Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jiji Lililojengwa Juu ya Mlima

Jiji Lililojengwa Juu ya Mlima

Jiji Lililojengwa Juu ya Mlima

“NYINYI ndio nuru ya ulimwengu. Jiji haliwezi kufichwa liwapo limesimama juu ya mlima,” Yesu akawaambia wanafunzi wake katika Mahubiri yake maarufu ya mlimani.—Mathayo 5:14.

Miji mingi ya Yudea na Galilaya ilijengwa juu ya milima badala ya kujengwa chini kwenye mabonde. Walifanya hivyo hasa kwa sababu ya usalama. Majeshi ya uvamizi na magenge ya wanyang’anyi yalikuwa yakipora makazi ya Waisraeli. (2 Wafalme 5:2; 24:2) Raia wenye ujasiri wangeweza kulinda kwa urahisi nyumba zilizojengwa karibu-karibu juu ya mlima kuliko mji uliojengwa chini kwenye uwanda, ambao ulihitaji kukingwa na ukuta mrefu.

Nyumba hizo zilizojengwa karibu-karibu juu ya mlima zingeweza kuonekana kutoka mbali kwa kuwa mara nyingi kuta za nyumba za Wayahudi zilipakwa chokaa. (Matendo 23:3) Huko Palestina, miji hiyo ya milimani iling’aa wakati wa jua kama mnara wa taa wa kuongozea meli. Miji ya Mediterania ambayo pia imejengwa juu ya milima, hung’aa vivyo hivyo leo.

Yesu alitumia miji hiyo ya Galilaya na Yudea iliyong’aa kwa njia yenye kuvutia kufundisha wafuasi wake daraka la Mkristo wa kweli. “Hivyohivyo acheni nuru yenu ing’ae mbele ya watu ili wapate kuona kazi zenu bora na kumpa utukufu Baba yenu aliye katika mbingu,” akawaambia. (Mathayo 5:16) Ingawa Wakristo hawafanyi kazi bora ili wasifiwe na watu, mwenendo wao mzuri huonekana wazi.—Mathayo 6:1.

Mwenendo huo mzuri huonekana wazi hasa wakati wa makusanyiko ya wilaya ya Mashahidi wa Yehova. Gazeti moja la habari nchini Hispania lilisema hivi kuhusu kusanyiko lililofanywa karibuni: ‘Ingawa wafuasi wa dini nyingine hawapendezwi sana na mafundisho ya Biblia, Mashahidi wa Yehova ni tofauti. Wao hulitumia Neno la Mungu maishani kwa kuwa hawataki Biblia ikose maana.’

Thomas, aliyekuwa mtunzaji wa uwanja ambao Mashahidi waliutumia kwa ukawaida, alifurahia sana kuwa karibu na watu waliotumia Neno la Mungu maishani mwao. Aliahirisha kustaafu kwake kwa majuma kadhaa ili aweze kuwepo kwenye kusanyiko la wilaya la Mashahidi wa Yehova. Wahudhuriaji wengi, kutia ndani watoto, walizungumza naye baada ya kusanyiko wakimshukuru kwa ushirikiano wake katika miaka iliyopita na kumtakia mema baada ya kustaafu kwake. Jambo hilo lilimfanya abubujikwe na machozi na kusema: “Jambo ambalo nimefurahia zaidi maishani mwangu ni kupata kuwajua ninyi.”

Jiji lililojengwa juu ya mlima huvutia mtazamaji kwa kuwa linaweza kuonekana vizuri na pia nyumba zozote nyeupe ndani yake hung’aa kwa nuru ya jua. Vivyo hivyo, Wakristo wa kweli ni tofauti kwa sababu wao hujitahidi kufuata viwango vya juu vya Maandiko kama vile unyofu, uadilifu, na huruma.

Isitoshe, Wakristo huangaza nuru ya kweli kupitia kazi yao ya kuhubiri. Mtume Paulo alisema hivi kuhusu Wakristo wa karne ya kwanza: “Kwa kuwa sisi tuna huduma hii kulingana na rehema tuliyoonyeshwa, hatufi moyo . . . bali kwa kufanya kweli iwe dhahiri [tunajipendekeza] wenyewe kwa kila dhamiri ya kibinadamu machoni pa Mungu.” (2 Wakorintho 4:1, 2) Ingawa walipingwa popote walipohubiri, Yehova alibariki huduma yao hivi kwamba kufikia mwaka wa 60 W.K., Paulo angeweza kuandika kwamba habari njema ilikuwa imehubiriwa “katika viumbe vyote chini ya mbingu.”—Wakolosai 1:23.

Leo, Mashahidi wa Yehova huchukua kwa uzito daraka lao la ‘kuacha nuru yao ing’ae mbele ya watu,’ kama Yesu alivyoamuru. Kupitia vinywa vyao na vichapo, Mashahidi wa Yehova hutangaza habari njema ya Ufalme katika nchi 235 ulimwenguni pote. Wanachapisha vichapo vyao vya Biblia katika lugha 370 hivi ili kweli ya Biblia iweze kufikia watu wengi iwezekanavyo.—Mathayo 24:14; Ufunuo 14:6, 7.

Katika maeneo mengi, Mashahidi wameanza kazi ngumu ya kujifunza lugha za watu ambao wamehamia nchi zao kutoka nchi ambako kazi ya kuhubiri imepigwa marufuku. Kwa mfano, watu wengi kutoka China na Urusi wamehamia majiji kadhaa ya Amerika Kaskazini. Mashahidi wa huko wamejitahidi kujifunza Kichina, Kirusi, na lugha nyingine ili kuwahubiria wageni hao habari njema. Hata kuna mitaala ya kufundisha baadhi ya lugha hizi kwa uharaka zaidi, kusudi habari njema ziweze kuhubiriwa watu wengine wakati shamba lingali ‘jeupe kwa ajili ya kuvunwa.’—Yohana 4:35.

Nabii Isaya alitabiri: “Itakuwa katika siku za mwisho, mlima wa nyumba ya BWANA utawekwa imara juu ya milima, nao utainuliwa juu ya vilima; na mataifa yote watauendea makundi makundi.” Kupitia mwenendo wao na huduma yao, Mashahidi wa Yehova wanawasaidia watu kila mahali waje kwenye “mlima wa nyumba ya BWANA” ili wafunzwe njia za Mungu na kujifunza kutembea katika mapito yake. (Isaya 2:2, 3) Kama Yesu alivyosema, wanapata matokeo yenye kufurahisha kwa kuwa wanaungana ‘kumtukuza Baba yao wa mbinguni,’ Yehova Mungu.—Mathayo 5:16; 1 Petro 2:12.