Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yesu Huokoa—Jinsi Gani?

Yesu Huokoa—Jinsi Gani?

Yesu Huokoa—Jinsi Gani?

“Yesu huokoa!” “Yesu ni Mwokozi wetu!” Katika nchi nyingi ulimwenguni pote, maneno hayo hubandikwa kwenye kuta za majengo na sehemu nyinginezo za umma. Mamilioni ya watu huamini kwa unyofu kwamba Yesu ni Mwokozi wao. Kama ungewauliza, “Yesu hutuokoa jinsi gani?” labda wangejibu, “Yesu alikufa kwa ajili yetu,” au, “Yesu alikufa kwa ajili ya dhambi zetu.” Naam, kifo cha Yesu hufanya tuokolewe. Lakini kifo cha mtu mmoja kinawezaje kulipia dhambi za wengi? Kama ungeulizwa, “Kifo cha Yesu hutuokoa jinsi gani?” Ungejibuje?

BIBLIA hujibu swali hilo kwa njia rahisi, iliyo wazi, na yenye maana kubwa. Hata hivyo, ili tuelewe umuhimu wa kifo chake, kwanza twahitaji kuona maisha na kifo cha Yesu kuwa suluhisho kwa tatizo gumu sana. Ndipo tutakapoweza kuelewa waziwazi thamani kubwa sana ya kifo cha Yesu.

Kwa kumruhusu Yesu atoe uhai wake, Mungu alikuwa anashughulikia hali iliyosababishwa na dhambi ya Adamu. Dhambi hiyo ilitokeza msiba ulioje! Mwanamume wa kwanza na mke wake, Hawa, walikuwa wakamilifu. Makao yao yalikuwa katika bustani nzuri ya Edeni. Mungu aliwapa kazi yenye kusudi ya kutunza makao yao ya bustani. Walipaswa kusimamia kwa upendo viumbe vyote vilivyo hai duniani. Kadiri wanadamu walivyoongezeka na kuijaza dunia, walipaswa kupanua paradiso ienee duniani pote. (Mwanzo 1:28) Hiyo ilikuwa kazi ya kupendeza na kusisimua kama nini! Isitoshe, wangeshirikiana kwa upendo. (Mwanzo 2:18) Hawakukosa chochote. Wangeishi milele kwa furaha.

Ni vigumu kuwazia jinsi Adamu au Hawa walivyotenda dhambi. Lakini wanadamu hao wa kwanza walimwasi Muumba wao—Yehova Mungu. Akitumia nyoka, kiumbe wa roho Shetani Ibilisi alimdanganya Hawa asimtii Yehova, naye Adamu akamwunga mke wake mkono.—Mwanzo 3:1-6.

Hakukuwa na shaka kuhusu jambo ambalo Muumba angewafanyia Adamu na Hawa. Tayari alikuwa ameeleza waziwazi matokeo ya kuvunja sheria, akisema: “Matunda ya kila mti wa bustani waweza kula, walakini matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula matunda ya mti huo utakufa hakika.” (Mwanzo 2:16, 17) Sasa suala muhimu sana lilihitaji kujibiwa.

Wanadamu Wakabili Tatizo Gumu

Baada ya dhambi ya awali, wanadamu walikabili suala gumu sana kutatuliwa. Adamu aliumbwa akiwa mwanadamu mkamilifu. Kwa hiyo, watoto wake wangeweza kufurahia uhai mkamilifu udumuo milele. Hata hivyo, Adamu alifanya dhambi kabla hajapata watoto. Jamii nzima ya wanadamu ilikuwa viunoni mwake alipopokea hukumu hii: “Kwa jasho la uso wako utakula chakula, hata utakapoirudia ardhi, ambayo katika hiyo ulitwaliwa; kwa maana u mavumbi wewe, nawe mavumbini utarudi.” (Mwanzo 3:19) Kwa hiyo Adamu alipofanya dhambi na kufa kama alivyosema Mungu, wanadamu wote walihukumiwa kifo pamoja naye.

Kwa kufaa, baadaye mtume Paulo aliandika hivi: “Kupitia mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikasambaa kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.” (Waroma 5:12) Naam, kwa sababu ya dhambi ya awali, watoto ambao wangezaliwa wakiwa wakamilifu na kuishi milele, walizaliwa wakiwa na magonjwa, uzee, na hatimaye wakafa.

“Hiyo si haki,” huenda mtu fulani akasema. “Si sisi tuliomkosea Mungu, ni Adamu. Kwa nini tupoteze taraja letu la uhai udumuo milele na furaha?” Tunajua kwamba kama mahakama ingemhukumu mwana na kumtia gerezani kwa sababu babake aliiba gari, mwana huyo angeweza kulalamika hivi kwa kufaa: “Hiyo si haki! Mimi sikufanya kosa lolote.”—Kumbukumbu la Torati 24:16.

Kwa kumshawishi mwanamume na mwanamke wa kwanza wafanye dhambi, huenda Shetani alifikiri kwamba jambo hilo lingemtatanisha Mungu kabisa. Ibilisi alishambulia mapema sana katika historia ya wanadamu—kabla watoto wowote hawajazaliwa. Adamu alipofanya dhambi tu, swali muhimu lilikuwa, Yehova atafanya nini kuhusu watoto ambao watazaliwa na Adamu na Hawa?

Yehova Mungu alitenda kwa haki. “Mungu kamwe hawezi kufanya uovu; Mungu mwenye nguvu hawezi kufanya kosa,” akasema Elihu mwadilifu. (Ayubu 34:10, Biblia Habari Njema) Naye nabii Musa aliandika hivi kumhusu Yehova: “Yeye Mwamba, kazi yake ni kamilifu; maana, njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, asiye na uovu, yeye ndiye mwenye haki na adili.” (Kumbukumbu la Torati 32:4) Suluhisho ambalo Mungu wa kweli alitoa kwa tatizo lililosababishwa na dhambi ya Adamu halituondolei matarajio ya kuishi milele katika paradiso duniani.

Mungu Aandaa Suluhisho Kamilifu

Fikiria suluhisho kamili aliloandaa Mungu alipomhukumu Shetani Ibilisi. Yehova alimwambia Shetani hivi: “Nitaweka uadui kati yako na huyo mwanamke [tengenezo la Mungu la kimbingu], na kati ya uzao wako [ulimwengu unaotawaliwa na Shetani] na uzao wake [Yesu Kristo]; huo utakuponda kichwa [Shetani], na wewe utamponda kisigino [kifo cha Yesu].” (Mwanzo 3:15) Katika unabii huo wa kwanza wa Biblia, Yehova alidokeza kusudi lake la kumtuma Yesu, Mwana wake wa roho wa kimbingu, aje duniani akiwa mwanadamu mkamilifu kisha afe—apondwe kisigino—akiwa bila dhambi.

Kwa nini Mungu alitaka mwanadamu mkamilifu afe? Hukumu ya Yehova Mungu kwa Adamu ingekuwa nini iwapo angefanya dhambi? Je, haikuwa kifo? (Mwanzo 2:16, 17) “Mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo,” akaandika mtume Paulo. (Waroma 6:23) Adamu alilipia dhambi zake kwa kifo chake. Alipewa uhai, akachagua kufanya dhambi, naye akapata adhabu ya kifo kwa ajili ya dhambi yake. (Mwanzo 3:19) Namna gani adhabu waliyopata wanadamu wote kwa sababu ya dhambi hiyo? Mtu fulani alipaswa kufa ili kulipia dhambi zao. Lakini ni kifo cha nani ambacho kingefunika dhambi za wanadamu wote kihalali?

Sheria ya Mungu kwa taifa la Israeli la kale ilidai “uhai kwa uhai.” (Kutoka 21:23) Kulingana na kanuni hii ya kisheria, kifo ambacho kingefunika dhambi za wanadamu kingepaswa kuwa na thamani sawa na kitu ambacho Adamu alipoteza. Kifo cha mwanadamu mwingine mkamilifu tu ndicho kingeweza kulipia dhambi. Yesu ndiye aliyestahili kwa sababu alikuwa mkamilifu. Kwa kweli, Yesu alikuwa “fidia inayolingana” ya kuokoa wazao wote wa Adamu wanaoweza kukombolewa.—1 Timotheo 2:6; Waroma 5:16, 17.

Kifo cha Yesu Kina Thamani Kubwa

Kifo cha Adamu hakikuwa na thamani yoyote; alistahili kufa kwa ajili ya dhambi yake. Hata hivyo, kifo cha Yesu kilikuwa na thamani kubwa kwa sababu alikufa bila dhambi. Yehova Mungu angekubali thamani ya uhai mkamilifu wa Yesu kuwa fidia kwa wazao watiifu wa Adamu mwenye dhambi. Na thamani ya dhabihu ya Yesu hailipii tu dhambi tulizofanya hapo awali. Kama ingekuwa hivyo, hatungekuwa na tumaini la wakati ujao. Kwa kuwa tumezaliwa katika dhambi, tuna mwelekeo wa kufanya dhambi tena. (Zaburi 51:5) Tunaweza kuonyesha uthamini ulioje kwamba kifo cha Yesu kinatuwezesha kuwa wakamilifu kama Yehova alivyokusudia hapo awali kwa wazao wa Adamu na Hawa!

Adamu anaweza kulinganishwa na baba aliyekufa na kutuacha tukiwa na deni kubwa sana (dhambi) hivi kwamba hatungeweza kwa vyovyote kulipa deni hilo. Kwa upande mwingine, Yesu ni kama baba mwema aliyekufa na kutuachia urithi unaotosha kulipia deni kubwa tuliloachiwa na Adamu na kututegemeza milele. Kifo cha Yesu hakiondoi tu dhambi za kale; ni uandalizi mzuri pia kwa ajili ya wakati wetu ujao.

Yesu ni mwokozi wa wanadamu kwa sababu alikufa kwa ajili yetu. Na kifo chake ni uandalizi wenye thamani kama nini! Tunapoona kifo chake kuwa sehemu ya suluhisho la Mungu kwa tatizo kubwa lililotokezwa na dhambi ya Adamu, imani yetu katika Yehova na jinsi anavyofanya mambo huimarishwa. Naam, kifo cha Yesu ni njia ya kukomboa “kila mtu anayedhihirisha imani” katika yeye kutokana na dhambi, magonjwa, uzee, na hata kifo. (Yohana 3:16) Je, unamshukuru Mungu kwa kuandaa mpango huo wenye upendo kwa ajili ya wokovu wetu?

[Picha katika ukurasa wa 5]

Adamu aliwaletea wanadamu dhambi na kifo

[Picha katika ukurasa wa 6]

Yehova aliandaa suluhisho kamilifu