Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Miti ya kubeba sanduku la agano iliwekwaje, kwa kuwa andiko la 1 Wafalme 8:8 laonyesha kwamba ilionekana kutoka Mahali Patakatifu?

Yehova alipompa Musa muundo wa tabenakulo huko nyikani, sehemu kuu ilikuwa sanduku la agano. Sanduku hilo lenye umbo la mstatili na lililofunikwa kwa dhahabu lilikuwa na mabamba ya Sheria na vitu vingine. Liliwekwa katika chumba cha ndani zaidi, Patakatifu Zaidi Sana. Kwenye kifuniko cha Sanduku la Agano kulikuweko maumbo mawili ya makerubi waliotengenezwa kwa dhahabu wakiwa wamenyosha mbawa. Sanduku la Agano lilikuwa na vikuku viwili kila upande ili liweze kubebwa kwa miti miwili ya mshita iliyofunikwa kwa dhahabu. Ni wazi kwamba miti hiyo iliwekwa kwenye vikuku, ikiwa sambamba na Sanduku la Agano. Kwa hiyo, Sanduku la Agano lilipokuwa katika Patakatifu Zaidi Sana kwenye tabenakulo, sehemu iliyoelekeana na upande wa mashariki, miti hiyo iliegemezwa kuelekea upande wa kaskazini-kusini. Baadaye, Solomoni alipojenga hekalu, Sanduku la Agano liliwekwa katika sehemu hiyohiyo. *Kutoka 25:10-22; 37:4-9; 40:17-21.

Patakatifu Zaidi Sana na Mahali Patakatifu (chumba cha nje) palitenganishwa na pazia. Makuhani wakiwa Mahali Patakatifu hawangeweza kuchungulia Mahali Patakatifu Zaidi Sana na kuona Sanduku la Agano, lililomwakilisha Mungu. (Waebrania 9:1-7) Kwa hiyo, huenda andiko la 1 Wafalme 8:8 likashangaza: “Ile miti kwa kuwa mirefu, ncha za miti zilionekana katika mahali patakatifu, mbele ya chumba cha ndani; lakini hazikuonekana nje.” Jambo hilohilo linatajwa katika andiko la 2 Mambo ya Nyakati 5:9. Mtu angeonaje miti hiyo akiwa Mahali Patakatifu pa hekalu?

Watu wengine wanawazia kwamba miti hiyo iligusa pazia, na hivyo kuibenua. Lakini jambo hilo halingewezekana ikiwa miti hiyo ilielekeana na upande wa kaskazini-kusini, huku pazia ikiwa sambamba na miti hiyo. (Hesabu 3:38) Kuna ufafanuzi unaoeleweka zaidi. Miti hiyo ingeweza kuonekana ikiwa kulikuwa na mwanya mdogo kati ya pazia na ukuta wa hekalu au wakati kuhani wa cheo cha juu alipoingia Patakatifu Zaidi Sana. Pazia ilizuia Sanduku la Agano lisionekane, lakini miti iliyochomoza kila upande ingeweza kuonekana kupitia mwanya huo. Ingawa ufafanuzi huu unaeleweka, hatuwezi kuushikilia bila msingi.

Bila shaka, kuna mambo mengi ambayo huenda tukajifunza baadaye. Mtume Paulo alitaja mambo machache katika barua yake kwa Waebrania. Kisha akasema: “Sasa sio wakati wa kusema kirefu kuhusu vitu hivi.” (Waebrania 9:5) Wakati waaminifu watakapofufuliwa, tutakuwa na fursa ya kujifunza kutoka kwa watu kama vile Musa, Aroni, Bezaleli na wengineo waliofahamu kwa undani kazi zilizofanywa ndani ya tabenakulo.—Kutoka 36:1.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Miti hiyo haikupaswa kutolewa kwenye vikuku hivyo hata wakati Sanduku la Agano lilipokuwa ndani ya tabenakulo. Kwa sababu hiyo, miti hiyo haingeweza kutumiwa kwa kusudi lingine lolote. Pia Sanduku la Agano halikupaswa kuguswa; ikiwa miti hiyo ingetolewa kwenye vikuku, kila mara liliposafirishwa, basi ingebidi wenye kulisafirisha waguse Sanduku la Agano ili kuingiza tena miti hiyo kwenye vikuku. Taarifa inayopatikana katika andiko la Hesabu 4:6 kuhusu “kuitia ile miti” huenda inarejezea kupanga au kurekebisha ile miti wakati wa kujitayarisha kubeba sanduku hilo zito kwenda kituo kingine.