Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unakumbuka?

Je, Unakumbuka?

Je, Unakumbuka?

Je, umefurahia kusoma matoleo ya hivi karibuni ya Mnara wa Mlinzi? Ona kama unaweza kujibu baadhi ya maswali yafuatayo:

Mahakama ya Jimbo ya Ujerumani ilichangiaje ushindi wa kisheria unaohusu dini?

Mahakama hiyo ilibatilisha uamuzi usiofaa wa mahakama nyingine uliohusu Mashahidi wa Yehova na kule kutambuliwa kwao kisheria kuwa shirika la kidini. Uamuzi huo wa ushindi ulitangaza kwamba mtu anaweza ‘kutii imani ya kidini’ zaidi ya sheria ya Serikali pasipo kukiuka uhuru wa ibada.—8/15, ukurasa wa 8.

Yobu aliteseka kwa muda mrefu kadiri gani?

Kitabu cha Ayubu hakionyeshi muda alioteseka. Huenda mateso ya Yobu na kukomeshwa kwa mateso hayo kulichukua muda wa miezi michache, labda muda unaopungua mwaka mmoja.—8/15, ukurasa wa 31.

Kwa nini twaweza kuwa na uhakika kwamba Ibilisi si ushirikina tu?

Yesu Kristo alijua kwamba Ibilisi alikuwa kiumbe halisi. Yesu alishawishiwa na kiumbe halisi, bali si uovu fulani uliokuwa ndani yake. (Mathayo 4:1-11; Yohana 8:44; 14:30)—9/1, ukurasa wa 5-6.

Andiko la Mithali 10:15 husema: “Mali ya mtu tajiri ni mji wake wa nguvu; uangamivu wa maskini ni umaskini wao.” Andiko hilo limethibitikaje kuwa la kweli?

Kama vile mji uliozingirwa kwa ukuta huandaa usalama wa kiasi fulani kwa watu wanaoishi humo, ndivyo mali inavyoweza kuwa ulinzi dhidi ya mambo fulani maishani yanayoweza kutokea pasipo kutarajiwa. Kwa upande mwingine, umaskini unaweza kutokeza madhara, mambo fulani yasiyotarajiwa yanapotokea.—9/15, ukurasa wa 24.

Ni katika maana gani watu walianza “kuliitia jina la BWANA [“Yehova,” NW]” katika siku za Enoshi? (Mwanzo 4:26)

Jina la Mungu lilikuwa limetumiwa tangu kuumbwa kwa mwanadamu; kwa hiyo, watu walipoanza kuliitia jina la Yehova katika siku za Enoshi, hawakufanya hivyo kwa imani. Huenda watu walikufuru kwa kujiita Yehova au kuwaita watu wengine jina hilo, wakisingizia kuwa wanamwabudu Mungu kupitia watu hao.—9/15, ukurasa wa 29.

Neno “nidhamu” linamaanisha nini kama linavyotumiwa katika Biblia?

Neno hilo halirejezei dhuluma au ukatili wa namna yoyote. (Mithali 4:13; 22:15) Neno la Kigiriki lililotafsiriwa “nidhamu” lahusiana hasa na maagizo, elimu, kusahihisha na nyakati nyingine, karipio thabiti lakini lenye upendo. Njia kuu ambayo wazazi wanaweza kumwiga Yehova ni kwa kujitahidi kudumisha mawasiliano na watoto wao. (Waebrania 12:7-10)—10/1, ukurasa wa 8, 10.

Wakristo wa kweli leo huonyeshaje kwamba wanaunga mkono utawala wa Mungu?

Wanapotetea Ufalme wa Mungu, Mashahidi wa Yehova hawajihusishi na siasa wala hawachochei uasi dhidi ya serikali, hata katika nchi ambapo wamepigwa marufuku. (Tito 3:1) Kama vile Yesu na wanafunzi wake wa mapema walivyofanya, Mashahidi hujitahidi kusaidia watu wafuate kanuni zinazofaa za Biblia, kama vile unyofu, usafi wa kiadili, na mazoea mazuri ya kazi.—10/15, ukurasa wa 6.

Maji ya uhai yanatiririkaje katika Milima ya Andes?

Mashahidi wa Yehova katika eneo hilo wanajitahidi kuwapelekea watu kweli za Biblia, hata katika lugha mbili zinazozungumzwa huko, za Quechua na Aymara. Mashahidi huwatembelea watu wanaoishi katika visiwa vya Ziwa Titicaca, kutia ndani visiwa “vinavyoelea” vilivyojengwa kwa nyasi ndefu zinazokua katika ziwa hilo.—10/15, ukurasa wa 8-10.

Mungu ametupatia kitu gani cha kutuongoza ambacho chaweza kulinganishwa na kompyuta zinazoongoza ndege za kisasa za kubeba abiria?

Mungu amewapa wanadamu uwezo wa kujiongoza kiadili, uwezo wa kupambanua mema na mabaya, yaani dhamiri tuliyorithi. (Waroma 2:14, 15)—11/1, ukurasa wa 3-4.

Kwa nini kifo cha Yesu kina thamani kubwa?

Mwanadamu mkamilifu Adamu alipofanya dhambi, alipoteza uhai wake na wa wazao wake. (Waroma 5:12) Akiwa mwanadamu mkamilifu, Yesu alidhabihu uhai wake wa kibinadamu, na kwa njia hiyo kuandaa fidia inayowawezesha wanadamu waaminifu wapate uhai udumuo milele.—11/15, ukurasa wa 5-6.

Wasikithe wanaotajwa katika andiko la Wakolosai 3:11 ni nani?

Wasikithe walikuwa watu wenye kuhama-hama waliomiliki nyika za Asia na Ulaya, kuanzia mwaka wa 700 hivi hadi 300 K.W.K. Walikuwa wapanda-farasi na wapiganaji wenye kutisha. Huenda andiko la Wakolosai 3:11 halikurejezea taifa fulani hususa bali watu wasio na ustaarabu kabisa.—11/15, ukurasa wa 24-25.

Kwa nini tunaweza kusema kwamba twapaswa kuzingatia kwa ukawaida ile Kanuni Bora?

Kanuni hii muhimu ya maadili imefafanuliwa na Dini ya Wayahudi, Ubudha, falsafa ya Wagiriki, na Ukonfyushasi. Hata hivyo, mambo aliyosema Yesu katika Mahubiri ya Mlimani hutaka watu wawatendee wengine mema, nayo huathiri maisha ya watu wa kila umri wanaoishi kila mahali. (Mathayo 7:12)—12/1, ukurasa wa 3.