Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tunafanya Yote Tuwezayo!

Tunafanya Yote Tuwezayo!

Tunafanya Yote Tuwezayo!

“FANYA yote uwezayo.” Shauri hilo linalofaa lilitolewa na mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova kwa mishonari mmoja wakati fulani. Lakini kwa nini mhudumu mwenye uzoefu apewe shauri hilo la msingi? Je, mishonari wengi si watu wajasiri ambao hukabiliana kila siku na kunguni, nyoka, joto, magonjwa, na magumu mengineyo?

Kwa kweli, mishonari wa Mashahidi wa Yehova ni wanaume na wanawake wa kawaida tu, ni Wakristo ambao kwa sababu wanampenda sana Yehova na wanadamu wenzao, wanachochewa kutumikia katika nchi za kigeni. Wanajitahidi kumtumikia Yehova kwa uwezo wao wote, wakimtegemea ili awaimarishe.—Waefeso 6:10.

Ili kujifunza mengi kuhusu kazi ya mishonari, na tuwazie kwamba tumeenda kutembea katika makao ya mishonari huko Afrika Magharibi.

Jinsi Mishonari Wanavyotumia Wakati Wao

Ni karibu saa 1:00 asubuhi. Tumefika katika makao ya mishonari mapema ili kuhudhuria mazungumzo ya Andiko la kila siku. Mishonari kumi wanatukaribisha kwa furaha na kutupatia mahali pa kuketi mezani. Tunapoendelea kufahamiana, mmoja wao ambaye amekuwa katika utumishi wa mishonari kwa miaka mingi, aanza kusimulia jambo lenye kuchekesha aliloona katika huduma. Lakini mazungumzo yetu yanakatizwa wakati ndugu anayeongoza mazungumzo siku hiyo anapokumbusha mishonari hao wenye furaha kwamba wakati umefika wa kuchunguza andiko la siku. Mazungumzo yatafanywa kwa Kifaransa. Ijapokuwa hatuzungumzi lugha hiyo, ni wazi kwamba mishonari hao waliozaliwa katika nchi za kigeni wamejitahidi sana kujua lugha hiyo.

Baada ya mazungumzo ya Kimaandiko, sala ya kutoka moyoni inatolewa, kisha tunapata kifungua-kinywa. Tunapopakua chakula cha nafaka, mishonari aliyeketi kando yetu atuhimiza tukatekate ndizi na kutia ndani ya chakula hicho. Tunamweleza kwamba hatupendi ndizi, lakini anatuhakikishia kwamba tutabadili maoni yetu tukionja ndizi zinazokuzwa katika nchi hiyo. Kwa hiyo tunaongezea vipande vichache vya ndizi katika chakula hicho. Amesema kweli kabisa! Ndizi hizo ni tamu kama aiskrimu! Na tunahakikishiwa kwamba mkate tulioandaliwa uliokwa asubuhi hiyohiyo katika sehemu ya kuokea mikate iliyo ng’ambo ya barabara kutoka makao ya mishonari.

Baada ya kifungua-kinywa, tutashinda pamoja na mishonari ambao ni wenzi wa ndoa, tutakaowapa majina Ben na Karen. Tumesikia kuhusu nchi hii yenye matokeo ya Afrika Magharibi, na tuna hamu ya kuthibitisha habari hizo.

Tunapowasili kwenye kituo cha basi, tunapata watu kadhaa wakisubiri. Muda si muda, mishonari tulioandamana nao wanaanza kuzungumza kwa uchangamfu na mama na mwana wake kuhusu habari fulani ya Biblia. Kwa kuwa hatujui Kifaransa, tunasimama tu na kutabasamu! Mwanamke huyo anapokubali magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, basi linakuja, kisha kila mtu anataka kuingia kwa wakati uleule! Tunapong’ang’ana kuingia, umati unatusukuma kutoka nyuma. Tunatupwa huku na huku tunapojaribu kusonga nyuma ya basi. Dereva anapowasha basi moto, tunajitayarisha kwa safari yenye msukosuko. Basi linasimama pindi kwa pindi, na kubeba watu zaidi. Abiria wote wanatabasamu. Jinsi tulivyotamani kuzungumza nao!

Basi letu linaposonga kwa kasi, tunachungulia dirishani na kuona shughuli nyingi zinazoendelea barabarani. Wanawake wawili wanatembea karibu karibu wakiwa wamebeba mizigo mizito vichwani. Mmoja wao anabeba mtungi mkubwa wa maji. Mwanamume mmoja mwenye ubunifu ametandika blanketi kando ya barabara na kupanga bidhaa za kujipamba zenye thamani ndogo ili kuziuza. Kila mahali kuna watu ambao wananunua au kuuza karibu kila kitu.

Kwa ghafula, Ben ambaye amesimama kando yangu, anahisi kitu fulani kikimdonoa mguuni. Ni kitu gani hicho? Basi limejaa watu kupita kiasi, lakini bado anadonolewa. Anafaulu kutazama chini. Ndani ya mfuko ulio karibu na miguu yake, kuna bata ambaye mara kwa mara anatoa kichwa chake nje na kumdonoa! Ben anasema kwamba labda mwenyewe anampeleka bata huyo sokoni akamwuze.

Tunapofika kwenye eneo letu, tunafurahi kujua kwamba tunazuru eneo ambalo wakazi wake ni Waafrika. Tunapokaribia nyumba ya kwanza, Ben anapiga makofi kwa nguvu ili kumwarifu mwenye nyumba kwamba tumefika. Katika nchi hii watu “hubisha mlango” kwa kupiga makofi. Mwanamume kijana atokea na kusema kwamba ana shughuli nyingi lakini anatuomba turudi baadaye asubuhi.

Kwenye nyumba inayofuata, twakutana na mwanamke ambaye haelewi lugha anayozungumza Ben. Anamwita mwana wake na kumwambia atafsiri mambo anayosema Ben. Ben anapomaliza kuzungumza, mwanamke huyo akubali broshua inayotegemea Biblia, naye mwana wake anaahidi kwamba atamwelezea mama yake yaliyomo kwenye broshua hiyo. Katika nyumba ya tatu, kuna vijana wengi ambao wameketi kwenye uga wa mbele. Wawili kati yao wanaondoka upesi kwenye viti vyao ili wageni waketi. Kisha kunakuwa na mazungumzo yenye kusisimua kuhusu kutumia msalaba katika ibada. Mipango inafanywa ili kuwe na mazungumzo zaidi juma litakalofuata. Sasa wakati umefika wa kumrudia yule mwanamume kijana aliyekuwa na shughuli nyingi ambaye tulimkuta katika nyumba ya kwanza. Kwa njia fulani, tayari amesikia mazungumzo tuliyokuwa nayo pamoja na vijana wa mtaa huo. Ana maswali mengi ya Biblia na anaomba afundishwe Biblia. Baada ya kuangalia kalenda yake, Ben anakubali kurudi wakati huohuo juma litakalofuata. Tunapokuwa njiani kurudi kwenye makao ya mishonari kwa chakula cha mchana, Ben na Karen wanasema kwamba wanahitaji kupanga mafunzo yao ya Biblia kwa makini kwa sababu wanaweza kuanzisha mafunzo mengi ya Biblia na kushindwa kuyaongoza.

Tunawapongeza kwa sababu ya kuzungumza Kifaransa kwa ufasaha. Ben na Karen wanasema kwamba wamekuwa wakitumikia wakiwa mishonari kwa miaka sita, na sasa wanaweza kuzungumza Kifaransa kwa ufasaha. Wanatuambia kwamba si rahisi kujifunza lugha geni, lakini wanatuhakikishia kwamba wamepata matokeo kwa sababu ya kuvumilia.

Ifikapo saa 6:30 mchana, mishonari wote wanakutana pamoja ili kula chakula cha mchana. Tunaelezwa kwamba kila siku mishonari fulani hupewa mgawo wa kutayarisha kifungua-kinywa na chakula cha mchana na kusafisha vyombo baadaye. Leo, mmojawapo wa mishonari amepika chakula kitamu sana, chipsi na kuku wa kukaangwa, pamoja na kachumbari ya nyanya—chakula anachojua kupika vizuri zaidi!

Ben na Karen wanapanga kufanya nini alasiri? Wanasema kwamba kila mtu hupumzika kwa sababu ya jua kali kati ya saa 7:00 na saa 9:00 alasiri, kwa hiyo kwa kawaida mishonari hutumia wakati huo kujifunza au kulala kidogo. Hatushangai Karen anapotuambia kwamba haiwachukui mishonari wapya muda mrefu kuzoea desturi hiyo!

Baada ya kulala kidogo, tunarudi katika huduma ya shambani. Mtu fulani ambaye Ben amejaribu kumtembelea kwa muda fulani, bado hapatikani nyumbani, lakini baada ya Ben kupiga makofi vijana wawili wanakuja mlangoni. Wanatuambia kwamba mwenye nyumba amewatajia kuhusu ziara za Ben na akapendekeza kwa dhati wachukue kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele. Tunafurahi kuwaachia kitabu hicho. Baada ya hapo, tunapanda basi litakalotupeleka hadi sehemu ambayo Karen ataongoza funzo la Biblia na mwanamke anayependezwa.

Tunapopita katikati ya barabara zenye watu wengi, Karen atueleza kwamba alikutana na mwanamke huyo siku moja walipokuwa wanasafiri kwa teksi na abiria wengine. Karen alimpa mwanamke huyo trakti asome wakati wa safari. Mwanamke huyo aliisoma trakti hiyo kisha akaomba apewe nyingine. Aliisoma hiyo nyingine pia na kuifurahia hata zaidi. Baada ya safari yao, Karen alifanya mipango ya kuzuru mwanamke huyo nyumbani kwake na akaanzisha funzo la Biblia lenye matokeo akitumia broshua Mungu Anataka Tufanye Nini? Leo, Karen atajifunza naye somo la tano katika broshua hiyo.

Tumefurahia sana utumishi wa shambani siku hii, lakini bado tuna maswali fulani kuhusu kazi ya mishonari. Wakaribishaji wetu wanatuhakikishia kwamba tutakaporudi nyumbani, watatutayarishia chakula chepesi na kujibu maswali yetu.

Jinsi Wanavyodumisha Ratiba Yao

Tunapoendelea kula mayai yaliyokaangwa, mkate, na jibini, tunajifunza mengi kuhusu maisha ya mishonari. Kwa kawaida mishonari hupumzika na kufanya mambo yao ya kibinafsi siku ya Jumatatu. Mishonari wengi hutumia wakati huo kuwaandikia barua watu wao wa familia na marafiki. Mishonari wanapenda sana kupokea habari kutoka nyumbani, nao hufurahia kuandika na kupokea barua.

Kwa kuwa mishonari huishi na kufanya kazi kwa ukaribu na wenzao, ni jambo la lazima wadumishe mawasiliano mazuri kwa kushirikiana na mishonari wenzao na kwa kuzungumzia mambo ya kiroho. Ili kutimiza lengo hilo, mbali na kuwa na ratiba ya kawaida ya kujifunza Biblia, kila Jumatatu jioni mishonari hujifunza Biblia wakitumia gazeti Mnara wa Mlinzi. Ben anasema kwamba mishonari wa malezi mbalimbali wanapoishi pamoja, kunatokea tofauti ndogo za maoni, lakini mpango wa kiroho wa kuwa na funzo la familia huwasaidia kudumisha amani na umoja. Pia akazia kwamba haifai kujiona kuwa bora kuliko wengine.

Ni muhimu pia kuwa mnyenyekevu. Mishonari hutumwa kutumikia, si kutumikiwa. Rafiki zetu wanasema kwamba mojawapo ya mambo magumu zaidi katika lugha yoyote ile ni kusema “naomba radhi,” hasa mtu anapoomba msamaha kwa jambo alilosema au kufanya pasipo kukusudia. Ben atukumbusha mfano mmoja katika Biblia wa Abigaili aliyerekebisha hali ambayo ingesababisha msiba kwa kuomba msamaha kwa niaba ya mume wake aliyetenda kikatili. (1 Samweli 25:23-28) Kuweza ‘kuishi kwa amani’ ni jambo muhimu ili kuwa mishonari mzuri.—2 Wakorintho 13:11.

Mishonari hukutana mara moja kwa mwezi ili kuzungumzia mambo yanayoathiri familia yao, na vilevile kufanya marekebisho ya ratiba ya kutunza makao ya mishonari. Baada ya hapo, wote hufurahia kitindamlo cha pekee. Tunaona mpango huo kuwa unafaa na wenye kupendeza.

Baada ya chakula cha jioni, tunazuru kifupi makao ya mishonari. Tunaona kwamba ingawa makao hayo si ya hali ya juu, mishonari hushirikiana ili kuyadumisha yakiwa safi kabisa. Kuna friji, mashine ya kufulia nguo, na jiko. Karen anatuambia kwamba katika nchi zenye joto, kama nchi hii ya Afrika Magharibi, unaweza kupata kifaa cha kufanya hewa iwe baridi. Nyumba zinazofaa, chakula kizuri, na kutunza afya husaidia mishonari wadumishe afya nzuri na kuwa wenye matokeo.

Fikiria Mambo Yanayofaa

Tumefurahia mambo yote tuliyoona. Je, tunaweza kuwa mishonari? Tutajuaje? Wakaribishaji wetu wanatuambia mambo machache ya kufikiria.

Kwanza, wanatuambia kwamba mishonari Wakristo hawatafuti kujifurahisha. Wanatafuta watu wenye mioyo minyoofu wanaotaka kujifunza ahadi nzuri za Mungu. Mishonari hutumia angalau muda wa saa 140 kwa mwezi katika utumishi wa shambani, kwa hiyo lazima mishonari apende huduma.

‘Lakini namna gani nyoka, mjusi, na kunguni?’ twauliza. Ingawa viumbe hawa hupatikana katika nchi nyingi wanakotumwa mishonari, Ben atuambia kwamba, mishonari huwazoea. Anaongeza kusema kwamba kila mgawo wa mishonari una uzuri wake, na baada ya muda, mishonari hukazia fikira mambo yanayofaa kuhusu mgawo wao. Hali ambazo hapo awali zingeonekana kuwa “tofauti” punde si punde huwa za kawaida, na nyakati nyingine hata zenye kufurahisha. Mishonari mmoja aliyetumika Afrika Magharibi kwa miaka mingi kabla ya kulazimika kurudi nyumbani kwa sababu ya madaraka ya kibinafsi alisema kwamba ilikuwa vigumu zaidi kuacha mgawo wake kuliko ilivyokuwa kuacha nchi ya kwao miaka mingi iliyopita. Alikuwa amezoea kabisa mgawo wake wa mishonari.

Je, Uko Tayari?

Ben na Karen wamefanya tufikirie mambo mengi. Namna gani wewe? Je, umewahi kufikiria kutumikia ukiwa mishonari katika nchi ya kigeni? Ikiwa ndivyo, huenda ukafikia mradi huo kwa urahisi kuliko ulivyofikiri. Mojawapo ya mambo ya msingi yanayohitajiwa ni kupenda huduma ya wakati wote na kufurahia kuwasaidia watu. Kumbuka kwamba mishonari ni wanaume na wanawake wa kawaida tu. Wanafanya yote wawezayo ili kutimiza kazi muhimu sana.

[Picha katika ukurasa wa 27]

Kila siku huanza kwa kuzungumzia andiko la Biblia

[Picha katika ukurasa wa 28, 29]

Picha mbalimbali kutoka Afrika

[Picha katika ukurasa wa 29]

Maisha ya mishonari yanaweza kuwa yenye kuridhisha sana