Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unamtumaini Mungu Aliye Halisi?

Je, Unamtumaini Mungu Aliye Halisi?

Je, Unamtumaini Mungu Aliye Halisi?

Wavumbuzi walifunga safari ya uvumbuzi iliyopangwa na wafanyakazi wa Jumba la Makumbusho la Marekani la Historia ya Asili ili kuchunguza nchi ya Aktiki, ambayo Robert E. Peary alisema kwamba alikuwa ameiona miaka saba mapema, katika mwaka wa 1906.

AKIWA kwenye Rasi ya Colgate iliyo kaskazini-magharibi mwa Amerika ya Kaskazini, Peary aliona vitu kama vilele vyeupe vya nchi ya mbali. Aliita nchi hiyo Crocker, jina la mfadhili wake. Wavumbuzi hao walifurahi kama nini walipoona kwa mbali eneo lenye milima, mabonde, na vilele vya milima vilivyofunikwa kwa theluji! Lakini punde si punde Peary na wenzake walitambua kwamba macho yao yalikuwa yakiwadanganya na tayari walikuwa wametumia wakati, nguvu, na mali nyingi wakijaribu kuvumbua kitu ambacho si halisi.

Leo, watu wengi hujitoa na hata kutumia wakati wao kuabudu miungu wanayoamini kuwa ni halisi. Katika siku za mitume wa Yesu, watu waliabudu miungu kama vile Hermesi na Zeusi. (Matendo 14:11, 12) Leo, mamilioni ya miungu huabudiwa na Washinto, Wahindu na watu wa dini nyinginezo ulimwenguni. Kwa kweli, kama isemavyo Biblia, ‘kuna “miungu” mingi na “mabwana” wengi.’ (1 Wakorintho 8:5, 6) Je, miungu hii yote yaweza kuwa halisi?

Miungu ‘Isiyoweza Kuokoa’

Kwa mfano, fikiria matumizi ya sanamu au mifano katika ibada. Watu wanaotumaini sanamu hizo huziona kuwa waokozi wenye uwezo unaopita wa kibinadamu wanaoweza kuwathawabisha watu au kuwaokoa kutoka kwa hatari. Lakini je, kweli sanamu hizo zinaweza kuokoa? Mtunga-zaburi aliimba hivi kuhusu sanamu hizo: “Sanamu za mataifa ni fedha na dhahabu, kazi ya mikono ya wanadamu. Zina vinywa lakini hazisemi, zina macho lakini hazioni, zina masikio lakini hazisikii, wala hamna pumzi vinywani mwake.” Kwa kweli ni miungu ‘isiyoweza kuokoa.’—Zaburi 135:15-17; Isaya 45:20.

Ni kweli kwamba, watu wanaochonga sanamu huenda wakasema zina uhai na uwezo. Nao wanaoziabudu huzitumaini. ‘Huichukua sanamu begani, huisimamisha mahali pake, ikasimama,’ akasema nabii Isaya. Aliongeza kusema: ‘Haitaondoka katika mahali pake, naam, mmoja atamwita, lakini hawezi kujibu, wala kumwokoa na taabu yake.’ (Isaya 46:7) Ukweli ni kwamba sanamu hazina uhai hata kama wale wanaozitumaini wanaamini kwa dhati kwamba zina uhai. Sanamu hizo za kuchongwa na za kuyeyushwa ni “miungu isiyofaa.”—Habakuki 2:18, NW.

Leo pia, ni jambo la kawaida kuwatukuza watumbuizaji, wanamichezo, mifumo ya kisiasa, na viongozi fulani wa kidini. Isitoshe, wengi huabudu pesa. Katika visa hivyo vyote, sanamu hizo hupewa sifa isivyostahili. Sanamu hizo haziwezi kuwasaidia kamwe wale wanaozitumaini. Kwa mfano, huenda pesa zikaonekana kuwa suluhisho kwa matatizo mengi, lakini nguvu za mali ni zenye udanganyifu. (Marko 4:19) Mtafiti mmoja aliuliza hivi: ‘Inakuwaje kwamba kitu kinachotamaniwa sana na watu wengi, na kinachoaminika kuwa kinaweza kutatua matatizo yote, kinapopatikana kinatamausha na kufadhaisha watu?’ Naam, huenda kufuatia mali kukamfanya mtu apuuze mambo yenye thamani ya kweli, kama vile afya njema, maisha ya familia yenye furaha, marafiki wa karibu, au uhusiano wenye thamani na Muumba. Kuabudu fedha na mali ni sawa na kuabudu ‘sanamu isiyo ya kweli’!—Yona 2:8, NW.

‘Hapakuwa na Aliyejibu’

Ni upumbavu kusema kwamba kitu kisicho halisi ni halisi. Waabudu wa mungu Baali katika siku za nabii Eliya walijifunza ukweli wa jambo hilo baada ya kupata magumu. Waliamini kwa dhati kwamba Baali alikuwa na uwezo wa kufanya moto ushuke kutoka mbinguni na kuteketeza dhabihu ya mnyama. Hata ‘waliliitia jina la Baali tangu asubuhi hata adhuhuri, wakisema, Ee Baali, utusikie.’ Je, Baali alikuwa na masikio ya kusikia na kinywa cha kusema? Simulizi laendelea kusema: “Hapakuwa na sauti, wala aliyejibu.” Kwa kweli, ‘hapakuwa na aliyeangalia.’ (1 Wafalme 18:26, 29) Baali hakuwa halisi, hai, wala hangeweza kufanya chochote.

Ni muhimu kama nini tumjue na kumwabudu Mungu aliye halisi! Lakini yeye ni nani? Na twaweza kunufaikaje kwa kumtumaini?

[Picha katika ukurasa wa 3]

Rafiki ya Peary, Egingwah atazama hadi upeo wa macho ili aone nchi kavu

Robert E. Peary

[Hisani]

Egingwah: From the book The North Pole: Its Discovery in 1909 Under the Auspices of the Peary Arctic Club, 1910; Robert E. Peary: NOAA

[Picha katika ukurasa wa 4]

Wengi hudanganywa na sanamu zinazoabudiwa katika ulimwengu huu