Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Watu Huenda Gileadi kwa Kuchochewa na Moyo wa Kupenda

Watu Huenda Gileadi kwa Kuchochewa na Moyo wa Kupenda

Watu Huenda Gileadi kwa Kuchochewa na Moyo wa Kupenda

SHULE ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower huwazoeza wanaume na wanawake waliojitoa kufanya utumishi wa mishonari katika nchi za kigeni. Ni nani wanaostahili kwenda Gileadi? Ni wale walio na moyo wa kupenda. (Zaburi 110:3) Bila shaka, jambo hilo lilionekana wazi Septemba 8, 2001, wakati wanafunzi wa darasa la 111 walipohitimu.

Baadhi ya wanafunzi wa darasa hilo tayari walikuwa wameacha familia, marafiki, na nchi zao ili kutumikia mahali palipo na uhitaji mkubwa zaidi. Kwa kufanya hivyo, walikuwa wakichanganua hali zao waone ikiwa wanaweza kufanya marekebisho fulani ili kuishi katika mazingira tofauti. Kwa mfano, Richer na Nathalie walipanga mambo yao ili wahamie Bolivia, Todd na Michelle wahamie Jamhuri ya Dominika, nao David na Monique wahamie nchi fulani huko Asia ili kutangaza habari njema za Ufalme wa Mungu. Wanafunzi wengine tayari walikuwa wametumikia katika nchi ya Nikaragua, Ekuado, na Albania.

Christy alitiwa moyo ajifunze Kihispania akiwa katika shule ya upili, jambo lililomsaidia kuweza kukaa nchini Ekuado miaka miwili kabla ya kuolewa. Wengine walijiunga na makutaniko yanayotumia lugha za kigeni katika nchi za kwao. Saul na Priscilla walionyesha moyo wa kupenda kwa kujitahidi sana kuboresha Kiingereza chao kabla ya kwenda katika shule ya Gileadi.

Majuma 20 ya kuzoezwa kuwa mishonari yalikwisha haraka. Siku ya kuhitimu ikafika, nao wanafunzi wakakusanyika pamoja na marafiki na familia kusikiliza mashauri ya hekima na maneno ya kuwaaga yenye kutia moyo.

Mwenyekiti wa programu alikuwa Theodore Jaracz, mhitimu wa darasa la saba la Shule ya Gileadi, ambaye sasa anatumikia akiwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova. Katika utangulizi wake alikazia kwamba tukiwa tengenezo, sikuzote tumezingatia kusudi la kuzoeza wanafunzi wa Gileadi, yaani kuhubiri habari njema za Ufalme katika dunia yote inayokaliwa. (Marko 13:10) Shule ya Gileadi huzoeza wanafunzi wanaostahili ili waendelee na kazi hii ya kuhubiri kwa kiwango kikubwa zaidi ya walivyofanya hapo awali na katika maeneo ya ulimwengu ambapo mishonari waliozoezwa wanahitajika sana. Ndugu Jaracz aliwashauri wanafunzi watumie ifaavyo mazoezi waliyopewa Gileadi wanapojiunga na mishonari ambao kwa sasa wanatumikia katika nchi 19 ambako wahitimu hawa wametumwa.

Shauri la Wakati Unaofaa kwa Wahitimu

Hotuba mfululizo zilitolewa. William Van De Wall, mshiriki wa Halmashauri ya Ofisi ya Tawi ya Marekani, alitoa hotuba yenye kichwa “Bidii ya Mishonari—Hutambulisha Wakristo wa Kweli.” Alikazia kazi ya “kufanya wanafunzi,” inayotajwa katika andiko la Mathayo 28:19, 20, naye akawahimiza wanafunzi hivi: “Mwigeni Yesu, aliyefanya mgawo wake wa mishonari kwa bidii na shauku.” Ili kuwasaidia mishonari wapya wadumishe bidii yao katika kazi ya mishonari, aliwatia moyo kwa kuwaambia: “Dumisheni ratiba inayofaa; dumisheni mazoea ya kujifunza kibinafsi, endeni sambamba na mambo ya kitheokrasi; na sikuzote mkumbuke ni kwa nini mko katika mgawo wenu.”

Hotuba iliyofuata ilitolewa na Guy Pierce, mshiriki wa Baraza Linaloongoza. Hotuba yake ilikuwa na kichwa “Endeleeni Kusitawisha ‘Nguvu Zenu za Kufikiri Kuzuri.’” (Waroma 12:1) Alitoa mashauri yanayofaa kwa wanafunzi waliokuwa wakihitimu, huku akiwatia moyo watumie uwezo wao wa kufikiri na kusababu ambao wamepewa na Mungu. “Endeleeni kutafakari mambo ambayo Yehova anasema kupitia Neno lake. Hilo litawalinda,” akasema. (Mithali 2:11) Ndugu Pierce pia aliwashauri wanafunzi wasiwe wakishikilia sana kauli zao ikiwa wanataka kudumisha “nguvu [zao] za kufikiri kuzuri.” Bila shaka, vikumbusho hivyo vya wakati unaofaa vitawasaidia wanafunzi wanaohitimu kutumikia wakiwa mishonari.

Baada ya hapo mwenyekiti alimkaribisha mmojawapo wa walimu wa Gileadi, Lawrence Bowen, aliyetoa hotuba yenye kichwa “Amua Kutojua Kitu Chochote.” Alisema kwamba mtume Paulo alipofanya kazi ya mishonari huko Korintho, alikuwa ‘ameamua kutojua kitu chochote ila Yesu Kristo, aliyekuwa ametundikwa mtini.’ (1 Wakorintho 2:2) Paulo alijua kwamba roho takatifu, ambayo ndiyo nguvu kuu zaidi ulimwenguni, ndiyo hutegemeza ujumbe unaopatikana katika Biblia nzima: kutetewa kwa enzi kuu ya Yehova kupitia Mbegu aliyeahidiwa. (Mwanzo 3:15) Wanafunzi 48 wenye kuhitimu walihimizwa wawe kama Paulo na Timotheo ili kufanikiwa wakiwa mishonari, huku wakidumisha “kiolezo cha maneno yenye afya.”—2 Timotheo 1:13.

Hotuba ya mwisho kwenye mfululizo wa hotuba za kwanza ilikuwa na kichwa “Thamini Pendeleo Lako, Ni Zawadi Kutoka kwa Mungu.” Wallace Liverance, msajili wa Shule ya Gileadi, aliwasaidia wahitimu wafahamu kwamba mapendeleo ya utumishi ni fadhili isiyostahiliwa ya Mungu wala si haki yao. Akitumia mfano wa mtume Paulo, Ndugu Liverance alisema hivi: “Yehova hakumchagua Paulo kuwa mtume wake kwa mataifa kwa sababu ya kazi zake, ili isionekane kwamba Paulo alikuwa na haki ya kupewa mgawo huo au aliwiwa mgawo huo. Mgawo huo haukutegemea muda ambao mtu alitumikia au uzoefu wake. Kwa maoni ya kibinadamu, huenda ingeonekana kwamba Barnaba ndiye aliyefaa kuchaguliwa. Mgawo huo haukutegemea uwezo wa mtu; yaonekana Apolo alikuwa mfasaha zaidi ya Paulo. Ilikuwa fadhili isiyostahiliwa ya Mungu.” (Waefeso 3:7, 8) Ndugu Liverance aliwatia moyo wahitimu watumie zawadi yao, au pendeleo la utumishi, kuwasaidia wengine wawe marafiki wa Mungu na kupokea “zawadi ambayo Mungu hutoa . . . , uhai udumuo milele kwa njia ya Kristo Yesu Bwana wetu.”—Waroma 6:23.

Baada ya hotuba hiyo, Mark Noumair, mwalimu mwingine wa Gileadi, alitoa hotuba yenye kuvutia kwa njia ya mahojiano pamoja na wanafunzi kadhaa iliyokuwa na kichwa “Matayarisho Huleta Matokeo Mema.” (Mithali 21:5) Mambo yaliyoonwa yalionyesha kwamba mhudumu anapojitayarisha vizuri kwa ajili ya huduma, hasa anapotayarisha moyo wake, atapendezwa na watu kikweli. Hatakosa jambo la kusema. Badala yake, atasema na kufanya mambo ya kusaidia watu kiroho. “Hivyo ndivyo mtu anavyoweza kufanikiwa akiwa mishonari,” akasema Ndugu Noumair, akitumia mambo aliyojionea mwenyewe alipokuwa mishonari barani Afrika.

Utumishi wa Mishonari Ni Kazi Inayoridhisha

Ralph Walls na Charles Woody waliwahoji baadhi ya mishonari wenye uzoefu, ambao walikuwa kwenye Kituo cha Elimu cha Patterson ili kupata mazoezi ya pekee. Katika mahojiano hayo, ilikaziwa kwamba kuwapenda watu hutokeza shangwe katika utumishi wa mishonari. Walipowasikiliza mishonari hao wenye uzoefu, wanafunzi, washiriki wa familia zao, na marafiki wao walipata uhakikisho kwamba utumishi wa mishonari ni kazi inayoridhisha.

John E. Barr, ambaye ni mshiriki wa Baraza Linaloongoza, alitoa hotuba ya msingi ya siku hiyo, iliyokuwa na kichwa “Mwimbieni Yehova Wimbo Mpya.” (Isaya 42:10, NW ) Ndugu Barr alisema kwamba usemi “wimbo mpya” unapatikana katika Biblia mara tisa. Aliuliza, “Wimbo huo mpya unamaanisha nini?” Kisha akajibu: “Muktadha unaonyesha kwamba wimbo huo mpya unaimbwa kwa sababu ya matukio mapya yanayohusu njia ambayo Yehova anatumia mamlaka yake.” Aliwahimiza wanafunzi waendelee kuimba sifa za Ufalme wa Mungu ambao umepata ushindi mikononi mwa Mfalme wa Kimesiya, Kristo Yesu. Ndugu Barr alisema kwamba mazoezi waliyopokea Gileadi yaliwasaidia kuelewa kwa kindani zaidi ya hapo awali mambo mbalimbali yanayohusu “wimbo [huo] mpya.” “Shule hii imewaonyesha umuhimu wa ‘kumwimbia’ Yehova sifa pamoja na ndugu na dada zenu popote mtakapoenda; sikuzote msitawishe umoja pamoja na wengine katika migawo yenu.”

Baada ya wanafunzi kupewa diploma zao, msemaji wa wanafunzi alisoma barua ya shukrani za kutoka moyoni kwa ajili ya mazoezi waliyopokea Gileadi.

Je, unaweza kuongeza utumishi wako kwa Mungu na kuufanya uwe na matokeo zaidi? Ikiwa ndivyo, uwe mwenye bidii kama wanafunzi hao wenye kuhitimu. Jambo hilo ndilo limewasaidia wastahili kuwa mishonari. Mtu anaweza kupata shangwe kubwa anapokuwa na moyo wa kupenda kumtumikia Mungu.—Isaya 6:8.

[Sanduku katika ukurasa wa 25]

TAKWIMU ZA DARASA

Idadi ya nchi zilizowakilishwa: 10

Idadi ya nchi ambako wametumwa: 19

Idadi ya wanafunzi: 48

Wastani wa umri: 33.2

Wastani wa miaka katika kweli: 16.8

Wastani wa miaka katika huduma ya wakati wote: 12.6

[Picha katika ukurasa wa 26]

Darasa la 111 Lililohitimu la Shule ya Biblia ya Gileadi ya Watchtower

Katika orodha iliyo chini, nambari za safu zinaanzia mbele kuelekea nyuma, na majina yameorodheshwa kuanzia kushoto kuelekea kulia katika kila safu.

(1) Yeomans, C.; Toukkari, A.; Nuñez, S.; Phillips, J.; Dawkin, M.; Silvestri, P. (2) Morin, N.; Biney, J.; López, M.; Van Hout, M.; Cantú, A.; Szilvassy, F. (3) Williams, M.; Itoh, M.; Van Coillie, S.; Levering, D.; Fuzel, F.; Geissler, S. (4) Yeomans, J.; Moss, M.; Hodgins, M.; Dudding, S.; Briseño, J.; Phillips, M. (5) López, J.; Itoh, T.; Sommerud, S.; Kozza, C.; Fuzel, G.; Moss, D. (6) Williams, D.; Dudding, R.; Geissler, M.; Morin, R.; Biney, S.; Cantú, L. (7) Dawkin, M.; Hodgins, T.; Levering, M.; Silvestri, S.; Van Hout, D.; Briseño, A. (8) Van Coillie, M.; Nuñez, A.; Kozza, B.; Sommerud, J.; Toukkari, S.; Szilvassy, P.