Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Dawa ya Macho ya Kusugua Katika Macho Yako”

“Dawa ya Macho ya Kusugua Katika Macho Yako”

“Dawa ya Macho ya Kusugua Katika Macho Yako”

DAWA hiyo ilipendekezwa na Yesu Kristo kwa kutaniko la Wakristo wa karne ya kwanza huko Laodikia, Asia Ndogo.

Yesu alisema: ‘Nunua dawa ya macho ya kusugua katika macho yako ili upate kuona.’ Kwa hiyo upofu wa kiroho ndio uliohitaji kutibiwa, bali si ugonjwa wa macho halisi. Wakristo walioishi Laodikia walikuwa wameathiriwa na mtazamo wa jiji hilo lenye ufanisi wa vitu vya kimwili na wakaacha kujishughulisha na mahitaji yao halisi ya kiroho.

Akieleza kwamba jambo hilo ndilo lililofanya waache kuona vizuri kiroho, Yesu alisema: “Wasema: ‘Mimi ni tajiri na nimejipatia utajiri na sihitaji kitu chochote hata kidogo,’ lakini hujui wewe ni mwenye taabu na wa kusikitikiwa na maskini na kipofu na uchi.” Hata ingawa hawakujua, washiriki wa kutaniko walihitaji “dawa ya macho” yenye kuponya ambayo ingeweza kupatikana tu kwa kukubali mafundisho na nidhamu ya Yesu Kristo. ‘Nunueni kutoka kwangu,’ akasema Yesu.—Ufunuo 3:17, 18.

Kama ilivyokuwa kwa Walaodikia, Wakristo wa kweli leo wanahitaji kujilinda dhidi ya kuathiriwa isivyofaa, labda pasipo kujua, na mtazamo uliopo wa kufuatia vitu vya kimwili na anasa. Dawa ya kudumisha mtazamo unaofaa wa kiroho inaonyeshwa katika shauri hili: ‘Nunua kutoka kwa Yesu dawa ya macho ya kusugua katika macho yako ili upate kuona.’

Jambo linalofaa kufikiriwa ni kwamba ‘dawa hii ya macho ya kusugua,’ inapaswa kununuliwa. Inagharimu kitu fulani. Lazima mtu atumie wakati kujifunza na kutafakari Neno la Mungu. Mtunga-zaburi atuhakikishia kwamba Neno hilo ni “safi, huyatia macho [ya kiroho] nuru.”—Zaburi 19:8.