Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ndugu Waliositawisha Mitazamo Tofauti

Ndugu Waliositawisha Mitazamo Tofauti

Ndugu Waliositawisha Mitazamo Tofauti

NI KWELI kwamba maamuzi yanayofanywa na wazazi huathiri watoto wao. Maamuzi ya wazazi leo huwaathiri watoto kama vile uamuzi uliofanywa katika bustani ya Edeni ulivyowaathiri wanadamu. Uasi wa Adamu na Hawa uliwaathiri sana wanadamu wote. (Mwanzo 2:15, 16; 3:1-6; Waroma 5:12) Hata hivyo, kila mmoja wetu anaweza kusitawisha uhusiano mzuri na Muumba wetu iwapo atachagua kufanya hivyo. Jambo hilo linaonyeshwa na masimulizi juu ya Kaini na Abeli, ndugu wa kwanza katika historia ya binadamu.

Biblia haisemi kama Mungu alizungumza na Adamu na Hawa baada ya kuwafukuza kutoka Edeni. Hata hivyo, Yehova alizungumza na wana wao. Yaelekea Kaini na Abeli waliambiwa na wazazi wao mambo yaliyotukia. Wangeweza kuwaona “Makerubi upande wa mashariki wa bustani ya Edeni, na upanga wa moto uliogeuka huko na huko, kuilinda njia ya mti wa uzima.” (Mwanzo 3:24) Wanaume hao pia waliona utimizo wa maneno ya Mungu kwamba wanadamu wangeishi kwa jasho na kwa maumivu.—Mwanzo 3:16, 19.

Bila shaka Kaini na Abeli walijua maneno ambayo Yehova alimwambia nyoka: “Nitaweka uadui kati yako na huyo mwanamke, na kati ya uzao [“mbegu,” NW] wako na uzao [“mbegu,” NW] wake; huo utakuponda kichwa, na wewe utamponda kisigino.” (Mwanzo 3:15) Mambo ambayo Kaini na Abeli walijua kumhusu Yehova yangewasaidia kusitawisha uhusiano mzuri pamoja naye.

Bila shaka, kutafakari juu ya unabii wa Yehova na sifa zake akiwa Mfadhili mwenye upendo kuliwachochea Kaini na Abeli watamani kibali cha Mungu. Lakini wangesitawisha tamaa hiyo kwa kadiri gani? Je, wangetenda kulingana na tamaa waliorithi ya kumwabudu Mungu na kusitawisha hali yao ya kiroho ili kuweza kuonyesha imani katika yeye?—Mathayo 5:3.

Ndugu Hao Watoa Dhabihu

Baada ya muda, Kaini na Abeli walimtolea Mungu dhabihu. Kaini alitoa matunda ya ardhi, naye Abeli akatoa wazao wa kwanza wa wanyama wake. (Mwanzo 4:3, 4) Huenda ikawa wanaume hao walikuwa na umri wa miaka 100, kwa kuwa Adamu alikuwa na umri wa miaka 130 alipomzaa mwanawe Sethi.—Mwanzo 4:25; 5:3.

Dhabihu za Kaini na Abeli zilionyesha kwamba walifahamu walikuwa watu wenye dhambi, waliohitaji kibali cha Mungu. Ni lazima wawe walifikiria ahadi ya Yehova kuhusu nyoka na Mbegu ya mwanamke. Hatujui Kaini na Abeli walijitahidi kadiri gani kusitawisha uhusiano unaofaa pamoja na Yehova. Lakini tunaweza kujua hisia za moyoni za kila mmoja wao kupitia jinsi Mungu alivyotenda kuelekea dhabihu zao.

Wasomi fulani wanadokeza kwamba Hawa alifikiri Kaini ndiye ile “mbegu” ambayo ingemharibu nyoka, kwa kuwa alipomzaa, alisema hivi: “Nimepata mtoto mwanamume kwa BWANA.” (Mwanzo 4:1) Ikiwa Kaini pia alifikiri hivyo, basi alikuwa amekosea kabisa. Kwa upande mwingine, Abeli alitoa dhabihu yake kwa imani. Hivyo, “kwa imani Abeli alimtolea Mungu dhabihu ya thamani kubwa zaidi kuliko Kaini.”—Waebrania 11:4.

Ndugu hao walikuwa tofauti sana. Abeli alikuwa na ufahamu wa kiroho lakini Kaini hakuwa nao. Hata mitazamo yao ilikuwa tofauti. Kwa hiyo, “Mwenyezi-Mungu akapendezwa na Abeli na dhabihu yake, lakini hakupendezwa na Kaini wala na dhabihu yake.” Yaelekea kwamba Kaini hakufikiria kwa uzito dhabihu yake, badala yake aliitoa tu ili kutimiza wajibu. Lakini Mungu hakubali ibada inayotolewa tu ili kutimiza wajibu. Kaini alikuwa amesitawisha moyo mbaya, na Yehova aliona kwamba alikuwa na nia mbaya. Mtazamo wa Kaini ulionekana wazi kupitia matendo yake wakati dhabihu yake ilipokataliwa. Badala ya kurekebisha mtazamo wake na nia yake, ‘Kaini alikasirika sana na uso wake ukakunjamana.’ (Mwanzo 4:5, BHN) Matendo yake yalionyesha alikuwa na mawazo na nia mbaya.

Onyo na Itikio

Kwa kuwa Mungu alijua mtazamo wa Kaini, yeye alimshauri hivi: “Kwa nini umekasirika, na kwa nini uso wako umekunjamana? Je, ukitenda vyema hutakubaliwa? Na usipotenda vyema, basi, dhambi inakuvizia mlangoni; inakutamani, lakini unapaswa kuishinda.”—Mwanzo 4:6,7, BHN.

Tunaweza kujifunza somo fulani kutokana na jambo hilo. Ni kweli kwamba dhambi hutuvizia mlangoni ikiwa tayari kutuangamiza. Hata hivyo, Mungu ametupatia uhuru wa kuchagua, na tunaweza kuchagua kufanya mambo yafaayo. Yehova alimwambia Kaini ‘atende vyema,’ lakini Yeye hakumlazimisha abadilike. Kaini alichagua yale aliyotaka kufanya.

Masimulizi hayo yaliyopuliziwa yanaendelea kusema: “Kaini akamwambia Habili [“Abeli,” NW] nduguye, [Twende uwandani]. Ikawa walipokuwapo uwandani, Kaini akamwinukia Habili nduguye, akamwua.” (Mwanzo 4:8) Hivyo, Kaini akawa mwuaji mkatili, asiyetii. Hakuonyesha majuto yoyote wakati Yehova alipomwuliza: ‘Yuko wapi Abeli ndugu yako?’ Badala yake, Kaini alimjibu hivi kikatili na bila heshima: “Sijui, mimi ni mlinzi wa ndugu yangu?” (Mwanzo 4:9) Ukatili wa Kaini ulifunuliwa aliposema uwongo waziwazi na kukataa kuhusika na kifo cha ndugu yake.

Yehova alimlaani Kaini na kumfukuza mbali na Edeni. Kwa sababu hiyo, yaonekana laana ambayo tayari ilikuwa imetolewa juu ya ardhi, ingefanya iwe vigumu hata zaidi kwa Kaini kulima na kupata mazao. Angekuwa mzururaji na mkimbizi duniani. Kaini alilalamika kwamba hukumu hiyo ilikuwa kali. Jambo hilo lilionyesha wasiwasi wake kwamba kifo cha ndugu yake kingelipizwa kisasi, lakini hakuonyesha toba ya kweli. Yehova alimtia Kaini “alama”—yaelekea alama hiyo ilikuwa agizo zito lililojulikana na kufuatwa na wengine na lililokusudiwa kuzuia asiuawe ili kulipiza kisasi.—Mwanzo 4:10-15.

Kisha Kaini “akatoka mbele za uso wa BWANA, akakaa katika nchi ya Nodi [“Ukimbizi,” NW] mbele ya Edeni.” (Mwanzo 4:16) Kaini alioa mmoja wa dada zake au mpwa wake, kisha akajenga jiji ambalo aliliita Enoki, jina la mtoto wake wa kwanza. Lameki aliyekuwa mzao wa Kaini alikuwa mwenye jeuri kama babu yake Kaini asiyemwogopa Mungu. Lakini ukoo wa Kaini uliangamizwa wakati wa Furiko la siku za Noa.—Mwanzo 4:17-24.

Masomo Kwetu

Tunaweza kujifunza mambo fulani kutokana na masimulizi ya Kaini na Abeli. Mtume Yohana anawashauri Wakristo wapendane, ‘wasiwe kama Kaini, ambaye alitokana na yule mwovu akamchinja ndugu yake. Kazi za Kaini zilikuwa mbovu, lakini zile za ndugu yake zilikuwa za uadilifu.’ Yohana pia anasema: “Kila mtu ambaye huchukia ndugu yake ni muua-binadamu-kikatili, nanyi mwajua kwamba hakuna muua-binadamu-kikatili aliye na uhai udumuo milele ukikaa katika yeye.” Naam, uhusiano wetu na Mungu na pia matazamio yetu ya wakati ujao huathiriwa na jinsi tunavyowatendea Wakristo wenzetu. Hatuwezi kumchukia yeyote wa waamini wenzetu na wakati huohuo tuwe na kibali cha Mungu.—1 Yohana 3:11-15; 4:20.

Bila shaka, Kaini na Abeli walilelewa katika mazingira yanayofanana, lakini Kaini hakuwa na imani katika Mungu. Kwa kweli, alidhihirisha roho ya Ibilisi, ambaye ndiye ‘muua-binadamu kikatili wa kwanza na baba ya uwongo.’ (Yohana 8:44) Mwenendo wa Kaini unaonyesha kwamba sote tunakabili uchaguzi, kwamba wale wanaochagua kutenda dhambi hujitenga na Mungu, na kwamba Yehova huwahukumu wasiotubu.

Kwa upande mwingine, Abeli alikuwa na imani katika Yehova. Naam, “kwa imani Abeli alimtolea Mungu dhabihu ya thamani kubwa zaidi kuliko Kaini, imani ambayo kupitia hiyo alitolewa ushahidi kwamba yeye alikuwa mwadilifu, Mungu akitoa ushahidi kwa habari ya zawadi zake.” Ingawa Maandiko hayanukuu maneno yoyote yaliyosemwa na Abeli, yeye “bado anasema” kupitia mfano bora wa imani yake.—Waebrania 11:4.

Abeli alikuwa wa kwanza kati ya watu wengi waliodumisha uaminifu-maadili. Damu yake ‘iliyomlilia Yehova kutoka katika ardhi,’ haijasahauliwa. (Mwanzo 4:10; Luka 11:48-51) Tukiwa na imani kama Abeli, sisi pia tunaweza kufurahia uhusiano wenye thamani na wenye kudumu pamoja na Yehova.

[Sanduku katika ukurasa wa 22]

MKULIMA NA MCHUNGAJI

Kulima ardhi na kutunza wanyama ni baadhi ya kazi ambazo Mungu alimpa Adamu. (Mwanzo 1:28; 2:15; 3:23) Mwanawe Kaini alikuwa mkulima, naye Abeli alikuwa mchungaji. (Mwanzo 4:2) Kwa kuwa kabla ya Furiko chakula cha mwanadamu kilikuwa matunda na mboga tu, kwa nini Abeli alifuga kondoo?—Mwanzo 1:29; 9:3, 4.

Kondoo wanahitaji kutunzwa na mwanadamu ili wakue vizuri. Kazi ya Abeli inaonyesha kwamba mwanadamu alifuga wanyama hao tangu hapo mwanzo. Maandiko hayaonyeshi kama wanadamu wa kwanza kabisa walitumia maziwa kama chakula, lakini hata wale wanaokula mboga pekee wanaweza kutumia manyoya ya kondoo. Nao kondoo wanapokufa, ngozi zao zinaweza kutumiwa kwa kazi mbalimbali. Kwa mfano, Mungu aliwavika Adamu na Hawa “mavazi ya ngozi.”—Mwanzo 3:21.

Vyovyote vile, ni jambo linalopatana na akili kusema kwamba mwanzoni Kaini na Abeli walifanya kazi kwa kushirikiana. Waliweza kuiandalia familia yao mavazi na chakula.

[Picha katika ukurasa wa 23]

‘Kazi za Kaini zilikuwa mbovu, lakini zile za ndugu yake zilikuwa za uadilifu’