Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yule Yesu Halisi

Yule Yesu Halisi

Yule Yesu Halisi

BAADA ya mitume wake kumwambia jinsi watu walivyofikiri juu yake, Yesu aliwauliza hivi: “Ingawa hivyo, nyinyi mwasema mimi ni nani?” Twapata jibu la Petro katika Injili ya Mathayo: “Wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai.” (Mathayo 16:15, 16) Wengine walikuwa na maoni hayohayo. Nathanaeli ambaye baadaye alipata kuwa mmoja wa mitume, alimwambia Yesu hivi: “Rabi, wewe ndiwe Mwana wa Mungu, wewe ndiwe Mfalme wa Israeli.” (Yohana 1:49) Yesu mwenyewe alitaja umuhimu wa daraka lake: “Mimi ndiyo njia na kweli na uhai. Hakuna ajaye kwa Baba ila kupitia mimi.” (Yohana 14:6) Katika pindi nyingi, alijiita “Mwana wa Mungu.” (Yohana 5:24, 25; 11:4) Naye alithibitisha jambo hilo kwa kufanya miujiza, hata kufufua wafu.

Je, Ni Shaka Zenye Msingi?

Lakini je, kweli twaweza kuamini masimulizi ya vitabu vya Injili kumhusu Yesu? Je, yanasimulia kuhusu yule Yesu halisi? Frederick F. Bruce, aliyekuwa profesa wa uchambuzi na ufafanuzi wa Biblia kwenye Chuo Kikuu cha Manchester, Uingereza, alisema: ‘Kwa kawaida haiwezekani kuthibitisha kihistoria kila habari kuhusu maandishi ya kale, yawe yamo katika Biblia au la. Inatosha kuwa na uhakika kwamba mwandishi ni mtu mwenye kutumainika; tukiwa na uhakika huo, basi inaelekea sana kwamba habari zake ni za kweli. Agano la Kale ni lenye kutegemeka kihistoria kwa sababu Wakristo walilipokea kama kichapo “kitakatifu.”’

Baada ya kuchunguza zile zinazoonekana kuwa shaka kuhusu Yesu anayetajwa katika vitabu vya Injili, James R. Edwards, profesa wa dini kwenye Chuo cha Jamestown, North Dakota, Marekani, aliandika hivi: ‘Twaweza kuthibitisha kwa uhakika kwamba Injili zina uthibitisho mbalimbali na ulio muhimu kuhusu Yesu. Jinsi ambavyo Injili humtambulisha Yesu hupatana na akili kwa sababu hivyo ndivyo alivyokuwa hasa. Injili zimehifadhi kwa uaminifu maoni ya wafuasi wake kumhusu, kwamba kwa kweli alitumwa na Mungu na kupewa mamlaka ya kuwa Mwana na Mtumishi wa Mungu.’ *

Kumtafuta Yesu

Namna gani vichapo vingine mbali na Biblia vinavyomtaja Yesu? Vinachanganuliwa jinsi gani? Vitabu vya Tacitus, Suetonius, Josephus, Pliny Mchanga, na waandishi wengine wa kale vina marejezo mengi kumhusu Yesu. Kichapo The New Encyclopædia Britannica (1995) chasema hivi kuhusu vichapo hivyo: ‘Masimulizi hayo yanathibitisha kwamba katika nyakati za kale hata wapinzani wa Ukristo hawakutilia shaka kamwe kuwepo kwa Yesu, ambako kulitiliwa shaka mara ya kwanza bila sababu zenye msingi mwishoni mwa karne ya 18, katika karne ya 19, na mwanzoni mwa karne ya 20.’

Inasikitisha kwamba wasomi wa kisasa wamekosa kumfahamu vizuri Yesu “halisi” au “anayetajwa katika historia” kwa sababu ya kukisiakisia kusiko na msingi, shaka zisizofaa, na nadharia zisizo na msingi. Kwa njia fulani, wao ndio wenye hatia ya kutunga hadithi zisizo za kweli huku wakiwalaumu kimakosa waandishi wa Injili. Wengine wana hamu nyingi sana ya kupata umashuhuri tu na kuwa wa kwanza kuanzisha nadharia mpya, hivi kwamba hawachunguzi kwa unyofu uthibitisho wa kuwepo kwa Yesu. Kwa kufanya hivyo, wanabuni “Yesu” ambaye ni wa kuwaziwa tu na wasomi.

Wale wanaotaka kumfahamu yule Yesu halisi wanaweza kufanya hivyo kwa kujifunza Biblia. Luke Johnson, profesa wa Agano Jipya na asili ya Ukristo kwenye Shule ya Theolojia ya Candler katika Chuo Kikuu cha Emory, adai kwamba utafiti mwingi kuhusu Yesu anayetajwa katika historia hupuuza malengo ya Biblia. Asema kwamba huenda ikapendeza kuchunguza mambo ya kijamii, kisiasa, kibinadamu, na kitamaduni yanayohusu maisha ya Yesu na kipindi alichoishi. Hata hivyo, anaendelea kusema kwamba, “lengo la Maandiko ni kufafanua zaidi utu wa Yesu,” ujumbe wake, na daraka analotimiza akiwa Mkombozi, badala ya kutambulisha yule ambaye wasomi wanamwita Yesu anayetajwa katika historia. Kwa hiyo, utu na ujumbe halisi wa Yesu ulikuwa nini?

Yule Yesu Halisi

Injili, yaani yale masimulizi manne ya Biblia kuhusu maisha ya Yesu—huonyesha Yesu kuwa mtu aliyeonyesha huruma nyingi. Yesu alichochewa na sikitiko na huruma kusaidia watu waliokuwa wakisumbuliwa na magonjwa, upofu, na matatizo mengine. (Mathayo 9:36; 14:14; 20:34) Kifo cha rafikiye Lazaro na jinsi kilivyowahuzunisha dada zake kilimfanya Yesu ‘apige kite na kutokwa na machozi.’ (Yohana 11:32-36) Kwa kweli, Injili huonyesha hisia mbalimbali za Yesu—alimhurumia mtu mwenye ukoma, alifurahia sana mafanikio ya wanafunzi wake, aliwakasirikia watu walioshikilia sana sheria bila huruma, na akahuzunikia Yerusalemu kwa kumkataa Mesiya.

Yesu alipofanya muujiza, mara nyingi alikazia sehemu iliyotimizwa na mtu aliyefanyiwa muujiza: “Imani yako imekufanya upone.” (Mathayo 9:22) Alimsifu Nathanaeli kuwa “Mwisraeli kwelikweli,” huku akisema: “Hamna hila ndani yake.” (Yohana 1:47, Union Version) Baadhi ya watu walipofikiri kwamba zawadi ambayo mwanamke fulani alitoa ili kuonyesha uthamini ilikuwa yenye thamani kupita kiasi, Yesu alimtetea na kusema kwamba ukarimu wake ungekumbukwa kwa muda mrefu. (Mathayo 26:6-13) Alikuwa rafiki wa kweli na mwenye upendo kwa wafuasi wake, ‘akiwapenda hadi mwisho.’—Yohana 13:1; 15:11-15.

Pia Injili huonyesha kwamba Yesu alitambua mara moja mahitaji ya watu aliokutana nao. Awe alikuwa akizungumza na mwanamke kwenye kisima, mwalimu wa dini kwenye bustani, au mvuvi aliyekuwa kando ya bahari, aliwafikia mioyo mara moja. Baada ya utangulizi wa Yesu, wengi wa watu hao walimweleza mambo yaliyokuwa mioyoni mwao. Aligusa hisia zao. Ingawa watu walioishi katika siku za Yesu huenda waliwaepuka watu wenye mamlaka, walimwendea Yesu. Watu walipenda kuwa pamoja na Yesu; Walistarehe wakiwa pamoja naye. Watoto walifurahi kuwa pamoja naye, na alipokuwa akitumia mtoto kama mfano, hakumweka mtoto huyo mbele ya wanafunzi wake tu, bali pia ‘alimkumbatia.’ (Marko 9:36; 10:13-16) Kwa kweli, Injili huonyesha kuwa Yesu alikuwa mtu mwenye kuvutia kwa njia ya kipekee hivi kwamba watu walikaa kwa muda wa siku tatu wakisikiliza tu maneno yake yenye kuvutia.—Mathayo 15:32.

Licha ya kwamba Yesu alikuwa mkamilifu, hakuwa mwenye kuchambua watu kupita kiasi au mwenye kujigamba na mwenye kukandamiza wanadamu wasio wakamilifu na wenye dhambi ambao aliishi miongoni mwao na kuwahubiria. (Mathayo 9:10-13; 21:31, 32; Luka 7:36-48; 15:1-32; 18:9-14) Yesu hakuwa mwenye kudai kamwe. Hakuwaongezea watu mizigo. Badala yake, alisema: “Njoni kwangu, nyinyi nyote mnaomenyeka . . . Nami hakika nitawaburudisha nyinyi.” Wanafunzi wake walimwona kuwa “mwenye tabia-pole na wa hali ya chini moyoni”; nira yake ilikuwa ya fadhili, na mzigo wake ulikuwa mwepesi.—Mathayo 11:28-30.

Masimulizi ya Injili hufunua utu wa Yesu kwa njia ya kweli isiyoweza kukanushwa. Haingekuwa rahisi watu wanne walio tofauti kubuni hadithi ya mtu asiye wa kawaida kisha waeleze juu ya mtu huyo kwa njia yenye upatano katika masimulizi yao manne. Ingekuwa vigumu sana kwa waandishi wanne walio tofauti kueleza juu ya mtu yuleyule na waonyeshe kwa upatano jinsi alivyo, iwapo mtu huyo hakupata kuishi.

Mwanahistoria Michael Grant auliza swali hili linaloamsha fikira: ‘Inawezekanaje kwamba Injili zote zinasimulia waziwazi juu ya mwanamume kijana mwenye kuvutia aliyeshirikiana kwa uhuru na wanawake wa kila namna, kutia ndani wanawake ambao bila shaka walikuwa na sifa mbaya, pasipo wasiwasi wowote wala kuvutiwa nao, huku akidumisha maadili yanayofaa wakati wote?’ Jibu linalopatana na akili ni kwamba kwa kweli kulikuwa na mtu wa namna hiyo ambaye alijiendesha kama isemavyo Biblia.

Yule Yesu Halisi na Wakati Wako Ujao

Mbali na kutueleza maisha ya yule Yesu halisi alipokuwa duniani, Biblia huonyesha kwamba alikuweko kabla ya kuwa binadamu, akiwa Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu, “mzaliwa wa kwanza wa uumbaji wote.” (Wakolosai 1:15) Karne ishirini zilizopita, Mungu aliuhamisha uhai wa Mwana wake wa kimbingu na kuutia ndani ya tumbo la uzazi la bikira Myahudi ili mwana huyo azaliwe akiwa binadamu. (Mathayo 1:18) Wakati wa huduma yake duniani, Yesu alitangaza Ufalme wa Mungu kuwa suluhisho pekee kwa wanadamu wanaoteseka, naye aliwazoeza wanafunzi wake ili waendeleze kazi hiyo ya kuhubiri.—Mathayo 4:17; 10:5-7; 28:19, 20.

Katika Nisani 14 (karibu Aprili 1), 33 W.K., Yesu alikamatwa, akahukumiwa na kuuawa kwa shtaka bandia la uchochezi. (Mathayo 26:18-20, 48–27:50) Kifo cha Yesu ni fidia inayowakomboa wanadamu wenye imani kutoka kwenye dhambi na hivyo kuwawezesha kupata uhai udumuo milele wote wanaodhihirisha imani katika yeye. (Waroma 3:23, 24; 1 Yohana 2:2) Katika Nisani 16, Yesu alifufuliwa, na muda mfupi baada ya hapo akapaa mbinguni. (Marko 16:1-8; Luka 24:50-53; Matendo 1:6-9) Akiwa Mfalme aliyewekwa rasmi na Yehova, Yesu aliyefufuliwa ana mamlaka kamili ya kutekeleza kusudi la Mungu la awali kwa mwanadamu. (Isaya 9:6, 7; Luka 1:32, 33) Naam, Biblia huonyesha kwamba Yesu ndiye yule mtu mkuu atakayetumiwa kutimiza makusudi ya Mungu.

Katika karne ya kwanza, umati wa watu ulimkubali Yesu kuwa Mesiya aliyeahidiwa, au Kristo, aliyetumwa duniani kutetea enzi kuu ya Yehova na kufa akiwa fidia kwa ajili ya wanadamu. (Mathayo 20:28; Luka 2:25-32; Yohana 17:25, 26; 18:37) Kwa sababu ya mnyanyaso mkali, watu hawangekubali kuwa wanafunzi wa Yesu kama hawakuwa na uhakika yeye ni nani. Kwa ujasiri na kwa bidii, walikubali kutekeleza utume aliowapa, wa ‘kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.’—Mathayo 28:19.

Leo, mamilioni ya Wakristo wanyofu na wenye ujuzi wanafahamu kwamba Yesu si mtu anayetajwa tu katika hekaya. Wanamkubali kuwa Mfalme aliyewekwa katika kiti cha Ufalme wa Mungu huko mbinguni, ambaye karibuni atatawala dunia. Serikali hiyo iliyosimamishwa na Mungu ni habari njema zinazothaminiwa sana kwa sababu itatatua matatizo ya ulimwengu. Wakristo wa kweli hudhihirisha kwamba wanaunga mkono kwa uaminifu Mfalme aliyechaguliwa na Yehova kwa kutangaza “habari njema hii ya ufalme” kwa wengine.—Mathayo 24:14.

Wale wanaounga mkono Ufalme huo kupitia Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai, wataishi na kufurahia manufaa za milele. Hata wewe unaweza kupokea manufaa hizo! Wachapishaji wa gazeti hili watafurahi kukusaidia kumjua yule Yesu halisi.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Kwa habari zaidi kuhusu masimulizi ya Injili, ona sura ya 5 hadi ya 7 ya kitabu Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu?, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6]

Yale Ambayo Wengine Wamesema

‘Ninamwona Yesu wa Nazareti kuwa mmojawapo wa walimu wakuu zaidi ambao wamepata kuishi ulimwenguni. . . . Nitawaambia Wahindu kwamba maisha yenu hayatakuwa kamili msipojifunza mafundisho ya Yesu.’—Mohandas K. Gandhi, The Message of Jesus Christ.

“Mtu aliye mbunifu sana, kamili, mwenye kutegemeka, mkamilifu, mwenye ubinadamu na hata hivyo anayezidi sana wanadamu wote kwa ukuu, haiwezekani alikuwa mtu bandia wala mtu wa kuwaziwa tu. . . . Ingebidi kuwe na mtu mwenye uwezo kuliko Yesu ili kumbuni Yesu.”—Philip Schaff, History of the Christian Church.

“Kwamba wanaume wachache wa kawaida wangeweza kwa kizazi kimoja kubuni mtu mwenye nguvu na mwenye uvutano mwingi kadiri hiyo, mwenye maadili ya hali ya juu kadiri hiyo na mtu mwenye kuonyesha ubinadamu sana kwa kadiri hiyo, ungekuwa muujiza wenye kustaajabisha mno zaidi ya wowote ulioandikwa katika Gospeli.”—Will Durant, Ceasar and Christ.

‘Huenda likaonekana kuwa jambo lisiloeleweka kwamba mtu wa kuwaziwa tu ambaye hajawahi kuishi angeweza kufaulu kuanzisha kundi la kidini linalopatikana ulimwenguni pote kwani watu wengi sana wamejaribu kufanya hivyo wakashindwa.’—Gregg Easterbrook, Beside Still Waters.

“Nikiwa mwanahistoria wa fasihi ninasadiki kabisa kwamba Gospeli si hekaya hata kidogo. Si za ubunifu vya kutosha kuwa hekaya. . . . Kuna mambo mengi tusiyoyajua kuhusu maisha ya Yesu, na watu wenye kubuni hekaya hawangekosa kueleza habari zote kuhusu maisha yake.”—C. S. Lewis, Mere Christianity.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Injili hufunua hisia mbalimbali za Yesu