Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Umepokea “Roho ya Ile Kweli”?

Je, Umepokea “Roho ya Ile Kweli”?

Je, Umepokea “Roho ya Ile Kweli”?

“Baba . . . atawapa nyinyi msaidiaji mwingine awe pamoja nanyi milele, roho ya ile kweli.”—YOHANA 14:16, 17.

1. Ni habari gani muhimu ambayo Yesu aliwapa wanafunzi wake saa za mwisho-mwisho alipokuwa pamoja nao katika chumba cha juu?

“BWANA, unaenda wapi?” Hilo lilikuwa mojawapo ya maswali ambayo mitume wa Yesu walimwuliza saa za mwisho-mwisho alipokuwa pamoja nao katika chumba cha juu huko Yerusalemu. (Yohana 13:36) Wakati wa mkutano huo, Yesu aliwaambia kwamba angewaacha na kurudi kwa Baba yake. (Yohana 14:28; 16:28) Hangeendelea kuwa pamoja nao kimwili ili kuwafundisha na kujibu maswali yao. Hata hivyo, aliwahakikishia hivi: “Nitamwomba Baba naye atawapa nyinyi msaidiaji [au, mfariji] mwingine awe pamoja nanyi milele.”—Yohana 14:16NW, kielezi-chini.

2. Yesu aliahidi angewatumia wanafunzi nini baada ya kuondoka kwake?

2 Yesu alimtaja msaidiaji huyo na akaeleza jinsi ambavyo angewasaidia wanafunzi wake. Aliwaambia hivi: “Mambo haya sikuwaambia nyinyi hapo kwanza, kwa sababu nilikuwa pamoja nanyi. Lakini sasa ninaenda kwake aliyenituma . . . Ni kwa manufaa yenu mimi ninaenda zangu. Kwa maana nisipoenda zangu, msaidiaji hatakuja kwenu kwa vyovyote; bali nikishika njia kwenda zangu, hakika nitamtuma yeye kwenu. . . . Wakati huyo awasilipo, roho ya ile kweli, atawaongoza nyinyi ndani ya kweli yote.”—Yohana 16:4, 5, 7, 13.

3. (a) Ni lini “roho ya ile kweli” ilipotumwa kwa Wakristo wa mapema? (b) Roho ilikuwa “msaidiaji” wao katika njia ipi muhimu?

3 Ahadi hiyo ilitimizwa katika Pentekoste 33 W.K., kama alivyothibitisha mtume Petro: “Yesu huyu Mungu alimfufua, uhakika ambao sisi sote ni mashahidi. Kwa hiyo kwa sababu alikwezwa kwenye mkono wa kuume wa Mungu na kupokea roho takatifu iliyoahidiwa kutoka kwa Baba, amemwaga hiki ambacho nyinyi mwakiona na kukisikia.” (Matendo 2:32, 33) Kama tutakavyoona baadaye, roho takatifu iliyomwagwa siku ya Pentekoste ilitimiza mambo mengi kwa Wakristo wa mapema. Lakini Yesu aliahidi kwamba “roho ya ile kweli” ‘ingewakumbusha mambo yote aliyowaambia.’ (Yohana 14:26) Ingewasaidia kukumbuka huduma na mafundisho ya Yesu, na hata maneno yake, na kuyaandika. Msaada huo ungemfaa sana mtume Yohana aliyekuwa amezeeka alipoanza kuandika simulizi la Injili mwishoni mwa karne ya kwanza W.K. Simulizi hilo linatia ndani shauri muhimu ambalo Yesu alitoa alipoanzisha Ukumbusho wa kifo chake.—Yohana, sura ya 13-17.

4. “Roho ya ile kweli” iliwasaidiaje Wakristo watiwa-mafuta wa mapema?

4 Pia Yesu aliahidi wanafunzi hao wa mapema kwamba roho ‘ingewafundisha mambo yote’ na ‘kuwaongoza ndani ya kweli yote.’ Roho ingewasaidia kuelewa mambo yenye kina kirefu ya Maandiko na kuhifadhi umoja wao katika kuwaza, kuelewa, na kuwa na kusudi moja. (1 Wakorintho 2:10; Waefeso 4:3) Kwa hiyo roho takatifu iliwapa nguvu Wakristo hao wa mapema watumike kwa pamoja wakiwa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” na kuwapa Wakristo watiwa-mafuta wakiwa mtu mmoja-mmoja ‘chakula cha kiroho kwa wakati ufaao.’—Mathayo 24:45.

Roho Hutoa Ushahidi

5. (a) Yesu aliwafunulia wanafunzi wake taraja gani usiku wa Nisani 14, 33 W.K.? (b) Roho takatifu ingehusikaje ili kutimiza ahadi ya Yesu?

5 Usiku wa Nisani 14, mwaka wa 33 W.K., Yesu aliwadokezea wanafunzi wake kwamba baadaye angewapokea wakae pamoja naye na Baba yake mbinguni. Aliwaambia hivi: “Katika nyumba ya Baba yangu mna makao mengi. Kama sivyo, ningaliwaambia nyinyi, kwa sababu nashika njia yangu kwenda kuwatayarishia nyinyi mahali. Pia, nikishika njia yangu kwenda na kuwatayarishia nyinyi mahali, mimi ninakuja tena na hakika nitawapokea nyinyi nyumbani kwangu mwenyewe, ili mahali nilipo nyinyi pia mpate kuwa.” (Yohana 13:36; 14:2, 3) Wangetawala pamoja naye katika Ufalme wake. (Luka 22:28-30) Ili wapokee tumaini hilo la kimbingu, wangelazimika ‘kuzaliwa kutokana na roho’ wakiwa wana wa roho wa Mungu na kutiwa mafuta ili kutumikia wakiwa wafalme na makuhani pamoja na Kristo mbinguni.—Yohana 3:5-8; 2 Wakorintho 1:21, 22; Tito 3:5-7; 1 Petro 1:3, 4; Ufunuo 20:6.

6. (a) Mwito wa kimbingu ulianza lini, na ni wangapi wanaopokea mwito huo? (b) Wale walioitwa wanabatizwa katika nini?

6 “Mwito [huo] wa kimbingu” ulianza kutolewa siku ya Pentekoste 33 W.K. na yaonekana mwito huo ulikoma hasa katikati ya miaka ya 1930. (Waebrania 3:1) Idadi ya wale waliotiwa muhuri na roho takatifu kuwa sehemu ya Israeli wa kiroho ni 144,000, ‘walionunuliwa kutoka miongoni mwa wanadamu.’ (Ufunuo 7:4; 14:1-4) Hao walibatizwa katika mwili wa kiroho wa Kristo, katika kutaniko lake, na katika kifo chake. (Waroma 6:3; 1 Wakorintho 12:12, 13, 27; Waefeso 1:22, 23) Baada ya kubatizwa kwa maji na kutiwa mafuta kwa roho takatifu, wanaanza maisha ya kujidhabihu, na kudumisha uaminifu-maadili hadi wanapokufa.—Waroma 6:4, 5.

7. Kwa nini ni Wakristo watiwa-mafuta pekee wanaostahili kushiriki kula mifano kwenye Ukumbusho?

7 Wakiwa Israeli wa kiroho, Wakristo hao watiwa-mafuta walikuwa katika agano jipya lililofanywa kati ya Yehova na “Israeli wa Mungu.” (Wagalatia 6:16; Yeremia 31:31-34) Agano jipya lilihalalishwa na damu iliyomwagwa ya Kristo. Yesu alitaja jambo hilo alipoanzisha Ukumbusho wa kifo chake. Luka aripoti hivi: “Akachukua mkate, akashukuru, akaumega, na kuwapa, akisema: ‘Huu wamaanisha mwili wangu ambao wapasa kutolewa kwa ajili yenu. Fulizeni kufanya hili katika ukumbuko wangu.’ Pia, kikombe kwa njia ileile baada ya wao kula mlo wa jioni, yeye akisema: ‘Kikombe hiki chamaanisha agano jipya kwa msingi wa damu yangu, ambayo yapasa kumwagwa kwa ajili yenu.’” (Luka 22:19, 20) Mabaki ya wale 144,000, ndio wanaostahili kushiriki kula mkate na divai ya mfano kwenye Ukumbusho wa kifo cha Kristo.

8. Watiwa-mafuta hujuaje kwamba wamepokea mwito wa kimbingu?

8 Watiwa-mafuta hujuaje kwamba wamepokea mwito wa kimbingu? Wanapokea ushahidi wa roho takatifu pasipo shaka yoyote. Mtume Paulo aliandika hivi kuwahusu: “Wote wenye kuongozwa na roho ya Mungu, hao ndio wana wa Mungu. . . . Hiyo roho yenyewe hutoa ushahidi pamoja na roho yetu kwamba sisi ni watoto wa Mungu. Basi, ikiwa sisi ni watoto, sisi pia ni warithi: warithi wa Mungu kwelikweli, lakini warithi-washirika pamoja na Kristo, mradi twateseka pamoja ili tupate pia kutukuzwa pamoja.” (Waroma 8:14-17) Ushahidi huo wa roho una nguvu sana hivi kwamba wale walio na shaka kidogo kwamba wamepokea mwito huo wanapaswa kufikia mkataa kwamba hawajaupokea, na hivyo kuepuka kushiriki kula mifano wakati wa Ukumbusho.

Roho na Kondoo Wengine

9. Ni vikundi gani viwili vilivyo tofauti ambavyo vinatajwa katika Injili na katika kitabu cha Ufunuo?

9 Yesu aliwataja kuwa “kundi dogo” Wakristo ambao wangeitwa ili kufanyiza Israeli wa kiroho kwa kuwa alijua kwamba wangekuwa wachache. Wakristo hao wanaingizwa katika “zizi” la agano jipya, tofauti na “kondoo wengine” wasio na hesabu ambao Yesu alisema angewakusanya pia. (Luka 12:32; Yohana 10:16) Wale wa kondoo wengine ambao wanakusanywa wakati wa mwisho watafanyiza “umati mkubwa” ambao utaokoka “dhiki kubwa,” ukiwa na taraja la kuishi milele katika paradiso duniani. Maono ambayo Yohana alipokea mwishoni mwa karne ya kwanza W.K. yanaonyesha tofauti iliyopo kati ya umati mkubwa na wale washiriki 144,000 wa Israeli wa kiroho. (Ufunuo 7:4, 9, 14) Je, kondoo wengine hupokea roho takatifu pia, na ikiwa ndivyo, inaathirije maisha yao?

10. Kondoo wengine hubatizwaje “katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu”?

10 Kwa kweli roho takatifu inatimiza fungu muhimu katika maisha ya kondoo wengine. Wanaonyesha wakfu wao kwa Yehova kwa kubatizwa “katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu.” (Mathayo 28:19) Wanatambua enzi kuu ya Yehova, wananyenyekea chini ya utawala wa Kristo akiwa Mfalme na Mkombozi wao, na kuruhusu roho au nguvu ya utendaji ya Mungu iwaongoze katika maisha yao. Wanajitahidi hatua kwa hatua kusitawisha maishani mwao “matunda ya roho,” yaani, “upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujidhibiti.”—Wagalatia 5:22, 23.

11, 12. (a) Watiwa-mafuta wametakaswaje kwa njia ya pekee sana? (b) Ni kwa njia gani kondoo wengine wametakaswa na kufanywa kuwa watakatifu?

11 Pia kondoo wengine wanapaswa kuruhusu Neno la Mungu na roho yake takatifu iwatakase. Watiwa-mafuta tayari wametakaswa kwa njia ya pekee sana, kwa kutangazwa kuwa waadilifu na watakatifu wakiwa bibi-arusi wa Kristo. (Yohana 17:17; 1 Wakorintho 6:11; Waefeso 5:23-27) Nabii Danieli anawataja kuwa “watakatifu wake Aliye juu,” ambao wanapokea Ufalme chini ya “mwana wa mtu,” Kristo Yesu. (Danieli 7:13, 14, 18, 27, Biblia Habari Njema) Hapo awali, Yehova aliliambia hivi taifa la Israeli kupitia Musa na Aroni: “Kwa kuwa mimi ni BWANA, Mungu wenu; takaseni nafsi zenu basi; iweni watakatifu, kwa kuwa mimi ni Mtakatifu.”—Mambo ya Walawi 11:44.

12 Neno “utakaso” hasa lamaanisha “tendo au hatua ya kufanya kitu kiwe kitakatifu, kukitenga, au kukiweka kando kwa ajili ya utumishi au matumizi ya Yehova Mungu; hali ya kitu kuwa kitakatifu, kimetakaswa.” Mapema katika mwaka wa 1938, gazeti Mnara wa Mlinzi la Kiingereza lilisema kwamba Wayonadabu, au kondoo wengine, “lazima wajue kwamba kujitoa [kujiweka wakfu] na utakaso unahitajiwa kutoka kwa kila mmoja wetu ambaye atakuwa sehemu ya umati mkubwa utakaoishi duniani.” Katika maono kuhusu mkutano mkubwa ambayo yameandikwa katika kitabu cha Ufunuo, wanatajwa kuwa “wamefua kanzu zao na kuzifanya nyeupe katika damu ya Mwana-Kondoo” na kuwa wanamtolea Yehova “utumishi mtakatifu mchana na usiku katika hekalu lake.” (Ufunuo 7:9, 14, 15) Kwa msaada wa roho takatifu, kondoo wengine hufanya yote wawezayo ili kutimiza matakwa ya Yehova ya utakatifu.—2 Wakorintho 7:1.

Kuwatendea Mema Ndugu za Kristo

13, 14. (a) Kulingana na mfano wa Yesu wa kondoo na mbuzi, wokovu wa kondoo wengine unategemea nini? (b) Katika wakati huu wa mwisho, kondoo wengine wamewaungaje mkono ndugu za Kristo?

13 Yesu alikazia uhusiano wa karibu kati ya kondoo wengine na kundi dogo katika mfano wake wa kondoo na mbuzi, unaotajwa katika unabii wake kuhusu “umalizio wa mfumo wa mambo.” Katika mfano huo, Kristo alionyesha waziwazi kwamba wokovu wa kondoo wengine unategemea sana jinsi wanavyowatendea watiwa-mafuta, ambao aliwaita “ndugu zangu.” Alisema hivi: “Mfalme atawaambia wale walio kwenye mkono wake wa kuume, ‘Njoni, nyinyi ambao mmebarikiwa na Baba yangu, rithini ufalme uliotayarishwa kwa ajili yenu tangu kuwekwa msingi wa ulimwengu. . . . Kwa kweli nawaambia nyinyi, Kwa kadiri ambayo mlimfanyia hilo mmoja wa wadogo zaidi sana wa ndugu zangu hawa, mlinifanyia mimi hilo.’”—Mathayo 24:3; 25:31-34, 40.

14 Usemi “kwa kadiri ambayo mlimfanyia” warejezea kuwatendea kwa upendo ndugu za Kristo waliozaliwa kwa roho, ambao ulimwengu wa Shetani umewatendea kama wageni, na hata kutia baadhi yao gerezani. Wamekuwa na uhitaji wa chakula, mavazi ya kutosha, na utunzaji wa afya. (Mathayo 25:35, 36NW, kielezi-chini) Wakati huu wa mwisho, tangu mwaka wa 1914, watiwa-mafuta wengi wamejikuta katika hali kama hizo. Rekodi ya kisasa ya Mashahidi wa Yehova yathibitisha kwamba watiwa-mafuta wameungwa mkono na waandamani wao waaminifu, kondoo wengine, ambao wanachochewa na roho.

15, 16. (a) Kondoo wengine wamewasaidia ndugu za Kristo watiwa-mafuta walio duniani katika kazi gani? (b) Watiwa-mafuta wameonyeshaje shukrani zao kwa kondoo wengine?

15 Ndugu za Kristo watiwa-mafuta walio duniani wakati huu wa mwisho hasa wameungwa mkono na kondoo wengine kufanya kazi waliyopewa na Mungu ya ‘kuhubiri habari njema hii ya ufalme katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya kuwa ushahidi kwa mataifa yote.’ (Mathayo 24:14; Yohana 14:12) Ingawa idadi ya watiwa-mafuta walio duniani imekuwa ikipungua katika miaka iliyopita, idadi ya kondoo wengine imeongezeka na kufikia milioni kadhaa. Maelfu kati yao wametumikia wakiwa waeneza-evanjeli wa wakati wote—mapainia na mishonari—wakihubiri habari njema za Ufalme hadi “sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.” (Matendo 1:8) Wengine hushiriki kazi ya kutoa ushahidi kwa kadiri wawezavyo na kutoa michango yao kwa furaha ili kutegemeza kazi hiyo muhimu.

16 Ndugu za Kristo wanashukuru kama nini kwa msaada huo unaotolewa kwa uaminifu na waandamani wao, kondoo wengine! Maoni yao yalielezwa vyema katika kitabu Usalama Ulimwenguni Pote Chini ya “Mwana-Mfalme wa Amani,” kilichochapishwa na jamii ya mtumwa katika mwaka wa 1986. Kinasema hivi: “Tangu Vita ya Ulimwengu ya Pili, utimizo wa unabii wa Yesu kwa ‘umalizio wa mfumo wa mambo’ kwa sehemu kubwa ni kwa sababu ya daraka linalotimizwa na ule ‘mkutano mkubwa’ wa ‘kondoo wengine.’ . . . Kwa hiyo shukrani nyingi sana, kwa ule mkutano mkubwa wa kimataifa, wenye kusema lugha nyingi kwa sababu ya sehemu kubwa ambayo umeshiriki katika kutimiza unabii wa [Yesu] yule Bwana-arusi kwenye Mathayo 24:14!”

‘Hawajafanywa Wakamilifu Bila Sisi’

17. Ni katika njia gani waaminifu wa kale watakaofufuliwa duniani ‘hawatafanywa wakamilifu bila’ watiwa-mafuta?

17 Akizungumza akiwa mmoja wa watiwa-mafuta na kurejezea wanaume na wanawake waaminifu walioishi kabla ya Kristo, mtume Paulo aliandika hivi: “Wote hawa, ijapokuwa walitolewa ushahidi kupitia imani yao, hawakupata utimizo wa ahadi, kwa kuwa Mungu aliona kimbele kitu fulani bora kwa ajili yetu sisi [watiwa-mafuta], ili wasipate kufanywa wakamilifu bila sisi.” (Waebrania 11:35, 39, 40) Wakati wa Milenia, Kristo na ndugu zake watiwa-mafuta 144,000 wakiwa mbinguni watatumikia wakiwa wafalme na makuhani na kuleta manufaa za dhabihu ya fidia ya Kristo hapa duniani. Hivyo kondoo wengine ‘watafanywa kuwa wakamilifu’ katika mwili na akili.—Ufunuo 22:1, 2.

18. (a) Kweli ya Biblia yapasa kusaidia kondoo wengine wafahamu jambo gani? (b) Kondoo wengine husubiri “kufunuliwa kwa wana wa Mungu” wakiwa na tumaini gani?

18 Kondoo wengine wanapaswa kufahamu vizuri ni kwa nini Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo hukazia sana Kristo na ndugu zake watiwa-mafuta na daraka lao muhimu katika kutimizwa kwa makusudi ya Yehova. Kwa hiyo kondoo wengine huona kuwa ni pendeleo kuunga mkono kwa njia yoyote wawezayo jamii ya watiwa-mafuta huku wakisubiri “kufunuliwa kwa wana wa Mungu” kwenye Har-Magedoni na wakati wa Milenia. Wanaweza kutazamia ‘kuwekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu na kuwa na uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.’—Waroma 8:19-21.

Kuungana Katika Roho Wakati wa Ukumbusho

19. “Roho ya ile kweli” imewafanyia nini watiwa-mafuta na waandamani wao, nao wataunganaje hasa jioni ya Machi 28?

19 Katika sala yake ya kumalizia usiku wa Nisani 14, mwaka wa 33 W.K., Yesu alisema: “Nafanya ombi, . . . ili wote wapate kuwa mmoja, kama vile wewe, Baba, umo katika muungano na mimi na mimi nimo katika muungano na wewe, ili wao pia wapate kuwa katika muungano na sisi, ili ulimwengu upate kuamini kwamba ulinituma mimi.” (Yohana 17:20, 21) Mungu alichochewa na upendo kumtuma Mwana wake atoe uhai wake ili kuokoa watiwa-mafuta na wanadamu watiifu. (1 Yohana 2:2) “Roho ya ile kweli” imeunganisha ndugu za Kristo na waandamani wao. Jioni ya Machi 28, baada ya jua kutua, vikundi vyote viwili vitakutana pamoja ili kukumbuka kifo cha Kristo na kukumbuka yote ambayo Yehova amewafanyia kupitia dhabihu ya Mwana wake mpendwa, Kristo Yesu. Umoja wao na uimarike wanapohudhuria sherehe hiyo muhimu, na waazimie upya kufanya mapenzi ya Mungu, na hivyo kuthibitisha kwamba wanafurahia kuwa miongoni mwa wale wanaopendwa na Yehova.

Kwa Kupitia

• “Roho ya ile kweli” ilitumwa lini kwa Wakristo wa mapema, nayo ilithibitikaje kuwa “msaidiaji”?

• Watiwa-mafuta hujuaje kwamba wamepokea mwito wa kimbingu?

• Roho ya Mungu hutenda katika njia zipi miongoni mwa kondoo wengine?

• Kondoo wengine wamewatendeaje mema ndugu za Kristo, na kwa nini ‘hawatafanywa kuwa wakamilifu bila’ watiwa-mafuta?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 21]

“Roho ya ile kweli” ilimwagwa kwa wanafunzi siku ya Pentekoste 33 W.K.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Kondoo wengine wamewatendea mema ndugu za Kristo kwa kuwaunga mkono kutimiza kazi waliyopewa na Mungu ya kuhubiri