Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Mke Mkristo anawezaje kuwa mwaminifu kwa Mungu na wakati huohuo ajitiishe kwa mume wake asiyeamini iwapo mume huyo anasherehekea sikukuu za kidini?

Mke atahitaji kuwa na hekima na busara kufanya hivyo. Lakini jitihada zake za kusawazisha majukumu hayo mawili zinafaa. Yesu alitoa ushauri huu kuhusu hali inayofanana na hiyo: “Mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari, lakini mlipeni Mungu vitu vya Mungu.” (Mathayo 22:21) Ni kweli kwamba Yesu alikuwa anazungumza kuhusu majukumu yetu kwa serikali, ambazo baadaye Wakristo waliambiwa wajitiishe kwazo. (Waroma 13:1) Hata hivyo, ushauri wake unafaa mke anapohitajika kusawazisha majukumu yake kwa Mungu na ujitiisho kwa mume wake, hata ikiwa mume huyo si mwamini.

Kila mtu anayeifahamu Biblia anajua inakazia kwamba jukumu la kwanza kwa Mkristo ni kwa Mungu Mweza Yote, kuwa mwaminifu-mshikamanifu kwake nyakati zote. (Matendo 5:29) Hata hivyo, mara nyingi mwabudu wa kweli anaweza kukubali kufanya mambo ambayo mtu mwenye mamlaka asiyeamini anaomba au anataka afanyiwe huku mwabudu huyo akiepuka kuvunja sheria za juu za Mungu.

Tunajifunza jambo fulani kutokana na mfano wa Waebrania watatu unaosimuliwa katika kitabu cha Danieli sura ya 3. Nebukadneza, aliyekuwa mkuu wa serikali, aliagiza kwamba Waebrania hao na watu wengineo waje kwenye uwanda wa Dura. Walipotambua kulikuwa na mipango ya kufanya ibada isiyo ya kweli huko, yaelekea Waebrania hao watatu hawakutaka kwenda huko. Labda Danieli alikuwa na sababu ya kutokwenda, lakini Waebrania hao wengine hawakuwa na sababu. * Kwa hiyo, wakakubali kwenda huko, lakini hawakushiriki ibada hiyo hata kidogo.—Danieli 3:1-18.

Vivyo hivyo, wakati wa sikukuu, mume asiyeamini anaweza kumwomba au kumtaka mkewe Mkristo afanye jambo ambalo mke huyo hangetaka kufanya. Ona mifano kadhaa: Anamwambia apike chakula fulani siku ambayo yeye na watu wengine watasherehekea sikukuu. Au anataka familia yake (kutia ndani mke) watembelee jamaa zake siku hiyo ili wale pamoja au wawajulie hali tu. Au hata kabla ya sikukuu, huenda akataka mke anapoenda dukani amnunulie vitu kama, vyakula vinavyoliwa wakati huo wa sikukuu, zawadi, au makaratasi ya kufungia zawadi na kadi za salamu zinazoambatana na zawadi hizo.

Mke Mkristo apaswa kuazimia kutoshiriki mambo yanayohusiana na dini zisizo za kweli, lakini atafanya nini akiombwa afanye mambo hayo? Mume ndiye kichwa cha familia, nalo Neno la Mungu linasema: “Nyinyi wake, iweni katika ujitiisho kwa waume zenu, kama inavyofaa katika Bwana.” (Wakolosai 3:18) Katika hali kama hizo, je, mke anaweza kujitiisha kwa mume wake na wakati huohuo kuwa mwaminifu kwa Mungu? Anapaswa kuona ni jinsi gani atamtii mume wake na wakati huohuo kumtii Yehova, jambo lililo muhimu hata zaidi.

Nyakati nyingine, huenda mume wake akamwomba apike chakula fulani, kwa sababu anakipenda au kwa sababu amezoea kula chakula hicho nyakati fulani. Mke atataka kumwonyesha upendo na pia kumwonyesha kwamba anatambua ukichwa wake. Je, angefanya hivyo kama mume wake angeomba apikiwe chakula hicho wakati wa sikukuu ? Baadhi ya wake Wakristo wanaweza kufanya hivyo kwa dhamiri safi, wakiona kazi hiyo kama upishi tu wa kawaida. Bila shaka, hakuna Mkristo mwaminifu ambaye angekiona chakula hicho kuwa na maana yoyote kuhusiana na sikukuu, hata kama mume wake angekiona hivyo. Vivyo hivyo, huenda mume huyo akataka mke wake aandamane naye anapotembelea jamaa zake nyakati fulani kila mwezi au mwaka. Je, angefanya hivyo, hata kama ni wakati wa sikukuu? Au je, anapoenda dukani, angekuwa tayari kununua vitu ambavyo mume anamwomba amnunulie, bila kujali anachonuia kufanya na vitu hivyo?

Bila shaka, mke Mkristo anapaswa kufikiria jinsi ununuzi huo utakavyowaathiri wengine. (Wafilipi 2:4) Atataka kuepuka kufanya watu wafikiri kwamba anasherehekea sikukuu hiyo kama vile inaelekea wale Waebrania watatu hawakutaka wengine wawaone wakisafiri kwenda kwenye uwanda wa Dura. Kwa hiyo, anaweza kusababu na mume wake kwa busara na kuona kama mume huyo angejifanyia mambo fulani yanayohusiana na sikukuu kwa kufikiria hisia za mke ambaye anampenda na kumheshimu mume wake. Huenda mume huyo akaona kuwa ni jambo la busara kutoruhusu hali inayoweza kuwaaibisha wote wawili iwapo mke atalazimika kukataa kushiriki vitendo fulani vya dini isiyo ya kweli. Naam, unaweza kutatua tatizo hilo kwa amani kwa kuzungumza naye mapema na kwa utulivu.—Mithali 22:3.

Hatimaye, Mkristo mwaminifu anapaswa kuchanganua mambo ya hakika na kuamua atafanya nini. Ni lazima kwanza amtii Mungu kama wale Waebrania watatu walivyofanya. (1 Wakorintho 10:31) Lakini kwa kufikiria jambo hilo, kila Mkristo anapaswa kuamua ni mambo gani yasiyopingana na imani yake ambayo yeye anaweza kumfanyia mtu mwenye mamlaka katika familia au katika jumuiya.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Ona “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Agosti 1, 2001.