Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, U Miongoni mwa Watu Wanaopendwa na Mungu?

Je, U Miongoni mwa Watu Wanaopendwa na Mungu?

Je, U Miongoni mwa Watu Wanaopendwa na Mungu?

“Yeye aliye na amri zangu na kuzishika, huyo ndiye ambaye hunipenda. Naye anipendaye mimi atapendwa na Baba yangu.”—YOHANA 14:21.

1, 2. (a) Yehova aliwaonyeshaje wanadamu upendo? (b) Yesu alianzisha nini usiku wa Nisani 14, mwaka wa 33 W.K.?

YEHOVA anawapenda wanadamu. Kwa kweli, anawapenda wanadamu “sana hivi kwamba a[li]toa Mwana mzaliwa-pekee wake, ili kila mtu anayedhihirisha imani katika yeye asipate kuangamizwa bali awe na uhai udumuo milele.” (Yohana 3:16) Wakati wa kuadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Kristo unapokaribia, Wakristo wa kweli wanapaswa kutambua hata zaidi kwamba Yehova “alitupenda akamtuma Mwana wake kuwa dhabihu yenye kufunika kwa ajili ya dhambi zetu.”—1 Yohana 4:10.

2 Usiku wa Nisani 14, mwaka wa 33 W.K., Yesu na mitume wake 12 walikutana katika chumba cha juu huko Yerusalemu kusherehekea Sikukuu ya Kupitwa, ili kukumbuka jinsi Waisraeli walivyokombolewa kutoka Misri. (Mathayo 26:17-20) Baada ya kusherehekea msherehekeo huo wa Kiyahudi, Yesu anamwambia Yuda Iskariote aondoke kisha anaanzisha mlo wa jioni wa kukumbukwa ambao ungekuwa Ukumbusho wa Kikristo wa kifo cha Kristo. * Akitumia mkate usiotiwa chachu na divai nyekundu kuwa mfano wa mwili na damu yake, Yesu alishiriki mlo huo pamoja na mitume wake 11 waliobaki. Habari zaidi kuhusu mlo huo zimeandikwa na Waandishi wa vitabu vya Injili, Mathayo, Marko, na Luka. Mtume Paulo pia aliandika kuhusu mlo huo na kuuita “mlo wa jioni wa Bwana.”—1 Wakorintho 11:20; Mathayo 26:26-28; Marko 14:22-25; Luka 22:19, 20.

3. Simulizi la mtume Yohana kuhusu saa za mwisho-mwisho ambazo Yesu alikuwa pamoja na wanafunzi wake kwenye chumba cha juu linatofautiana katika njia zipi muhimu na masimulizi ya wengine?

3 Mtume Yohana hakutaja kupitishwa kwa mkate na divai, labda kwa sababu wakati alipoandika simulizi lake la Injili (yapata mwaka wa 98 W.K.), tayari Wakristo wa mapema walikuwa wamezoea kufanya hivyo. (1 Wakorintho 11:23-26) Hata hivyo, akiwa amepuliziwa, ni Yohana peke yake anayetoa habari muhimu kuhusu mambo ambayo Yesu alisema na kufanya kabla na baada ya kuanzisha Ukumbusho wa kifo Chake. Habari hizo zenye kusisimua zinapatikana katika sura nyingi za Injili ya Yohana. Zinaonyesha waziwazi ni watu wa aina gani wanaopendwa na Mungu. Na tuchunguze Yohana sura ya 13 hadi 17.

Jifunze Kutokana na Upendo Bora wa Yesu

4. (a) Yohana alikaziaje kichwa kikuu cha mkutano ambao Yesu alifanya pamoja na wanafunzi wake alipoanzisha Ukumbusho? (b) Ni ipi sababu moja kubwa inayofanya Yehova ampende Yesu?

4 Upendo umekaziwa sana katika sura hizo zenye mashauri ambayo Yesu alitoa kuwaaga wafuasi wake. Kwa kweli, maneno mbalimbali yanayohusiana na “upendo” yametajwa mara 31. Katika sura hizo, twaona waziwazi upendo mwingi ambao Yesu alikuwa nao kwa Baba yake, Yehova, na kwa wanafunzi wake. Katika masimulizi ya Injili, twaona waziwazi upendo wa Yesu kwa Yehova, lakini ni Yohana pekee aliyeandika maneno haya ya Yesu yaliyo wazi: “Nampenda Baba.” (Yohana 14:31) Yesu alisema pia kwamba Yehova anampenda na akaeleza sababu. Alisema: “Kama vile Baba amenipenda mimi nami nimewapenda nyinyi, kaeni katika upendo wangu. Mkishika amri zangu, mtakaa katika upendo wangu, kama vile mimi nimeshika amri za Baba na kukaa katika upendo wake.” (Yohana 15:9, 10) Naam, Yehova anampenda Mwana wake kwa kuwa Mwana huyo humtii kabisa. Ni somo zuri kama nini kwa wafuasi wote wa Yesu Kristo!

5. Yesu alionyeshaje upendo kwa wanafunzi wake?

5 Upendo mwingi ambao Yesu alikuwa nao kwa wafuasi wake, unakaziwa mwanzoni kabisa mwa simulizi la Yohana kuhusu mkutano wa mwisho ambao Yesu alifanya na mitume wake. Yohana alisema: “Sasa, kwa sababu alijua kabla ya msherehekeo wa sikukuu ya kupitwa kwamba saa yake ilikuwa imekuja ya kuhama kutoka katika ulimwengu huu kwenda kwa Baba, Yesu, akiisha kuwa amependa walio wake mwenyewe waliokuwa ulimwenguni, aliwapenda hadi mwisho.” (Yohana 13:1) Katika jioni hiyo ya kukumbukwa, aliwafundisha somo lenye thamani la kuwatumikia wengine kwa upendo. Aliwaosha miguu. Kila mmoja wao angekuwa tayari kumwosha Yesu miguu na kuwaosha ndugu zake pia, lakini walisita kufanya hivyo. Yesu alifanya kazi hiyo ya chini kisha akawaambia wanafunzi wake hivi: “Ikiwa mimi, nijapokuwa Bwana na Mwalimu, niliosha miguu yenu, nyinyi pia mwapaswa kuoshana miguu. Kwa maana mimi niliweka kiolezo kwa ajili yenu, ili, kama vile nilivyowafanyia nyinyi, nyinyi mpaswe kufanya pia.” (Yohana 13:14, 15) Wakristo wa kweli wanapaswa kuwa tayari kutumikia ndugu zao kwa furaha.—Mathayo 20:26, 27NW, kielezi-chini; Yohana 13:17.

Fuata Amri Mpya

6, 7. (a) Ni habari gani muhimu alizotaja Yohana kuhusu kuanzishwa kwa Ukumbusho? (b) Ni amri gani mpya ambayo Yesu aliwapa wanafunzi wake na kwa nini ilikuwa mpya?

6 Ni Yohana pekee anayesimulia kuondoka kwa Yuda Iskariote kutoka kwenye chumba cha juu usiku wa Nisani 14. (Yohana 13:21-30) Tunapolinganisha masimulizi ya Injili twaona kwamba Yesu alianzisha Ukumbusho wa kifo Chake baada ya msaliti huyo kuondoka. Kisha akazungumza kwa undani na mitume wake waaminifu, na kuwapa mashauri na maagizo ya kuwaaga. Tunapojitayarisha kuhudhuria Ukumbusho, tunapaswa kupendezwa sana na mambo aliyosema Yesu wakati huo, na hasa kwa sababu tungependa kuwa miongoni mwa watu wanaopendwa na Mungu.

7 Maagizo ya kwanza ambayo Yesu aliwapa wanafunzi wake baada ya kuanzisha Ukumbusho wa kifo chake, yalikuwa mapya. Alisema: “Mimi ninawapa nyinyi amri mpya, kwamba mpendane; kama vile nimewapenda nyinyi, kwamba nyinyi pia mpendane. Kwa hilo wote watajua kwamba nyinyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo miongoni mwenu wenyewe.” (Yohana 13:34, 35) Kwa nini amri hii ilikuwa mpya? Baadaye jioni hiyo, Yesu alifafanua mambo kwa kusema: “Hii ndiyo amri yangu, kwamba mpendane kama vile mimi nimewapenda nyinyi. Hakuna aliye na upendo mkubwa zaidi kuliko huu, kwamba mtu fulani aisalimishe nafsi yake kwa niaba ya marafiki wake.” (Yohana 15:12, 13) Sheria ya Musa iliwaamuru Waisraeli ‘wawapende jirani zao kama nafsi zao.’ (Mambo ya Walawi 19:18) Lakini amri ya Yesu ilihusisha mengi zaidi. Wakristo walipaswa kupendana kama vile Kristo alivyowapenda, na kuwa tayari kutoa uhai wao kwa ajili ya ndugu zao.

8. (a) Upendo wa kujidhabihu unahusisha nini? (b) Mashahidi wa Yehova huonyeshaje upendo wa kujidhabihu leo?

8 Wakati wa Ukumbusho ni pindi inayofaa kujichunguza wenyewe tukiwa mtu mmoja-mmoja au tukiwa kutaniko na kuona kama kwa kweli tuna alama inayowatambulisha Wakristo wa kweli—upendo kama wa Kristo. Upendo huo wa kujidhabihu unaweza kumaanisha, na nyakati nyingine umemaanisha kwamba Mkristo atahatarisha maisha yake badala ya kuwasaliti ndugu zake. Hata hivyo, kwa kawaida upendo huo unahusisha utayari wetu wa kudhabihu mapendezi ya kibinafsi ili kusaidia na kutumikia ndugu zetu na wengineo. Mtume Paulo aliweka kielelezo kizuri kuhusiana na jambo hilo. (2 Wakorintho 12:15; Wafilipi 2:17) Mashahidi wa Yehova wanajulikana ulimwenguni pote kwa sababu ya roho yao ya kujidhabihu, ya kusaidia ndugu na jirani zao, na kujitoa kabisa kuwaeleza wanadamu wenzao kweli ya Biblia. *Wagalatia 6:10.

Uhusiano Unaopaswa Kuthaminiwa Sana

9. Ili kudumisha uhusiano wenye thamani pamoja na Mungu na Mwanaye, tunafurahi kufanya nini?

9 Hakuna jambo lenye thamani kwetu kuliko kupendwa na Yehova Mungu na Mwanaye, Kristo Yesu. Hata hivyo, ili tuweze kuwa na upendo huo, lazima tufanye jambo fulani. Usiku huo wa mwisho akiwa pamoja na wanafunzi wake, Yesu alisema hivi: “Yeye aliye na amri zangu na kuzishika, huyo ndiye ambaye hunipenda. Naye anipendaye mimi atapendwa na Baba yangu, nami hakika nitampenda na hakika nitajionyesha wazi kwake.” (Yohana 14:21) Kwa kuwa tunathamini sana uhusiano wetu na Mungu na Mwanaye, tunatii amri zao kwa furaha. Hiyo inatia ndani amri mpya ya kuonyesha upendo wa kujidhabihu na pia amri ambayo Kristo alitoa baada ya kufufuliwa ya ‘kuwahubiri watu na kutoa ushahidi kamili,’ tukijitahidi ‘kuwafanya wanafunzi’ watu wanaokubali habari njema.—Matendo 10:42; Mathayo 28:19, 20.

10. Watiwa-mafuta na “kondoo wengine” wanaweza kufurahia uhusiano gani wenye thamani pamoja na Yehova na Mwanaye?

10 Baadaye usiku huo, alipokuwa akijibu swali aliloulizwa na mtume mwaminifu Yuda (Tadayo), Yesu alisema: “Ikiwa yeyote anipenda mimi, atashika neno langu, na Baba yangu atampenda, nasi hakika tutakuja kwake na kufanya kao letu pamoja naye.” (Yohana 14:22, 23) Hata wanapokuwa duniani, Wakristo watiwa-mafuta, ambao wamepewa mwito wa kutawala na Kristo mbinguni, wana uhusiano wa karibu sana na Yehova na Mwanaye. (Yohana 15:15; 16:27; 17:22; Waebrania 3:1; 1 Yohana 3:2, 24) Lakini waandamani wao “kondoo wengine” walio na tumaini la kuishi milele duniani, pia wanakuwa na uhusiano wenye thamani na “mchungaji [wao] mmoja,” Yesu Kristo, na Mungu wao, Yehova, maadamu wanaendelea kuonyesha utii.—Yohana 10:16; Zaburi 15:1-5; 25:14.

“Nyinyi Si Sehemu ya Ulimwengu”

11. Yesu aliwapa wanafunzi wake onyo gani lenye kuamsha fikira?

11 Kwenye mkutano huu wa mwisho pamoja na wanafunzi wake waaminifu kabla ya kifo chake, Yesu aliwapa onyo hili lenye kuamsha fikira: Mtu akipendwa na Mungu, atachukiwa na ulimwengu. Alisema: “Ikiwa ulimwengu wawachukia nyinyi, mwajua kwamba huo umenichukia mimi kabla ya huo kuwachukia nyinyi. Kama mngekuwa sehemu ya ulimwengu, ulimwengu ungependa sana kilicho chao wenyewe. Sasa kwa sababu nyinyi si sehemu ya ulimwengu, bali nimewachagua nyinyi kutoka ulimwenguni, kwa ajili ya hili ulimwengu huwachukia nyinyi. Zingatieni akilini neno nililowaambia, Mtumwa si mkubwa zaidi kuliko bwana-mkubwa wake. Ikiwa wameninyanyasa mimi, watawanyanyasa nyinyi pia; ikiwa wameshika neno langu, watashika lenu pia.”—Yohana 15:18-20.

12. (a) Kwa nini Yesu aliwaonya wanafunzi wake kwamba ulimwengu ungewachukia? (b) Sote twapaswa kufikiria nini Ukumbusho unapokaribia?

12 Yesu alitoa onyo hilo kwa mitume hao 11, na wote ambao wangekuwa Wakristo wa kweli ili wasivunjike moyo na kukata tamaa kwa sababu ya kuchukiwa na ulimwengu. Aliongeza kusema hivi: “Mimi nimewaambia nyinyi mambo haya ili msipate kukwazika. Watu watawafukuza nyinyi katika sinagogi. Kwa kweli, saa inakuja wakati kila mtu awauaye nyinyi atawazia amemtolea Mungu utumishi mtakatifu. Lakini watafanya mambo haya kwa sababu hawajaja kumjua ama Baba ama mimi.” (Yohana 16:1-3) Kamusi moja ya Biblia yasema kwamba namna moja ya kitenzi kilichotumiwa hapa ‘kukwaza’ chamaanisha “kufanya mtu aache kumtumaini na kumtii mtu aliyepaswa kumtumaini na kumtii; kufanya mtu akane imani.” Wakati wa kuadhimisha Ukumbusho unapokaribia, wote wanapaswa kufikiria mwenendo wa watu waaminifu wa kale na wa sasa, na kuiga kielelezo chao cha uaminifu chini ya jaribu. Usiruhusu upinzani au mnyanyaso ufanye umwache Yehova na Yesu, bali azimia kuwatumaini na kuwatii.

13. Yesu aliomba nini kwa niaba ya wafuasi wake katika sala kwa Baba yake?

13 Katika sala yake ya mwisho kabla ya kuondoka kutoka kwenye chumba cha juu huko Yerusalemu, Yesu alimwambia hivi Baba yake: “Nimewapa wao neno lako, lakini ulimwengu umewachukia, kwa sababu wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile mimi si sehemu ya ulimwengu. Nakuomba wewe, si uwachukue kutoka ulimwenguni, bali uwalinde kwa sababu ya yule mwovu. Wao si sehemu ya ulimwengu, kama vile mimi si sehemu ya ulimwengu.” (Yohana 17:14-16) Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova huwaangalia wale anaowapenda, ili kuwaimarisha wanapoendelea kujitenga na ulimwengu.—Isaya 40:29-31.

Kaeni Katika Upendo wa Baba na wa Mwana

14, 15. (a) Yesu alijilinganisha na nini, tofauti na ‘mzabibu usiofaa’? (b) “Matawi” ya “mzabibu wa kweli” ni nani?

14 Wakati wa mazungumzo ya kirafiki aliyokuwa nayo na wanafunzi wake waaminifu usiku wa Nisani 14, Yesu alijilinganisha na “mzabibu wa kweli,” tofauti na ‘mzabibu usiofaa’ wa Waisraeli wasio waaminifu. Alisema hivi: “Mimi ndio mzabibu wa kweli, na Baba yangu ndiye mlimaji.” (Yohana 15:1) Karne kadhaa mapema, nabii Yeremia aliandika maneno haya ya Yehova kwa watu wake walioasi: “Nalikuwa nimekupanda, mzabibu mwema sana, . . . umegeukaje, basi, kuwa mche usiofaa wa mzabibu-mwitu machoni pangu?” (Yeremia 2:21) Naye nabii Hosea aliandika hivi: “Israeli ni mzabibu usiofaa. Anaendelea kutokeza matunda kwa ajili yake mwenyewe. . . . Moyo wao umekuwa wa unafiki.”—Hosea 10:1, 2NW.

15 Badala ya kutokeza matunda ya ibada ya kweli, Israeli waliasi imani na kutokeza matunda kwa ajili yao wenyewe. Siku tatu kabla ya mkutano wake wa mwisho pamoja na wanafunzi wake waaminifu, Yesu aliwaambia hivi viongozi Wayahudi wanafiki: “Nawaambia nyinyi, Ufalme wa Mungu utachukuliwa kutoka kwenu na kupewa kwa taifa lenye kutokeza matunda yao.” (Mathayo 21:43) Taifa hilo jipya ni “Israeli wa Mungu,” linalofanyizwa na Wakristo watiwa-mafuta 144,000 ambao wanalinganishwa na “matawi” ya “mzabibu wa kweli,” Kristo Yesu.—Wagalatia 6:16; Yohana 15:5; Ufunuo 14:1, 3.

16. Yesu aliwahimiza mitume 11 waaminifu wafanye nini, na twaweza kusema nini kuhusu mabaki waaminifu wanaoishi wakati huu wa mwisho?

16 Yesu aliwaambia hivi mitume 11 waliokuwa pamoja naye kwenye chumba cha juu: “Kila tawi katika mimi lisilozaa matunda yeye huliondolea mbali, na kila linalozaa matunda yeye hulisafisha, lipate kuzaa matunda zaidi. Kaeni katika muungano nami, na mimi katika muungano nanyi. Kama vile tawi lisivyoweza kuzaa matunda likiwa pekee isipokuwa likae katika mzabibu, katika njia hiyohiyo wala nyinyi hamwezi, isipokuwa mkae katika muungano nami.” (Yohana 15:2, 4) Historia ya kisasa ya watu wa Yehova inaonyesha kwamba mabaki ya Wakristo watiwa-mafuta waaminifu wamekaa katika muungano na Kichwa chao, Kristo Yesu. (Waefeso 5:23) Wamekubali kusafishwa na kupogolewa. (Malaki 3:2, 3) Tangu mwaka wa 1919, wametokeza matunda ya Ufalme kwa wingi, kwanza wametokeza Wakristo wengine watiwa-mafuta na, tangu mwaka wa 1935, wakatokeza waandamani wao wa “umati mkubwa” unaozidi kuongezeka.—Ufunuo 7:9; Isaya 60:4, 8-11.

17, 18. (a) Ni maneno gani ya Yesu ambayo huwasaidia watiwa-mafuta na kondoo wengine wakae katika upendo wa Yehova? (b) Kuhudhuria Ukumbusho kutatusaidiaje?

17 Maneno haya ya Yesu yawahusu Wakristo wote watiwa-mafuta pamoja na waandamani wao: “Baba yangu hutukuzwa katika hili, kwamba mfulize kuzaa matunda mengi na kujithibitisha wenyewe kuwa wanafunzi wangu. Kama vile Baba amenipenda mimi nami nimewapenda nyinyi, kaeni katika upendo wangu. Mkishika amri zangu, mtakaa katika upendo wangu, kama vile mimi nimeshika amri za Baba na kukaa katika upendo wake.”—Yohana 15:8-10.

18 Sote tungependa kukaa katika upendo wa Mungu, na jambo hilo hutuchochea tuwe Wakristo wanaozaa matunda. Tunafanya hivyo kwa kutumia kila nafasi kuhubiri ‘habari njema ya ufalme.’ (Mathayo 24:14) Pia tunajitahidi kadiri tuwezavyo kuonyesha “matunda ya roho” katika maisha yetu. (Wagalatia 5:22, 23) Kuhudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo kutatuimarisha tuazimie kufanya hivyo, kwa kuwa tutakumbushwa jinsi Mungu na Kristo wanavyotupenda sana.—2 Wakorintho 5:14, 15.

19. Ni msaada gani mwingine utakaozungumziwa katika makala inayofuata?

19 Baada ya kuanzisha Ukumbusho, Yesu aliahidi kwamba Baba yake angewatumia wafuasi wake waaminifu “msaidiaji, roho takatifu.” (Yohana 14:26) Makala ifuatayo itaonyesha jinsi ambavyo roho hii huwasaidia watiwa-mafuta na kondoo wengine wakae katika upendo wa Yehova.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Kulingana na kalenda ya Biblia, mwaka huu wa 2002 Nisani 14 itaanza Alhamisi, Machi 28 baada ya jua kutua. Jioni hiyo, Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote watakutana ili kukumbuka kifo cha Bwana, Yesu Kristo.

^ fu. 8 Ona sura ya 19 na 32 ya kitabu Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Maswali ya Kupitia

• Ni somo gani la kuwatumikia wengine kwa upendo ambalo Yesu aliwafunza wanafunzi wake?

• Inafaa tujichunguze kuhusiana na jambo gani wakati wa Ukumbusho?

• Kwa nini hatupaswi kukwazwa na onyo la Yesu kuhusu chuki na mnyanyaso kutoka kwa ulimwengu?

• Ni nani aliye “mzabibu wa kweli”? “Matawi” ni nani, na wanatazamiwa kufanya nini?

[Maswali ya Funzo]

[Maelezo ya Picha katika ukurasa wa 15]

Yesu aliwafundisha mitume wake somo lenye thamani la kuwatumikia wengine kwa upendo

[Maelezo ya Picha katika ukurasa wa 16, 17]

Wanafunzi wa Kristo hutii amri yake ya kuonyesha upendo wa kujidhabihu