Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Ni Mungu Mstahimilivu

Yehova Ni Mungu Mstahimilivu

Yehova Ni Mungu Mstahimilivu

“Yehova, Mungu mwenye rehema na neema, si mwepesi wa hasira bali ni mwingi wa fadhili-upendo.”—KUTOKA 34:6, NW.

1, 2. (a) Ni nani walionufaika na ustahimilivu wa Yehova hapo zamani? (b) Neno “ustahimilivu” lamaanisha nini?

WATU wa siku za Noa, Waisraeli waliokuwa wakivuka nyika wakiwa pamoja na Musa, Wayahudi waliokuwepo Yesu alipokuwa duniani—wote waliishi chini ya hali tofauti. Lakini wote walinufaika na sifa ileile nzuri ya Yehova—ustahimilivu. Sifa hiyo hata iliokoa baadhi yao. Ustahimilivu wa Yehova unaweza kutuokoa pia.

2 Ustahimilivu ni nini? Yehova huonyesha sifa hiyo wakati gani na kwa nini? “Ustahimilivu” unadokeza wazo la kuvumilia kwa saburi kosa au kuudhiwa, pasipo kukata tamaa kwamba uhusiano ulioharibika unaweza kuboreka. Kwa hiyo, sifa ya ustahimilivu huonyeshwa kukiwa na sababu fulani. Ustahimilivu hunufaisha hasa mtu anayeharibu mahusiano. Hata hivyo, kuwa mstahimilivu hakumaanishi kuachilia makosa. Kusudi la kuonyesha sifa ya ustahimilivu linapotimizwa, au kusipokuwa na uhitaji wa kuvumilia tena hali fulani, ustahimilivu hukoma.

3. Yehova ameonyesha ustahimilivu kwa kusudi gani, nao ustahimilivu wake utafikia kikomo lini?

3 Ingawa wanadamu wanaweza kuwa wastahimilivu, Yehova ndiye kielelezo bora zaidi cha ustahimilivu. Tangu dhambi ilipoharibu uhusiano kati ya Yehova na wanadamu, Muumba wetu ametuvumilia kwa saburi na ameandaa njia ili wanadamu wanaoonyesha toba waweze kuboresha uhusiano wao pamoja naye. (2 Petro 3:9; 1 Yohana 4:10) Lakini ustahimilivu wake utakapotimiza kusudi lake, Mungu atachukua hatua dhidi ya wakosaji wa kukusudia, na kukomesha mfumo huu mwovu.—2 Petro 3:7.

Unapatana na Sifa Kuu za Mungu

4. (a) Ustahimilivu unafafanuliwa jinsi gani katika Maandiko ya Kiebrania? (b) Nabii Nahumu anamfafanua Yehova jinsi gani, na hilo hufunua nini kuhusu ustahimilivu wa Yehova?

4 Katika Maandiko ya Kiebrania, wazo la ustahimilivu linafafanuliwa kwa maneno mawili ya Kiebrania ambayo yametafsiriwa “si mwepesi wa hasira” katika Biblia ya New World Translation. Akizungumza juu ya ustahimilivu wa Mungu, nabii Nahumu alisema: “Mwenyezi-Mungu hakasiriki upesi, lakini amejaa nguvu, Mwenyezi-Mungu kamwe hatawaachilia wenye hatia.” (Nahumu 1:3, Biblia Habari Njema) Kwa hiyo, ustahimilivu wa Yehova una mipaka nao si ishara ya udhaifu. Kwa kuwa Mungu mweza yote ni mwenye nguvu nyingi na vilevile si mwepesi wa hasira, basi ustahimilivu wake unatokana na kujizuia akiwa na kusudi fulani. Anaweza kutoa adhabu, lakini yeye hujizuia kufanya hivyo mara moja ili ampe mkosaji fursa ya kubadilika. (Ezekieli 18:31, 32) Kwa hiyo, ustahimilivu wa Yehova hudhihirisha upendo wake, na huonyesha jinsi anavyotumia uweza wake kwa hekima.

5. Ni katika njia gani ustahimilivu wa Yehova hupatana na haki yake?

5 Pia ustahimilivu wa Yehova hupatana na haki na uadilifu wake. Alijifunua kwa Musa kuwa “Mungu mwenye rehema na neema, si mwepesi wa hasira [“mstahimilivu,” King James Version] ni mwingi wa fadhili-upendo na kweli.” (Kutoka 34:6, NW) Miaka mingi baadaye, Musa alimwimbia Yehova sifa hivi: “Njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, asiye na uovu, yeye ndiye mwenye haki na adili.” (Kumbukumbu la Torati 32:4) Naam, rehema, ustahimilivu, haki, na adili ya Yehova hupendeza sana.

Ustahimilivu wa Yehova Kabla ya Furiko

6. Yehova ameonyesha ustahimilivu jinsi gani kwa njia yenye kutokeza sana kuelekea wazao wa Adamu na Hawa?

6 Uasi wa Adamu na Hawa huko Edeni ulikatisha kabisa uhusiano wao wenye thamani pamoja na Muumba wao mwenye upendo, Yehova. (Mwanzo 3:8-13, 23, 24) Mtengano huo uliathiri wazao wao, ambao walirithi dhambi, kutokamilika, na kifo. (Waroma 5:17-19) Ingawa wenzi wa kwanza wawili walitenda dhambi kimakusudi, Yehova aliwaruhusu wazae watoto. Baadaye, aliandaa kwa upendo njia ambayo wazao wa Adamu na Hawa wangeweza kupatanishwa naye. (Yohana 3:16, 36) Mtume Paulo alieleza hivi: “Mungu apendekeza upendo wake mwenyewe kwetu kwa kuwa, tulipokuwa tungali watenda-dhambi, Kristo alikufa kwa ajili yetu. Kwa hiyo, ni zaidi sana kwa kuwa tumetangazwa kuwa waadilifu sasa kwa damu yake, kwamba tutaokolewa kutokana na hasira ya kisasi kupitia yeye. Kwa maana, ikiwa tulipokuwa maadui, tulipata kuwa wenye kupatanishwa na Mungu kupitia kifo cha Mwana wake, ni zaidi sana sisi tutaokolewa kwa uhai wake.”—Waroma 5:8-10.

7. Yehova alionyeshaje ustahimilivu kabla ya Furiko, na kwa nini kuharibiwa kwa kizazi kilichoishi kabla ya Furiko kulikuwa kwa haki?

7 Yehova alionyesha ustahimilivu katika siku za Noa. Zaidi ya karne moja kabla ya Furiko, ‘Mungu aliiona dunia, na tazama imeharibika; maana kila mwenye mwili amejiharibia njia yake duniani.’ (Mwanzo 6:12) Hata hivyo, kwa muda fulani, Yehova alionyesha ustahimilivu kuelekea wanadamu. Alisema: “Roho yangu haitashindana na mwanadamu milele, kwa kuwa yeye naye ni nyama; basi siku zake zitakuwa miaka mia na ishirini.” (Mwanzo 6:3) Miaka hiyo 120 ilimpa Noa mwaminifu wakati wa kupata watoto, na akapewa amri ya Mungu ya kujenga safina na kuonya watu walioishi siku zake juu ya Furiko ambalo lingekuja. Mtume Petro aliandika hivi: “Subira [sifa inayohusiana na ustahimilivu wa] Mungu ilipokuwa ikingoja katika siku za Noa, huku safina ilipokuwa ikijengwa, ambayo ndani yayo watu wachache, yaani, nafsi nane, walichukuliwa salama kupitia maji.” (1 Petro 3:20) Ni kweli kwamba wale ambao hawakuwa watu wa jamaa ya Noa “hawakujali” mahubiri yake. (Mathayo 24:38, 39) Lakini kwa kumwagiza Noa ajenge safina na labda atumikie kwa miongo kadhaa akiwa “mhubiri wa uadilifu,” Yehova aliwapa watu walioishi siku za Noa nafasi ya kutosha kutubu kuhusiana na matendo yao ya jeuri na kugeuka na kumtumikia. (2 Petro 2:5; Waebrania 11:7) Uharibifu uliopata kizazi hicho hatimaye, ulikuwa wa haki kabisa.

Ustahimilivu Usio na Kifani Kuelekea Israeli

8. Yehova alionyesha ustahimilivu kuelekea taifa la Israeli jinsi gani?

8 Yehova aliwaonyesha Waisraeli ustahimilivu kwa muda unaozidi miaka 120. Katika historia yao nzima ya miaka zaidi ya 1,500 wakiwa watu waliochaguliwa na Mungu, mara nyingi Waisraeli waliujaribu sana ustahimilivu wa Mungu. Majuma machache tu baada ya kukombolewa kimuujiza kutoka Misri, walianza kuabudu sanamu, na hivyo kumdharau kabisa Mwokozi wao. (Kutoka 32:4; Zaburi 106:21) Miaka iliyofuata, Waisraeli walilalamika kuhusu chakula ambacho Yehova aliwaandalia kimuujiza wakiwa jangwani, wakamnung’unikia Musa na Aroni, wakasema vibaya kuhusu Yehova, wakafanya uasherati na wapagani, na hata kushiriki ibada ya Baali. (Hesabu 11:4-6; 14:2-4; 21:5; 25:1-3; 1 Wakorintho 10:6-11) Yehova angekuwa na haki ya kuwaangamiza watu wake, badala yake alionyesha ustahimilivu.— Hesabu 14:11-21.

9. Yehova alijionyesha kuwa Mungu mstahimilivu jinsi gani wakati wa Waamuzi na wakati wa utawala wa wafalme?

9 Wakati wa Waamuzi, Waisraeli waliabudu sanamu mara kwa mara. Walipofanya hivyo, Yehova aliwaacha wanyanyaswe na maadui wao. Lakini walipotubu na kumwomba msaada, alionyesha ustahimilivu na kuwapa waamuzi wa kuwakomboa. (Waamuzi 2:17, 18) Katika miaka mingi ya utawala wa wafalme, ni wafalme wachache waliodhihirisha ujitoaji kwa Yehova usiohusisha wengine. Hata wakati wa utawala wa wafalme waaminifu, mara nyingi watu walichanganya ibada ya kweli na ibada isiyo ya kweli. Yehova alipotuma manabii watoe onyo dhidi ya kukosa uaminifu, mara nyingi watu waliamua kusikiliza makuhani wafisadi na manabii wasio wa kweli. (Yeremia 5:31; 25:4-7) Hata Waisraeli waliwanyanyasa manabii waaminifu wa Yehova na wakaua baadhi yao. (2 Mambo ya Nyakati 24:20, 21; Matendo 7:51, 52) Hata hivyo, Yehova aliendelea kuonyesha ustahimilivu.—2 Mambo ya Nyakati 36:15.

Ustahimilivu wa Yehova Haukukoma

10. Ustahimilivu wa Yehova ulikoma lini?

10 Hata hivyo, historia yaonyesha kwamba ustahimilivu wa Mungu una kikomo. Katika mwaka wa 740 K.W.K. aliruhusu Waashuri washinde ufalme wa Israeli wa makabila kumi na kupeleka wakazi wake uhamishoni. (2 Wafalme 17:5, 6) Na mwishoni mwa karne iliyofuata, aliruhusu Wababuloni wavamie ufalme wa Yuda wa makabila mawili na kuharibu Yerusalemu na hekalu lake.—2 Mambo ya Nyakati 36:16-19.

11. Yehova alionyesha ustahimilivu jinsi gani hata wakati alipokuwa akitekeleza hukumu?

11 Hata hivyo, Yehova alipotekeleza hukumu yake dhidi ya Israeli na Yuda hakusahau kuwa mstahimilivu. Kupitia nabii wake Yeremia, Yehova alitabiri kurudishwa kwa watu wake waliochaguliwa. Alisema hivi: “Babeli utakapotimiziwa miaka sabini, nitawajilia ninyi, na kulitimiza neno langu jema kwenu, kwa kuwarudisha mahali hapa. Nami nitaonekana kwenu . . . nami nitawarudisha watu wenu waliofungwa, nami nitawakusanya ninyi, nikiwatoa katika mataifa yote, na katika mahali pote, nilikowafukuza.”—Yeremia 29:10, 14.

12. Kuja kwa Mesiya kulithibitisha jinsi gani kwamba Yehova ndiye aliyewaongoza mabaki ya Wayahudi kurudi Yuda?

12 Kwa kweli miongoni mwa Wayahudi waliopelekwa uhamishoni kulikuweko mabaki waliorudi Yuda na kuanzisha tena ibada ya Yehova katika hekalu lililojengwa upya Yerusalemu. Katika kutimizwa kwa makusudi ya Yehova, mabaki hao wangekuwa kama “umande utokao kwa BWANA,” ambao huleta burudisho na ufanisi. Pia wangekuwa wajasiri na wenye nguvu kama “simba kati ya wanyama wa msituni.” (Mika 5:7, 8) Huenda usemi huo wa mwisho ulitimizwa katika enzi ya Wamakabayo. Wakati huo Wayahudi wakiwa chini ya utawala wa familia ya Wamakabayo waliwafukuza maadui wao kutoka Bara Lililoahidiwa na kuweka wakfu tena hekalu lililokuwa limetiwa unajisi. Kwa hiyo, hekalu na bara hilo lilihifadhiwa ili mabaki wengine waaminifu waweze kumpokea Mwana wa Mungu alipotokea huko akiwa Mesiya.—Danieli 9:25; Luka 1:13-17, 67-79; 3:15, 21, 22.

13. Hata baada ya Wayahudi kumwua Mwana wake, Yehova aliendelea kuwaonyesha ustahimilivu jinsi gani?

13 Hata baada ya Wayahudi kumwua Mwana wake, Yehova aliendelea kuwaonyesha ustahimilivu kwa muda wa miaka mitatu na nusu zaidi, na kuwapa nafasi ya kipekee ya kuitwa kuwa sehemu ya mbegu ya kiroho ya Abrahamu. (Danieli 9:27) * Kabla na baada ya mwaka wa 36 W.K., baadhi ya Wayahudi walikubali mwito huo, hivyo baadaye Paulo alisema, “kumetokea pia mabaki kulingana na kuchaguliwa ambako ni kwa sababu ya fadhili isiyostahiliwa.”—Waroma 11:5.

14. (a) Katika mwaka wa 36 W.K, ni nani waliopewa pendeleo la kuwa sehemu ya mbegu ya kiroho ya Abrahamu? (b) Paulo alielezaje maoni yake kuhusu jinsi ambavyo Yehova huchagua washiriki wa Israeli wa kiroho?

14 Kwa mara ya kwanza, watu ambao hawakuwa Wayahudi au wageuzwa-imani walipewa pendeleo la kuwa sehemu ya mbegu ya kiroho ya Abrahamu katika mwaka wa 36 W.K. Pia yeyote aliyekubali mwito huo alipokea ustahimilivu na fadhili isiyostahiliwa ya Yehova. (Wagalatia 3:26-29; Waefeso 2:4-7) Akionyesha jinsi alivyoshukuru sana kwa hekima na kusudi la ustahimilivu wa Yehova la kutokeza idadi kamili ya wale walioitwa kuwa Waisraeli wa kiroho, Paulo alisema hivi kwa mkazo: “Lo! kina cha utajiri wa Mungu na hekima na ujuzi! Jinsi hukumu zake zisivyotafutikana na njia zake zapita uwezo wa kufuatilia!”—Waroma 11:25, 26, 33; Wagalatia 6:15, 16.

Ni Mstahimilivu kwa Ajili ya Jina Lake

15. Kwa nini Mungu huonyesha ustahimilivu hasa, na ni suala gani lililohitaji kujibiwa?

15 Kwa nini Yehova huonyesha ustahimilivu? Hasa ni kwa kusudi la kutukuza jina lake takatifu na kutetea enzi yake kuu. (1 Samweli 12:20-22) Suala la kiadili lililozushwa na Shetani kuhusu jinsi Yehova anavyotawala lilihitaji wakati ili kujibiwa kwa njia yenye kuridhisha viumbe wote. (Ayubu 1:9-11; 42:2, 5, 6) Kwa hiyo, wakati watu wake walipokuwa wananyanyaswa huko Misri, Yehova alimwambia Farao hivi: “Nilikusimamisha wewe kwa sababu hii hii, ili nikuonyeshe uweza wangu, tena kwamba jina langu litangazwe katika dunia yote.”—Kutoka 9:16.

16. (a) Ustahimilivu wa Yehova uliwezeshaje watu fulani watayarishwe kwa ajili ya jina lake? (b) Jina la Yehova litatakaswa jinsi gani na enzi yake kuu itatetewaje?

16 Maneno ya Yehova kwa Farao yalinukuliwa na mtume Paulo alipoeleza jinsi ustahimilivu wa Mungu unavyohusiana na kutukuzwa kwa jina Lake takatifu. Kisha Paulo akaandika: “Basi, ikiwa Mungu, ingawa anayo nia ya kuonyesha hasira ya kisasi yake na kujulisha nguvu yake, alivumilia kwa ustahimilivu mwingi vyombo vya hasira ya kisasi vilivyofanywa kufaa kwa ajili ya uharibifu, ili apate kujulisha utajiri wa utukufu wake juu ya vyombo vya rehema, alivyotayarisha kimbele kwa ajili ya utukufu, yaani, sisi, alioita si kutoka miongoni mwa Wayahudi tu bali pia kutoka miongoni mwa mataifa, kuna ubaya gani? Ni kama asemavyo pia katika Hosea: ‘Wale ambao si watu wangu hakika nitawaita “watu wangu.”’” (Waroma 9:17, 22-25) Kwa kuwa Yehova alionyesha ustahimilivu, aliweza kuchukua kutoka kwa mataifa “watu kwa ajili ya jina lake.” (Matendo 15:14) Chini ya Kichwa chao, Yesu Kristo, “watakatifu” hao ni warithi wa Ufalme ambao Yehova atatumia kutakasa jina Lake kuu na kutetea enzi Yake kuu.—Danieli 2:44; 7:13, 14, 27; Ufunuo 4:9-11; 5:9, 10.

Ustahimilivu wa Yehova Huleta Wokovu

17, 18. (a) Tunawezaje kuchambua ustahimilivu wa Yehova pasipo kujua? (b) Tunatiwa moyo tuoneje ustahimilivu wa Yehova?

17 Yehova amekuwa Mungu mstahimilivu tangu wanadamu walipofanya dhambi hadi sasa. Ustahimilivu wake kabla ya Furiko uliruhusu wakati ili onyo litolewe na njia ya wokovu itayarishwe. Lakini ustahimilivu wake ulifikia kikomo, nalo Furiko likaja. Vivyo hivyo, leo, Yehova anaonyesha ustahimilivu mkubwa, na ni kana kwamba amekuwa mstahimilivu kwa muda mrefu kuliko wengine walivyotarajia. Hata hivyo, hiyo si sababu ya kukata tamaa. Kufanya hivyo kungekuwa sawa na kumchambua Mungu kwa sababu ya ustahimilivu wake. Paulo aliuliza: “Wewe wadharau utajiri wa fadhili yake na uvumilivu wenye subira na ustahimilivu, kwa sababu hujui kwamba sifa ya fadhili ya Mungu inajaribu kukuongoza wewe kwenye toba?”—Waroma 2:4.

18 Hakuna yeyote kati yetu anayeweza kujua ni kwa kadiri gani Mungu anahitaji kutuonyesha ustahimilivu ili tuwe na uhakika wa kupata kibali chake na kuokoka. Paulo atushauri ‘tufulize kufanyiza wokovu wetu wenyewe kwa hofu na kutetemeka.’ (Wafilipi 2:12) Mtume Petro aliwaandikia Wakristo wenzake hivi: “Yehova si wa polepole kwa habari ya ahadi yake, kama watu fulani waonavyo kuwa ni upolepole, bali yeye ni mwenye subira kwenu kwa sababu hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.”—2 Petro 3:9.

19. Tunaweza kunufaika na ustahimilivu wa Yehova jinsi gani?

19 Kwa hiyo tusikose subira kuhusu jinsi Yehova anavyoshughulikia mambo. Badala yake, acheni tuendelee kutii shauri la Petro na ‘kuiona subira ya Bwana wetu kuwa wokovu.’ Wokovu wa nani? Wetu, na zaidi ya hilo, wokovu wa wengine wengi ambao bado wanahitaji kusikia ‘habari njema ya ufalme.’ (2 Petro 3:15; Mathayo 24:14) Hilo litatusaidia tuthamini jinsi ambavyo Yehova ametuonyesha ustahimilivu mwingi sana na tutachochewa kuwa wastahimilivu tunaposhughulika na wengine.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 13 Ili kupata maelezo zaidi kuhusu unabii huu, ona kitabu Sikiliza Unabii wa Danieli!, ukurasa wa 191-194, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Je, Unaweza Kueleza?

• Katika Biblia, neno “ustahimilivu” linamaanisha nini?

• Yehova alionyeshaje ustahimilivu wake kabla ya Furiko, baada ya utekwa wa Babeli, na katika karne ya kwanza?

• Yehova ameonyesha ustahimilivu kwa sababu gani muhimu?

• Tuuoneje ustahimilivu wa Yehova?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 9]

Ustahimilivu wa Yehova kabla ya Furiko uliwapa watu nafasi ya kutosha kutubu

[Picha katika ukurasa wa 10]

Baada ya Babeli kuanguka, Wayahudi walinufaika na ustahimilivu wa Yehova

[Picha katika ukurasa wa 11]

Katika karne ya kwanza, Wayahudi na watu wasio Wayahudi walinufaika na ustahimilivu wa Yehova

[Picha katika ukurasa wa 12]

Leo Wakristo hujinufaisha na ustahimilivu wa Yehova