Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Usafi Unamaanisha Nini Hasa?

Usafi Unamaanisha Nini Hasa?

Usafi Unamaanisha Nini Hasa?

KWA sababu ya hali chafu zenye kushtusha barani Ulaya na Marekani katika karne ya 18 na ya 19, mishonari wa wakati huo walihubiri kile kinachoweza kuitwa “kanuni ya usafi.” Kanuni hiyo ilifananisha uchafu na dhambi na kuonyesha kwamba usafi ulifanya mtu awe na ukaribu zaidi na Mungu. Labda hiyo ndiyo iliyofanya usemi “Usafi ni karibu na uchamungu” uvutie watu wengi.

Kanisa la Jeshi la Wokovu lililoanzishwa na William na Catherine Booth lilifuata kanuni hiyo. Kulingana na kitabu Health and Medicine in the Evangelical Tradition, mojawapo ya miito ya mapema ya kanisa hilo ilikuwa: ‘Usafi, Chakula, na Wokovu.’ Kisha, wakati Louis Pasteur na wengineo walipothibitisha pasipo shaka kwamba viini vya bakteria husababisha magonjwa, watu wakaanza kuzingatia usafi zaidi kwa kuwa walikuwa na sababu za kisayansi za kufanya hivyo.

Baadhi ya hatua zilizochukuliwa mara moja ni kutomlazimisha shahidi mahakamani aape kwa kuibusu Biblia na kukomesha desturi ya kutumia kikombe kimoja cha kunywea kwenye shule na vituo vya magari-moshi. Jitihada pia zilifanywa ili kila mtu awe na kikombe chake cha kunywea divai wakati wa ibada badala ya watu wote kutumia kikombe kimoja. Naam, inaonekana watu hao walioanzisha jitihada hizo za usafi walifanikiwa sana kubadili maoni ya watu kuhusu usafi. Walifanikiwa sana hivi kwamba mwandishi mmoja aliyaita matokeo ya jitihada zao “shauku ya usafi inayopita kiasi.”

Hata hivyo, yaonekana ‘shauku hiyo ya usafi inayopita kiasi’ ilikuwa ya kijuujuu tu. Baada ya muda mfupi, wafanyabiashara wabunifu waligeuza sabuni ya kawaida kuwa bidhaa ya urembo. Matangazo ya biashara yaliyofanywa kwa ujanja yaliwasadikisha wanunuzi kwamba kutumia bidhaa fulani za usafi kungewafanya waonekane kuwa watu wa hali ya juu hivi kwamba wengine wangewaonea wivu. Televisheni huendeleza maoni hayo yasiyo ya kweli. Ni mara chache sana utawaona watu mashuhuri na wenye kuvutia, ambao hutumiwa kwenye matangazo ya biashara na mifululizo ya drama za televisheni na redio, wakisafisha nyumba, wakifagia, wakiokota takataka, au kuondoa kinyesi cha mbwa au paka wao.

Pia kuna wale wanaosababu kwamba kazi ya kuajiriwa huwawezesha kugharimia mahitaji ya maisha, lakini kazi ya nyumbani au kazi nyingine za usafi haziwanufaishi kifedha. Hawaoni haja yoyote ya kutunza mazingira kwa kuwa kufanya hivyo hakuwanufaishi kifedha. Kwa sababu hiyo watu fulani leo hufikiri kwamba usafi wa kimwili pekee ndio muhimu.

Maoni ya Mungu Kuhusu Usafi

Hapana shaka kwamba jitihada hizo za mapema za kufundisha watu usafi ziliboresha hali yao ya maisha. Jambo hilo ni kweli kwa kuwa usafi ni sifa inayotokana na Yehova Mungu, aliye mtakatifu na safi. Yeye hutufundisha ili tupate faida kwa kuwa watakatifu na safi katika mwenendo wetu.—Isaya 48:17; 1 Petro 1:15.

Yehova Mungu hutuwekea kielelezo kizuri kuhusiana na usafi. Usafi, na vilevile sifa zake nyingine ambazo hazionekani, zaonekana wazi katika uumbaji wake. (Waroma 1:20) Tunaona kwamba uumbaji wenyewe hausababishi uchafuzi wenye kudumu. Dunia iliyokusudiwa iwe mahali safi na panapofaa pa kuishi ina mifumo ya ikolojia ambayo huiwezesha ijisafishe kwa njia ya ajabu. Uumbaji huo safi ungetokezwa tu na Mbuni mwenye kuzingatia usafi. Kwa hiyo, tunaweza kuona kutokana na uumbaji kwamba waabudu wa Mungu wanapaswa kuwa safi katika sehemu zote za maisha yao.

Sehemu Nne za Usafi

Biblia hutaja sehemu nne ambazo waabudu wa Mungu wapaswa kujitahidi kuwa safi. Na tuchunguze kila mojawapo ya sehemu hizo.

Kiroho. Hii ndiyo inayoweza kusemwa kuwa sehemu muhimu zaidi ya usafi kwa sababu inahusiana na matarajio ya mtu ya kupata uhai udumuo milele. Hata hivyo, sehemu hii ya usafi ndiyo hupuuzwa zaidi. Kwa ufupi, kuwa safi kiroho humaanisha kutovuka mipaka ambayo Mungu ameweka kati ya ibada ya kweli na ibada isiyo ya kweli, kwa kuwa Mungu huiona ibada yoyote isiyo ya kweli kuwa chafu. Mtume Paulo aliandika: “‘Kwa hiyo tokeni miongoni mwao, na jitengeni wenyewe,’ asema Yehova, ‘na komeni kugusa kitu kisicho safi’; ‘na hakika mimi nitawakaribisha ndani.’” (2 Wakorintho 6:17) Kuhusu jambo hilo, mwanafunzi Yakobo anataja mambo waziwazi: “Namna ya ibada iliyo safi na isiyo na unajisi kwa maoni ya Mungu wetu na Baba ni hii: . . . kufuliza kujitunza mwenyewe bila doa kutokana na ulimwengu.”—Yakobo 1:27.

Mungu alionyesha waziwazi kwamba yeye hakubali ibada yake safi ichanganywe na ibada isiyo ya kweli. Mara nyingi ibada isiyo ya kweli huhusisha mazoea yasiyo safi, sanamu, na miungu yenye kuchukiza. (Yeremia 32:35) Hivyo, Wakristo wa kweli wanahimizwa waepuke kabisa ibada isiyo safi.—1 Wakorintho 10:20, 21; Ufunuo 18:4.

Kiadili. Kuhusu usafi wa kiadili Mungu pia huweka mipaka kati ya kilicho safi na kisicho safi. Ulimwengu wote kwa ujumla umekuwa kama inavyofafanuliwa kwenye andiko la Waefeso 4:17-19: ‘Wako katika giza kiakili, na kufanywa wageni kwa uhai ambao ni wa Mungu. Wakiisha kuishiwa na hisia zote za adili, walijikabidhi wenyewe kwenye mwenendo mlegevu ili wafanye ukosefu wa usafi wa kila namna pamoja na pupa.’ Wakristo wanahitaji kuwa waangalifu kwa kuwa mawazo machafu hujitokeza katika njia mbalimbali, zilizo wazi na zisizo wazi.

Wanaompenda Mungu wanajua kwamba ukahaba, ngono kati ya wanaume kwa wanaume au kati ya wanawake kwa wanawake, ngono kabla ya ndoa, na kutazama picha chafu huvunja viwango vya Mungu vya usafi wa kiadili. Hata hivyo, mazoea hayo ni ya kawaida katika ulimwengu wa burudani na mitindo. Kwa hiyo, Wakristo wanapaswa kuwa macho kuhusiana na mazoea hayo. Kwenda kwenye mikutano ya Kikristo au kwenye vikusanyiko vya kirafiki huku umevalia mavazi yanayoonyesha sehemu za mwili zisizopaswa kuonekana huvuta fikira kwa njia isiyofaa kwenye mwili wako, na huonyesha kwamba unapuuza usafi wa kiadili. Mbali na kuleta mawazo ya kilimwengu katika ushirika wa Kikristo, kuvalia hivyo kunaweza kufanya wengine waanze kufikiria mambo yasiyofaa. Hii ni sehemu ambayo Wakristo wanapaswa kujitahidi sana kuonyesha “hekima ya kutoka juu.”—Yakobo 3:17.

Kiakili. Hupaswi kuchafua akili yako kwa mawazo yasiyo safi. Yesu alionya kuhusu mawazo yasiyo safi aliposema: “Kila mtu ambaye hufuliza kumtazama mwanamke ili kuwa na harara kwa ajili yake tayari amefanya uzinzi pamoja naye moyoni mwake.” (Mathayo 5:28; Marko 7:20-23) Maneno hayo pia yanahusu kutazama picha na sinema chafu, kusoma vitabu vinavyoeleza vitendo vichafu vya ngono, na kusikiliza nyimbo zinazopendekeza mambo yasiyofaa. Hivyo, Wakristo hawapaswi kufikiria mambo machafu yanayoweza kuwafanya waseme na kutenda mambo machafu, yasiyo matakatifu.—Mathayo 12:34; 15:18.

Kimwili. Katika Biblia, utakatifu na usafi wa kimwili ni mambo yanayohusiana sana. Kwa mfano, Paulo aliandika: “Wapendwa, acheni tujisafishe wenyewe kila unajisi wa mwili na wa roho, tukikamilisha utakatifu katika hofu ya Mungu.” (2 Wakorintho 7:1) Kwa hiyo, Wakristo wa kweli wanapaswa kujitahidi kudumisha miili yao, nyumba zao, na mazingira yao yakiwa safi na nadhifu kwa kadiri wawezavyo. Hata mahali ambapo maji ya kuosha au kuoga ni haba, Wakristo wanapaswa kujitahidi kwa kadiri wawezavyo kuwa safi na nadhifu.

Usafi wa kimwili unamaanisha pia kuepuka kabisa kutumia tumbaku, kulewa, na kutumia dawa za kulevya, mazoea ambayo huchafua na kudhuru mwili. Mchungaji aliyetajwa katika Wimbo Ulio Bora alifurahia harufu nzuri ya msichana Mshulami. (Wimbo Ulio Bora 4:11) Tunaonyesha upendo kwa kudumisha usafi, kwa kuwa hatutaki kuwasumbua watu walio karibu nasi kwa harufu mbaya. Marashi yanaweza kuwa yenye kupendeza, lakini hayo pekee hayatoshi. Tunapaswa kuoga kwa ukawaida na kuvalia mavazi safi.

Kudumisha Maoni Yenye Usawaziko

Watu wanaweza kujishughulisha na usafi wa kimwili kupita kiasi. Kwa upande mmoja, kujishughulisha na usafi kupita kiasi kunaweza kutunyima furaha. Kunaweza pia kuchukua wakati mwingi. Kwa upande mwingine, nyumba chafu zisizo nadhifu zinaweza kugharimu pesa nyingi kuzirekebisha. Badala ya kushughulikia usafi kupita kiasi au kuwa wachafu, inafaa tuwe na usawaziko na kudumisha nyumba zetu zikiwa safi na nadhifu.

Usijaze nyumba vitu usivyohitaji. Ni vigumu kusafisha nyumba au vyumba ambavyo vimejaa vitu vilivyowekwa ovyoovyo, na katika nyumba kama hiyo, huenda pia ikawa vigumu kuona uchafu mahali ulipo. Inachukua muda mfupi zaidi kusafisha nyumba zenye vitu vichache, vilivyopangwa vizuri. Biblia inapendekeza sana kuishi maisha sahili: “Tukiwa na riziki na cha kujifunika, tutakuwa wenye kuridhika na vitu hivi.”—1 Timotheo 6:8.

Dumisha nyumba yako ikiwa nadhifu. Kudumisha nyumba ikiwa safi ni daraka la kila mtu anayeishi humo. Uchafu nyumbani huanzia kwenye vyumba vya kulala. Kuwa nadhifu humaanisha kuweka kila kitu mahali pake pafaapo. Kwa mfano, nguo chafu hazipaswi kuwekwa kwenye sakafu ya chumba cha kulala. Ni hatari pia kuviacha ovyoovyo vifaa vya watoto vya kuchezea na vifaa vinginevyo. Aksidenti nyingi hutokea nyumbani kwa sababu ya kuacha vitu ovyoovyo.

Ni wazi kwamba usafi na Ukristo ni mambo mawili yasiyoweza kutenganishwa. Kuhusu maisha ya kimungu, nabii Isaya anataja “Njia ya utakatifu.” Naye anaongezea maneno yenye kuamsha fikira kwamba “wasio safi hawatapita juu yake.” (Isaya 35:8) Naam, kusitawisha mazoea mazuri ya usafi sasa huthibitisha kwamba tuna imani katika ahadi ya Mungu kwamba karibuni atatokeza dunia paradiso iliyo safi. Kisha, watu wote katika kila sehemu ya dunia hiyo nzuri watamtukuza Yehova Mungu kwa kufuata kikamili viwango vyake vikamilifu vya usafi.—Ufunuo 7:9.

[Maelezo ya Picha katika ukurasa wa 6]

Kudumisha nyumba ikiwa safi ni daraka la kila mtu anayeishi humo

[Maelezo ya Picha katika ukurasa wa 7]

Dunia ina uwezo wa ajabu wa kujisafisha