Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Jivikeni Wenyewe Ustahimilivu’

‘Jivikeni Wenyewe Ustahimilivu’

‘Jivikeni Wenyewe Ustahimilivu’

“Jivikeni wenyewe shauku nyororo za huruma . . . na ustahimilivu.” —WAKOLOSAI 3:12.

1. Simulia mfano mzuri wa ustahimilivu.

RÉGIS, anayeishi kusini-magharibi mwa Ufaransa alibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova mwaka wa 1952. Kwa miaka mingi, mke wake alifanya yote awezayo ili kumzuia asimtumikie Yehova. Alijaribu kutoboa magurudumu ya gari lake ili kumzuia asiende mikutanoni. Wakati mmoja hata alimfuata alipokuwa akihubiri ujumbe wa Biblia nyumba hadi nyumba na kumdhihaki alipokuwa akiongea na wenye nyumba kuhusu habari njema za Ufalme. Licha ya upinzani huo usiokoma, Régis aliendelea kuwa mstahimilivu. Kwa hiyo, Régis ni mfano mzuri kwa Wakristo wote, kwa kuwa Yehova hutaka waabudu wake wote wawe wastahimilivu wanaposhughulika na wengine.

2. Neno “ustahimilivu” linadokeza nini?

2 Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo hutumia neno “ustahimilivu” mara kumi, “subira” mara tatu, na “kudhihirisha subira” mara moja. Neno la Kiebrania na la Kigiriki lililotafsiriwa “ustahimilivu” linadokeza subira, uvumilivu, na kutokasirika haraka.

3. Maoni ya Wakristo kuhusu ustahimilivu yalitofautianaje na ya Wagiriki wa karne ya kwanza?

3 Wagiriki wa karne ya kwanza hawakuona ustahimilivu kuwa sifa ya wema. Wanafalsafa wa Stoa hawakutumia kamwe neno hilo. Msomi wa Biblia William Barclay, alisema kwamba ustahimilivu “ni sifa iliyo kinyume kabisa na sifa ya wema ya Wagiriki,” ambao walijivunia “kutovumilia matusi yoyote au kukosewa.” Anasema hivi: “Wagiriki waliona mtu mashuhuri kuwa yule ambaye angefanya chochote ili kulipiza kisasi. Wakristo huona mtu mashuhuri kuwa yule ambaye halipizi kisasi ajapokuwa na uwezo wa kufanya hivyo.” Huenda Wagiriki waliona ustahimilivu kuwa ishara ya udhaifu, lakini kuhusiana na habari hii, “kitu kipumbavu cha Mungu ni chenye hekima zaidi kuliko wanadamu, na kitu dhaifu cha Mungu ni chenye nguvu zaidi kuliko wanadamu.”—1 Wakorintho 1:25.

Mfano wa Kristo wa Ustahimilivu

4, 5. Yesu aliweka mfano gani mzuri wa ustahimilivu?

4 Kristo Yesu ndiye anayemfuata Yehova kwa kuonyesha mfano bora wa ustahimilivu. Alipokuwa chini ya mkazo mwingi, Yesu alijizuia kwa njia ya kustaajabisha. Ilitabiriwa hivi kumhusu: “Alionewa, lakini alinyenyekea, wala hakufunua kinywa chake; kama mwana-kondoo apelekwaye machinjoni, na kama vile kondoo anyamazavyo mbele yao wakatao manyoya yake; naam, hakufunua kinywa chake.”—Isaya 53:7.

5 Yesu alionyesha ustahimilivu ulioje wakati wa huduma yake duniani! Alivumilia maswali yenye hila ya maadui wake na kutukanwa na wapinzani wake. (Mathayo 22:15-46; 1 Petro 2:23) Alikuwa mwenye subira kwa wanafunzi wake, hata walipozozana mara kwa mara kuhusu ni nani aliyekuwa mkubwa zaidi. (Marko 9:33-37; 10:35-45; Luka 22:24-27) Na Yesu alionyesha uvumilivu ulioje usiku aliosalitiwa wakati Petro na Yohana walipolala usingizi baada ya kuambiwa ‘wafulize kulinda’!—Mathayo 26:36-41.

6. Paulo alinufaikaje na ustahimilivu wa Yesu, nasi twajifunza nini kutokana na hilo?

6 Baada ya kufa na kufufuliwa, Yesu aliendelea kuwa mstahimilivu. Mtume Paulo alifahamu jambo hilo vizuri, kwa kuwa hapo awali alikuwa akiwanyanyasa Wakristo. Paulo aliandika hivi: “Wa uaminifu na wenye kustahili ukubalifu kamili ni usemi wa kwamba Kristo Yesu alikuja katika ulimwengu ili kuokoa watenda-dhambi. Kati ya hao mimi ni wa kwanza kabisa. Hata hivyo, sababu kwa nini nilionyeshwa rehema ilikuwa ili kwa njia ya mimi nikiwa kisa cha kwanza kabisa Kristo Yesu apate kuonyesha wote ustahimilivu wake wote kuwa mfano wa wale watakaoweka imani yao juu yake kwa ajili ya uhai udumuo milele.” (1 Timotheo 1:15, 16) Hata tuwe tuliishi maisha ya aina gani hapo awali, tukiwa na imani katika Yesu, atatuonyesha ustahimilivu—ingawa bila shaka, atatarajia tuonyeshe “kazi zinazofaa toba.” (Matendo 26:20; Waroma 2:4) Ujumbe ambao Kristo alituma kwa makutaniko saba huko Asia Ndogo waonyesha kwamba ingawa yeye ni mstahimilivu, anatarajia tuboreshe mwenendo wetu.—Ufunuo, sura ya 2 na 3.

Tunda la Roho

7. Kuna uhusiano gani kati ya ustahimilivu na roho takatifu?

7 Katika sura ya 5 ya barua yake kwa Wagalatia, Paulo atofautisha kazi za mwili na matunda ya roho. (Wagalatia 5:19-23) Kwa kuwa ustahimilivu ni mojawapo ya sifa za Yehova, sifa hii hutoka kwake nayo ni tunda la roho yake. (Kutoka 34:6, 7) Kwa kweli, ustahimilivu unaorodheshwa kuwa tunda la nne katika matunda ya roho aliyotaja Paulo ambayo ni “upendo, shangwe, amani, . . . fadhili, wema, imani, upole, kujidhibiti.” (Wagalatia 5:22, 23) Kwa hiyo, watumishi wa Mungu huongozwa na roho takatifu kuonyesha subira au ustahimilivu kama wa Mungu.

8. Ni nini kitakachotuwezesha kusitawisha matunda ya roho, kutia ndani ustahimilivu?

8 Hata hivyo, hii haimaanishi kwamba Yehova humpa mtu roho yake kwa lazima. Ni lazima tuwe na nia ya kuiruhusu ituongoze. (2 Wakorintho 3:17; Waefeso 4:30) Tunaruhusu roho hiyo itende maishani mwetu kwa kusitawisha matunda yake katika mambo yote tunayofanya. Baada ya kuorodhesha kazi za mwili na matunda ya roho, Paulo aliongezea hivi: “Ikiwa tunaishi kwa roho, acheni sisi tuendelee kutembea kwa utaratibu pia kwa roho. Msiongozwe vibaya: Mungu si wa kudhihakiwa. Kwa maana lolote lile mtu analopanda, hilo atavuna pia; kwa sababu yeye anayepanda katika mwili wake atavuna ufisadi kutokana na mwili wake, lakini yeye anayepanda katika roho atavuna uhai udumuo milele kutokana na roho.” (Wagalatia 5:25; 6:7, 8) Ikiwa tutafaulu kusitawisha ustahimilivu, ni lazima pia tusitawishe matunda mengine ambayo roho takatifu hutokeza katika Wakristo.

“Upendo Ni Wenye Ustahimilivu”

9. Kwa nini huenda Paulo aliwaambia Wakorintho kwamba “upendo ni wenye ustahimilivu”?

9 Paulo alionyesha kwamba kuna uhusiano wa pekee kati ya upendo na ustahimilivu aliposema: “Upendo ni wenye ustahimilivu.” (1 Wakorintho 13:4) Msomi mmoja wa Biblia, Albert Barnes, adokeza kwamba Paulo alikazia jambo hilo kwa sababu ya ugomvi na zogo lililokuwako katika kutaniko la Kikristo huko Korintho. (1 Wakorintho 1:11, 12) Barnes asema hivi: ‘Neno lililotumiwa hapa [kumaanisha ustahimilivu] ni kinyume cha kufanya mambo haraka haraka: kusema na kuwaza kwa hasira, na kuudhika. Lamaanisha hali ya akili ya KUVUMILIA KWA MUDA MREFU unapodhulumiwa au kukasirishwa.’ Upendo na ustahimilivu unachangia sana amani ya kutaniko la Kikristo.

10. (a) Upendo hutusaidiaje tuwe wastahimilivu, na mtume Paulo atoa shauri gani kuhusiana na habari hiyo? (b) Msomi mmoja wa Biblia alisema nini kuhusu fadhili na ustahimilivu wa Mungu? (Ona kielezi-chini.)

10 “Upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fadhili. Upendo . . . hautafuti masilahi yao wenyewe, haupati kuwa wenye kuchokozeka.” Kwa hiyo, katika njia nyingi upendo hutusaidia tuwe wastahimilivu. * (1 Wakorintho 13:4, 5) Upendo hutuwezesha kuchukuliana kwa subira na kukumbuka kwamba sisi sote ni watu wasio wakamilifu na walio na udhaifu. Hutusaidia tuwe wenye kuwafikiria wengine na wenye kusamehe. Mtume Paulo anatutia moyo tutembee ‘tukiwa na hali kamili ya akili ya kujishusha chini na upole, tukiwa na ustahimilivu, tukichukuliana mtu na mwenzake katika upendo, tukijitahidi sana kwa bidii kushika umoja wa roho katika kifungo chenye kuunganisha cha amani.’—Waefeso 4:1-3.

11. Kwa nini ni muhimu hasa kwa Wakristo wanaoishi pamoja kuwa wastahimilivu?

11 Wakristo wanaoishi pamoja, iwe ni katika makutaniko, makao ya Betheli, makao ya mishonari, vikundi vya wajenzi, au kwenye shule wanakuwa na amani na furaha wanapoonyesha ustahimilivu. Kwa sababu ya tofauti za utu, mapendezi, malezi, tabia, hata usafi, nyakati nyingine huenda kukatokea hali zenye kuudhi. Hali zenye kuudhi zinaweza kutokea katika familia pia. Ni muhimu kutokuwa mwepesi wa hasira. (Mithali 14:29; 15:18; 19:11) Wote wanahitaji kuonyesha ustahimilivu, yaani uvumilivu wenye subira, wakiwa na matumaini kwamba hali zitabadilika na kuwa bora.—Waroma 15:1-6.

Ustahimilivu Hutusaidia Kuvumilia

12. Kwa nini uvumilivu ni muhimu tunapopatwa na majaribu?

12 Ustahimilivu hutusaidia kuvumilia majaribu ambayo huonekana kuwa ya kudumu au yasiyoweza kusuluhishwa upesi. Régis, aliyetajwa mwanzoni alikabili hali kama hiyo. Mke wake alimpinga kwa miaka mingi asimtumikie Yehova. Hata hivyo, siku moja alimjia huku akitokwa na machozi na kusema: “Najua hii ndiyo kweli. Nisaidie. Nataka funzo la Biblia.” Hatimaye alibatizwa na kuwa Shahidi. Régis asema: “Jambo hilo lilithibitisha kwamba Yehova alibariki jitihada, subira, na uvumilivu nilioonyesha kwa miaka hiyo.” Alithawabishwa kwa sababu ya kuwa mstahimilivu.

13. Ni nini kilichomwezesha Paulo kuvumilia, na mfano wake unaweza kutusaidiaje kuvumilia?

13 Katika karne ya kwanza W.K., mtume Paulo aliweka mfano mzuri wa ustahimilivu. (2 Wakorintho 6:3-10; 1 Timotheo 1:16) Paulo alipokuwa anakaribia kufa alimshauri rafiki yake mchanga Timotheo, akimwambia kwamba Wakristo wote wangekabili majaribu. Paulo alitaja mfano wake mwenyewe na akadokeza sifa za msingi za Kikristo ambazo ni za lazima ili kuvumilia. Aliandika hivi: “Wewe umefuata kwa ukaribu fundisho langu, mwendo wangu wa maisha, kusudi langu, imani yangu, ustahimilivu wangu, upendo wangu, uvumilivu wangu, minyanyaso yangu, mateso yangu, namna ya mambo yaliyotukia kwangu Antiokia, Ikoniamu, Listra, namna ya minyanyaso ambayo nimestahimili; na bado kutoka katika hayo yote Bwana alinikomboa mimi. Kwa kweli, wote wale wanaotamani kuishi kwa ujitoaji-kimungu katika ushirika na Kristo Yesu watanyanyaswa pia.” (2 Timotheo 3:10-12; Matendo 13:49-51; 14:19-22) Ili kuvumilia, sote twahitaji imani, upendo, na ustahimilivu.

Wamevikwa Ustahimilivu

14. Paulo alilinganisha sifa za kimungu kama vile ustahimilivu na nini, naye alitoa shauri gani kwa Wakristo huko Kolosai?

14 Mtume Paulo alilinganisha ustahimilivu na pia sifa nyingine za kimungu na mavazi ambayo Mkristo anapaswa kuvaa baada ya kuvua tabia za “utu wa zamani.” (Wakolosai 3:5-10) Aliandika hivi: “Kama wachaguliwa wa Mungu, watakatifu na wapendwa, jivikeni wenyewe shauku nyororo za huruma, fadhili, hali ya akili ya kujishusha chini, upole, na ustahimilivu. Endeleeni kuchukuliana mtu na mwenzake na kusameheana kwa hiari mtu na mwenzake ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika dhidi ya mwingine. Kama vile Yehova alivyowasamehe nyinyi kwa hiari, fanyeni hivyo nyinyi pia. Lakini, zaidi ya mambo haya yote, jivikeni wenyewe upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.”—Wakolosai 3:12-14.

15. Kunakuwa na matokeo gani Wakristo ‘wanapojivika wenyewe’ ustahimilivu na sifa nyingine za kimungu?

15 Washiriki wa kutaniko ‘wanapojivika wenyewe’ shauku nyororo za huruma, fadhili, hali ya akili ya kujishusha chini, upole, ustahimilivu, na upendo, wanaweza kutatua matatizo na kuendelea kumtumikia Yehova kwa muungano. Waangalizi Wakristo hasa wapaswa kuwa wastahimilivu. Nyakati nyingine watahitaji kukaripia Mkristo mwingine, lakini kuna njia mbalimbali za kufanya hivyo. Paulo alieleza njia iliyo bora kabisa ya kufanya hivyo alipomwandikia Timotheo hivi: “Karipia, kemea, himiza kwa bidii, kwa ustahimilivu wote na usanifu wa kufundisha.” (2 Timotheo 4:2) Naam, sikuzote, kondoo za Yehova wapaswa kutendewa kwa ustahimilivu, heshima, na wororo.—Mathayo 7:12; 11:28; Matendo 20:28, 29; Waroma 12:10.

“Wenye Ustahimilivu Kuelekea Wote”

16. Huenda kukawa na matokeo gani tunapokuwa “wenye ustahimilivu kuelekea wote”?

16 Ustahimilivu wa Yehova kuelekea wanadamu unatufanya tuwe na daraka la kuwa “wenye ustahimilivu kuelekea wote.” (1 Wathesalonike 5:14) Hii yamaanisha kuwaonyesha subira washiriki wa familia ambao si Mashahidi, majirani, wafanyakazi wenzetu, na wanashule wenzetu. Mashahidi wamevumilia chuki nyingi, na nyakati nyingine wamedhihakiwa au kupingwa moja kwa moja na wafanyakazi au wanashule wenzao. (Wakolosai 4:5, 6) Mtume Petro aliandika hivi: “Dumisheni mwenendo wenu ukiwa bora miongoni mwa mataifa, ili, katika jambo ambalo katika hilo wao wanasema dhidi yenu kuwa watenda-maovu, likiwa tokeo la kazi zenu bora ambazo wamekuwa mashahidi wa kujionea wapate kumtukuza Mungu katika siku ya ukaguzi wake.”—1 Petro 2:12.

17. Tunawezaje kuiga upendo na ustahimilivu wa Yehova, na kwa nini twapaswa kufanya hivyo?

17 Mamilioni ya watu wataokoka kwa sababu ya ustahimilivu wa Yehova. (2 Petro 3:9, 15) Tukiiga upendo na ustahimilivu wa Yehova, tutaendelea kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu kwa subira na kufundisha wengine wajitiishe chini ya utawala wa Ufalme wa Kristo. (Mathayo 28:18-20; Marko 13:10) Ikiwa tungeacha kuhubiri, ingekuwa ni kana kwamba tunazuia ustahimilivu wa Yehova na kukosa kutambua kusudi la uvumilivu huo ambalo ni kuwapa watu nafasi watubu.—Waroma 2:4.

18. Paulo alisali kuhusu nini kwa ajili ya Wakolosai?

18 Katika barua yake kwa Wakristo huko Kolosai, Asia Ndogo, Paulo aliandika: “Hiyo ndiyo sababu pia sisi, tangu siku tuliposikia juu ya hilo, hatujaacha kusali kwa ajili yenu na kuomba ili nyinyi mpate kujazwa ujuzi sahihi wa mapenzi yake katika hekima yote na ufahamivu wa kiroho, kusudi mtembee kwa kumstahili Yehova kwa madhumuni ya kumpendeza yeye kikamili mnapoendelea kuzaa matunda katika kila kazi njema na kuongezeka katika ujuzi sahihi wa Mungu, mkifanywa wenye nguvu nyingi kwa nguvu zote kwa kadiri ya uweza wake wenye utukufu ili kuvumilia kikamili na kuwa wenye ustahimilivu pamoja na shangwe.”—Wakolosai 1:9-11.

19, 20. (a) Tunawezaje kuepuka kuona ustahimilivu ambao Yehova ameendelea kuonyesha kuwa jaribu? (b) Tutapata manufaa gani kwa kuwa wastahimilivu?

19 Ikiwa ‘tumejazwa ujuzi sahihi wa mapenzi yake,’ ambayo ni kwamba “watu wa namna zote waokolewe na kuja kwenye ujuzi sahihi wa kweli,” hatutaona ustahimilivu au subira ambayo Yehova ameendelea kuonyesha kuwa jaribu. (1 Timotheo 2:4) ‘Tutaendelea kuzaa matunda katika kila kazi njema,’ hasa ile ya kuhubiri “habari njema hii ya ufalme.” (Mathayo 24:14) Tukiendelea kufanya hivyo kwa uaminifu, Yehova atatufanya tuwe “wenye nguvu nyingi kwa nguvu zote,” na kutuwezesha “kuvumilia kikamili na kuwa wenye ustahimilivu pamoja na shangwe.” Tunapofanya hivyo, ‘tutatembea kwa kumstahili Yehova,’ na tutakuwa na amani inayotokana na kujua kwamba ‘tunampendeza yeye kikamili.’

20 Na tuwe na uhakika kwamba Yehova ameonyesha hekima kwa kuwa mstahimilivu. Inatuokoa na kuwaokoa wale wanaosikiliza mahubiri na mafundisho yetu. (1 Timotheo 4:16) Kusitawisha matunda ya roho—upendo, fadhili, wema, upole, na kujidhibiti—kutatuwezesha kuonyesha ustahimilivu kwa shangwe. Kutatuwezesha kuishi kwa amani pamoja na washiriki wa familia zetu na vilevile ndugu na dada zetu kutanikoni. Ustahimilivu utatuwezesha pia kuwa wenye subira kuelekea wafanyakazi na wanashule wenzetu. Na ustahimilivu wetu utakuwa na kusudi la kuwaokoa wakosaji, na kumtukuza Mungu mwenye ustahimilivu, Yehova.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Akieleza taarifa ya Paulo kwamba “upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fadhili,” msomi wa Biblia Gordon D. Fee aandika hivi: “Katika theolojia ya Paulo sifa ya [ustahimilivu na fadhili] yaonyesha mtazamo wa Mungu kuelekea wanadamu (linganisha Rom. 2:4). Kwa upande mmoja, uvumilivu wa Mungu unaonyeshwa na jinsi anavyozuia hasira yake dhidi ya uasi wa wanadamu; kwa upande mwingine, fadhili zake zaonekana kwa jinsi anavyoonyesha sana rehema yake. Kwa hiyo ufafanuzi wa Paulo kuhusu upendo unaanza kwa ufafanuzi huu wenye maana mbili wa Mungu, ambaye kupitia Kristo ameonyesha uvumilivu na fadhili zake kuelekea wale wanaostahili kupata hukumu yake kali.”

Je, Unaweza Kueleza?

• Kristo ni mfano mzuri wa ustahimilivu jinsi gani?

• Ni nini kitakachotusaidia kusitawisha ustahimilivu?

• Ustahimilivu husaidiaje familia, Wakristo wanaoishi pamoja, na wazee?

• Kuwa wastahimilivu kwaweza kutunufaishaje sisi na wengine?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 15]

Hata alipokuwa chini ya mkazo mwingi, Yesu aliwaonyesha wanafunzi wake subira

[Picha katika ukurasa wa 16]

Waangalizi Wakristo wanahimizwa waweke mfano mzuri wa ustahimilivu wanaposhughulika na ndugu zao

[Picha katika ukurasa wa 17]

Tukiiga upendo na ustahimilivu wa Yehova, tutaendelea kuhubiri habari njema

[Picha katika ukurasa wa 18]

Paulo alisali kwamba Wakristo ‘wawe wenye ustahimilivu pamoja na shangwe’