Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jifunze Kutoka kwa Nikodemo

Jifunze Kutoka kwa Nikodemo

Jifunze Kutoka kwa Nikodemo

“IKIWA yeyote ataka kunifuata, na ajikane mwenyewe na kuchukua mti wake wa mateso siku baada ya siku na kunifuata kwa kuendelea.” (Luka 9:23) Wavuvi wa hali ya chini na mkusanya-kodi mwenye kuchukiwa waliitikia mwito huo bila kusita. Waliacha kila kitu wakamfuata Yesu.—Mathayo 4:18-22; Luka 5:27, 28.

Yesu bado anatoa mwito huo leo, na wengi wameitikia. Hata hivyo, wengi wanaofurahia kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova husita ‘kujikana wenyewe na kuchukua mti wao wa mateso.’ Wanasita kuchukua daraka na pendeleo la kuwa wanafunzi wa Yesu.

Kwa nini wengine husita kukubali mwaliko wa Yesu na kujiweka wakfu kwa Yehova Mungu? Ni kweli kwamba huenda watu ambao hawakulelewa katika dini ya Wayahudi na ya Kikristo inayofundisha kuwepo kwa Mungu mmoja wakachukua muda mrefu kabla ya kufahamu kwamba kuna Muumba mweza yote mwenye utu. Hata hivyo, wengine bado husita kufuata hatua za Yesu hata baada ya kuhakikishiwa kwamba Mungu ni halisi. Huenda wakaogopa wataonwaje na watu wa ukoo na marafiki ikiwa watakuwa Mashahidi wa Yehova. Wengine ambao hupuuza uharaka wa wakati tunamoishi, huanza kutafuta umashuhuri na mali. (Mathayo 24:36-42; 1 Timotheo 6:9, 10) Hata hali iweje, wale wanaoahirisha-ahirisha kufanya uamuzi wao wa kuwa wafuasi wa Yesu, wanaweza kujifunza somo fulani kutokana na masimulizi kuhusu Nikodemo, mtawala tajiri Myahudi aliyeishi siku za Yesu.

Nikodemo Apata Fursa Nzuri

Miezi sita tu baada ya Yesu kuanza huduma yake duniani, Nikodemo anamtambua ‘kuwa mwalimu kutoka kwa Mungu.’ Kwa kuvutiwa na miujiza ambayo Yesu alikuwa amefanya karibuni huko Yerusalemu kwenye Sikukuu ya Kupitwa ya mwaka wa 30 W.K., Nikodemo anakuja usiku kukiri kwamba anamwamini Yesu na pia kujifunza mengi zaidi kuhusu mwalimu huyo. Hivyo, Yesu anamfunza Nikodemo ukweli muhimu kuhusu uhitaji wa ‘kuzaliwa tena’ ili kuingia katika Ufalme wa Mungu. Katika pindi hiyo pia Yesu anasema maneno haya: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akatoa Mwana mzaliwa-pekee wake, ili kila mtu anayedhihirisha imani katika yeye asipate kuangamizwa bali awe na uhai udumuo milele.”—Yohana 3:1-16.

Nikodemo ana taraja zuri kama nini! Anaweza kuwa mshiriki wa karibu wa Yesu na kujionea moja kwa moja mambo mbalimbali yanayotukia katika maisha ya Yesu duniani. Akiwa mtawala wa Wayahudi na mwalimu wa Israeli, Nikodemo analijua vizuri Neno la Mungu. Pia ana ufahamu mwingi kwa kuwa anaweza kutambua kwamba Yesu ni mwalimu aliyetumwa na Mungu. Nikodemo anapendezwa na mambo ya kiroho, na ni mnyenyekevu isivyo kawaida. Ni jambo gumu kama nini kwa mshiriki wa mahakama kuu zaidi ya Wayahudi kukiri kwamba mwana wa seremala tu ni mtu aliyetumwa na Mungu! Sifa hizo zote ni muhimu sana ili mtu awe mwanafunzi wa Yesu.

Nikodemo anazidi kupendezwa na mtu huyu kutoka Nazareti. Miaka miwili na nusu baadaye, kwenye Msherehekeo wa Vibanda, Nikodemo anahudhuria mkutano wa Sanhedrini. Wakati huo, Nikodemo bado ni “mmoja wao.” Makuhani wakuu na Mafarisayo wanawatuma maofisa kwenda kumkamata Yesu. Maofisa hao wanarudi na kusema: “Hajasema kamwe mtu mwingine kama hivi.” Mafarisayo wanaanza kuwadhihaki wakisema: “Nyinyi hamjaongozwa vibaya pia, ndivyo? Hakuna hata mmoja wa watawala au wa Mafarisayo ambaye ameweka imani katika yeye, ndivyo? Lakini umati huu usiojua Sheria ni watu waliolaaniwa.” Nikodemo hawezi kuendelea kunyamaza, hivyo anasema: “Sheria yetu haimhukumu mtu isipokuwa kwanza iwe imesikia kutoka kwake na kuja kujua analofanya, ndivyo?” Kisha Mafarisayo wenzake wanaanza kumchambua wakisema: “Wewe pia si wa kutoka Galilaya, ndivyo? Chunguza uone kwamba hakuna nabii atakayeinuliwa kutoka Galilaya.”—Yohana 7:1, 10, 32, 45-52.

Miezi sita baadaye, kwenye Sikukuu ya Kupitwa ya mwaka wa 33 W.K., Nikodemo anaona mwili wa Yesu ukiondolewa kwenye mti wa mateso. Anaungana na Yosefu wa Arimathea, mshiriki mwingine wa Sanhedrini, kutayarisha mwili wa Yesu ili kuuzika. Hivyo, Nikodemo analeta “kikuto cha manemane na udi” zenye uzito upatao ratili 100 kulingana na kipimo cha Roma, ambazo ni sawa na ratili 72 kulingana na kipimo cha Uingereza. Vitu hivyo vinamgharimu pesa nyingi. Pia anahitaji kuwa jasiri kuhusianishwa na “laghai huyo,” kama Mafarisayo wenzake wanavyomwita Yesu. Wanatayarisha mwili wa Yesu haraka nao wanauzika katika kaburi jipya la ukumbusho lililo karibu. Lakini hata wakati huu, Nikodemo bado si mwanafunzi wa Yesu!—Yohana 19:38-42; Mathayo 27:63; Marko 15:43.

Sababu Iliyomfanya Asichukue Hatua

Katika masimulizi haya, Yohana hasemi sababu iliyomfanya Nikodemo asite ‘kuchukua mti wake wa mateso’ na kumfuata Yesu. Hata hivyo, aliandika mambo kadhaa yanayoweza kutusaidia kujua sababu iliyomfanya Farisayo huyu asite kuchukua hatua.

Kwanza kabisa, Yohana anasema kwamba mtawala huyo wa Wayahudi “alimjia [Yesu] wakati wa usiku.” (Yohana 3:2) Msomi mmoja wa Biblia anadokeza: “Nikodemo alikuja usiku si kwa sababu aliogopa, bali kwa sababu alitaka kuepuka umati ambao ungekatiza mazungumzo yake pamoja na Yesu.” Hata hivyo, Yohana anamtaja Nikodemo kuwa “yule mtu aliyemjia [Yesu] usiku mara ya kwanza” na katika muktadha huohuo anamtaja Yosefu wa Arimathea kuwa “mwanafunzi wa Yesu lakini wa siri kutokana na kuhofu kwake Wayahudi.” (Yohana 19:38, 39) Kwa hiyo, inaelekea kwamba Nikodemo alimjia Yesu usiku kwa ‘kuhofu Wayahudi,’ kama vile wengine walioishi wakati huo walivyohofu kuhusianishwa na Yesu.—Yohana 7:13.

Je, umeahirisha kufanya uamuzi wa kuwa mmoja wa wanafunzi wa Yesu kwa kuogopa yale ambayo huenda watu wa ukoo, marafiki, au washirika wako wakasema? “Kuwaogopa wanadamu huleta mtego,” mithali moja inasema. Unawezaje kukabiliana na woga huo? Mithali hiyo inaendelea kusema: “Bali amtumainiye BWANA atakuwa salama.” (Mithali 29:25) Ili kusitawisha tumaini hilo katika Yehova, unahitaji kujionea mwenyewe kwamba Mungu atakutegemeza ukiwa katika hali ngumu. Sali kwa Yehova, ukimwomba akupe ujasiri wa kufanya hata maamuzi madogo yanayohusiana na ibada yako. Hatua kwa hatua, imani yako na tumaini lako katika Yehova litakua hivi kwamba utaweza kufanya maamuzi makubwa kupatana na mapenzi yake.

Huenda ikawa cheo na umashuhuri wa Nikodemo akiwa mshiriki wa jamii yenye kutawala zilimzuia pia asichukue hatua muhimu ya kujikana. Wakati huo, lazima alikuwa bado anapenda sana cheo chake akiwa mshiriki wa Sanhedrini. Je, unasita kuchukua hatua ya kuwa mfuasi wa Kristo kwa sababu huenda ukapoteza cheo maarufu katika jamii au ukapoteza matarajio fulani ya kupanda cheo? Hakuna yoyote ya mambo hayo yanayoweza kulinganishwa na pendeleo la kumtumikia Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu, ambaye yu tayari kujibu maombi unayofanya kupatana na mapenzi yake.—Zaburi 10:17; 83:18; 145:18.

Labda sababu nyingine iliyomfanya Nikodemo akawie kufanya uamuzi wake ni mali alizokuwa nazo. Kwa kuwa alikuwa Farisayo huenda aliathiriwa na Mafarisayo wenzake “waliokuwa wapenda-fedha.” (Luka 16:14) Nikodemo alikuwa tajiri kwa kuwa angeweza kununua kikuto cha manemane na udi. Wengine leo hukawia kufanya uamuzi wao kuwa Wakristo kwa sababu wanahangaikia mali zao. Hata hivyo, Yesu aliwashauri hivi wafuasi wake: “Komeni kuhangaikia nafsi zenu kuhusu ni nini mtakula au ni nini mtakunywa, au juu ya miili yenu kuhusu ni nini mtavaa. . . . Kwa maana Baba yenu wa kimbingu ajua mwahitaji vitu hivi vyote. Basi, fulizeni kutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, na vitu vingine vyote hivi mtaongezewa.”—Mathayo 6:25-33.

Nikodemo Alikosa Mambo Mengi

Jambo la kushangaza ni kwamba masimulizi kuhusu Nikodemo yanayopatikana katika Injili ya Yohana pekee hayasemi kama Nikodemo alipata kuwa mfuasi wa Yesu au la. Kulingana na hekaya moja, Nikodemo aliamua kuwa mfuasi wa Yesu na kubatizwa, jambo lililofanya anyanyaswe na Wayahudi, akapokonywa cheo chake, na hatimaye akafukuzwa Yerusalemu. Vyovyote vile, jambo moja ni hakika: Nikodemo alikosa mambo mengi kwa kukawia kufanya uamuzi wakati Yesu alipokuwa angali duniani.

Kama Nikodemo angalianza kumfuata Yesu wakati alipokutana na Bwana kwa mara ya kwanza, angalikuwa mfuasi wa karibu wa Yesu. Nikodemo angalikuwa mwanafunzi mzuri sana kwa sababu alikuwa mwenye ujuzi, mwenye ufahamu, mnyenyekevu, na alitambua mahitaji yake ya kiroho. Naam, angaliweza kusikiliza hotuba nzuri za Mwalimu Mkuu, akajifunza mambo muhimu kutokana na mifano ya Yesu, akajionea miujiza ya ajabu aliyofanya, na kutiwa nguvu na ushauri ambao Yesu alitoa alipowaaga mitume wake. Lakini alikosa hayo yote.

Nikodemo alikosa mambo mengi kwa kusita kuamua. Kati ya mambo aliyokosa ni mwaliko huu mchangamfu wa Yesu: “Njoni kwangu, nyinyi nyote mnaomenyeka na kulemezwa mizigo, nami hakika nitawaburudisha nyinyi. Chukueni nira yangu juu yenu na mjifunze kutoka kwangu, kwa maana mimi ni mwenye tabia-pole na wa hali ya chini moyoni, nanyi mtapata burudisho kwa ajili ya nafsi zenu. Kwa maana nira yangu ni ya fadhili na mzigo wangu ni mwepesi.” (Mathayo 11:28-30) Nikodemo alikosa burudisho hilo kihalisi kutoka kwa Yesu mwenyewe!

Namna Gani Wewe?

Tangu mwaka wa 1914, Yesu Kristo amekuwapo mbinguni akiwa Mfalme wa Ufalme wa mbinguni wa Mungu. Alipotabiri mambo ambayo yangetokea wakati wa kuwapo kwake, Yesu alisema: “Habari njema hii ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14) Lazima kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote itimizwe kwanza kabla ya mwisho kuja. Yesu Kristo hufurahia kuona wanadamu wasio wakamilifu wakifanya kazi hiyo. Wewe pia unaweza kuifanya.

Nikodemo alitambua kwamba Yesu alitoka kwa Mungu. (Yohana 3:2) Huenda wewe pia umetambua jambo hilo kupitia funzo la Biblia. Huenda umefanya mabadiliko fulani ili kuishi kupatana na viwango vya Biblia. Huenda ikawa unahudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova ili upate ujuzi zaidi wa Biblia. Unapongezwa kwa jitihada zako. Hata hivyo, Nikodemo alihitaji kufanya mengi zaidi ya kutambua kwamba Yesu alitumwa na Mungu. Alihitaji ‘ajikane mwenyewe na kuchukua mti wake wa mateso siku baada ya siku na kumfuata Yesu kwa kuendelea.’—Luka 9:23.

Fikiria kwa makini anayotuambia mtume Paulo. Aliandika: “Tukiwa tunafanya kazi pamoja naye, twawasihi sana nyinyi pia msiipokee fadhili isiyostahiliwa ya Mungu na kukosa kusudi layo. Kwa maana yeye asema: ‘Wakati wenye kukubalika nilikusikia, na siku ya wokovu nilikusaidia.’ Tazameni! Sasa ndio wakati wenye kukubalika hasa. Tazameni! Sasa ndiyo siku ya wokovu.”—2 Wakorintho 6:1, 2.

Huu ndio wakati wa kusitawisha imani inayokuchochea kuchukua hatua. Ili kufanya hivyo, tafakari mambo unayojifunza katika Biblia. Sali kwa Yehova, ukimwomba msaada ili uwe na imani kama hiyo. Unapopata msaada wake, uthamini wako na upendo wako kwake utakuchochea utake ‘kujikana mwenyewe na kuchukua mti wako wa mateso siku baada ya siku na kumfuata Yesu Kristo kwa kuendelea.’ Je, utachukua hatua sasa?

[Picha katika ukurasa wa 9]

Mwanzoni, Nikodemo alimtetea Yesu kwa ujasiri

[Picha katika ukurasa wa 9]

Licha ya upinzani, Nikodemo alisaidia kutayarisha mwili wa Yesu ili kuuzika

[Picha katika ukurasa wa 10]

Funzo la kibinafsi na sala zinaweza kukuimarisha kuchukua hatua

[Picha katika ukurasa wa 10]

Je, utakubali pendeleo la kufanya kazi chini ya uongozi wa Yesu Kristo?