Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Hofu Yehova na Kushika Amri Zake

Hofu Yehova na Kushika Amri Zake

Hofu Yehova na Kushika Amri Zake

“Hofu Mungu wa kweli na kushika amri zake. Maana kwa jumla huo ndio wajibu wa mtu wa mtu.”—MHUBIRI 12:13, NW.

1, 2. (a) Hofu inaweza kutulinda kimwili jinsi gani? (b) Kwa nini wazazi wenye hekima hujitahidi kusaidia watoto wao wasitawishe hofu inayofaa?

“UJASIRI huhatarisha maisha, nayo hofu huyalinda,” akasema Leonardo da Vinci. Ujasiri pasipo busara humzuia mtu asione hatari, lakini hofu humfanya mtu awe mwangalifu. Kwa mfano, tunapokaribia kwenye ukingo wa jabali na kuona umbali tunaoweza kuanguka, wengi wetu hujikuta tu tumerudi nyuma. Vivyo hivyo, hofu inayofaa hutusaidia tuwe na uhusiano mzuri na Mungu, kama tulivyojifunza katika makala iliyotangulia, na pia hutulinda na madhara.

2 Hata hivyo, mtu anahitaji kujifunza kusitawisha hofu ya hatari nyingi za kisasa. Kwa kuwa watoto wachanga hawaelewi hatari za umeme au za magari barabarani, wanaweza kupatwa na aksidenti mbaya sana. * Wazazi wenye hekima hujaribu kusaidia watoto wao wasitawishe hofu inayofaa, wakiwaonya mara kwa mara kuhusu hatari zinazowazunguka. Wazazi wanajua kwamba hofu hiyo inaweza kuwaokoa watoto wao.

3. Yehova hutuonya kuhusu hatari za kiroho jinsi gani na kwa nini?

3 Hivyo ndivyo Yehova huhangaikia hali yetu njema. Akiwa Baba mwenye upendo, anatufundisha kupitia Neno lake na tengenezo lake ili tujinufaishe. (Isaya 48:17) Programu hiyo ya mafundisho ya Mungu inatia ndani kutuonya “mara kwa mara” kuhusu hatari za kiroho ili tusitawishe hofu inayofaa kuelekea hatari hizo. (2 Mambo ya Nyakati 36:15, BHN; 2 Petro 3:1) Katika muda wote wa historia, misiba mingi ya kiroho na kuteseka kwingi kungeweza kuzuiwa ‘ikiwa watu wangekuwa na moyo wa kumhofu Mungu na kushika amri zake.’ (Kumbukumbu la Torati 5:29) Katika “nyakati [hizi] za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,” tunaweza kusitawishaje moyo wa kumhofu Mungu na kuepuka hatari ya kiroho?—2 Timotheo 3:1.

Jiepushe na Maovu

4. (a) Wakristo wapaswa kusitawisha chuki ya aina gani? (b) Yehova huonaje mwenendo wenye dhambi? (Ona kielezi-chini.)

4 Biblia hueleza kwamba “kumcha [“kumhofu,” NW] BWANA ni kuchukia uovu.” (Mithali 8:13) Kamusi moja ya Biblia yafafanua chuki hiyo kuwa ‘kukirihi watu na vitu visivyopendwa, vinavyokubalika, na ambavyo mtu hangependa kujihusisha navyo kamwe.’ Kwa hiyo, hofu ya kimungu inatia ndani kuchukia kabisa kila kitu ambacho ni kiovu machoni pa Yehova. * (Zaburi 97:10) Hofu hiyo hutuchochea tuache lililo ovu, kama vile sisi hujikuta tu tumeondoka kutoka kwenye ukingo wa jabali tunapohisi hatari. “Kwa kumcha [“kumhofu,” NW] BWANA watu hujiepusha na maovu,” yasema Biblia.—Mithali 16:6.

5. (a) Tunawezaje kuimarisha hofu yetu ya kimungu na kuchukia lililo ovu? (b) Historia ya taifa la Israeli inatufundisha nini kuhusiana na habari hii?

5 Tunaweza kuimarisha hofu hiyo inayofaa na kuchukia lililo ovu kwa kuchunguza matokeo mabaya ambayo bila shaka huletwa na dhambi. Biblia hutuhakikishia kwamba tutavuna kile tunachopanda—iwe tunapanda kulingana na mwili au kulingana na roho. (Wagalatia 6:7, 8) Kwa sababu hiyo Yehova anaeleza kinaganaga matokeo ya kupuuza amri zake na kuacha ibada ya kweli. Pasipo kulindwa na Mungu, taifa dogo na dhaifu la Israeli halingeweza kujilinda dhidi ya majirani wake wakatili na wenye nguvu. (Kumbukumbu la Torati 28:15, 45-48) Matokeo mabaya yaliyopata taifa la Israeli kwa sababu ya kutotii yaliandikwa kwa kirefu katika Biblia “kuwa onyo” ili tujifunze somo hilo na kusitawisha hofu ya kimungu.—1 Wakorintho 10:11.

6. Twaweza kufikiria mifano gani inayopatikana katika Maandiko tunapojifunza kuhusu hofu ya kimungu? (Ona kielezi-chini.)

6 Mbali na mambo yaliyolipata taifa la Israeli kwa ujumla, Biblia husimulia mambo yaliyowapata watu fulani waliokuwa na wivu, pupa, kiburi au waliojihusisha katika mwenendo usiofaa. * Baadhi ya watu hao walimtumikia Yehova kwa miaka mingi, lakini wakashindwa kumhofu Mungu ilipohitajika pindi fulani maishani mwao, walipatwa na matokeo mabaya. Kutafakari mifano hiyo inayopatikana katika Maandiko kwaweza kuimarisha azimio letu la kutofanya makosa kama hayo. Lingekuwa jambo lenye kusikitisha kama nini iwapo tungengoja hadi tupatwe na msiba ndipo tuzingatie shauri la Mungu! Kinyume na vile watu wengi wanavyoamini, si lazima upatwe na msiba—hasa kwa kutimiza tamaa za kibinafsi—ndio ujue ubaya wake.—Zaburi 19:7.

7. Yehova hualika nani katika hema yake ya mfano?

7 Sababu nyingine kubwa ya kusitawisha hofu ya kimungu ni ile tamaa ya kulinda uhusiano wetu pamoja na Mungu. Tunahofu kutompendeza Yehova kwa sababu tunathamini urafiki wetu pamoja naye. Ni nani anayeweza kuwa rafiki ya Mungu, na kualikwa katika hema yake ya mfano? Ni yule tu “aendaye kwa ukamilifu, na kutenda haki.” (Zaburi 15:1, 2) Ikiwa tunathamini uhusiano huo pamoja na Muumba wetu, tutakuwa waangalifu na kutembea kwa ukamilifu machoni pake.

8. Ni katika njia gani baadhi ya Waisraeli katika siku za Malaki walikosa kutilia maanani urafiki wao pamoja na Mungu?

8 Kwa kusikitisha, baadhi ya Waisraeli katika siku za Malaki hawakutilia maanani urafiki wao pamoja na Mungu. Badala ya kuhofu na kumheshimu Yehova, walitoa dhabihu za wanyama wagonjwa na vilema kwenye madhabahu yake. Pia mtazamo wao kuelekea ndoa ulionyesha kwamba hawakumhofu Mungu. Waliwataliki wake zao wa ujanani kwa sababu ndogondogo ili waoe wanawake wachanga. Malaki aliwaambia kwamba Yehova anachukia “talaka” na kwamba mtazamo wao wa hila uliwatenganisha na Mungu. Mungu angewezaje kukubali dhabihu zao huku madhabahu ikiwa imefunikwa kwa machozi ya mfano—machozi ya uchungu ya wake zao walioachwa? Kwa kutoheshimu kimakusudi viwango vyake, hali hiyo ilimfanya Yehova aulize hivi: “Hofu yangu i wapi?”—Malaki 1:6-8; 2:13-16.

9, 10. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunathamini kuwa rafiki za Yehova?

9 Vivyo hivyo, leo Yehova anaona jinsi wenzi wa ndoa na watoto wengi wasio na hatia wanavyoteseka sana kwa sababu ya kuachwa na waume au baba ama na wake na akina mama wenye ubinafsi na wasio na maadili. Bila shaka anahuzunishwa na jambo hilo. Mtu ambaye ni rafiki ya Mungu ataona mambo jinsi Mungu anavyoyaona na atajitahidi kuimarisha ndoa yake, na kuepuka maoni ya watu wa ulimwengu ambao hawaheshimu kifungo cha ndoa, na pia ‘ataukimbia uasherati.’—1 Wakorintho 6:18.

10 Katika ndoa na vilevile katika sehemu nyingine za maisha yetu, kuchukia lililo ovu machoni pa Yehova, na kuthamini sana kuwa rafiki zake, kutaleta kibali cha Yehova. Mtume Petro alisema hivi kwa uhakika: “Kwa hakika nahisi kwamba Mungu si mwenye ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye humhofu na kutenda uadilifu akubalika kwake.” (Matendo 10:34, 35) Tuna mifano mingi inayopatikana katika Maandiko ambayo inaonyesha jinsi hofu ya kimungu ilivyochochea watu fulani wafanye mambo yanayofaa chini ya hali mbalimbali zenye kujaribu.

Watu Watatu Waliomhofu Mungu

11. Abrahamu alitajwa kuwa mwenye ‘kumhofu Mungu’ chini ya hali gani?

11 Kuna mtu mmoja katika Biblia ambaye Yehova alimtaja kuwa rafiki yake—mzee wa ukoo Abrahamu. (Isaya 41:8) Hofu ya kimungu ya Abrahamu ilijaribiwa Mungu alipomtaka Abrahamu amtoe dhabihu mwana wake wa pekee, Isaka, ambaye kupitia kwake uzao wa Abrahamu ungekuwa taifa kubwa kwa utimizo wa ahadi ya Mungu. (Mwanzo 12:2, 3; 17:19) Je, “rafiki ya Yehova” angefaulu mtihani huo wenye kusononesha? (Yakobo 2:23) Wakati tu Abrahamu alipoinua kisu chake kumwua Isaka, malaika wa Yehova alisema: “Usimnyoshee kijana mkono wako, wala usimtendee neno; kwa maana sasa ninajua ya kuwa unamcha [“unamhofu,” NW] Mungu, iwapo hukunizuilia mwanao, mwanao wa pekee.”—Mwanzo 22:10-12.

12. Ni nini kilichomchochea Abrahamu amhofu Mungu, nasi twaweza kuonyeshaje mtazamo huo?

12 Ijapokuwa hapo awali Abrahamu alikuwa amethibitisha kwamba anamhofu Yehova, kwenye pindi hiyo alionyesha hofu hiyo kwa njia ya pekee. Nia yake ya kumtoa Isaka kuwa dhabihu ilionyesha mengi zaidi ya utii wenye staha. Abrahamu alimtumaini kabisa Baba yake wa kimbingu kwamba angetimiza ahadi Yake kwa kumfufua Isaka iwapo ingekuwa lazima. Kama alivyoandika Paulo, Abrahamu alikuwa ‘amesadikishwa kikamili kwamba jambo ambalo Mungu alikuwa ameahidi alikuwa na uwezo pia wa kufanya.’ (Waroma 4:16-21) Je, tuko tayari kufanya mapenzi ya Mungu hata tunapolazimika kujidhabihu sana? Je, tuna uhakika kamili kwamba utii huo utaleta manufaa ya kudumu, huku tukijua kwamba Yehova ni “mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii”? (Waebrania 11:6) Huko ndiko kumhofu Mungu kikweli.—Zaburi 115:11.

13. Kwa nini Yosefu angeweza kusema kwa kufaa kwamba alikuwa mtu ‘aliyemhofu Mungu wa kweli’?

13 Na tuchunguze mfano wa mtu mwingine aliyemhofu Mungu, yaani Yosefu. Akiwa mtumwa katika nyumba ya Potifa, sikuzote Yosefu alikabili mkazo wa kufanya uasherati. Yaonekana hangeweza kwa vyovyote kumkwepa mke wa bwana wake, aliyemtongoza daima. Hatimaye, ‘alipomshika,’ Yosefu ‘alikimbia nje.’ Ni nini kilichomchochea ajiepushe na uovu mara moja? Bila shaka, ni hofu ya kimungu, ile tamaa ya kuepuka kutenda ‘uovu huo mbaya na kumkosea Mungu.’ (Mwanzo 39:7-12, BHN) Kwa kufaa, Yosefu angeweza kusema kwamba alikuwa mtu ‘aliyemhofu Mungu wa kweli.’—Mwanzo 42:18, NW.

14. Yosefu alithibitishaje kupitia rehema yake kwamba alimhofu Mungu kikweli?

14 Miaka mingi baadaye, Yosefu alikutana uso kwa uso na nduguze waliomwuza utumwani bila huruma. Kwa sababu walikuwa na uhitaji mkubwa wa chakula, Yosefu angeweza kutumia fursa hiyo kulipiza kisasi kwa kosa walilomtendea. Lakini kutendea watu kikatili ni kutomhofu Mungu. (Mambo ya Walawi 25:43) Kwa hiyo, Yosefu alipopata uthibitisho wa kutosha kwamba nduguze walikuwa wamebadili maoni yao, aliwasamehe. Kama Yosefu, hofu yetu ya kimungu itatuchochea kushinda ubaya kwa wema, na vilevile itatuzuia tusishindwe na kishawishi.—Mwanzo 45:1-11; Zaburi 130:3, 4; Waroma 12:17-21.

15. Kwa nini mwenendo wa Yobu uliufurahisha moyo wa Yehova?

15 Yobu ni mfano mwingine wenye kutokeza wa mtu aliyemhofu Mungu. Yehova alimwambia hivi Ibilisi: “Je! umemwangalia huyo mtumishi wangu Ayubu [“Yobu,” NW]? kwa kuwa hapana mmoja aliye kama yeye duniani, mtu mkamilifu na mwelekevu, mwenye kumcha [“kumhofu,” NW] Mungu na kuepukana na uovu.” (Ayubu 1:8) Kwa miaka mingi, mwenendo wa Yobu usiolaumika uliufurahisha moyo wa Baba yake wa kimbingu. Yobu alimhofu Mungu kwa sababu alijua kwamba ni jambo linalofaa kufanya hivyo na hiyo ni njia bora ya maisha. “Tazama, kumcha [“kumhofu,” NW] Bwana ndiyo hekima, na kujitenga na uovu ndio ufahamu,” akasema Yobu. (Ayubu 28:28) Akiwa mwanamume aliyeoa, Yobu hakuvutiwa isivyofaa na wanawake wachanga, wala hakunuia kufanya uzinzi nao moyoni. Ijapokuwa alikuwa tajiri, hakutumainia utajiri, naye alijiepusha na kila namna ya ibada ya sanamu.—Ayubu 31:1, 9-11, 24-28.

16. (a) Yobu alionyeshaje fadhili-upendo? (b) Yobu alionyeshaje kwamba alikuwa mtu mwenye kusamehe?

16 Hata hivyo, kumhofu Mungu kunamaanisha kufanya yaliyo mema na vilevile kujiepusha na uovu. Kwa hiyo, Yobu aliwaonea huruma vipofu, vilema, na maskini. (Mambo ya Walawi 19:14; Ayubu 29:15, 16) Yobu alifahamu kwamba “anayekataa kumhurumia [“kumwonyesha fadhili-upendo,” NW] rafiki yake, anakataa kumcha [“kumhofu,” NW] Mungu mwenye nguvu.” (Ayubu 6:14, BHN) Kutoonyesha fadhili-upendo kunaweza kuwa sawa na kutosamehe, au kuweka kinyongo. Kwa mwelekezo wa Mungu, Yobu alisali kwa niaba ya rafikize watatu waliomsononesha sana. (Ayubu 42:7-10) Je, tunaweza kuonyesha mtazamo huo wa kusamehe mwabudu mwenzetu ambaye huenda alituudhi kwa njia fulani? Kusali kwa unyofu kwa niaba ya mtu aliyetukosea kunaweza kutusaidia sana tusimwekee kinyongo. Vitu vizuri alivyopata Yobu kwa sababu ya kumhofu Mungu vyatuonyesha kimbele ‘fadhili nyingi ambazo Yehova amewawekea wanaomhofu.’—Zaburi 31:19; Yakobo 5:11.

Jinsi Kumhofu Mungu Kunavyotofautiana na Kumhofu Mwanadamu

17. Twaweza kupatwa na nini kwa kuwahofu wanadamu, na kwa nini kufanya hivyo huonyesha kwamba hatufikirii wakati ujao?

17 Ingawa kumhofu Mungu kwaweza kutuchochea tufanye linalofaa, kumhofu mwanadamu kwaweza kudhoofisha imani yetu. Kwa sababu hiyo, Yesu alipokuwa akiwatia moyo mitume wake wawe wahubiri wa habari njema wenye bidii, aliwaambia hivi: “Msiwe wenye kuwahofu wale wauuao mwili lakini hawawezi kuiua nafsi; lakini badala ya hivyo mhofuni yeye awezaye kuangamiza vyote viwili nafsi na mwili katika Gehena.” (Mathayo 10:28) Kuhofu wanadamu huonyesha kwamba hatufikirii wakati ujao, kwa kuwa Yesu alisema kwamba wanadamu hawawezi kukatiza matazamio yetu ya wakati ujao. Isitoshe, tunamhofu Mungu kwa kuwa tunatambua nguvu zake kuu, zinapolinganishwa na nguvu duni za mataifa. (Isaya 40:15) Kama Abrahamu, tuna uhakika kamili katika nguvu za Yehova za kufufua watumishi Wake waaminifu. (Ufunuo 2:10) Kwa hiyo, tunasema kwa uhakika: “Ikiwa Mungu yuko upande wetu, nani atakayekuwa dhidi yetu?”—Waroma 8:31.

18. Yehova huwathawabishaje wale wanaomhofu?

18 Iwe mpinzani wetu ni mshiriki wa familia au mchokozi shuleni, tutaona kwamba “kumcha [“kumhofu,” NW] BWANA ni tumaini imara.” (Mithali 14:26) Tunaweza kusali kwa Mungu atupe nguvu, tukijua kwamba atatusikia. (Zaburi 145:19) Yehova hasahau kamwe wale wanaomhofu. Anatupa uhakikisho huu kupitia nabii wake Malaki: “Ndipo wale waliomcha [“waliomhofu,” NW] BWANA waliposemezana wao kwa wao. Naye BWANA akasikiliza, akasikia; na kitabu cha ukumbusho kikaandikwa mbele zake, kwa ajili ya hao waliomcha [“waliomhofu,” NW] BWANA, na kulitafakari jina lake.”—Malaki 3:16.

19. Ni aina zipi za hofu zitakazotoweka, lakini ni aina gani itakayodumu milele?

19 Hivi karibuni kila mtu duniani atamwabudu Yehova bila kuhofu wanadamu. (Isaya 11:9) Watu hawatahofu tena njaa, magonjwa, uhalifu, na vita. Lakini hofu ya kimungu itadumu milele huku watumishi wake waaminifu walio mbinguni na walio duniani wakiendelea kumpa staha, utii, na heshima anayostahili. (Ufunuo 15:4) Kwa sasa, sote na tuzingatie shauri lililopuliziwa la Solomoni: “Moyo wako usiwahusudu wenye dhambi; bali mche [“mhofu,” NW] BWANA mchana kutwa; maana bila shaka iko thawabu; na tumaini lako halitabatilika.”—Mithali 23:17, 18.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Baadhi ya watu wazima huacha kuhofu hatari kwa sababu kazi yao huwafanya wakabili hatari daima. Alipoulizwa ni kwa nini maseremala wengi hawana kidole kimoja, seremala mmoja ambaye amefanya kazi hiyo kwa muda mrefu alijibu hivi bila kusita: “Wao huacha kuhofu misumeno ya umeme inayokwenda kwa kasi.”

^ fu. 4 Yehova mwenyewe huchukizwa kabisa na maovu. Kwa mfano, andiko la Waefeso 4:29 linafafanua lugha mbaya kuwa “usemi uliooza.” Neno la Kigiriki “-liooza” larejezea kihalisi tunda, samaki, au nyama iliyooza. Neno hilo linaonyesha kinaganaga jinsi tunavyopaswa kuhisi kuhusu lugha chafu au ya matusi. Vivyo hivyo, katika Maandiko mara nyingi sanamu zinaitwa “mavi.” (Kumbukumbu la Torati 29:17; Ezekieli 6:9, NW) Kama vile tunavyochukia kabisa mavi au kinyesi, ndivyo Mungu anavyochukia kabisa kila namna ya ibada ya sanamu.

^ fu. 6 Kwa mfano, fikiria masimulizi yanayopatikana katika Maandiko kuhusu Kaini (Mwanzo 4:3-12); Daudi (2 Samweli 11:2–12:14); Gehazi (2 Wafalme 5:20-27); na Uzia (2 Mambo ya Nyakati 26:16-21).

Je, Unakumbuka?

• Tunajifunza kuchukia lililo ovu jinsi gani?

• Baadhi ya Waisraeli katika siku za Malaki walikosaje kutilia maanani urafiki wao pamoja na Yehova?

• Tunaweza kujifunza nini kuhusu hofu ya kimungu kutokana na Abrahamu, Yosefu, na Yobu?

• Ni hofu ya aina gani ambayo haitawahi kutoweka, na kwa nini?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 19]

Wazazi wenye hekima husaidia watoto wao wasitawishe hofu inayofaa

[Picha katika ukurasa wa 20]

Kama vile hofu hutufanya tuepuke hatari, hofu ya kimungu hutuepusha na lililo ovu

[Picha katika ukurasa wa 23]

Yobu alidumisha hofu yake ya kimungu hata alipokabiliana na marafiki watatu bandia

[Hisani]

Kutoka kwa tafsiri ya Biblia ya Vulgata Latina, 1795