Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Watu Wanasema Kwamba Mimi Ni Nani?”

“Watu Wanasema Kwamba Mimi Ni Nani?”

“Watu Wanasema Kwamba Mimi Ni Nani?”

NI WAKATI wa Krismasi. Ulimwenguni pote watu wameamua kusherehekea siku ya kuzaliwa. Kuzaliwa kwa nani? Je, ni kuzaliwa kwa Mwana wa Mungu au kwa Myahudi fulani tu aliyejitoa na aliyekuwa na nia ya kubadili dini iliyoenea sana huko kwao katika karne ya kwanza? Je, ni siku ya kuzaliwa kwa mtetezi wa maskini, mwasi aliyetisha Milki ya Roma na hivyo akauawa, au labda mtu fulani mwenye hekima aliyekazia sana ujuzi na hekima ya kibinafsi? Una sababu ya kujiuliza, ‘Kwa kweli, Yesu Kristo alikuwa nani?’

Yesu mwenyewe alitaka kujua maoni ya watu kuhusu swali hilo. Pindi moja aliwauliza wanafunzi wake, “Watu wanasema kwamba mimi ni nani?” (Marko 8:27) Kwa nini aliuliza swali hilo? Tayari wengi walikuwa wameacha kumfuata. Yaonekana wengine walikuwa wametatanika na kufadhaika baada ya Yesu kukataa kufanywa mfalme. Isitoshe, alipokabiliwa na maadui wake, Yesu hakutoa ishara kutoka mbinguni ili kuthibitisha alikuwa nani. Kwa kujibu swali hilo, mitume walisema yeye ni nani? Walitaja baadhi ya maoni yaliyoenea wakati huo: “Baadhi yao husema Yohana Mbatizaji, wengine Eliya, bado wengine Yeremia au mmoja wa manabii.” (Mathayo 16:13, 14) Hawakutaja majina mengi ya kumshushia Yesu heshima ambayo yalikuwa yamevuma huko Palestina—mkufuru, mlaghai, nabii asiye wa kweli, hata mtu asiye na akili timamu.

Mambo Mengi Kumhusu Yesu

Ikiwa Yesu angezusha swali hilo leo, labda angeuliza hivi: “Wasomi wanasema mimi ni nani?” Tena, majibu yangekuwa kama ifuatavyo: Kuna maoni mengi mbalimbali. “Yesu amekuwa farasi ambaye ameendeshwa na watu tofauti-tofauti akielekezwa sehemu mbalimbali,” akasema David Tracy wa Chuo Kikuu cha Chicago. Katika karne iliyopita, wasomi wametumia njia tata za kuchunguza mambo ya kijamii na hekaya wakitafuta kujua Yesu alikuwa nani. Baada ya kutumia njia hizo, wanafikiri Yesu alikuwa nani?

Wasomi fulani wanadai kwamba Yesu anayetajwa katika historia alikuwa nabii Myahudi aliyehubiri kuhusu mwisho wa ulimwengu, na kuwasihi watu watubu. Hata hivyo, hawamwiti Mwana wa Mungu, Mesiya, au Mkombozi. Wengi hutilia shaka simulizi la Biblia kuhusu asili yake ya kimbingu na kufufuliwa kwake. Wengine humwona Yesu kuwa mtu wa kawaida tu ambaye maisha na mafundisho yake mazuri yalichochea kuanzishwa kwa dini kadhaa ambazo baadaye zilipata kuwa sehemu ya Ukristo. Kama ilivyotajwa katika kichapo Theology Today, bado wengine humwona Yesu kuwa ‘mchambuzi, mtu mwenye hekima aliyetangatanga, mkulima asiyejulikana vizuri; msimamzi wa jamii, mshairi mwasi-mila mwenye kuchambua utengamano wa jamii, au mchochezi stadi aliyeeleza maoni yake miongoni mwa wanakijiji wa hali ya chini wenye hasira ambao walikuwa tayari kutenda jeuri.’

Pia kuna maoni mengine yasiyo ya kawaida. Nyimbo za rapu, vitu vya sanaa vinavyopatikana mijini na hata dansi zinamwonyesha kuwa mtu mweusi. * Wengine hata wanakisia kwamba Yesu alikuwa mwanamke. Katika mwaka wa 1993, watu walioenda kwenye Maonyesho ya Jimbo la Orange huko California waliona sanamu ya Christie,” “Kristo” wa kike asiye na nguo akiwa msalabani. Karibu wakati huohuo, huko New York, kulikuwa na “Christa”—“Yesu” wa kike aliyesulubiwa. Sanamu hizo mbili zilitokeza ubishi mkubwa. Na mapema katika mwaka wa 1999, watu wangeweza kununua kitabu “kinachozungumzia upendo [ambao] ulikuwa kati ya Mvulana Yesu na mbwa wake, Malaika.” Uhusiano wao unafafanuliwa kuwa “wa kiroho na unaonyesha jinsi kila mmoja wao alivyo tayari kudhabihu uhai wake kwa ajili ya mwenzake.”

Je, Ni Muhimu Kujua Yesu Alikuwa Nani?

Kwa nini utake kujua Yesu alikuwa nani na yeye ni nani? Kwanza kabisa, tukimnukuu Napoleon, “Yesu Kristo amekuwa na uvutano na ameongoza raia Zake bila ya Yeye kuwapo katika mwili wenye kuonekana.” Kwa mafundisho yake madhubuti na jinsi alivyoishi, Yesu ameathiri sana maisha ya mabilioni ya watu kwa muda upatao miaka elfu mbili. Kwa kufaa, mwandikaji mmoja alisema hivi: “Majeshi yote yaliyopata kupiga miguu, na manowari zote zilizopata kuundwa, na mabunge yote yaliyopata kuwa na kikao, wafalme wote waliopata kutawala, wakijumlishwa pamoja hawakupata kuwa na uvutano juu ya maisha za wanadamu katika dunia hii kwa nguvu nyingi jinsi iyo hiyo.”

Isitoshe, unahitaji kujua Yesu alikuwa nani na yeye ni nani kwa kuwa Yesu anahusika moja kwa moja na wakati wako ujao. Una fursa ya kuwa raia wa serikali iliyosimamishwa mbinguni—Ufalme wa Mungu chini ya Yesu. Yesu atasimamia kazi ya kuboresha tena mazingira ya dunia yetu yenye matatizo na viumbe wa namna mbalimbali. Unabii wa Biblia unatuhakikishia kwamba Ufalme wa Yesu utalisha wenye njaa, utawahangaikia maskini, utaponya wagonjwa, na kuwafufua wafu.

Bila shaka ungependa kujua ni mtu wa aina gani atakayekuwa mfalme wa serikali hiyo inayohitajiwa sana. Makala inayofuata itakusaidia kumfahamu yule Yesu halisi.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Kuhusu sura ya Yesu, ona makala “Yesu Alifananaje?,” katika toleo la Amkeni! la Desemba 8, 1998.