Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Wakristo leo wapaswa kutii kwa kadiri gani vizuizi vya ndoa kati ya watu wa jamaa vilivyowekwa katika Sheria ya Musa?

Sheria ambayo Yehova alilipa taifa la Israeli haisemi mengi kuhusu utaratibu na sherehe za arusi. Hata hivyo, sheria hiyo ina vizuizi kuhusu ndoa fulani. Kwa mfano, katika andiko la Mambo ya Walawi 18:6-20, tunapata orodha ya uhusiano wa ngono uliokatazwa kati ya ‘mtu aliye wa jamaa ya karibu.’ Mistari hiyo inafafanua kinaganaga ni watu gani wa jamaa ya karibu wasiopaswa kuwa na uhusiano wa ngono. Bila shaka, Wakristo hawako chini ya Sheria ya Musa wala hawajafungwa na amri zake. (Waefeso 2:15; Wakolosai 2:14) Hata hivyo, hiyo haimaanishi kwamba Wakristo wanaweza kupuuza tu sheria hiyo wanapochagua mwenzi wa ndoa. Kuna sababu nyingi za kutopuuza sheria hiyo.

Kwanza kabisa, nchi mbalimbali zina sheria zinazozuia ndoa kati ya watu wa jamaa ya karibu, nao Wakristo wanapaswa kutii sheria za nchi wanakoishi. (Mathayo 22:21; Waroma 13:1) Bila shaka, sheria hizo hutofautiana katika nchi mbalimbali. Sheria nyingi za kisasa kuhusu ndoa za namna hiyo, zimewekwa kwa kufikiria hasa kasoro za urithi zinazoweza kutokea. Ni jambo linalojulikana wazi kwamba ikiwa watu wa jamaa ya karibu wataoana yaelekea watazaa watoto wenye kasoro za urithi na magonjwa. Kwa sababu hiyo na kwa sababu ya ‘kujitiisha kwa mamlaka zilizo kubwa,’ Wakristo wanaofunga ndoa hutii sheria za kwao kuhusu ndoa.

Kisha kuna mambo yanayokubalika na yasiyokubalika katika jumuiya ambako mtu anaishi. Karibu kila utamaduni una sheria na desturi zinazokataza ndoa kati ya watu wa jamaa ya karibu, na mara nyingi ndoa hizo huonwa kuwa sawa na kufanya ngono na mtu wa familia na hivyo ni mwiko. Ijapokuwa tamaduni mbalimbali huenda zikatofautiana sana kuhusu vizuizi vya ndoa hususa, ‘kwa kawaida mwiko huo huzingatiwa hata zaidi ikiwa watu ni wa jamaa za karibu zaidi ili kuwakataza kuwa na uhusiano wa ngono,’ chasema kichapo The Encyclopædia Britannica. Kwa hiyo, hata kusipokuwa na uhusiano wa ngono kati ya watu wa jamaa ya karibu, Wakristo hawangependa kupuuza kabisa desturi au maoni ya jumuiya na kuleta suto kwa kutaniko la Kikristo au kwa jina la Mungu.—2 Wakorintho 6:3.

Hatupaswi pia kupuuza dhamiri tuliyopewa na Mungu. Watu wote huzaliwa wakiwa na uwezo wa kutofautisha lililo sahihi na lililo kosa, mema na mabaya. (Waroma 2:15) Dhamiri yao huwaambia mambo yanayokubalika na yanayofaa na mambo yasiyokubalika na yanayoudhi, isipokuwa iwe imepotoshwa au imefanywa kuwa sugu na mazoea mapotovu. Yehova alidokeza jambo hilo alipowapa Waisraeli sheria yake inayokataza ndoa kati ya watu wa jamaa ya karibu. Twasoma hivi: “Nanyi msifanye matendo kama yale ya nchi ya Misri mliyokaa; wala msifanye matendo kama yale ya nchi ya Kanaani, nitakayowapeleka; wala msiende katika amri zao hao.” (Mambo ya Walawi 18:3) Wakristo huthamini sana dhamiri yao iliyozoezwa na Biblia na hawairuhusu ipotoshwe na viwango vya mataifa vilivyopotoka vya kuamua mema na mabaya.—Waefeso 4:17-19.

Kwa hiyo, tunaweza kufikia mkataa gani? Ingawa Wakristo hawako chini ya Sheria ya Musa, dhamiri yao huwaonyesha waziwazi kwamba ndoa kati ya watu wa jamaa ya karibu—kama vile baba na binti, mama na mwana, ndugu na dada—haikubaliki kabisa katika kutaniko la Kikristo. * Kadiri ukoo unavyozidi kuwa wa mbali, Wakristo hutambua kwamba kuna sheria na amri kuhusu ndoa zilizofungwa kisheria na kwamba kuna viwango vinavyokubalika kijamii na kitamaduni. Mambo hayo yapasa kufikiriwa kwa makini ili tuweze kutii amri hii ya Kimaandiko: “Acheni ndoa iwe yenye kuheshimika miongoni mwa wote.”—Waebrania 13:4.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Kwa habari zaidi, tafadhali ona makala yenye kichwa “Wakristo Waoneje Ndoa Kati ya Watu wa Jamaa ya Karibu?” katika gazeti Mnara wa Mlinzi, Machi 15, 1978, ukurasa wa 25-26 la Kiingereza.