Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Nani Atakayetutenganisha na Upendo wa Mungu?

Ni Nani Atakayetutenganisha na Upendo wa Mungu?

Ni Nani Atakayetutenganisha na Upendo wa Mungu?

“Kwa habari yetu, twapenda, kwa sababu yeye alitupenda sisi kwanza.”—1 YOHANA 4:19.

1, 2. (a) Kwa nini ni muhimu kwetu kujua kwamba tunapendwa? (b) Tunahitaji upendo wa nani hasa?

KWA nini ni muhimu kujua kwamba unapendwa? Maisha ya wanadamu huwa bora wanapoonyeshwa upendo tangu utotoni hadi utu uzima. Je, umemtazama mtoto anaposhikwa kwa upendo na mamake? Hata iwe kunatendeka nini karibu naye, mara nyingi mtoto hustarehe na kutulia mikononi mwa mama yake mwenye upendo, atazamapo uso wake wenye tabasamu. Au je, unakumbuka jinsi ulivyokuwa wakati wa miaka yenye misukosuko ya utineja? (1 Wathesalonike 2:7) Nyakati nyingine, labda hata hukujua ulichotaka au hata jinsi ulivyohisi. Hata hivyo, lilikuwa jambo muhimu kama nini kujua kwamba baba na mama yako walikupenda! Je, haikufariji kujua kwamba ungeweza kuwaeleza tatizo lolote au kuwauliza swali lolote lile? Naam, uhitaji wetu mkubwa maishani ni kuhisi kwamba tunapendwa. Upendo huo huthibitisha kwamba tu wenye thamani.

2 Bila shaka upendo wenye kudumu wa wazazi humsaidia sana mtoto akue kwa njia ifaayo na kuwa na usawaziko. Hata hivyo, ili tuwe na hali nzuri kiroho na kihisia-moyo, ni jambo muhimu sana kuwa na hakika kwamba Yehova, Baba yetu wa mbinguni, anatupenda. Huenda baadhi ya wasomaji wa gazeti hili walilelewa na wazazi ambao hawakuwajali kikweli. Ikiwa wazazi wako walikuwa hivyo, usivunjike moyo. Hata ikiwa hawakukupenda, upendo wa Mungu kwako ni mshikamanifu.

3. Yehova amewapa watu wake uhakikisho gani kwamba anawapenda?

3 Kupitia nabii wake Isaya, Yehova alisema kwamba mama anaweza “kusahau” mtoto wake anyonyaye, lakini Yehova hawezi kuwasahau watu wake. (Isaya 49:15) Vivyo hivyo, Daudi alisema hivi kwa uhakika: “Baba yangu na mama yangu wameniacha, bali BWANA atanikaribisha kwake.” (Zaburi 27:10) Ni uhakikisho ulioje! Hata hali zako ziweje, ikiwa una uhusiano pamoja na Yehova kupitia wakfu wako kwake, sikuzote unapaswa kukumbuka kwamba upendo wa Yehova kwako ni mkubwa sana kuliko wa mwanadamu yeyote!

Jitunze Mwenyewe Katika Upendo wa Mungu

4. Wakristo wa karne ya kwanza walipewa uhakikisho gani kwamba Mungu anawapenda?

4 Ulipata kujua upendo wa Yehova lini kwa mara ya kwanza? Yaelekea kwa njia fulani hali yako ilikuwa kama ya Wakristo wa karne ya kwanza. Sura ya 5 ya barua ya Paulo kwa Waroma yaeleza vizuri jinsi watenda-dhambi, ambao wakati mmoja walikuwa wametengwa na Mungu, walivyopata kujua upendo wa Yehova. Twasoma hivi kwenye mstari wa 5: “Upendo wa Mungu umemwagwa ndani ya mioyo yetu kupitia roho takatifu, tuliyopewa.” Kwenye mstari wa 8, Paulo aongeza kusema: “Mungu apendekeza upendo wake mwenyewe kwetu kwa kuwa, tulipokuwa tungali watenda-dhambi, Kristo alikufa kwa ajili yetu.”

5. Ulipata kufahamu ukuu wa upendo wa Mungu jinsi gani?

5 Hali kadhalika, roho takatifu ya Yehova ilianza kufanya kazi ndani ya moyo wako ulipofundishwa kweli ya Neno la Mungu na kuanza kuwa na imani. Kwa njia hiyo ulianza kufahamu tendo kuu la Yehova la kumtuma Mwana wake mpendwa afe kwa ajili yako. Hivyo, Yehova alikusaidia kujua jinsi anavyowapenda wanadamu. Je, hukuguswa moyo ulipotambua kwamba ingawa ulizaliwa ukiwa mtenda-dhambi aliyetengwa na Yehova, yeye alifanya iwezekane kwa wanadamu kutangazwa kuwa waadilifu na kuwa na matazamio ya kupata uhai wa milele? Je, hukuhisi kwamba unampenda Yehova?—Waroma 5:10.

6. Kwa nini nyakati nyingine tunaweza kuhisi kana kwamba hatuna uhusiano wa karibu na Yehova?

6 Baada ya kuvutwa na upendo wa Baba yako wa mbinguni na kurekebisha maisha yako ili ukubalike kwake, ulijiweka wakfu kwa Mungu. Sasa una amani pamoja na Mungu. Lakini je, nyakati nyingine wewe huhisi kana kwamba huna uhusiano wa karibu na Yehova? Yeyote kati yetu anaweza kuhisi hivyo. Lakini sikuzote kumbuka kwamba Mungu habadiliki. Upendo wake ni thabiti kama jua, ambalo daima huangaza dunia kwa miali yake yenye joto. (Malaki 3:6; Yakobo 1:17) Kwa upande mwingine, sisi tunaweza kubadilika—hata ikiwa ni kwa muda. Dunia izungukapo, nusu yake hufunikwa kwa giza. Vivyo hivyo, tukimwacha Mungu, hata ikiwa ni kwa muda, uhusiano wetu naye unaweza kuanza kupoa. Tunaweza kufanya nini ili kurekebisha hali hiyo?

7. Kujichunguza wenyewe kunaweza kutusaidia jinsi gani kudumu katika upendo wa Mungu?

7 Tukihisi kwamba tumetengwa na upendo wa Mungu kwa kiasi fulani, tunapaswa kujiuliza: ‘Je, nimepuuza upendo wa Mungu? Je, nimejitenga kwa njia fulani na Mungu aliye hai na mwenye upendo, nikionyesha kwa njia mbalimbali imani inayodhoofika? Je, nimekazia fikira “mambo ya mwili,” badala ya “mambo ya roho”?’ (Waroma 8:5-8; Waebrania 3:12) Ikiwa tumejitenga na Yehova, tunaweza kuchukua hatua za kurekebisha hali hiyo ili kurudia uhusiano wa karibu na mchangamfu pamoja naye. Yakobo anatusihi: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia.” (Yakobo 4:8) Fikiria maneno haya ya Yuda: “Wapendwa, kwa kujijenga wenyewe juu ya imani yenu takatifu zaidi sana, na kusali mkiwa na roho takatifu, jitunzeni wenyewe katika upendo wa Mungu.”—Yuda 20, 21.

Hali Zilizobadilika Haziathiri Upendo wa Mungu

8. Ni mabadiliko gani yanayoweza kutokea kwa ghafula maishani mwetu?

8 Maisha yetu katika mfumo huu wa mambo yanaweza kubadilika kwa njia nyingi. Mfalme Solomoni aliona kwamba ‘wakati na tukio lisilotazamiwa hutupata sote.’ (Mhubiri 9:11, NW) Maisha yetu yanaweza kubadilika kabisa kwa ghafula. Siku moja tunaweza kuwa wenye afya nzuri na siku inayofuata tuwe wagonjwa sana. Siku moja kazi yetu ya kimwili inaonekana kuwa yenye kutegemeka, siku inayofuata hatuna kazi. Mtu tunayempenda anaweza kufa kwa ghafula. Wakristo katika nchi fulani wanaweza kufurahia amani kwa muda fulani, kisha mnyanyaso utokee kwa ghafula. Labda tumeshtakiwa isivyo kweli na kwa sababu hiyo, tunatendewa isivyo haki. Naam, maisha si hakika wala si salama kabisa.—Yakobo 4:13-15.

9. Kwa nini ingefaa kuchunguza sehemu fulani ya kitabu cha Waroma sura ya 8?

9 Tunapopatwa na mambo yenye kuhuzunisha, tunaweza kuanza kuhisi kwamba tumeachwa, hata kuwaza kwamba upendo wa Mungu kwetu umepungua. Kwa kuwa sote tunapatwa na mambo hayo, inatupasa kufikiria kwa makini maneno yenye kufariji sana ambayo mtume Paulo aliwaandikia Wakristo watiwa-mafuta katika Waroma sura ya 8. Kanuni inayopatikana katika maneno hayo inatumika pia kwa kondoo wengine ambao, kama Abrahamu aliyeishi kabla ya Ukristo, wametangazwa kuwa waadilifu wakiwa rafiki za Mungu.—Waroma 4:20-22; Yakobo 2:21-23.

10, 11. (a) Nyakati nyingine maadui hufanya mashtaka gani dhidi ya watu wa Mungu? (b) Kwa nini mashtaka hayo hayawababaishi Wakristo?

10 Soma Waroma 8:31-34. Paulo anauliza: “Ikiwa Mungu yuko upande wetu, nani atakayekuwa dhidi yetu?” Ni kweli kwamba Shetani na ulimwengu wake mwovu uko dhidi yetu. Huenda maadui wakatushtaki isivyo kweli, hata katika mahakama za nchi. Wazazi fulani Wakristo wameshutumiwa kuwa wanawachukia watoto wao kwa sababu wamekataa wasipewe matibabu yanayovunja sheria ya Mungu na hawawaruhusu washiriki katika sherehe za kipagani. (Matendo 15:28, 29; 2 Wakorintho 6:14-16) Wakristo wengine waaminifu wameshtakiwa isivyo kweli kwamba wao ni wachochezi kwa sababu wamekataa kuua wanadamu wenzao vitani au kushiriki katika siasa. (Yohana 17:16) Wapinzani wengine wameeneza uwongo mbaya kwenye vyombo vya habari, hata wakiwashtaki Mashahidi wa Yehova isivyo kweli kwamba wao ni madhehebu hatari.

11 Lakini usisahau kwamba katika siku za mitume, ilisemwa hivi: “Kwa habari ya farakano hili yajulikana kwetu kwamba kila mahali huwa lasemwa vibaya.” (Matendo 28:22) Mashtaka hayo yasiyo ya kweli hayatubabaishi kwa kuwa Mungu ndiye hutangaza Wakristo wa kweli kuwa waadilifu, ikitegemea imani yao katika dhabihu ya Kristo. Yehova anawezaje kuacha kuwapenda waabudu wake baada ya kuwapa zawadi yenye thamani kubwa zaidi—Mwana wake mpendwa? (1 Yohana 4:10) Sasa kwa vile Kristo amefufuliwa kutoka kwa wafu na amewekwa kwenye mkono wa kuume wa Mungu, yeye huwatetea Wakristo kwa bidii. Ni nani anayeweza kwa kweli kumpinga Kristo asiwatetee wafuasi wake au kufanikiwa kupinga maoni ya Mungu yafaayo kuelekea waaminifu wake? Hakuna hata mmoja!—Isaya 50:8, 9; Waebrania 4:15, 16.

12, 13. (a) Ni hali zipi zisizoweza kututenganisha na upendo wa Mungu? (b) Shetani hutusababishia magumu akiwa na kusudi gani? (c) Kwa nini Wakristo hupata ushindi kamili?

12 Soma Waroma 8:35-37. Ni sisi wenyewe tu tunaoweza kujitenga na upendo wa Yehova na Mwana wake Kristo Yesu. Shetani anaweza kutumia wawakilishi wake duniani kuwataabisha Wakristo. Katika karne iliyopita, wengi wa ndugu na dada zetu Wakristo walinyanyaswa vikali katika nchi nyingi. Katika sehemu fulani leo, ndugu zetu hukabili hali ngumu ya kiuchumi kila siku. Baadhi yao hawana chakula wala mavazi ya kutosha. Ibilisi husababisha hali hizo ngumu kwa kusudi gani? Angalau mojawapo ya makusudi yake ni kuwavunja moyo waache ibada ya kweli ya Yehova. Shetani anataka tuamini kwamba Mungu hatupendi. Lakini, je, hivyo ndivyo ilivyo?

13 Kama Paulo, aliyenukuu Zaburi 44:22, tumejifunza Neno la Mungu lililoandikwa. Tunajua ni kwa ajili ya jina la Mungu kwamba mambo haya yanatupata sisi “kondoo” wake. Kutakaswa kwa jina la Mungu na kutetewa kwa enzi yake kuu ya ulimwengu wote kunahusika. Mungu huruhusu majaribu kwa sababu ya masuala hayo muhimu wala si kwa sababu yeye hatupendi. Hata hali hiyo ngumu iwe nini, tunahakikishiwa kwamba upendo wa Mungu kwa watu wake, kutia ndani kila mmoja wetu, haubadiliki. Tukidumisha uaminifu-maadili tutashinda hali yoyote ionekanayo kuwa ngumu. Tunaimarishwa na kutegemezwa na uhakikisho wa kwamba upendo wa Mungu ni thabiti.

14. Kwa nini Paulo alikuwa na hakika kwamba Mungu anawapenda Wakristo licha ya magumu ambayo huenda yakawapata?

14 Soma Waroma 8:38, 39. Ni nini kilichomhakikishia Paulo kwamba hakuna chochote kiwezacho kutenganisha Wakristo na upendo wa Mungu? Yaelekea mambo yaliyompata Paulo akiwa kwenye huduma yaliimarisha uhakika wake kwamba magumu hayawezi kuathiri upendo wa Mungu kwetu. (2 Wakorintho 11:23-27; Wafilipi 4:13) Pia, Paulo alijua kusudi la milele la Yehova na jinsi alivyoshughulika na watu Wake zamani. Je, kifo kinaweza kushinda upendo wa Mungu kwa wale ambao wamemtumikia kwa uaminifu-mshikamanifu? La, hasha! Waaminifu hao wanaokufa wataendelea kuishi katika kumbukumbu kamilifu ya Mungu, naye atawafufua katika wakati ufaao.—Luka 20:37, 38; 1 Wakorintho 15:22-26.

15, 16. Simulia baadhi ya mambo yasiyoweza kamwe kumfanya Mungu aache kuwapenda watumishi wake waaminifu.

15 Hata tukipatwa na hali gani mbaya maishani leo—iwe ni aksidenti yenye kulemaza, ugonjwa wenye kufisha, au janga la kiuchumi—hakuna kitu kiwezacho kufanya Mungu aache kupenda watu wake. Malaika wenye nguvu, kama vile yule malaika asiyetii aliyegeuka kuwa Shetani, hawawezi kumfanya Yehova aache kuwapenda watumishi wake wenye kujitoa. (Ayubu 2:3) Serikali zinaweza kuwapiga marufuku, kuwatia gerezani, na kuwatendea vibaya watumishi wa Mungu na hata kuwaita “watu wasiotakikana.” (1 Wakorintho 4:13) Chuki hiyo ya mataifa isiyo na msingi inaweza kusukuma wanadamu watupinge, lakini haiwezi kumfanya Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote atuache.

16 Tukiwa Wakristo, hatuna haja ya kuogopa kwamba yoyote kati ya yale ambayo Paulo aliyaita “mambo yaliyo hapa sasa,” yaani, matukio na hali za mfumo huu wa mambo wala “mambo yatakayokuja” baadaye, yanaweza kuvunja upendo wa Mungu kwa watu wake. Japo wenye mamlaka mbinguni na duniani hupigana nasi, upendo mwaminifu-mshikamanifu wa Mungu unatutegemeza. Paulo alikazia kwamba upendo wa Mungu hauwezi kuzuiwa na “kimo wala kina.” Naam, hakuna kitu chochote kinachoonekana kuwa chenye kuvunja moyo au chenye nguvu kutushinda, ambacho kinaweza kututenganisha na upendo wa Mungu; wala hakuna uumbaji mwingine wowote uwezao kuharibu uhusiano wa Muumba pamoja na watumishi wake waaminifu. Upendo wa Mungu haushindwi kamwe; ni wa milele.—1 Wakorintho 13:8.

Thamini Fadhili-Upendo za Mungu Milele

17. (a) Kwa nini kupendwa na Mungu ni ‘jambo jema kuliko uhai’? (b) Tunaonyesha kwa njia gani kwamba tunathamini fadhili-upendo za Mungu?

17 Kupendwa na Mungu ni jambo muhimu kadiri gani kwako? Je, unahisi kama Daudi aliyeandika hivi: “Maana fadhili [“fadhili-upendo,” NW] zako ni njema kuliko uhai; midomo yangu itakusifu. Ndivyo nitakavyokubariki maadamu ni hai; kwa jina lako nitaiinua mikono yangu.” (Zaburi 63:3, 4) Je, kweli tunaweza kupata chochote katika ulimwengu huu ambacho ni bora kuliko kufurahia upendo wa Mungu na urafiki wake mwaminifu-mshikamanifu? Kwa mfano, je, kufuatia kazi ya kimwili yenye mapato makubwa ni bora kuliko kuwa na amani ya akili na furaha itokanayo na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu? (Luka 12:15) Wakristo fulani wamelazimika kuchagua kati ya kumkana Yehova na kifo. Wengi wa Mashahidi wa Yehova katika kambi za mateso za Nazi walilazimika kufanya uchaguzi huo wakati wa Vita ya Pili ya Ulimwengu. Ndugu zetu Wakristo walichagua kudumu katika upendo wa Mungu, wakiwa tayari kufa ikiwa lazima. Ni wachache tu waliomkana Yehova. Wale wanaodumu katika upendo wa Mungu wanaweza kuwa na hakika kwamba Mungu atawapa uhai udumuo milele, kitu ambacho ulimwengu hauwezi kuwapa. (Marko 8:34-36) Lakini mengi zaidi yanahusika kuliko tu uhai udumuo milele.

18. Kwa nini uhai udumuo milele unavutia sana?

18 Japo haiwezekani kuishi milele bila Yehova, hebu wazia jinsi maisha marefu sana bila Muumba yawezavyo kuwa. Yangekuwa bila maana, bila kusudi la kweli. Yehova amewapa watu wake kazi yenye kuridhisha siku hizi za mwisho. Hivyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba tutakapopata uhai udumuo milele kutoka kwa Yehova, Mkusudiaji Mkuu, tutajifunza na kufanya mambo mengi yafaayo na yenye kusisimua. (Mhubiri 3:11) Hata tujifunze mambo mengi kadiri gani katika milenia zitakazofuata, hatutaweza kamwe kufahamu kabisa “kina cha utajiri wa Mungu na hekima na ujuzi.”—Waroma 11:33.

Baba Ana Shauku na Nyinyi

19. Yesu Kristo aliwapa wanafunzi wake uhakikisho gani alipowaaga?

19 Wakati wa jioni yake ya mwisho pamoja na mitume wake waaminifu 11, katika Nisani 14, 33 W.K., Yesu alisema mambo mengi ya kuwaimarisha kuhusiana na mambo ambayo yangewapata baadaye. Wote walishikamana naye wakati wa majaribu yake nao walijua kwamba aliwapenda. (Luka 22:28, 30; Yohana 1:16; 13:1) Kisha Yesu akawahakikishia hivi: “Baba mwenyewe ana shauku na nyinyi.” (Yohana 16:27) Bila shaka maneno hayo yaliwasaidia wanafunzi kutambua kwamba Baba yao wa mbinguni aliwapenda.

20. Umeazimia kufanya nini, na unaweza kuwa na hakika katika jambo gani?

20 Wengi walio hai sasa wamemtumikia Yehova kwa uaminifu kwa miaka mingi. Yaelekea tutakabili majaribu mengi zaidi kabla ya mfumo huu mwovu wa mambo kukoma. Usiache majaribu au magumu yafanye utilie shaka upendo mwaminifu-mshikamanifu wa Mungu kwako. Jambo hili ni hakika kabisa: Yehova ana shauku nawe. (Yakobo 5:11) Sote na tuendelee kufanya yale yatupasayo, na kushika amri za Mungu kwa uaminifu-mshikamanifu. (Yohana 15:8-10) Na tutumie kila fursa kulisifu jina lake. Twapaswa kuimarisha azimio letu la kuendelea kuwa na ukaribu na Yehova kupitia sala na kujifunza Neno lake. Hata hali iweje baadaye, iwapo tunafanya yote tuwezayo kumpendeza Yehova, tutakuwa na amani, tukiwa na hakika kamili kwamba hataacha kutupenda.—2 Petro 3:14.

Ungejibuje?

• Tunahitaji hasa upendo wa nani ili tudumishe usawaziko kiroho na kihisia-moyo?

• Ni mambo gani yasiyoweza kamwe kumfanya Yehova aache kuwapenda watumishi wake?

• Kwa nini kupendwa na Yehova ni ‘jambo jema kuliko uhai’?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 13]

Tukihisi kwamba tumetengwa na upendo wa Mungu tunaweza kujitahidi kurekebisha hali hiyo

[Picha katika ukurasa wa 15]

Paulo alijua ni kwa nini alinyanyaswa