Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kitulizo Kinachofaa cha Mkazo

Kitulizo Kinachofaa cha Mkazo

Kitulizo Kinachofaa cha Mkazo

“Njoni kwangu, nyinyi nyote mnaomenyeka na kulemezwa mizigo, nami hakika nitawaburudisha nyinyi.”—MATHAYO 11:28.

1, 2. (a) Biblia ina nini kinachosaidia kupunguza mkazo unaopita kiasi? (b) Mafundisho ya Yesu yalikuwa na matokeo gani?

YAELEKEA utakubali kwamba mkazo mwingi unatokeza matatizo. Biblia husema kwamba uumbaji wote wa kibinadamu una matatizo mengi sana hivi kwamba wengi wanangojea kwa hamu kuwekwa huru kutokana na maisha ya sasa yenye mikazo mingi. (Waroma 8:20-22) Lakini Maandiko yanaonyesha pia kwamba tunaweza kupata kitulizo kikubwa kutokana na matatizo ya wakati huu. Tunaweza kupata kitulizo hicho kwa kufuata ushauri na kielelezo cha mwanamume mmoja kijana aliyeishi karne 20 zilizopita. Alikuwa seremala, hata hivyo, alipenda watu kuliko kazi yake ya useremala. Alivutia mioyo ya watu, akashughulikia mahitaji yao, akawasaidia waliokuwa dhaifu, na kuwafariji walioshuka moyo. Isitoshe, aliwasaidia wengi wafanye maendeleo ya kiroho. Hivyo wakapata kitulizo kutokana na mkazo unaopita kiasi. Wewe pia unaweza kupata kitulizo.—Luka 4:16-21; 19:47, 48; Yohana 7:46.

2 Mtu huyo, Yesu Mnazareti, hakuongozwa na elimu ya juu ya kilimwengu ambayo wengi walitafuta huko Roma ya kale, Athene, au Aleksandria. Hata hivyo, mafundisho yake yanajulikana sana. Kichwa cha mafundisho hayo kilikuwa: serikali ambayo Mungu atatumia kuitawala dunia kwa mafanikio. Yesu pia alieleza kanuni za msingi za maisha—kanuni ambazo kwa kweli zina manufaa leo. Wale wanaojifunza na kufuata mafundisho ya Yesu hunufaika sasa na hupata kitulizo kutokana na mkazo unaopita kiasi. Je, ungependa kupata kitulizo hicho?

3. Yesu alitoa mwaliko gani wenye kuvutia?

3 Huenda ukawa na shaka. ‘Je, mtu aliyeishi zamani sana hivyo anaweza kuathiri maisha yangu sasa?’ Hebu sikiliza maneno ya Yesu yenye kuvutia: “Njoni kwangu, nyinyi nyote mnaomenyeka na kulemezwa mizigo, nami hakika nitawaburudisha nyinyi. Chukueni nira yangu juu yenu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mwenye tabia-pole na wa hali ya chini moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili ya nafsi zenu. Kwa maana nira yangu ni ya fadhili na mzigo wangu ni mwepesi.” (Mathayo 11:28-30) Alimaanisha nini? Na tuchunguze maneno haya kwa undani zaidi tuone jinsi yanavyoweza kutusaidia kupata kitulizo kutokana na mkazo wenye kulemea.

4. Yesu alizungumza na nani, na kwa nini ingeweza kuwa vigumu kwa wasikilizaji wake kufanya yale aliyotaka wafanye?

4 Yesu alizungumza na wengi waliokuwa wanajitahidi kuifuata sheria lakini wakawa ‘wamelemezwa mizigo’ kwa sababu viongozi Wayahudi walifanya dini iwe kitu chenye kuchosha. (Mathayo 23:4) Walikazia fikira sheria nyingi zilizohusu karibu kila sehemu ya maisha. Je, haichoshi sikuzote kusikia maneno “usifanye” hili wala lile? Kinyume cha hilo, mwaliko wa Yesu ungewaongoza watu waliomsikiliza kwenye ile kweli, uadilifu, na maisha bora. Naam, kumjua Mungu wa kweli kulitia ndani kumsikiliza Yesu Kristo, kwa kuwa kupitia yeye wanadamu wangeweza—na wanaweza—kufahamu jinsi Yehova alivyo. Yesu alisema: “Yeye ambaye ameniona mimi amemwona Baba pia.”—Yohana 14:9.

Je, Maisha Yako Yana Mkazo Unaopita Kiasi

5, 6. Hali za kazi na mishahara ya wakati wa Yesu zilikuwaje zikilinganishwa na zetu leo?

5 Unaweza kuwa na mkazo kwa sababu kazi yako au hali ya familia yako inakulemea sana. Au madaraka mengine yanaweza kuonekana kuwa yenye kulemea. Ikiwa ndivyo ilivyo, basi hali yako ni kama ya watu wanyofu ambao Yesu alikutana nao na kuwasaidia. Kwa mfano, fikiria tatizo la kupata riziki. Wengi hupambana na tatizo hilo leo, kama vile wengi walivyofanya wakati wa Yesu.

6 Wakati huo wa Yesu, kibarua alifanya kazi ngumu kwa muda wa saa 12 kwa siku, siku 6 kwa juma, naye kwa kawaida alilipwa dinari moja kwa kazi ya siku nzima. (Mathayo 20:2-10) Hebu linganisha mshahara huo na mshahara wako au wa rafiki zako? Inaweza kuwa vigumu kulinganisha mishahara ya zamani na ya leo. Njia moja ya kufanya hivyo ni kufikiria vitu ambavyo pesa zinaweza kununua. Msomi mmoja anasema kwamba wakati wa Yesu mkate mmoja uliookwa kwa vikombe vinne vya unga wa ngano uligharimu mshahara wa kazi ya muda wa saa nzima. Msomi mwingine anasema kwamba kikombe kimoja cha divai nzuri kiligharimu mshahara wa kazi ya muda wa saa mbili hivi. Kutokana na habari hizo, unaweza kuona kwamba wakati huo watu walifanya kazi ngumu kwa muda wa saa nyingi ili wapate riziki. Walihitaji kitulizo na burudisho kama sisi. Ikiwa umeajiriwa, huenda ukahisi umekazwa kufanya kazi yenye matokeo zaidi. Mara nyingi hatupati wakati wa kufanya maamuzi yaliyofikiriwa vizuri. Huenda ukakubali kwamba unataka sana kupata kitulizo.

7. Watu waliitikiaje ujumbe wa Yesu?

7 Ni wazi kwamba mwaliko wa Yesu kwa wale wote ‘wanaomenyeka na kulemezwa mizigo’ ulivutia sana wasikilizaji wengi wakati huo. (Mathayo 4:25; Marko 3:7, 8) Kumbuka kwamba Yesu aliongeza ahadi hii, “nami hakika nitawaburudisha nyinyi.” Ahadi hiyo bado inatumika leo. Inaweza kutumika kwetu iwapo ‘tunamenyeka na kulemezwa mizigo.’ Na pia inaweza kutumika kwa wapendwa wetu, ambao yaelekea hali zao ni kama hizo.

8. Kulea watoto na uzee huzidishaje mkazo?

8 Kuna mambo mengine yanayowalemea watu. Kulea watoto ni jambo gumu sana. Hata kuwa mtoto kunaweza kuwa jambo gumu. Idadi inayozidi kuongezeka ya watu wa umri wote wanapatwa na magonjwa ya kimwili na ya kiakili. Na ingawa huenda watu wakaishi kwa muda mrefu zaidi, walio wazee wanakabili matatizo ya pekee, licha ya maendeleo ambayo yamefanywa kuhusiana na mambo ya kitiba.—Mhubiri 12:1.

Kufanya Kazi Chini ya Nira

9, 10. Hapo zamani nira ilikuwa ishara ya nini, na kwa nini Yesu aliwaalika watu wachukue nira yake?

9 Je, uliona kwamba katika maneno yaliyonukuliwa kutoka katika andiko la Mathayo 11:28, 29, Yesu alisema: “Chukueni nira yangu juu yenu na mjifunze kutoka kwangu.” Wakati huo, huenda mtu wa kawaida alihisi kana kwamba alifanya kazi chini ya nira. Tangu zamani, nira ilikuwa ishara ya utumwa. (Mwanzo 27:40; Mambo ya Walawi 26:13; Kumbukumbu la Torati 28:48) Wengi wa vibarua ambao Yesu alikutana nao walitumia nira halisi kubebea mizigo mizito kwenye mabega yao. Nira ingeweza kubebeka kwa urahisi au kuchubua shingo na mabega ikitegemea jinsi ilivyotengenezwa. Kwa kuwa Yesu alikuwa seremala, huenda alitengeneza nira, na alijua jinsi ya kutengeneza nira “ya fadhili.” Labda alifunga kwa ngozi au vipande vya nguo sehemu za nira ambazo ziligusana na mwili ili kuifanya iwe rahisi zaidi kubebeka.

10 Yesu aliposema, “Chukueni nira yangu juu yenu,” huenda alikuwa akijifananisha na mtu aliyeuza nira zilizotengenezwa vizuri ambazo zingekuwa zenye “fadhili” kwa shingo na mabega ya mfanyakazi. Hivyo, Yesu aliongeza kusema: “Mzigo wangu ni mwepesi.” Hilo lilimaanisha kwamba nira hiyo ilikuwa rahisi kubeba, nayo kazi haikuwa ya kitumwa. Ni kweli kwamba kwa kuwaalika wasikilizaji wake wakubali nira yake, Yesu hakuwa akitoa kitulizo cha papo hapo kutokana na hali zote zenye kulemea wakati huo. Hata hivyo, maoni yake tofauti kuhusu nira yangeleta burudisho kubwa. Kurekebisha mtindo wa maisha yao na njia yao ya kufanya mambo kungewaletea kitulizo pia. Jambo lililo muhimu zaidi ni kwamba tumaini hakika na lenye nguvu lingesaidia kupunguza mkazo katika maisha yao.

Unaweza Kupata Burudisho

11. Kwa nini Yesu hakuwa akipendekeza tu ubadilishaji nira?

11 Tafadhali ona kwamba, Yesu hakusema kwamba watu wangebadilisha nira yao. Roma ilikuwa bado inatawala nchi hiyo, kama vile serikali za leo zinavyotawala nchi ambako Wakristo wanaishi. Kodi iliyotozwa na Waroma katika karne ya kwanza haingeondolewa. Magonjwa na matatizo ya kiuchumi yangeendelea kuwepo. Hali ya kutokamilika na dhambi zingeendelea kuathiri watu. Hata hivyo, wangepata burudisho kwa kukubali mafundisho ya Yesu. Sisi pia tunaweza kupata burudisho kwa kufanya hivyo.

12, 13. Yesu alikazia jambo gani ambalo lingeleta burudisho, na wengine waliitikiaje?

12 Matumizi muhimu na yaliyo wazi ya mfano wa Yesu wa nira yalihusiana na kazi ya kufanya wanafunzi. Hapana shaka kwamba kazi kuu aliyofanya Yesu ni kuwafundisha wengine, huku akikazia Ufalme wa Mungu. (Mathayo 4:23) Kwa hiyo aliposema, “Chukueni nira yangu juu yenu,” hapana shaka kwamba kuchukua nira yake kungemaanisha kufanya kazi hiyohiyo. Maandishi ya Injili yanaonyesha kwamba Yesu alichochea watu wanyofu wabadili kazi zao, ambazo zilionwa na wengi kuwa muhimu sana maishani. Kumbuka mwito wake kwa Petro, Andrea, Yakobo, na Yohana: “Nifuateni, nami nitawafanya nyinyi kuwa wavuvi wa watu.” (Marko 1:16-20) Aliwaonyesha wavuvi hao jinsi ambavyo wangeridhika kama wangefanya kazi aliyotanguliza maishani mwake, wakifanya hivyo chini ya mwongozo na msaada wake.

13 Baadhi ya Wayahudi waliomsikiliza walielewa mafundisho ya Yesu na kuyafuata. Hebu wazia mambo yaliyokuwa yakifanyika kando ya bahari kama tunavyosoma kwenye Luka 5:1-11. Wavuvi wanne walikuwa wamemenyeka usiku kucha lakini hawakuvua samaki wowote. Kwa ghafula nyavu zao zikajaa! Jambo hilo halikutokea tu lenyewe; Yesu ndiye aliyelisababisha. Walipotazama ufuoni, waliona watu wengi waliopendezwa sana na mafundisho ya Yesu. Jambo hilo liliwasaidia kuelewa yale Yesu aliyowaambia wavuvi hao wanne: ‘Tangu sasa na kuendelea mtakuwa mkivua watu wakiwa hai.’ Waliitikiaje? “Wakarudisha hizo mashua kwenye nchi kavu, na kuacha kila kitu wakamfuata.”

14. (a) Tunawezaje kupata burudisho leo? (b) Yesu alitangaza habari njema zipi zenye kuburudisha?

14 Hata wewe unaweza kuitikia vivyo hivyo. Kazi ya kufundisha watu kweli ya Biblia bado inaendelea. Mashahidi wa Yehova wapatao milioni sita ulimwenguni pote wamekubali mwaliko wa Yesu wa ‘kuchukua nira yake juu’ yao, nao wamekuwa “wavuvi wa watu.” (Mathayo 4:19) Wengine hufanya kazi hiyo wakati wote; huku wengine wakiifanya kulingana na uwezo wao. Wote wanaburudishwa na kazi hiyo, kwa hiyo maisha yao hayana mkazo sana. Kazi hiyo inahusisha kufanya jambo wanalofurahia, yaani, kuwahubiria wengine habari njema—“habari njema za ufalme.” (Mathayo 4:23) Sikuzote inafurahisha kuzungumza kuhusu habari njema, hasa habari njema za ufalme. Biblia ina habari za msingi tunazohitaji ili kuwasadikisha wengi kwamba wanaweza kuishi maisha yasiyo na mkazo mwingi.—2 Timotheo 3:16, 17.

15. Unaweza kunufaikaje na mafundisho ya Yesu kuhusu maisha?

15 Kwa kadiri fulani, hata watu ambao wameanza kujifunza juu ya Ufalme wa Mungu hivi karibuni wamenufaika na mafundisho ya Yesu kuhusu jinsi ya kuishi. Wengi wanaweza kusema kwa unyofu kwamba mafundisho ya Yesu yamewaburudisha na kuwasaidia kubadili maisha yao kabisa. Unaweza kuthibitisha jambo hilo kwa kuchunguza kanuni fulani kuhusu maisha zilizotajwa katika masimulizi ya maisha na huduma ya Yesu. Masimulizi hayo yanapatikana hasa katika vitabu vya Injili ambavyo viliandikwa na Mathayo, Marko, na Luka.

Njia ya Kupata Burudisho

16, 17. (a) Unaweza kupata wapi baadhi ya mafundisho makuu ya Yesu? (b) Ni nini kinachohitajiwa ili kupata burudisho kwa kufuata mafundisho ya Yesu?

16 Katika masika ya mwaka wa 31 W.K., Yesu alitoa hotuba ambayo inajulikana sana hata leo. Hotuba hiyo inaitwa Mahubiri ya Mlimani. Imeandikwa kwenye kitabu cha Mathayo sura ya 5 hadi 7 na kitabu cha Luka sura ya 6. Sura hizo zinaeleza kwa ufupi mengi ya mambo aliyofundisha. Unaweza kupata mafundisho mengine ya Yesu katika sura nyinginezo za vitabu vya Injili. Mengi ya mambo ambayo Yesu alisema ni rahisi kueleweka, ingawa inaweza kuwa vigumu kuyatenda. Mbona usisome sura hizo kwa makini? Nguvu za mawazo ya Yesu na ziongoze fikira na mtazamo wako.

17 Ni wazi kwamba mafundisho ya Yesu yanaweza kupangwa katika njia mbalimbali. Na tupange mafundisho makuu ili tuwe na fundisho moja kila siku katika mwezi, tukiwa na lengo la kuyafuata maishani. Jinsi gani? Usiyapitie kijuujuu tu mafundisho hayo. Kumbuka yule mtawala tajiri aliyemwuliza Yesu Kristo hivi: “Ni kwa kufanya nini mimi nitarithi uhai udumuo milele?” Yesu alipotaja matakwa muhimu ya Sheria ya Mungu, mtu huyo alijibu kwamba tayari alikuwa anayatimiza. Hata hivyo, alitambua kwamba alihitaji kufanya mengi zaidi. Yesu alimwambia ajitahidi zaidi kufuata kanuni za Mungu kwa matendo na awe mwanafunzi mwenye bidii. Yaonekana mwanamume huyo hakutaka kufanya hivyo. (Luka 18:18-23) Hivyo, yeyote anayetaka kujua mafundisho ya Yesu leo anahitaji kukumbuka kwamba kuna tofauti kati ya kukubali, na kufuata mafundisho hayo na hivyo kupunguza mkazo.

18. Onyesha jinsi unavyoweza kutumia kwa manufaa sanduku lililoonyeshwa.

18 Kama hatua ya kwanza ya kuchunguza na kufuata mafundisho ya Yesu, tazama fundisho la kwanza kwenye sanduku lililoonyeshwa. Fundisho hilo larejezea Mathayo 5:3-9. Naam, yeyote kati yetu anaweza kutafakari kwa muda mrefu ushauri mzuri unaotolewa kwenye mistari hiyo. Hata hivyo, unapotazama mistari hiyo kwa ujumla, unaweza kusema nini kuhusu mtazamo? Iwapo kwa kweli unataka kushinda madhara ya mkazo unaopita kiasi katika maisha yako, ni nini kitakachokusaidia? Unaweza kufaidikaje kwa kukazia uangalifu zaidi mambo ya kiroho? Je, kuna jambo linalokuhangaisha maishani ambalo unahitaji kulipuuza na badala yake kukazia uangalifu zaidi mambo ya kiroho? Ukifanya hivyo, utakuwa mwenye furaha zaidi sasa.

19. Unaweza kufanya nini ili upate ufahamu na uelewevu zaidi?

19 Kuna jambo jingine unaloweza kufanya. Mbona usizungumzie mistari hiyo na mtumishi mwingine wa Mungu, labda mwenzi wako wa ndoa, jamaa wa karibu, au rafiki? (Mithali 18:24; 20:5) Kumbuka kwamba mtawala huyo tajiri alimwuliza mtu mwingine—Yesu—juu ya jambo lililohusiana na habari waliyokuwa wakizungumzia. Jibu alilopata lingezidisha matarajio yake ya kupata furaha na uhai wa milele. Mwamini mwenzako unayezungumza naye kuhusu mistari hiyo hatakuwa sawa na Yesu; lakini, mazungumzo kuhusu mafundisho ya Yesu yatawanufaisha nyote wawili. Jaribu kufanya hivyo haraka iwezekanavyo.

20, 21. Unaweza kufuata programu gani ili kujua mafundisho ya Yesu, na unawezaje kupima maendeleo yako?

20 Tazama tena sanduku, “Mafundisho ya Kukusaidia.” Mafundisho hayo yamepangwa ili angalau uweze kufikiria fundisho moja kwa siku. Kwanza unaweza kusoma mambo aliyosema Yesu kwenye mistari iliyoonyeshwa. Kisha fikiria maneno yake. Tafakari jinsi unavyoweza kuyatumia maishani mwako. Ukiwa unahisi kwamba tayari unafanya hivyo, tafakari uone ni mambo gani zaidi unayoweza kufanya ili uishi kupatana na fundisho hilo la Mungu. Jaribu kutumia fundisho hilo siku hiyo. Ukiona ni jambo gumu kulielewa au kujua jinsi ya kulitumia, litafakari siku nyingine. Hata hivyo, kumbuka kwamba si lazima ulielewe kabisa ndipo utafakari fundisho jingine. Unaweza kufikiria fundisho jingine siku inayofuata. Mwishoni mwa juma, unaweza kuangalia uone jinsi ambavyo umefanikiwa kuyatumia mafundisho manne au matano ya Yesu. Juma la pili fikiria mafundisho zaidi, siku kwa siku. Ukiona kwamba umeshindwa kutumia mafundisho fulani, usivunjike moyo. Kila Mkristo atahisi hivyo. (2 Mambo ya Nyakati 6:36; Zaburi 130:3; Mhubiri 7:20; Yakobo 3:8) Endelea kufanya hivyo katika juma la tatu na la nne.

21 Baada ya mwezi mmoja hivi, huenda ukafaulu kuchunguza mafundisho yote 31. Vyovyote vile, utahisije? Je, hutakuwa mwenye furaha zaidi, labda mwenye kustarehe zaidi? Hata kama hali yako itakuwa imeboreka kidogo, yaelekea mkazo utapungua, au angalau utashughulika na mkazo huo vizuri zaidi, na utajua jinsi ya kuendelea kufanya hivyo. Usisahau kwamba kuna mafundisho mengine mazuri ya Yesu ambayo hayakuorodheshwa kwenye sanduku. Kwa nini usitafute baadhi ya mafundisho hayo na kujaribu kuyafuata?—Wafilipi 3:16.

22. Tunaweza kupata matokeo gani kwa kufuata mafundisho ya Yesu, lakini ni mambo gani mengine yanayostahili kuchunguzwa?

22 Unaweza kuona kwamba nira ya Yesu ina fadhili kweli ingawa ina uzito fulani. Mzigo wa mafundisho yake na uanafunzi ni mwepesi. Baada ya kujionea mambo kwa zaidi ya miaka 60, mtume Yohana aliyekuwa rafiki mpendwa wa Yesu, alikubaliana na jambo hilo kwa kusema: “Hivi ndivyo kumpenda Mungu humaanisha, kwamba tushike amri zake; na bado amri zake si zenye kulemea.” (1 Yohana 5:3) Wewe pia unaweza kuwa na uhakika kama huo. Kadiri unavyozidi kufuata mafundisho ya Yesu, ndivyo utakavyotambua kwamba maisha yako hayatakuwa na mkazo sana kama maisha ya watu wengi leo. Utaona kwamba umepata kitulizo kikubwa. (Zaburi 34:8) Hata hivyo, kuna jambo jingine unalohitaji kufikiria kuhusiana na nira ya Yesu yenye fadhili. Yesu pia alitaja kwamba yeye ni “mwenye tabia-pole na wa hali ya chini moyoni.” Sifa hiyo inahusianaje na kujifunza na kumwiga Yesu? Tutachunguza jambo hilo katika makala ifuatayo.—Mathayo 11:29.

Unajibuje?

• Kwa nini tumtegemee Yesu tunapotafuta kitulizo cha mkazo unaopita kiasi?

• Nira ilikuwa ishara ya nini, na kwa nini?

• Kwa nini Yesu aliwaalika watu wachukue nira yake?

• Unawezaje kupata burudisho la kiroho?

[Maswali ya Funzo]

[Blabu katika ukurasa wa 14]

Andiko la mwaka la Mashahidi wa Yehova katika mwaka wa 2002 litakuwa: “Njoni kwangu, . . . nami hakika nitawaburudisha nyinyi.”—Mathayo 11:28.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 12, 13]

Mafundisho ya Kukusaidia

Ni mambo gani mazuri unayoweza kupata katika Mathayo sura ya 5 hadi 7? Sura hizo zina mafundisho yaliyotolewa na Mwalimu Stadi, Yesu, akiwa kwenye ubavu wa kilima cha Galilaya. Tafadhali soma mistari inayoonyeshwa chini katika Biblia yako mwenyewe, kisha ujiulize maswali yanayohusiana na mistari hiyo.

1. 5:3-9 Mistari hii inaniambia nini kuhusu mtazamo wangu kwa ujumla? Ninawezaje kujitahidi kupata furaha zaidi? Ninawezaje kukazia uangalifu zaidi mahitaji yangu ya kiroho?

2. 5:25, 26 Ni afadhali kufanya nini kuliko kuiga roho ya ubishi inayoonyeshwa na watu wengi?—Luka 12:58, 59.

3. 5:27-30 Maneno ya Yesu yanakazia nini kuhusu kuwaziawazia mambo ya kingono? Kuepuka kufanya hivyo kutanisaidiaje kuwa na furaha na amani ya akili?

4. 5:38-42 Kwa nini nijitahidi kuepuka sifa ya watu wa siku hizi ya kushikilia maoni yao kupita kiasi?

5. 5:43-48 Nitanufaikaje kwa kufahamiana zaidi na watu ambao huenda niliwaona kuwa adui? Yaelekea kufanya hivyo kutanisaidiaje kupunguza au kuondoa mkazo?

6. 6:14, 15 Iwapo nyakati nyingine ninakuwa na mwelekeo wa kutosamehe, je, huenda ikawa ni kwa sababu nina wivu au kinyongo? Ninawezaje kubadili hali hiyo?

7. 6:16-18 Je, nina mwelekeo wa kujishughulisha zaidi na sura yangu ya nje kuliko nilivyo moyoni? Ninapaswa kuwa mwangalifu zaidi kuhusu nini?

8. 6:19-32 Matokeo yanaweza kuwa nini nikihangaikia zaidi pesa au mali? Nitadumisha usawaziko katika jambo hilo kwa kufikiria nini?

9. 7:1-5 Ninahisije ninapokuwa karibu na watu wenye kushutumu na kuchambua, ambao sikuzote hutafuta-tafuta makosa? Kwa nini ni muhimu niepuke kuwa hivyo?

10. 7:7-11 Ikiwa inafaa kuendelea kumwomba Mungu jambo fulani, mbona nisiwe na mtazamo kama huo katika hali nyingine maishani?—Luka 11:5-13.

11. 7:12 Ingawa ninajua ile Kanuni Bora, ninaitumia mara nyingi kadiri gani ninaposhughulika na wengine?

12. 7:24-27 Kwa kuwa maisha yangu yamo mikononi mwangu, ninawezaje kujitayarisha vizuri zaidi kwa ajili ya magumu na matatizo? Kwa nini nifikirie mambo hayo sasa?—Luka 6:46-49.

Mafundisho mengine ninayoweza kufikiria:

13. 8:2, 3 Ninawezaje kuwaonyesha huruma wale walio katika hali ngumu, kama Yesu alivyofanya mara nyingi?

14. 9:9-38 Je, mimi huonyesha huruma, na ninaweza kuionyeshaje hata zaidi?

15. 12:19 Ninapojifunza kutokana na unabii kumhusu Yesu, je, ninajitahidi kuepuka mabishano?

16. 12:20, 21 Ninaweza kuwanufaishaje wengine kwa kutowaumiza kwa maneno au kwa matendo?

17. 12:34-37 Mimi hutumia wakati mwingi nikizungumzia nini? Ninajua kwamba ninapokamua chungwa, ninapata maji ya chungwa, hivyo basi, kwa nini nifikirie yaliyo moyoni mwangu?—Marko 7:20-23.

18. 15:4-6 Ninajifunza nini kutokana na maelezo ya Yesu kuhusu kuwatunza kwa upendo walio wazee?

19. 19:13-15 Ninahitaji kuchukua wakati kufanya nini?

20. 20:25-28 Kwa nini hainufaishi kutumia mamlaka isivyofaa. Ninawezaje kumwiga Yesu katika jambo hilo?

Mafundisho mengine yaliyoandikwa na Marko:

21. 4:24, 25 Kwa nini ni muhimu kufikiria jinsi ninavyowatendea wengine?

22. 9:50 Ikiwa mambo ninayosema na kufanya yanafaa, inaelekea kutakuwa na matokeo gani mazuri?

Hatimaye, mafundisho kadhaa yaliyoandikwa na Luka:

23. 8:11, 14 Matokeo yatakuwa nini ikiwa wasiwasi, mali, au anasa zitatawala maisha yangu?

24. 9:1-6 Yesu alitanguliza nini ingawa alikuwa na uwezo wa kuponya wagonjwa?

25. 9:52-56 Je, ninaudhika upesi? Je, ninaepuka roho ya kutaka kulipiza kisasi?

26. 9:62 Nioneje daraka langu la kuzungumza kuhusu Ufalme wa Mungu?

27. 10:29-37 Ninaweza kuthibitishaje kwamba mimi ni jirani, wala si mtu asiyejali?

28. 11:33-36 Ninapaswa kufanya mabadiliko gani ili maisha yangu yawe sahili zaidi?

29. 12:15 Kuna uhusiano gani kati ya uhai na mali?

30. 14:28-30 Iwapo ninachukua wakati kuchanganua maamuzi kwa makini, ninaweza kuepuka nini na matokeo yawe nini?

31. 16:10-12 Ninaweza kupata manufaa gani kwa kudumisha uaminifu-maadili?

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kazi ya kuokoa uhai chini ya nira ya Yesu inaburudisha