Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Je, agizo la Mungu katika andiko la Yeremia 7:16 linamaanisha kwamba Wakristo hawapaswi kusali kwa ajili ya mtu ambaye ametengwa na kutaniko la Kikristo kwa kuwa yeye ni mtenda-dhambi asiyetubu?

Baada ya kuwahukumu watu wa Yuda wasio waaminifu, Yehova alimwambia hivi Yeremia: “Wewe usiwaombee watu hawa, wala usiwapazie sauti yako, wala kuwaombea dua, wala usinisihi kwa ajili yao; kwa maana sitakusikiliza.”—Yeremia 7:16.

Kwa nini Yehova alimkataza Yeremia asiwaombee Waisraeli? Ni wazi kwamba alifanya hivyo kwa sababu walivunja Sheria yake kimakusudi. Walikuwa ‘wanaiba, kuua, kuzini, na kuapa kwa uongo, na kumfukizia Baali uvumba, na kuifuata miungu mingine’ waziwazi bila aibu. Kwa sababu hiyo, Yehova aliwaambia hivi Wayahudi hao wasio na imani: “Nitawatupa ninyi mbali na macho yangu, kama nilivyowatupa ndugu zenu wote, yaani, wazao wote wa Efraimu.” Bila shaka, haingefaa kwa Yeremia, au kwa mtu mwingine yeyote, kumwomba Yehova abadilishe hukumu Yake.—Yeremia 7:9, 15.

Kupatana na jambo hilo, mtume Yohana aliandika kuhusu sala ambayo Mungu husikia. Kwanza, aliwahakikishia hivi Wakristo: “Hata iwe ni nini ambacho twaomba kulingana na mapenzi yake, yeye hutusikia.” (1 Yohana 5:14) Kisha, kuhusu kusali kwa ajili ya wengine, Yohana anaendelea kusema: “Yeyote akiona ndugu yake anafanya dhambi, dhambi ambayo haipasishi kifo, ataomba, na yeye atampa uhai, ndiyo, kwa wale ambao hawafanyi dhambi hata kupasisha kifo. Kuna dhambi ambayo yapasisha kifo. Ni kuhusu dhambi hiyo kwamba simwambii afanye ombi.” (1 Yohana 5:16) Yesu pia alitaja dhambi ambayo ‘haitasamehewa,’ yaani, dhambi dhidi ya roho takatifu.—Mathayo 12:31, 32.

Je, hilo linamaanisha kwamba wote wale wanaotengwa na kutaniko la Kikristo kwa kufanya dhambi bila kutubu wamefanya dhambi ambazo ‘zinapasisha kifo,’ na hivyo hatupaswi kusali kwa ajili yao? Haipasi kuwa hivyo kwa sababu dhambi nyingine hazipasishi kifo. Kwa kweli, ni vigumu kujua kama zinapasisha kifo. Dhambi za Mfalme Manase ni mfano mzuri. Alijenga madhabahu kwa miungu isiyo ya kweli, akawatoa wanawe dhabihu, akawasiliana na roho, na kuweka mifano ya kuchongwa katika hekalu la Yehova. Hata Biblia inasema kwamba Manase na watu ‘walifanya mabaya, kuliko mataifa BWANA aliowaharibu mbele za wana wa Israeli.’ Kwa sababu ya dhambi hizo zote, Yehova alimwadhibu Manase kwa kumpeleka Babiloni akiwa mateka, huku ametiwa pingu.—2 Wafalme 21:1-9; 2 Mambo ya Nyakati 33:1-11.

Ingawa dhambi za Manase zilikuwa nzito sana, je, zilikuwa dhambi zinazopasisha kifo? Yaonekana la, kwa kuwa masimulizi hayo yanaendelea kusema: “Hata alipokuwa katika taabu, akamsihi BWANA, Mungu wake, akajinyenyekeza sana mbele za Mungu wa baba zake. Akamwomba; naye akamtakabali, akayasikia maombi yake; akamrudisha tena Yerusalemu katika ufalme wake. Ndipo Manase akajua ya kwamba BWANA ndiye Mungu.”—2 Mambo ya Nyakati 33:12, 13.

Hivyo, hatupaswi kukata kauli kwamba ni lazima mtu awe ametenda dhambi inayopasisha kifo kwa sababu tu ametengwa na kutaniko. Huenda muda ukapita kabla ya kujua hali halisi ya moyoni ya mtu huyo. Mara nyingi mojawapo ya sababu zinazotolewa za kutenga mtenda-dhambi ni kumfanya arudiwe na fahamu, ikitarajiwa kwamba atatubu na kugeuka kabisa.

Kwa kuwa mtu huyo hayumo kutanikoni, huenda badiliko lolote la moyo au la mtazamo likaonekana kwanza na wale walio karibu naye, kama vile mwenzi wa ndoa au watu wa familia. Huenda wale wanaoona mabadiliko hayo wakakata kauli kwamba mtenda-dhambi huyo hakufanya dhambi inayopasisha kifo. Huenda wakachochewa kusali ili mtenda-dhambi apate nguvu kutoka kwa Neno la Mungu lililopuliziwa. Huenda pia wakasali ili Yehova amtendee kulingana na mapenzi Yake.—Zaburi 44:21; Mhubiri 12:14.

Ingawa wengine wanaweza kuona uthibitisho wa kutosha kwamba mtenda-dhambi ametubu, huenda washiriki wa kutaniko kwa ujumla wasiweze kuona jambo hilo. Wanaweza kushangaa, kuwa na wasiwasi, na hata kukwazika wakisikia mtu akisali hadharani kwa ajili ya mtenda-dhambi huyo. Kwa sababu hiyo, wale wanaochochewa kusali kwa ajili ya mtenda-dhambi wanapaswa kufanya hivyo faraghani, na kuacha mambo mengine yanayohusiana na mtenda-dhambi huyo mikononi mwa wazee wa kutaniko waliohusika.

[Picha katika ukurasa wa 31]

Manase alisamehewa dhambi zake nzito alipojinyenyekeza mbele za Yehova

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 30]

Reproduced from Illustrirte Pracht - Bibel/Heilige Schrift des Alten und Neuen Testaments, nach der deutschen Uebersetzung D. Martin Luther’s