Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maji ya Uhai Yatiririka Katika Milima ya Andes

Maji ya Uhai Yatiririka Katika Milima ya Andes

Maji ya Uhai Yatiririka Katika Milima ya Andes

Milima ya Andes imeigawanya Peru katikati kuwa maeneo mawili, eneo kavu la mwambao upande wa magharibi, na eneo lenye misitu upande wa mashariki. Zaidi ya thuluthi ya raia milioni 27 wa Peru huishi kwenye safu ya milima hii. Wanaishi ama katika nyanda za juu zenye miinuko mikali au katika korongo zenye kina kirefu na mabonde yenye rutuba ya milima hiyo.

SI RAHISI kufika kwenye safu hiyo ya Milima ya Andes yenye mawemawe. Kwa sababu hiyo, mamilioni ya watu wanaoishi huko ni kana kwamba wamejitenga, na mara nyingi hawajui mambo yanayotokea mbali na eneo lao.

Vijiji vidogo vimejengwa kandokando ya vijito ili kupata kwa urahisi maji yanayohitajiwa na mimea na mifugo ya lama, alpaca, vicuña, na kondoo. Hata hivyo, kuna aina nyingine ya maji yaliyo muhimu ambayo yanatiririka huko Andes—maji ya kiroho yenye kuburudisha yanayotoka kwa Yehova, ambaye ni “chemchemi ya maji ya uzima.” (Yeremia 2:13) Mungu hutumia Mashahidi wake wawasaidie watu wanaoishi juu ya Milima ya Andes wapate ujuzi sahihi kumhusu na kuhusu makusudi yake.—Isaya 12:3; Yohana 17:3.

Kwa kuwa mapenzi ya Mungu ni kwamba “watu wa namna zote waokolewe na kuja kwenye ujuzi sahihi wa kweli,” wahudumu hawa hujitahidi sana kutembelea jumuiya zisizoweza kufikiwa kwa urahisi na kuwapelekea ujumbe wa Biblia unaotoa uhai. (1 Timotheo 2:4) Ujumbe huo unaotegemea Biblia huelimisha na ni wa hali ya juu. Ujumbe huo umewaweka huru watu wanyofu kutokana na ushirikina, desturi na mawazo yaliyowafanya waogope wafu, roho waovu, na kani za asili. Jambo lililo muhimu hata zaidi ni kwamba ujumbe huo huwapa tumaini tukufu la uhai wa milele katika paradiso duniani.

Kufanya Jitihada ya Kuwafikia Watu

Wahubiri wa Ufalme wanaotembelea maeneo haya ya mbali wanahitaji kufanya marekebisho mengi. Ili kufikia mioyo ya watu kwa ujumbe wa Biblia, walimu wa Biblia wanahitaji kufahamu kwa kiasi fulani lugha zinazozungumzwa huko za Quechua au Aymara.

Si rahisi kufika kwenye vijiji vya Andes. Hakuna reli nyingi katika maeneo hayo. Usafiri hautegemeki nao hukabiliwa na hali mbaya ya hewa na mandhari isiyo ya kawaida. Basi, Mashahidi hufikishaje ujumbe wa Ufalme kwa watu hawa?

Wahubiri wa habari njema walio wajasiri wamekubali kufanya kazi hiyo ngumu na wameonyesha mtazamo kama wa nabii Isaya: “Mimi hapa, nitume mimi.” (Isaya 6:8) Wametumia nyumba tatu za kukokotwa ili kusafiri hadi kaskazini, eneo la kati, na kusini. Wakiwa na Biblia na vichapo vingi vinavyotegemea Biblia, mapainia wenye bidii, au wahudumu wa wakati wote, wamepanda mbegu za kweli ya Biblia kwa watu wanaoishi huko ambao ni wenye urafiki, wakarimu, na wanyofu.

Barabara za milima hiyo zimejipinda kwa njia hatari sana. Ili kupiga baadhi ya kona hizo, magari hulazimika kwenda kombokombo. Wakati fulani walipokuwa wakisafiri, mishonari mmoja aliyekuwa ameketi kwenye kiti cha nyuma katika basi alichungulia dirishani na kuona kwamba gurudumu moja la nyuma lilikuwa limekanyaga ukingoni kabisa mwa mteremko mkali wa jabali, wenye kimo cha meta zaidi ya 190! Alifunga macho yake hadi basi lilipopita mahali hapo.

Barabara nyingine zimeharibika na ni nyembamba sana. Mojawapo ya nyumba hizo za kukokotwa ilipokuwa ikiteremka kwenye sehemu hiyo yenye mawemawe, ilikutana na lori iliyokuwa ikipanda. Nyumba hiyo ya kukokotwa ilihitaji kurudi nyuma kwenye mlima hadi sehemu ambayo ingeweza kupishana na lori hiyo.

Hata hivyo, kumekuwa na matokeo mazuri sana kwa sababu ya jitihada hizo nyendelevu. Je, ungependa kujifunza mengi zaidi kuhusu jitihada hizo?

“Kutilia Maji” Ziwa Titicaca

Ziwa Titicaca lililo katika bonde la Milima ya Andes yenye kimo cha meta 3,800 juu ya usawa wa bahari, ndilo ziwa pekee barani linalotumiwa na vyombo vikubwa vya majini. Vilele vya milima vilivyofunikwa kwa theluji, ambavyo baadhi yavyo vina kimo cha meta zaidi ya 6,400, ni chemchemi ya karibu mito yote 25 inayoishia Titicaca. Kwa sababu sehemu hiyo imeinuka sana, tabia ya nchi ni baridi, na watu ambao si wenyeji, hupambana na magonjwa yanayopatikana katika nyanda za juu.

Miaka kadhaa iliyopita, kikundi cha mapainia wanaosema lugha ya Quechua na Aymara walifunga safari hadi Amantani na visiwa vya Taquile kwenye Ziwa Titicaca. Walibeba slaidi yenye kichwa “Kuchunguza Makanisa kwa Makini,” ambayo inaonyesha waziwazi uwongo wa Jumuiya ya Wakristo. Watu walifurahia sana slaidi hiyo. Mtu mmoja aliwakaribisha akina ndugu nyumbani mwake na kuwapa chumba kikubwa ambacho wangetumia kama makao na mahali pa kufundisha watu Biblia.

Mkutano wa kwanza huko Amantani ulihudhuriwa na watu 100, nao mkutano uliofanywa Taquile ukahudhuriwa na watu 140. Ulifanywa katika lugha ya Quechua. Wenzi fulani wa ndoa waliokuwa wameishi katika bara hilo hapo awali walisema hivi: “Wakati umefika kwa Mashahidi wa Yehova kutukumbuka. Tumekuwa tukisali mje.”

Mbali na visiwa hivi viwili vikubwa zaidi, habari njema pia zimehubiriwa katika visiwa vipatavyo 40 “vinavyoelea” kwenye Ziwa Titicaca. Visiwa vinavyoelea? Naam, visiwa hivi vimefanyizwa kwa totora, aina ya nyasi kubwa zinazokua katika sehemu fulani zisizo na kina za ziwa hilo. Nyasi hizo hukua na kuchomoza juu ya maji. Ili kujenga kisiwa, wenyeji hukunja nyasi hizo, zikiwa bado na mizizi, na kuzisokota ili kutengeneza jukwaa. Kisha jukwaa hilo hujazwa matope na kuimarishwa kwa kuongezewa nyasi zaidi. Watu huishi katika vibanda vilivyojengwa kwa nyasi juu ya jukwaa hizo.

Mashahidi wa Yehova walitumia mashua kuhubiria watu wanaoishi katika visiwa vya Ziwa Titicaca. Mashua hiyo inaweza kubeba abiria 16. Inapoegeshwa kwenye visiwa vinavyoelea, Mashahidi hutembea juu ya jukwaa lililojengwa kwa nyasi kutoka nyumba moja hadi nyingine. Wanasema kwamba kwa kawaida wao huhisi mtikiso fulani wanapokanyaga chini. Watu wanaoshikwa na kichefuchefu wanaposafiri kwa gari au kwa meli hawawezi kutembea katika eneo hili!

Watu wanaosema lugha ya Aymara, wanaishi katika jumuiya na vijiji vingi vilivyo kandokando ya pwani na kwenye peninsula inayochomoza katika ziwa. Ni rahisi zaidi kufika kwenye vijiji hivyo kwa kutumia mashua kuliko gari. Kwa ujumla, inakadiriwa kwamba kuna watu wapatao 400,000 wanaoishi katika maeneo ambayo huhubiriwa ujumbe wa Ufalme kwa kutumia mashua. Mashua hizo zitaendelea kutumiwa kwa muda.

Kukata Kiu ya Kiroho

Flavio aliishi katika kijiji cha Santa Lucía, karibu na Juliaca, kwenye Milima ya Andes. Katika Kanisa lake la Kievanjeli, alikuwa amefundishwa kuhusu moto wa mateso. Kwa miaka mingi, aliishi kwa kuogopa adhabu ya moto wa milele. Mara nyingi alijiuliza, Mungu mwenye upendo anawezaje kuwatesa wanadamu milele katika moto? Tito, mhudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova, alimtembelea Flavio alipozuru kijiji hicho.

Swali la kwanza ambalo Flavio alimwuliza ni, “Je, dini yako hufundisha kwamba watu huteswa katika moto wa mateso?” Tito alijibu kwamba wazo hilo humchukiza Muumba na pia huleta suto kwa jina la Yehova, Mungu mwenye upendo. Akitumia Biblia ya Flavio, Tito alimwonyesha kwamba wafu hawajui neno lolote na kwamba wanangoja kufufuliwa hapa duniani chini ya Ufalme wa Mungu. (Mhubiri 9:5; Yohana 5:28, 29) Flavio alijifunza mambo mapya kupitia habari hiyo. Alikubali funzo la Biblia mara moja na punde si punde akabatizwa na kuwa Mkristo.

Wanakijiji Wenye Shukrani

Hebu wazia jinsi inavyosisimua kuhubiria wanakijiji ambao hawajawahi kuiona Biblia, au kuhubiri katika vijiji ambapo watu hawajawahi kusikia juu ya Mashahidi wa Yehova, wala kusikia habari njema wanazohubiri! Dada watatu mapainia, Rosa, Alicia, na Cecilia, walifurahi kuhubiri huko. Walihubiri katika vijiji vya Izcuchaca na Conayca, vilivyo katika nyanda za juu zenye kimo cha meta zaidi ya 3,600 katikati mwa Peru.

Walipofika kwenye kijiji cha kwanza, hawakuwa na mahali pa kulala. Walizungumza na kamanda wa polisi na kumweleza kusudi la ziara yao. Matokeo yakawaje? Alikubali walale kwenye kituo cha polisi usiku huo. Siku iliyofuata, mapainia hao walipata nyumba na wakawa wanafanya shughuli zao kutoka huko.

Punde si punde, wakati ulifika wa kuadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Kristo unaofanywa kila mwaka. Mapainia walikuwa wamezuru nyumba zote katika kijiji cha Izcuchaca, wakawaachia watu wengi Biblia, na kuanzisha mafunzo kadhaa ya Biblia. Kabla ya Ukumbusho, waliwaalika watu kwenye sherehe hiyo, wakieleza kusudi la mwadhimisho huo na maana ya mifano inayotumiwa wakati wa mwadhimisho. Ndugu kadhaa walialikwa kusaidia kwenye sherehe hiyo, na mmoja wao akatoa hotuba. Ilikuwa shangwe iliyoje kuona watu 50 kutoka kijiji hicho kidogo kwenye sherehe hiyo ya pekee! Kwa mara ya kwanza, walielewa maana hasa ya Mlo wa Jioni wa Bwana. Pia, walithamini kama nini kushika Biblia mikononi mwao!

Kuondolewa Mizigo Mizito

Kupelekea wafungwa wa dini zisizo za kweli maji ya kweli ya Biblia yenye kuburudisha, huleta shangwe sikuzote. Pisac ilikuwa ngome ya Milki ya kale ya Inca. Watu wengi wanaoishi huko leo wamefundishwa fundisho lisilopatana na Maandiko la moto wa mateso. Makasisi wao huwaambia kwamba wanaweza kwenda mbinguni tu kwa kuombewa na makasisi.

Yaeleweka ni kwa nini watu hao wana kiu ya maji yenye kuburudisha ya kweli ya Biblia. Alipokuwa akihubiri nyumba kwa nyumba, Santiago, ambaye ni mhudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova, alipata nafasi ya kumweleza mwanamume fulani kwamba waadilifu wataishi katika paradiso duniani. (Zaburi 37:11) Akitumia Biblia, Santiago alimwonyesha kwamba wafu watafufuliwa na kwamba wanadamu watafundishwa njia kamilifu za Yehova na kuwa na taraja la uhai udumuo milele. (Isaya 11:9) Kufikia wakati huo, mwanamume huyo alikuwa Mkatoliki thabiti, alikuwa amejihusisha na uwasiliani-roho, na alikuwa akilewa sana. Sasa alipata tumaini linalotegemea Biblia na akawa na mradi fulani maishani—kuishi katika Paradiso. Alichoma vitu vyake vyote vya uwasiliani-roho na akaacha ulevi. Alikusanya familia yake na akakubali funzo la Biblia. Baada ya muda, wote katika familia hiyo walijiweka wakfu kwa Yehova Mungu na kubatizwa.

Ukarimu Wapokelewa

Watu wanaoishi milimani ni wakarimu sana. Ijapokuwa wana nyumba za kiasi na ni maskini, watu hao huwapa wageni kile walicho nacho. Kabla ya kujifunza viwango vya juu vya Biblia, huenda mwenye nyumba akampa mgeni majani ya coca aendelee kutafuna wanapozungumza. Lakini anapokuwa Shahidi, huenda akampa kijiko kimoja cha sukari, ambacho bei yake ni sawa na majani ya coca katika mikoa ya mbali.

Mishonari mmoja aliombwa na ndugu fulani ampeleke kwenye ziara ya kurudia. Baada ya safari ngumu ya kupanda mlima, walipiga makofi ili kumjulisha mwenye nyumba kwamba wamewasili. Walikaribishwa ndani ya nyumba yenye paa la nyasi, ambapo walilazimika kuinama ili kuweza kupita kwenye mlango huo mdogo. Walitembea kwa uangalifu karibu na sehemu ya katikati ya sakafu ya udongo, ambapo mama alikuwa amechimba shimo, akaingiza blanketi na kumweka mtoto wake. Mtoto huyo ambaye hangeweza kujitoa mahali hapo, aliridhika na kupiga kelele kwa furaha huku watu wazima wakizungumza. Baada ya mazungumzo yao yenye kuchangamsha kuhusu baraka za Ufalme, mwanamke huyo alileta pombe ya kienyeji ndani ya mtungi mkubwa. Punde si punde ndugu hao wakateremka mlima huo ili kufanya ziara nyingine za kurudia.

Mavuno Mengi

Sasa katika eneo hili, kuna vikundi vilivyotawanyika vipatavyo mia moja vyenye watu zaidi ya elfu moja wanaojifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Wahitimu wa Shule ya Mazoezi ya Kihuduma nchini Lima hutumwa wakasaidie vikundi hivyo viwe makutaniko. Watu wanaopenda uadilifu ambao wamekuwa wafungwa wa dini zisizo za kweli na ushirikina kwa muda mrefu wamepata uhuru kupitia habari njema za Ufalme! (Yohana 8:32) Kiu yao ya kupata maji ya kweli inatoshelezwa.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kuhubiri kwenye visiwa “vinavyoelea” vya Ziwa Titicaca