Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Noa Auhukumu Ulimwengu kwa Imani Yake

Noa Auhukumu Ulimwengu kwa Imani Yake

Noa Auhukumu Ulimwengu kwa Imani Yake

JE, UMEWAHI kusikia juu ya Noa, mtu mwenye kumwogopa Mungu ambaye alijenga safina ili kuokoa uhai wakati wa furiko lililotokea duniani pote? Licha ya kwamba hadithi hii ni ya kale, inajulikana na mamilioni ya watu. Hata hivyo, wengi hawatambui kwamba maisha ya Noa yana maana kwetu sote.

Kwa nini tupendezwe na simulizi lililotokea maelfu ya miaka iliyopita? Je, hali za Noa zafanana na zetu? Ikiwa zinafanana, twaweza kunufaikaje na mfano wake?

Ulimwengu wa Siku za Noa

Mpangilio wa matukio ya Bibliawaonyesha kwamba Noa alizaliwa mwaka wa 2970 K.W.K.—miaka 126 baada ya Adamu kufa. Katika siku za Noa, dunia ilikuwa na jeuri nyingi sana, na wazao wengi wa Adamu waliamua kufuata mfano mbaya wa wazazi wao wa kwanza. Kwa hiyo, “BWANA akaona ya kuwa maovu ya mwanadamu ni makubwa duniani na kwamba kila kusudi analowaza moyoni mwake ni baya tu sikuzote.”—Mwanzo 6:5, 11, 12.

Yehova hakukasirishwa tu na uasi wa wanadamu. Simulizi la Mwanzo latoa maelezo haya: “Wana wa Mungu waliwaona hao binti za wanadamu ya kuwa ni wazuri; wakajitwalia wake wowote waliowachagua. . . . Nao Wanefili walikuwako duniani siku zile; tena, baada ya hayo, wana wa Mungu walipoingia kwa binti za wanadamu, wakazaa nao wana; hao ndio waliokuwa watu hodari zamani, watu wenye sifa.” (Mwanzo 6:2-4) Tunapolinganisha mistari hii na taarifa ya mtume Petro twaona kwamba “wana wa Mungu” ni malaika wasiotii. Wanefili walikuwa wazao wa malaika waasi waliojivika miili ya kibinadamu na kufanya ngono haramu na wanawake.—1 Petro 3:19, 20.

Neno “wanefili” linalomaanisha “Waangushaji,” larejezea watu waliowaangusha wengine. Walikuwa wanyanyasaji-wakatili, na dhambi ya baba zao wasio na adili inalinganishwa na upotovu wa Sodoma na Gomora. (Yuda 6, 7) Wakiwa pamoja, walifanya kuwe na uovu mwingi sana duniani.

“Mkamilifu Katika Vizazi Vyake”

Uovu ulikuwa umeenea sana hivi kwamba Mungu akaamua kuwaharibu wanadamu. Lakini simulizi lililopuliziwa lasema: “Nuhu [“Noa,” NW] akapata neema machoni pa BWANA. . . . Nuhu alikuwa mtu wa haki, mkamilifu katika vizazi vyake. Nuhu alikwenda [“alitembea,” NW] pamoja na Mungu.” (Mwanzo 6:8, 9) Iliwezekanaje ‘kutembea pamoja na Mungu’ katika ulimwengu usiomwogopa Mungu uliopaswa tu kuharibiwa?

Bila shaka, Noa alijifunza mambo mengi kutoka kwa baba yake, Lameki, mtu mwenye imani aliyeishi wakati wa Adamu. Alipokuwa akimpa mwana wake jina Noa (linalodhaniwa kuwa lamaanisha “Pumziko,” au “Faraja”), Lameki alitabiri hivi: “Huyu ndiye atakayetufariji kwa kazi yetu na kwa taabu ya mikono yetu katika nchi aliyoilaani BWANA.” Unabii huo ulitimizwa Mungu alipoondoa laana kutoka katika ardhi.—Mwanzo 5:29; 8:21.

Kuzaliwa na wazazi wanaomwogopa Mungu hakumaanishi kwamba watoto watakuwa watu wa kiroho, kwa kuwa kila mtu anapaswa kusitawisha uhusiano wake mwenyewe na Yehova. Noa ‘alitembea pamoja na Mungu’ kwa kuwa na mwenendo uliokubalika na Mungu. Mambo ambayo Noa alijifunza yalimchochea kumtumikia Mungu. Imani ya Noa haikuyumbayumba alipojulishwa kusudi la Mungu la ‘kuharibu kila kitu chenye mwili katika gharika.’—Mwanzo 6:13, 17.

Akiwa na uhakika kwamba msiba huo usio na kifani ungetokea, Noa alitii amri ya Yehova: “Ujifanyie safina ya mti wa mvinje; fanya na vyumba ndani ya safina, ukaifunike ndani na nje kwa lami.” (Mwanzo 6:14) Haikuwa rahisi kutimiza masharti hayo ya Mungu kuhusu safina. Hata hivyo, “ndivyo alivyofanya Nuhu, sawasawa na vyote alivyoamuru Mungu.” Kwa kweli, “hivyo ndivyo alivyofanya.” (Mwanzo 6:22) Noa alisaidiwa na mke wake na wana wao Shemu, Hamu, na Yafethi na wake zao. Yehova alibariki imani yao. Wao ni vielelezo vizuri kama nini kwa familia leo!

Kujenga safina kungehusisha nini? Yehova alimwagiza Noa ajenge sanduku kubwa sana la mbao lisilovuja maji, lenye orofa tatu, la urefu wa meta zipatazo 133, upana wa meta 22 na kimo cha meta 13. (Mwanzo 6:15, 16) Meli hiyo ingekuwa na uwezo wa kubeba mizigo sawa na wa meli za mizigo za kisasa.

Hiyo ilikuwa kazi kubwa kama nini! Yaelekea, kazi hiyo ilihusisha kukata miti mingi, kuisafirisha hadi mahali pa ujenzi, na kuikata iwe mbao au nguzo. Ilimaanisha kujenga jukwaa, kutengeneza vigingi, kutafuta lami ya kuziba mianya, kutafuta makasha na vifaa vya ujenzi, na kadhalika. Huenda kazi hiyo ilihusisha kufanya mapatano na wafanyabiashara na kulipia bidhaa na huduma mbalimbali. Yaonekana kazi hiyo ilihitaji ustadi wa seremala ili kuunganisha mbao kwa usahihi na kujenga chombo kilicho thabiti. Na hebu wazia—labda kazi ya ujenzi ilichukua muda wa miaka 50 au 60 hivi!

Baada ya hapo, Noa angelazimika kukusanya chakula cha kutosha. (Mwanzo 6:21) Angelazimika kukusanya na kuingiza wanyama ndani ya safina. Noa alifanya mambo yote aliyoagizwa na Mungu, na kazi ikakamilika. (Mwanzo 6:22) Kwa sababu ya baraka za Yehova, kazi hiyo ilikamilika kwa mafanikio.

“Mhubiri wa Uadilifu”

Mbali na kujenga safina, Noa alitoa onyo na kumtumikia Mungu kwa uaminifu akiwa “mhubiri wa uadilifu.” Lakini watu “hawakujali mpaka furiko likaja na kuwafagilia mbali wote.”—2 Petro 2:5; Mathayo 24:38, 39.

Kwa kufikiria hali mbaya ya kiroho na ya kiadili ya siku hizo, unaweza kuelewa ni kwa nini familia ya Noa ilichekwa na kudhihakiwa na majirani wenye kutilia shaka. Lazima watu wawe waliwaona kuwa wenye kichaa. Hata hivyo, Noa alifanikiwa kutoa kitia-moyo cha kiroho kwa familia yake, kwa kuwa hawakuathiriwa kamwe na mwenendo wa jeuri, usio wa adili, na uasi wa watu walioishi wakati huo ambao hawakumwogopa Mungu. Noa aliuhukumu ulimwengu wa wakati huo kwa maneno na matendo yake yaliyodhihirisha imani.—Waebrania 11:7.

Wahifadhiwa Wakati wa Furiko

Muda mfupi kabla mvua haijaanza, Mungu alimwambia Noa aingie ndani ya safina iliyokuwa imekamilika. Baada ya familia ya Noa na wanyama kuingia ndani ya safina, “Yehova aliufunga mlango,” na hivyo kuwazuia wadhihaki wowote wasiingie. Furiko lilipokuja, yaonekana malaika wasiotii walijivika miili ya roho na kuokoka uharibifu. Lakini namna gani watu wengine? Kila kiumbe hai kiendacho juu ya ardhi kilichokuwa nje ya safina, kutia ndani Wanefili, waliangamia! Ni Noa na familia yake peke yao waliookoka.—Mwanzo 7:1-23, NW.

Noa na watu wa familia yake walikaa ndani ya safina kwa muda wa mwaka mmoja na siku kumi. Walikuwa na kazi nyingi ya kulisha na kuwapa wanyama maji, kuondoa takataka, na kuhesabu wakati. Kitabu cha Mwanzo kinarekodi awamu zote za Furiko kwa usahihi, sawa na kifaa cha kurekodi safari za meli.—Mwanzo 7:11, 17, 24; 8:3-14.

Alipokuwa ndani ya safina, bila shaka Noa aliongoza familia yake katika mazungumzo ya kiroho na kumshukuru Mungu. Yaonekana, historia ya kabla ya Furiko ilihifadhiwa kupitia Noa na familia yake. Wangenufaika sana kuzungumzia mapokeo yenye kutegemeka au habari fulani za kihistoria walizokuwa nazo wakati huo wa Gharika.

Ni lazima Noa na familia yake wawe walifurahi kama nini kukanyaga nchi kavu tena! Jambo la kwanza alilofanya lilikuwa kujenga madhabahu na kutumikia akiwa kuhani kwa niaba ya familia yake na kutoa dhabihu kwa Mungu aliyewaokoa.—Mwanzo 8:18-20.

“Kama Vile Siku za Noa Zilivyokuwa”

Yesu Kristo alisema: “Kama vile siku za Noa zilivyokuwa, ndivyo kuwapo kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa.” (Mathayo 24:37) Hali kadhalika leo Wakristo ni wahubiri wa uadilifu, wanaowasihi watu watubu. (2 Petro 3:5-9) Kwa kufikiria ulinganisho huo, huenda tukajiuliza, Noa alikuwa akifikiria nini kabla ya Gharika? Je, aliwahi kuhisi kwamba kazi yake ya kuhubiri ilikuwa bure? Je, alichoka nyakati fulani? Biblia haituambii. Tunaambiwa tu kwamba Noa alimtii Mungu.

Je, unaona jinsi hali ya Noa inavyohusiana na yetu? Alimtii Yehova licha ya upinzani na magumu. Ndiyo sababu Yehova alimwona kuwa mwadilifu. Familia ya Noa haikujua wakati hususa ambapo Mungu angeleta Gharika, lakini ilijua kwamba gharika ingekuja. Imani katika neno la Mungu ilimtegemeza Noa kwa miaka mingi ya kazi ngumu, na kazi ya kuhubiri iliyoonekana kuwa isiyo na matokeo. Kwa kweli, tunaambiwa hivi: “Kwa imani Noa, baada ya kupewa onyo la kimungu la mambo yasiyoonwa bado, alionyesha hofu ya kimungu akajenga safina kwa ajili ya kuokoa watu wa nyumbani mwake; na kupitia imani hiyo aliuhukumu ulimwengu kuwa wastahili adhabu, naye akawa mrithi wa uadilifu ulio kulingana na imani.”—Waebrania 11:7.

Noa alisitawishaje imani hiyo? Yaonekana alifikiria kila jambo alilojua kuhusu Yehova naye akaacha ujuzi huo umwongoze. Bila shaka, Noa alizungumza na Mungu katika sala. Kwa hakika, alimfahamu Yehova sana hivi kwamba ‘alitembea pamoja na Mungu.’ Akiwa kichwa cha familia, Noa alifurahi kuwa na familia yake na kuitunza kwa upendo. Hiyo ilitia ndani kushughulikia masilahi ya kiroho ya mke wake, wana wake watatu, na binti-wakwe zake.

Kama vile Noa, leo Wakristo wa kweli wanajua kwamba hivi karibuni Yehova atakomesha mfumo huu wa mambo usiomwogopa Mungu. Hatujui siku hiyo wala saa, lakini tunajua kwamba kuiga imani na utii wa “mhubiri [huyo] wa uadilifu” kutatokeza “kuhifadhi hai nafsi.”—Waebrania 10:36-39.

[Sanduku katika ukurasa wa 29]

Je, Lilitukia Kweli?

Wataalamu wa mambo ya wanadamu wamekusanya hekaya zipatazo 270 kutoka karibu makabila na mataifa yote. “Simulizi la furiko linapatikana ulimwenguni pote,” asema msomi Claus Westermann. “Kama vile simulizi la uumbaji, simulizi la furiko ni sehemu ya utamaduni wetu wa msingi tuliorithi. Inashangaza kweli: kila mahali duniani tunapata masimulizi kuhusu furiko kubwa la kale.” Twaweza kuelezaje jambo hilo? Mtangazaji Enrico Galbiati asema: ‘Imani kuhusu furiko ambayo hupatikana miongoni mwa watu mbalimbali ni ishara ya kwamba mapokeo hayo ni ya kweli kihistoria.’ Hata hivyo, jambo lililo la maana zaidi kwa Wakristo kuliko maoni ya wasomi ni kujua kwamba Yesu mwenyewe alizungumza juu ya Furiko kuwa jambo lililotukia kihalisi katika historia ya mwanadamu.—Luka 17:26, 27.

[Sanduku katika ukurasa wa 30]

Je, Wanefili Wanatajwa Katika Ngano?

Hadithi kuhusu uhusiano haramu wa kingono kati ya miungu na wanadamu—na “mashujaa” au “miungu nusu” waliozaliwa kutokana na uhusiano huo—zilikuwa za kawaida katika elimu ya kidini ya Wagiriki, Wamisri, Wagariti, Wahuri, na Wamesopotamia. Miungu inayotajwa katika ngano za Wagiriki ilikuwa na umbo lenye kuvutia sana la kibinadamu. Miungu hiyo ilikunywa, ikala, ikalala, ikafanya ngono, ikagombana, ikapigana, ikatongoza, na kubaka. Ingawa miungu hiyo ilidhaniwa kuwa mitakatifu, ilidanganya na kufanya uhalifu. Mashujaa kama vile Achilles walisemekana kuwa na asili ya kimungu na kibinadamu na walikuwa na uwezo unaopita wa kibinadamu ingawa wangeweza kufa. Kwa hiyo, mambo yanayotajwa katika kitabu cha Mwanzo kuhusu Wanefili hutujulisha kile kinachoweza kuwa chanzo cha ngano hizo.