Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ile Kanuni Bora—Ni Fundisho la Ulimwenguni Pote

Ile Kanuni Bora—Ni Fundisho la Ulimwenguni Pote

Ile Kanuni Bora—Ni Fundisho la Ulimwenguni Pote

“Kwa hiyo, mambo yote mtakayo watu wawafanyie nyinyi, lazima mwafanyie wao pia hivyohivyo.”—Mathayo 7:12.

MANENO hayo yalisemwa na Yesu Kristo miaka ipatayo elfu mbili iliyopita katika Mahubiri yake maarufu ya Mlimani. Katika karne zilizofuata, mengi yamesemwa na kuandikwa kuhusu maneno hayo sahili. Kwa mfano, yamesifiwa kuwa “maneno yaliyo muhimu zaidi katika Maandiko,” “maelezo mafupi ya daraka la Mkristo kwa jirani yake,” na “kanuni ya msingi ya maadili.” Maneno hayo ni maarufu sana hivi kwamba mara nyingi yanarejezewa kuwa Kanuni Bora.

Hata hivyo, Kanuni hiyo Bora haifuatwi tu katika nchi zinazodai kuwa za Kikristo. Dini ya Wayahudi, Ubudha, na falsafa ya Wagiriki zilifafanua kanuni hii muhimu ya maadili kwa njia mbalimbali. Watu wa Mashariki ya Mbali wanajua sana maneno yaliyosemwa na Confucius ambaye amesifiwa katika nchi za Mashariki kuwa mwalimu mkuu na mtu mwenye hekima nyingi. Maneno hayo yametajwa mara tatu katika kitabu The Analects, ambacho ni cha tatu kati ya vile Vitabu Vinne vya Confucius. Confucius alisema hivi mara mbili alipokuwa akijibu maswali ya wanafunzi wake: “Yale ambayo hutaki ufanyiwe, usiwafanyie wengine.” Pindi moja, mwanafunzi wake Zigong alisema maneno haya kwa majivuno, “Yale ambayo sitaki wengine wanifanyie, mimi siwafanyii.” Mwalimu huyo alimjibu kwa maneno haya yenye kuamsha fikira: “Ndiyo, lakini huwezi kufanya unavyosema.”

Unaposoma maneno ya Confucius unaweza kuona kwamba yanaonyesha wazo la kutendewa, kinyume na maneno ambayo Yesu alisema baadaye. Tofauti iliyo wazi ni kwamba Kanuni Bora iliyotajwa na Yesu hutaka mtu awatendee wengine mema. Hapana shaka kwamba ulimwengu wa sasa ungekuwa mahali pazuri sana kama watu wangetenda kupatana na maneno hayo ya Yesu kwa kuwajali wengine, kuchukua hatua kuwasaidia, na kuishi kupatana na kanuni hiyo kila siku.

Hata kanuni hiyo iwe inaleta wazo la kutendea, kutendewa, au wazo lolote lile, kilicho muhimu ni kwamba watu wa malezi mbalimbali na walioishi nyakati tofauti na katika maeneo tofauti, wameitumamini sana Kanuni hiyo Bora. Jambo hili linaonyesha kwamba maneno ya Yesu katika Mahubiri ya Mlimani ni fundisho la ulimwenguni pote linaloathiri maisha ya watu kipindi chochote kile, mahali popote pale.

Jiulize: ‘Je, ningependa kutendewa kwa heshima, bila ubaguzi, na kwa unyofu? Je, ningependa kuishi katika ulimwengu usio na ubaguzi wa rangi, uhalifu, na vita? Je, ningependa kuishi katika familia ambayo kila mtu anajali hisia na hali njema ya wengine?’ Ni nani kwa kweli asingependa hali kama hizo? Lakini ukweli ni kwamba watu wachache sana ndio hufurahia hali hizo. Watu walio wengi hawawezi hata kutarajia kufurahia hali kama hizo.

Kanuni Bora Yapotoshwa

Katika historia yote, wanadamu wametendewa vibaya na haki zao kupuuzwa kabisa. Vitendo hivyo vinatia ndani biashara ya watumwa kutoka Afrika, watu kuuawa katika kambi za Nazi, kulazimisha watoto wafanye kazi ya kuajiriwa, na mauaji makubwa ya kinyama katika sehemu mbalimbali. Kuna vitendo vingine vingi vibaya ambavyo havijatajwa hapa.

Leo, ulimwengu wetu ulioendelea sana kitekinolojia una ubinafsi. Watu wachache huwafikiria wengine wakati hali yao njema au zile wanazodhania kuwa haki zao zinapokuwa hatarini. (2 Timotheo 3:1-5) Kwa nini watu wengi sana wamekuwa na ubinafsi, wakatili, na wasiojali? Je, si kwa sababu Kanuni Bora, ingawa inajulikana sana, inapuuzwa, ikionwa kuwa ya zamani na isiyofaa? Inasikitisha kwamba hata wengi wanaodai kumwamini Mungu wanaipuuza pia. Na kulingana na vile hali ilivyo, watu watazidi tu kuwa na ubinafsi.

Kwa hiyo, masuala muhimu yanayopaswa kufikiriwa ni: Inamaanisha nini kuishi kupatana na Kanuni Bora? Je, kuna yeyote ambaye bado anaishi kupatana na kanuni hiyo? Na je, kuna wakati ambapo watu wote wataishi kupatana na Kanuni hiyo Bora? Ili upate majibu ya kweli kwa maswali hayo, tafadhali soma makala inayofuata.

[Picha katika ukurasa wa 3]

Confucius na wengineo walifundisha Kanuni Bora kwa njia mbalimbali