Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Endelea Kuonyesha Sifa ya Wema

Endelea Kuonyesha Sifa ya Wema

Endelea Kuonyesha Sifa ya Wema

“Matunda ya nuru huwa yana kila namna ya wema na uadilifu na kweli.”—WAEFESO 5:9.

1. Mamilioni ya watu leo wanaonyeshaje kwamba wanakubaliana na andiko la Zaburi 31:19?

KUMTUKUZA Yehova ndilo jambo jema zaidi ambalo mwanadamu yeyote anaweza kufanya. Leo, mamilioni ya watu wanafanya hivyo kwa kumsifu Mungu kwa wema wake. Tukiwa Mashahidi wa Yehova waaminifu-washikamanifu, tunakubaliana kwa moyo wote na mtunga-zaburi aliyeimba: “Jinsi gani ulivyo mwingi wema wako, uliowawekea wale wanaokucha!”—Zaburi 31:19, BHN.

2, 3. Ni nini kiwezacho kutukia ikiwa kazi yetu ya kufanya wanafunzi haiambatani na matendo mazuri?

2 Hofu yenye staha kwa Yehova hutuchochea tumsifu kwa wema wake. Pia hutuchochea ‘kumshukuru BWANA, kumhimidi, na kujulisha utukufu wa ufalme wake.’ (Zaburi 145:10-13) Ndiyo sababu sisi hushiriki kwa bidii kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Bila shaka, ni lazima kazi yetu ya kuhubiri iambatane na mwenendo mzuri. La sivyo, tunaweza kuliletea suto jina takatifu la Yehova.

3 Watu wengi hudai kumwabudu Mungu, lakini mwenendo wao auambatani na viwango ambavyo vimeonyeshwa katika Neno lake lililopuliziwa. Paulo aliandika hivi kuhusu watu fulani ambao hawakuishi kupatana na madai yao ya kufanya lililo jema: “Je, wewe unayemfundisha mtu mwingine, hujifundishi mwenyewe? Wewe, unayehubiri ‘Usiibe,’ je, wewe huiba? Wewe, unayesema ‘Usifanye uzinzi,’ je, wewe hufanya uzinzi? . . . ‘Jina la Mungu linafanyiwa kufuru miongoni mwa mataifa kwa sababu ya nyinyi watu’; kama vile imeandikwa.”—Waroma 2:21, 22, 24.

4. Mwenendo wetu mzuri una matokeo gani?

4 Badala ya kuliletea suto jina la Yehova, sisi hujitahidi kulitukuza kwa mwenendo wetu mzuri. Jambo hilo huwa na matokeo mazuri kwa wale walio nje ya kutaniko la Kikristo. Kwanza, mwenendo wetu mzuri husaidia kuwanyamazisha wapinzani. (1 Petro 2:15) Jambo lililo muhimu hata zaidi ni kwamba mwenendo wetu mzuri huvuta watu kwenye tengenezo la Yehova, na hivyo wanaweza kumtukuza na kupata uhai udumuo milele.—Matendo 13:48.

5. Tunapaswa kuchunguza maswali gani sasa?

5 Kwa kuwa sisi si wakamilifu, tunawezaje kuepuka mwenendo unaoweza kumvunjia Yehova heshima na kukwaza watu wanaotafuta ile kweli? Naam, tunaweza kufanikiwaje kuonyesha sifa ya wema?

Tunda la Nuru

6. “Kazi zisizozaa matunda zilizo za giza” ni zipi, lakini Wakristo wanapaswa kuonyesha matunda gani?

6 Tukiwa Wakristo waliojiweka wakfu, tuna jambo fulani linalotusaidia kuepuka “kazi zisizozaa matunda zilizo za giza.” Kazi hizo zinatia ndani mambo yanayomvunjia Mungu heshima kama vile kusema uwongo, kuiba, usemi wenye kuudhi, mazungumzo yasiyofaa kuhusu ngono, mwenendo wa aibu, kufanya mzaha wenye aibu, na ulevi. (Waefeso 4:25, 28, 31; 5:3, 4, 11, 12, 18) Badala ya kushiriki mambo hayo, sisi ‘tunaendelea kutembea kama watoto wa nuru.’ Mtume Paulo anasema kwamba “matunda ya nuru huwa yana kila namna ya wema na uadilifu na kweli.” (Waefeso 5:8, 9) Kwa hiyo tunaweza kuendelea kuonyesha sifa ya wema kwa kutembea katika nuru. Lakini hii ni nuru ya aina gani?

7. Ni nini tunachopaswa kufanya ili kuendelea kuonyesha tunda la wema?

7 Licha ya kasoro zetu, tunaweza kuonyesha sifa ya wema kwa kutembea katika nuru ya kiroho. “Neno lako ni taa ya miguu yangu, na mwanga wa njia yangu,” akaimba mtunga-zaburi. (Zaburi 119:105) Ikiwa tunataka kuendelea “kuonyesha matunda ya nuru” kupitia “kila namna ya wema,” tunapaswa kutumia kwa ukawaida nuru ya kiroho inayopatikana katika Neno la Mungu, ambalo linafafanuliwa vizuri katika vichapo vya Kikristo, na huzungumziwa kwa ukawaida kwenye mikutano yetu ya ibada. (Luka 12:42; Waroma 15:4; Waebrania 10:24, 25) Tunapaswa pia kuzingatia kwa makini kielelezo na mafundisho ya Yesu Kristo, aliye “nuru ya ulimwengu” na “mrudisho wa utukufu wa [Yehova].”—Yohana 8:12; Waebrania 1:1-3.

Tunda la Roho

8. Kwa nini tunaweza kuonyesha sifa ya wema?

8 Bila shaka, nuru ya kiroho hutusaidia kuonyesha sifa ya wema. Isitoshe, tunaweza kuonyesha sifa hiyo kwa sababu tunaongozwa na roho takatifu, au nguvu ya utendaji ya Mungu. Sifa ya wema ni sehemu ya “matunda ya roho.” (Wagalatia 5:22, 23) Tukijitiisha chini ya mwongozo wa roho takatifu ya Yehova, roho hiyo itatokeza ndani yetu lile tunda zuri la wema.

9. Tunawezaje kutenda kupatana na maneno ya Yesu katika andiko la Luka 11:9-13?

9 Tamaa yetu nyingi ya kutaka kumpendeza Yehova kwa kuonyesha tunda la roho la wema yapaswa kutuchochea kutenda kupatana na maneno haya ya Yesu: “Fulizeni kuomba, nanyi mtapewa; fulizeni kutafuta sana, nanyi mtapata; fulizeni kubisha hodi, nanyi mtafunguliwa. Kwa maana kila mtu anayeomba hupokea, na kila mtu anayetafuta sana hupata, na kwa kila mtu anayebisha hodi hufunguliwa. Kwa kweli, ni baba yupi miongoni mwenu ambaye, ikiwa mwana wake aomba samaki, labda atampa nyoka badala ya samaki? Au ikiwa pia aomba yai, atampa nge? Kwa hiyo, ikiwa nyinyi, mjapokuwa [watu wasio wakamilifu na hivyo waovu kwa kulinganishwa na Mungu], mwajua jinsi ya kuwapa watoto wenu zawadi zilizo njema, je, si zaidi sana yule Baba aliye mbinguni atawapa roho takatifu wale wanaomwomba!” (Luka 11:9-13) Na tufuate ushauri wa Yesu kwa kusali tupate roho ya Yehova ili tuweze kuendelea kuonyesha tunda la wema.

“Fuliza Kufanya Lililo Jema”

10. Ni sehemu zipi za wema wa Yehova ambazo zinatajwa kwenye kitabu cha Kutoka 34:6, 7?

10 Tunaweza ‘kufuliza kufanya lililo jema’ kwa kutumia nuru ya kiroho kutoka katika Neno la Mungu na kwa msaada wa roho takatifu ya Mungu. (Waroma 13:3) Kupitia funzo la Biblia la ukawaida, tunajifunza mengi zaidi kuhusu jinsi tunavyoweza kuiga wema wa Yehova. Makala iliyotangulia ilizungumzia sehemu mbalimbali za wema wa Mungu kama unavyotajwa katika tangazo ambalo Musa aliandika kwenye kitabu cha Kutoka 34:6, 7, ambapo tunasoma: “BWANA, BWANA, Mungu mwingi wa huruma [“rehema,” NW], mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema [“fadhili-upendo,” NW] na kweli; mwenye kuwaonea huruma [“huwaonyesha fadhili-upendo,” NW] watu elfu elfu, mwenye kusamehe uovu na makosa na dhambi; wala si mwenye kumhesabia mtu mwovu kuwa hana hatia kamwe.” Tutasaidiwa ‘kufuliza kufanya lililo jema’ kwa kuchunguza sehemu hizi mbalimbali za wema wa Yehova.

11. Tunapaswa kuathiriwaje kwa kujua kwamba Yehova ni mwenye rehema na mwenye fadhili?

11 Tangazo hilo la Mungu hutusaidia kuona uhitaji wa kumwiga Yehova kwa kuwa wenye rehema na wenye fadhili. Yesu alisema, “Wenye furaha ni wenye rehema, kwa kuwa wao wataonyeshwa rehema.” (Mathayo 5:7; Luka 6:36) Kwa kuwa tunajua kwamba Yehova ni mwenye fadhili, tunachochewa kuwa wenye fadhili na urafiki tunaposhughulika na wengine, kutia ndani watu tunaowahubiria. Jambo hilo linapatana na ushauri huu wa Paulo: “Acheni tamko lenu liwe na [fadhili] sikuzote, lenye kukolezwa chumvi, ili kujua jinsi mpaswavyo kumpa jibu kila mmoja.”—Wakolosai 4:6.

12. (a) Kwa kuwa Mungu si mwepesi wa hasira, tunapaswa kuwatendeaje wengine? (b) Fadhili-upendo za Yehova hutuchochea kufanya nini?

12 Kwa kuwa Mungu si mwepesi wa hasira, ‘kufuliza kufanya lililo jema’ hutuchochea kuvumilia kasoro ndogo-ndogo za waamini wenzetu na kukazia fikira sifa zao nzuri. (Mathayo 7:5; Yakobo 1:19) Fadhili-upendo za Yehova hutuchochea kuonyesha upendo mwaminifu-mshikamanifu, hata chini ya hali ngumu sana. Bila shaka, jambo hilo linapendeza sana.—Mithali 19:22.

13. Twapaswa kutendaje kuonyesha kwamba Yehova ni ‘mwingi wa kweli’?

13 Kwa kuwa Baba yetu wa mbinguni ni ‘mwingi wa kweli,’ sisi hujitahidi ‘kujipendekeza wenyewe kuwa wahudumu wa Mungu kwa kusema kweli.’ (2 Wakorintho 6:3-7) “Ulimi wa uongo” na “shahidi wa uongo asemaye uongo” ni baadhi ya mambo saba ambayo Yehova huchukia. (Mithali 6:16-19) Kwa hiyo tamaa yetu ya kutaka kumpendeza Yehova imetuchochea ‘kuweka mbali ukosefu wa lililo kweli na kusema kweli.’ (Waefeso 4:25) Na tuonyeshe sifa ya wema katika njia hiyo muhimu.

14. Kwa nini tuwe wenye kusamehe?

14 Tangazo la Mungu kwa Musa linapaswa kutuchochea tuwe wenye kusamehe kwa kuwa Yehova yu tayari kusamehe. (Mathayo 6:14, 15) Bila shaka, Yehova huwaadhibu watenda-dhambi wasiotubu. Kwa hiyo, ni lazima tufuate viwango vyake vya wema kuhusiana na kudumisha usafi wa kiroho wa kutaniko—Mambo ya Walawi 5:1; 1 Wakorintho 5:11, 12; 1 Timotheo 5:22.

“Fulizeni Kuangalia Sana”

15, 16. Ushauri wa Paulo kwenye andiko la Waefeso 5:15-19 unaweza kutusaidiaje kuendelea kuonyesha sifa ya wema?

15 Ili kuendelea kudumisha sifa ya wema katika ulimwengu mwovu unaotuzunguka, tunahitaji kujazwa roho ya Mungu na kuangalia jinsi tunavyotembea. Hivyo, Paulo aliwahimiza Wakristo wa Efeso hivi: “Fulizeni kuangalia sana kwamba jinsi mnavyotembea si kama wasio na hekima bali kama watu wenye hekima, mkijinunulia kabisa wakati unaofaa, kwa sababu siku ni za uovu. Kwa ajili ya hili acheni kuwa wenye kukosa akili, bali endeleeni kufahamu mapenzi ya Yehova ni nini. Pia, msiwe mkilewa divai, ambayo katika hiyo mna ufasiki, bali fulizeni kujazwa roho, mkijisemesha nyinyi wenyewe kwa zaburi na sifa kwa Mungu na nyimbo za kiroho, mkiimba na kufuatanisha sauti zenu wenyewe na muziki katika mioyo yenu kwa Yehova.” (Waefeso 5:15-19) Bila shaka, ushauri huo unatufaa siku hizi za mwisho zilizo hatari.—2 Timotheo 3:1.

16 Ikiwa tutaendelea kuonyesha sifa ya wema, tunapaswa kuwa waangalifu sana ili tutembee kama watu walio na hekima ya Mungu. (Yakobo 3:17) Tunapaswa kuepuka dhambi nzito na tunapaswa kujazwa roho takatifu, na kuacha ituongoze. (Wagalatia 5:19-25) Kwa kutumia mafundisho ya kiroho tunayopata kwenye mikutano, makusanyiko, na mikusanyiko ya Kikristo tunaweza kuendelea kufanya lililo jema. Maneno ya Paulo kwa Waefeso yanaweza pia kutukumbusha kwamba sisi hunufaika sana tunapoimba “nyimbo za kiroho” kutoka moyoni kwenye mingi ya mikutano yetu ya ibada. Nyingi za nyimbo hizo hukazia sifa za kiroho kama vile wema.

17. Wakristo walio wagonjwa sana wanaweza kuwa na uhakika wa jambo gani hata kama hawawezi kuhudhuria mikutano kwa ukawaida?

17 Namna gani waamini wenzetu wasioweza kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida kwa sababu ni wagonjwa sana? Huenda wakavunjika moyo kwa sababu hawawezi kumwabudu Yehova sikuzote kwa kushirikiana moja kwa moja na ndugu na dada zao wa kiroho. Lakini wanaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova anaelewa hali zao, atawasaidia wadumu katika kweli, atawapa roho yake takatifu, na kuwasaidia waendelee kufanya lililo jema.—Isaya 57:15.

18. Ni nini kitakachotusaidia kuendelea kutenda wema?

18 Ili kuendelea kutenda wema tunahitaji kuwa waangalifu kuhusu mashirika yetu na kuepuka watu “wasio na upendo wa mema.” (2 Timotheo 3:2-5; 1 Wakorintho 15:33) Kutumia ushauri huo hutusaidia kuepuka ‘kuitia kihoro roho takatifu ya Mungu’ kwa kutenda kinyume cha mwongozo wa roho hiyo. (Waefeso 4:30) Isitoshe, tunasaidiwa kufanya lililo jema ikiwa tutashirikiana kwa ukaribu na watu ambao maisha yao yanaonyesha kwamba wanapenda wema na wanaongozwa na roho takatifu ya Yehova.—Amosi 5:15; Waroma 8:14; Wagalatia 5:18.

Sifa ya Wema Huleta Matokeo Mema

19-21. Simulia mambo yaliyoonwa yanayoonyesha matokeo ya kuonyesha sifa ya wema.

19 Kutembea katika nuru ya kiroho, kuacha roho ya Mungu ituongoze, na kuangalia jinsi tunavyotembea kutatusaidia kuepuka yaliyo mabaya na ‘kufuliza kufanya lililo jema.’ Kufanya hivyo huleta matokeo mema. Hebu fikiria kisa cha Zongezile, ambaye ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova huko Afrika Kusini. Asubuhi moja alipokuwa akienda shuleni, alipitia kwenye benki kuangalia pesa kidogo alizokuwa nazo akibani. Mashine ya kutunza na kutoa pesa ilionyesha kimakosa kwamba alikuwa na pesa za ziada, dola 6,000 za Marekani. Mlinzi wa benki na watu wengine walimhimiza atoe pesa hizo na kujiwekea akiba katika benki nyingine. Wenzi wa ndoa aliokuwa akiishi nao, ambao ni Mashahidi, ndio tu waliompongeza kwa kutotoa pesa hizo.

20 Siku iliyofuata, Zongezile alijulisha wasimamizi wa benki kosa hilo. Iligunduliwa kwamba namba ya akaunti ya Zongezile ilikuwa sawa na ya mfanya-biashara tajiri ambaye aliweka pesa hizo kimakosa kwenye akaunti ya Zongezile. Mfanya-biashara huyo alistaajabu kwamba Zongezile hakutumia pesa hizo, na kumwuliza: “Wewe ni wa dini gani?” Zongezile alimjibu kwamba yeye ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Wasimamizi wa benki walimpongeza sana na kusema: “Laiti watu wote wangekuwa wanyofu kama Mashahidi wa Yehova.” Ni kweli kwamba matendo ya unyofu na ya wema yanaweza kufanya wengine wamtukuze Yehova.—Waebrania 13:18.

21 Si lazima matendo ya wema yawe ya kipekee ili yawe na matokeo mazuri. Kwa mfano: Shahidi mmoja mchanga ambaye ni mweneza-evanjeli wa wakati wote alienda kwenye hospitali moja katika kimojawapo cha visiwa vya Samoa. Watu walikuwa wanangojea kumwona daktari, naye Shahidi huyo aliona kwamba mwanamke mmoja mzee-mzee aliyekuwa ameketi karibu naye alikuwa mgonjwa sana. Zamu ya Shahidi huyo ya kumwona daktari ilipofika, alimruhusu mwanamke huyo amtangulie ili aweze kupata matibabu haraka. Baadaye, Shahidi huyo alikutana na mwanamke huyo mzee-mzee sokoni. Mwanamke huyo alikumbuka jinsi alivyotendewa kwa wema huko hospitalini. “Sasa ninajua kwamba Mashahidi wa Yehova wanawapenda jirani zao kikweli,” akasema. Ingawa hapo awali mwanamke huyo hakuwa anapendezwa na ujumbe wa Ufalme, wema alioonyeshwa na Shahidi huyo ulikuwa na matokeo mazuri. Alikubali funzo la Biblia nyumbani na akaanza kujifunza Neno la Mungu.

22. Ni ipi njia moja muhimu hasa ya ‘kufuliza kufanya lililo jema’?

22 Pengine hata wewe una mambo yaliyoonwa yanayoonyesha manufaa ya kuonyesha sifa ya wema. Njia moja muhimu hasa ya ‘kufuliza kufanya lililo jema’ ni kushiriki kwa ukawaida kutangaza habari njema za Ufalme wa Mungu. (Mathayo 24:14) Na tuendelee kufanya kazi hii yenye thamani, tukijua kwamba hiyo ni njia moja ya kufanya lililo jema, hasa kwa wale wanaotusikiliza. Jambo lililo muhimu hata zaidi ni kwamba huduma yetu na mwenendo wetu mwema humtukuza Yehova, chanzo cha wema.—Mathayo 19:16, 17.

Endeleeni “Kufanya Lililo Jema”

23. Kwa nini huduma ya Kikristo ni kazi njema?

23 Bila shaka huduma yetu ni kazi njema. Inaweza kutuokoa na pia kuwaokoa wale wanaosikiliza ujumbe wa Biblia na hivyo kuwa na matarajio ya kupata uhai udumuo milele. (Mathayo 7:13, 14; 1 Timotheo 4:16) Tunapokabili maamuzi, huenda tamaa ya kufanya lililo jema ikafanya tujiulize hivi: ‘Uamuzi huu utaathirije kazi yangu ya kuhubiri Ufalme? Je, uamuzi ninaotaka kufanya ni wa hekima kweli? Je, utafanya iwe rahisi kwangu kuwasaidia wengine wakubali “habari njema idumuyo milele” na kuwa na uhusiano wa karibu na Yehova Mungu?’ (Ufunuo 14:6) Utapata furaha kubwa kwa kufanya uamuzi unaoendeleza masilahi ya Ufalme.—Mathayo 6:33; Matendo 20:35.

24, 25. Ni kwa njia zipi tunaweza kufanya wema kutanikoni, na tunaweza kuwa na uhakika wa jambo gani ikiwa tutaendelea kuonyesha sifa ya wema?

24 Na tusipuuze kamwe manufaa ya sifa ya wema. Tunaweza kuendelea kuonyesha sifa hiyo kwa kuliunga mkono kutaniko la Kikristo na kufanya yale tuwezayo ili kuliweka katika hali nzuri. Bila shaka, tunafanya vyema kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida na kushiriki kwa kutoa maelezo. Kuwepo kwetu kwenye mikutano huwatia moyo waabudu wenzetu, nayo maelezo yetu yaliyotayarishwa vizuri huwajenga kiroho. Tunafanya vyema pia tunapotumia mali zetu kudumisha Jumba la Ufalme katika hali nzuri na kusaidia kulitunza ifaavyo. (2 Wafalme 22:3-7; 2 Wakorintho 9:6, 7) Naam, “kwa kweli maadamu tuna wakati wenye kufaa kwa ajili ya hilo, acheni sisi tufanye lililo jema kuelekea wote, lakini hasa kuelekea wale ambao katika imani ni jamaa zetu.”—Wagalatia 6:10.

25 Hatuwezi kujua kimbele kila hali ambayo itahitaji tuonyeshe sifa ya wema. Basi, tukabilipo magumu mapya, na tutafute ujuzi kutoka katika Maandiko, tuombe roho takatifu ya Yehova, na kufanya yote tuwezayo kutimiza mapenzi yake mema na makamilifu. (Waroma 2:9, 10; 12:2) Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatubariki sana tunapoendelea kuonyesha sifa ya wema.

Ungejibuje?

• Tunawezaje kutimiza jambo lililo jema zaidi?

• Kwa nini sifa ya wema inaitwa ‘tunda la nuru’?

• Kwa nini sifa ya wema inaitwa ‘tunda la roho’?

• Mwenendo wetu mwema una matokeo gani?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 17]

Neno la Mungu na roho yake takatifu hutusaidia kuonyesha sifa ya wema

[Picha katika ukurasa wa 18]

Kuonyesha sifa ya wema huleta matokeo mema