwa wamekusanyika kwenye Nyanda za Moabu kabla ya kuingia katika Bara Lililoahidiwa: “Yawekeni mioyoni mwenu maneno yote ambayo nashuhudia kwenu hivi leo; nayo waamuruni watoto wenu, wayatunze na kuyafanya maneno yote ya torati hii.” (Kumbukumbu la Torati 32:46) Waisraeli walipaswa kusikiliza vizuri. Wangeweza tu kuwafundisha watoto wao amri za Mungu ikiwa wao wenyewe wangezifahamu barabara.—Kumbukumbu la Torati 6:6-8.

7. Inamaanisha nini ‘kuweka moyoni mwetu’ Neno la Mungu?

7 Ili kujipatia moyo safi ni muhimu kupata ujuzi sahihi wa mapenzi na makusudi ya Mungu. Ujuzi huo unaweza kupatikana tu katika Neno la Mungu lililopuliziwa. (2 Timotheo 3:16, 17) Ujuzi pekee hautatusaidia kujipatia moyo unaompendeza Yehova. Ni lazima ‘tuweke moyoni mwetu,’ au “tuyatie moyoni,” yale tunayojifunza ili ujuzi uweze kufikia hisia zetu za ndani. (Kumbukumbu la Torati 32:46, An American Translation) Tutafanya hivyo kwa njia gani? Mtunga-zaburi Daudi anaeleza: “Nimezikumbuka siku za kale, nimeyatafakari matendo yako yote, naziwaza kazi za mikono yako.”—Zaburi 143:5.

8. Tunaweza kutafakari maswali gani tunapojifunza?

8 Sisi pia tunapaswa kuyatafakari kwa shukrani matendo ya Yehova. Tunaposoma Biblia au vichapo vinavyotegemea Biblia, tunahitaji kutafakari maswali kama: ‘Jambo hili linanifundisha nini kumhusu Yehova? Ni sifa gani za Yehova ninazoona hapa? Masimulizi haya yananifunza nini kuhusu yale ambayo Yehova hupenda na yale ambayo huchukia? Ni nini matokeo ya kufuata mwenendo ambao Yehova hupenda kwa kulinganisha na mwenendo ambao yeye huchukia? Habari hii inahusiana jinsi gani na yale ambayo tayari ninajua?’

9. Ni muhimu kadiri gani kuwa na funzo la kibinafsi na kutafakari?

9 Lisa * mwenye umri wa miaka 32 aeleza jinsi alivyoanza kuthamini manufaa ya kujifunza na kutafakari akiwa na kusudi maalum: “Baada ya kubatizwa mwaka wa 1994, nilikuwa mwenye bidii sana katika kweli kwa muda wa miaka miwili hivi. Nilihudhuria mikutano yote ya Kikristo, nikatumia muda wa saa 30 hadi 40 kila mwezi kwenye huduma ya shambani, na kushirikiana na Wakristo wenzangu. Kisha bidii yangu ikaanza kufifia. Hali yangu ilikuwa mbaya sana kiasi kwamba nilivunja sheria ya Mungu. Lakini nilirudiwa na fahamu na nikaamua kuishi kupatana na Biblia. Ninafurahi kama nini kwamba Yehova amenikubali na kukubali toba yangu! Mara kwa mara nimejiuliza: ‘Kwa nini nilifanya dhambi?’ Sikuzote mimi hukumbuka kwamba nilipuuza kujifunza na kutafakari nikiwa na kusudi maalum. Kweli ya Biblia haikuwa imepenya ndani ya moyo wangu. Kuanzia sasa na kuendelea, sikuzote nitakazia uangalifu sana funzo la kibinafsi na kutafakari.” Tuzidipo kupata ujuzi kumhusu Yehova, Mwana wake, na Neno lake, ni muhimu kama nini kutenga wakati ili kutafakari tukiwa na kusudi maalum!

10. Kwa nini ni muhimu tutafute wakati wa kujifunza kibinafsi na kutafakari?

10 Katika ulimwengu huu wenye shughuli nyingi, si rahisi hata kidogo kupata wakati wa kujifunza na kutafakari. Hata hivyo, Wakristo leo wamekaribia sana kuingia katika Bara zuri Lililoahidiwa—ulimwengu mpya wa Mungu. (2 Petro 3:13) Matukio yenye kutisha, kama vile kuharibiwa kwa “Babiloni Mkubwa” na kushambuliwa kwa watu wa Yehova na “Gogu wa nchi ya Magogu” kunakaribia. (Ufunuo 17:1, 2, 5, 15-17; Ezekieli 38:1-4, 14-16; 39:2) Huenda mambo yatakayotukia baadaye yakajaribu upendo wetu kwa Yehova. Ni muhimu kwamba tununue wakati ufaao sasa na kuweka Neno la Mungu moyoni mwetu!—Waefeso 5:15, 16.

‘Tayarisha Moyo Wako Kutafuta Ushauri wa Neno la Mungu’

11. Moyo wetu unaweza kulinganishwa na udongo jinsi gani?

11 Moyo wa mfano unaweza kulinganishwa na udongo ambamo mbegu ya ile kweli inaweza kupandwa. (Mathayo 13:18-23) Kwa kawaida udongo halisi hutayarishwa ili mimea iweze kukua ikiwa na afya. Vivyo hivyo, moyo unapaswa kutayarishwa ili uweze kuwa mwepesi zaidi kusikiliza Neno la Mungu. Kuhani Ezra “a[li]tayarisha moyo wake kutafuta ushauri wa sheria ya Yehova na kuitenda.” (Ezra 7:10, NW) Tunaweza kutayarisha moyo wetu jinsi gani?

12. Ni nini kitakachosaidia kutayarisha moyo wakati wa funzo?

12 Sala ya kutoka moyoni hutayarisha moyo wetu vema zaidi tunapotafuta ushauri wa Neno la Mungu. Mikutano ya Kikristo ya waabudu wa kweli huanza na kumalizika kwa sala. Inafaa kama nini kuanza kila kipindi cha funzo la kibinafsi la Biblia kwa sala ya kutoka moyoni, kisha kutafuta msaada wa Mungu hata wakati wa funzo!

13. Tunapaswa kufanya nini ili tujipatie moyo unaompendeza Yehova?

13 Moyo wa mfano unapaswa kutayarishwa ili kuondoa maoni uliyokuwa nayo hapo awali. Viongozi wa kidini wa siku za Yesu hawakutaka kufanya hivyo. (Mathayo 13:15) Kwa upande mwingine, Maria, mama ya Yesu alikata kauli “moyoni mwake” akitegemea kweli alizokuwa amesikia. (Luka 2:19, 51) Akawa mwanafunzi mwaminifu wa Yesu. Lidia wa Thiatira alimsikiliza Paulo, “na Yehova akafungua wazi moyo wake ukazie uangalifu.” Yeye pia akawa mwamini. (Matendo 16:14, 15) Basi, na tusishikilie kwa ushupavu maoni ya kibinafsi au mafundisho ya kidini tunayopenda sana. Badala yake, na tuwe tayari ‘kuacha Mungu apate kuonekana kuwa wa kweli, lakini kila binadamu apate kuonekana kuwa mwongo.’—Waroma 3:4.

14. Tunaweza kutayarisha moyo wetu jinsi gani ili kusikiliza kwenye mikutano ya Kikristo?

14 Ni muhimu sana kutayarisha moyo ili kusikiliza kwenye mikutano ya Kikristo. Huenda vikengeusha-fikira vikafanya tusisikilize yale yanayosemwa. Hatutanufaika kikamili na yale yanayosemwa ikiwa tunafikiria mambo yaliyotukia mchana au tunafikiria yale tutakayofanya siku inayofuata. Tunahitaji kuazimia kusikiliza na kujifunza ikiwa tutanufaika na yale yanayosemwa. Tunaweza kupata manufaa yaliyoje iwapo tutaazimia kuelewa maandiko yanayofafanuliwa na kuelezwa!—Nehemia 8:5-8, 12.

15. Unyenyekevu hutusaidia jinsi gani kuweza kufundishwa kwa urahisi zaidi?

15 Kama vile kuongeza mbolea ifaayo kwenye udongo kunavyoweza kuuboresha, vivyo hivyo moyo wetu wa mfano unaweza kuboreshwa kwa kusitawisha unyenyekevu, hamu ya mambo ya kiroho, tumaini, hofu ya kimungu, na upendo kwa Mungu. Unyenyekevu hufanya moyo wetu uwe mwororo, na hivyo kuweza kufundishwa kwa urahisi zaidi. Yehova alimwambia hivi Mfalme Yosia wa Yuda: “Kwa kuwa moyo wako ulikuwa mwororo, nawe ukajinyenyekesha mbele za BWANA, hapo ulipoyasikia maneno niliyoyanena . . . ukalia mbele zangu; basi, mimi nami nimekusikia wewe.” (2 Wafalme 22:19) Moyo wa Yosia ulikuwa mnyenyekevu na mwepesi kusikiliza. Unyenyekevu uliwawezesha wanafunzi wa Yesu, watu “wasio na elimu na wa kawaida tu,” waelewe na kutumia kweli za kiroho ambazo “wenye hekima na walio na akili” hawakuelewa. (Matendo 4:13; Luka 10:21) Na ‘tujinyenyekeze mbele za Mungu’ tunapojitahidi kujipatia moyo unaompendeza Yehova.—Ezra 8:21.

16. Kwa nini jitihada inahitajiwa ili tusitawishe hamu ya chakula cha kiroho?

16 Yesu alisema: “Wenye furaha ni wale wanaoona uhitaji wao wa kiroho.” (Mathayo 5:3) Japo tumepewa uwezo wa kuwa watu wa kiroho, mikazo ya ulimwengu huu mwovu au tabia kama uvivu zaweza kufanya tusione uhitaji wetu wa kiroho. (Mathayo 4:4) Lazima tusitawishe hamu ifaayo ya chakula cha kiroho. Hata ikiwa mwanzoni hatutafurahia usomaji wa Biblia na funzo la kibinafsi, tukiendelea bila kuacha, ujuzi ‘utapendeza nafsi yetu,’ hivi kwamba tutakuwa tukingojea kwa hamu vipindi vya kujifunza.—Mithali 2:10, 11.

17. (a) Kwa nini inastahili tumtumaini Yehova kabisa? (b) Tunaweza kusitawisha tumaini katika Mungu jinsi gani?

17 “Mtumaini BWANA kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe,” akashauri Mfalme Solomoni. (Mithali 3:5) Moyo unaomtumaini Yehova unajua kwamba chochote ambacho Yeye hutaka au kuagiza kupitia Neno lake kinafaa sikuzote. (Isaya 48:17) Bila shaka, inastahili tumtumaini Yehova kabisa. Ana uwezo wa kutimiza yote ambayo amekusudia. (Isaya 40:26, 29) Hata maana halisi ya jina lake ni, “Yeye Husababisha Iwe,” jambo ambalo hutoa uhakikisho kwamba ana uwezo wa kutimiza yale ambayo ameahidi! Ni “mwenye haki katika njia zake zote, na mwenye fadhili [“mwaminifu-mshikamanifu,” NW ] juu ya kazi zake zote.” (Zaburi 145:17) Bila shaka, ili tusitawishe tumaini katika yeye, tunahitaji ‘kuonja tuone ya kuwa BWANA yu mwema’ kwa kutumia maishani mwetu yale tunayojifunza katika Biblia na kutafakari jinsi yanavyotunufaisha.—Zaburi 34:8.

18. Kumhofu Mungu hutusaidia jinsi gani kuwa wepesi kufuata mwongozo wake?

18 Akionyesha sifa nyingine ambayo hufanya moyo wetu uwe mwepesi kufuata mwongozo wa Mungu, Solomoni alisema: “Mche [“mhofuni,” NW] BWANA, ukajiepushe na uovu.” (Mithali 3:7) Yehova alisema hivi kuhusu Waisraeli wa kale: “Laiti wangekuwa na moyo kama huu ndani yao sikuzote, wa kunicha [“kunihofu,” NW], na kushika amri zangu zote sikuzote, wapate kufanikiwa wao na watoto wao milele!” (Kumbukumbu la Torati 5:29) Naam, wale wanaomhofu Mungu humtii. Yehova ana uwezo wa ‘kujionyesha mwenye nguvu kwa ajili ya hao, waliokamilika moyo kuelekea kwake’ na kuwaadhibu wasiomtii. (2 Mambo ya Nyakati 16:9) Hofu yenye staha ya kutotaka kumchukiza Mungu na iongoze matendo yetu, mawazo, na hisia zetu.

‘Mpende Yehova kwa Moyo Wako Wote’

19. Upendo hutimiza fungu gani katika kufanya moyo wetu uitikie mwongozo wa Yehova?

19 Kati ya sifa nyingine zote, upendo ndio hasa hufanya moyo wetu uitikie mwongozo wa Yehova. Moyo uliojaa upendo kwa Mungu hufanya mtu awe na hamu ya kujua yale yanayompendeza Mungu na yale yasiyompendeza. (1 Yohana 5:3) Yesu alisema: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.” (Mathayo 22:37) Na tuzidishe upendo wetu kwa Mungu kwa kuwa na mazoea ya kutafakari wema wake, kwa kuzungumza naye kama rafiki yetu wa karibu, na kwa kuzungumza na wengine kwa shauku kumhusu.

20. Tunaweza kujipatia moyo unaompendeza Yehova jinsi gani?

20 Kwa kujikumbukusha: Kujipatia moyo unaompendeza Yehova humaanisha kuruhusu Neno la Mungu lifikie hisia zetu za ndani, yule mtu wa siri wa moyoni. Tunapaswa kujifunza Maandiko tukiwa na kusudi maalum na kutafakari kwa shukrani. Ili kufanya hivyo tunahitaji kuwa na moyo uliotayarishwa—moyo ulioacha maoni uliyokuwa nayo hapo awali, uliojaa sifa zinazotufanya tuwe wenye kufundishika! Naam, kwa msaada wa Yehova, tunaweza kujipatia moyo unaompendeza. Hata hivyo, tunaweza kuchukua hatua gani kulinda moyo wetu?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Jina limebadilishwa.

Ungejibuje?

• Ni moyo gani wa mfano ambao Yehova huchunguza?

• Tunaweza ‘kuweka Neno la Mungu moyoni mwetu’ jinsi gani?

• Tunapaswa kutayarisha moyo wetu jinsi gani ili kutafuta ushauri wa Neno la Mungu?

• Baada ya kujifunza habari hii, umechochewa kufanya nini?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 17]

Daudi alitafakari kwa shukrani mambo ya kiroho. Je, wewe hufanya hivyo?

[Picha katika ukurasa wa 18]

Tayarisha moyo wako kabla ya kujifunza Neno la Mungu