Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Alitufundisha Kuwa Wavumilivu na Wastahimilivu

Yehova Alitufundisha Kuwa Wavumilivu na Wastahimilivu

Simulizi la Maisha

Yehova Alitufundisha Kuwa Wavumilivu na Wastahimilivu

LIMESIMULIWA NA ARISTOTELIS APOSTOLIDIS

Chini ya Milima ya Caucasus, upande wa kaskazini, kuna jiji moja la Urusi liitwalo Pyatigorsk, linalojulikana sana kwa sababu ya maji yake ya chemchemi yenye madini na hali ya hewa yenye kupendeza. Nilizaliwa jijini humo mwaka wa 1929 na wazazi Wagiriki waliokuwa wakimbizi. Miaka kumi baada ya hofu kuu na maangamizi ya kijamii yaliyosababishwa na utawala wa Stalin, tulijikuta tukiwa wakimbizi tena, kwa kuwa tulilazimika kuhamia Ugiriki.

BAADA ya kuhamia Piraiévs, Ugiriki, tulielewa neno “wakimbizi” kwa njia tofauti kabisa. Tulihisi kama wageni kabisa. Ingawa mimi na ndugu yangu tuliitwa majina ya wanafalsafa maarufu wa Ugiriki, Socrates na Aristotle, majina hayo yalitumiwa mara chache sana. Kila mtu alituita Warusi wadogo.

Mamangu mpendwa alikufa punde tu baada ya Vita ya Pili ya Ulimwengu kuanza. Yeye alikuwa nguzo muhimu katika familia yetu, na tulihuzunishwa sana na kifo chake. Kwa kuwa aliugua kwa muda, alinizoeza kufanya kazi nyingi za nyumbani. Mazoezi hayo yalinisaidia sana baadaye.

Vita na Ukombozi

Vita, uvamizi wa Nazi, na makombora yaliyorushwa mfululizo na majeshi ya Muungano yalifanya tuone kila siku kama ndiyo siku yetu ya mwisho. Kulikuwa na umaskini mwingi, njaa, na vifo. Ili kutosheleza mahitaji yetu tukiwa watatu, nilianza kufanya kazi kwa bidii pamoja na babangu tangu nilipokuwa na umri wa miaka 11. Sikuweza kupata elimu nzuri kwa sababu sikujua Kigiriki vizuri, na pia kwa sababu ya vita na madhara yake.

Uvamizi wa Ujerumani katika nchi ya Ugiriki ulikoma Oktoba mwaka wa 1944 na muda mfupi baadaye nikakutana na Mashahidi wa Yehova. Tumaini la Biblia la wakati ujao mzuri chini ya Ufalme wa Mungu lilinigusa moyo wakati huo nilipokuwa nimehuzunika na kukata tamaa. (Zaburi 37:29) Ahadi ya Mungu ya kuishi milele katika hali zenye amani hapa duniani ilinituliza sana. (Isaya 9:7) Mwaka wa 1946 mimi na babangu tulibatizwa, kuonyesha wakfu wetu kwa Yehova.

Mwaka uliofuata, nilifurahi kupata mgawo wangu wa kwanza kama mtumishi wa utangazaji (ambaye baadaye aliitwa mtumishi wa magazeti) katika kutaniko la pili lililoanzishwa huko Piraiévs. Eneo letu lilianzia Piraiévs hadi Eleusis, umbali wa kilometa 50 hivi. Wakati huo, kutaniko letu lilikuwa na Wakristo wengi watiwa-mafuta. Nilipata pendeleo la kufanya kazi nao na kujifunza kutoka kwao. Nilifurahi kushirikiana nao kwa kuwa walisimulia mambo mengi sana yaliyoonwa kuonyesha jitihada nyingi inayohitajiwa ili kufanya kazi ya kuhubiri. Maisha yao yalidhihirisha kwamba ili kumtumikia Yehova kwa uaminifu, tunahitaji subira na ustahimilivu mwingi. (Matendo 14:22) Ninafurahi kama nini kwamba kuna makutaniko zaidi ya 50 ya Mashahidi wa Yehova katika eneo hilo leo!

Magumu Yasiyotazamiwa

Baada ya muda fulani, nilijuana na Eleni, mwanamke Mkristo mchanga mwenye bidii na mwenye kuvutia kutoka jiji la Patras. Tulifikia uamuzi wa kuoana mwishoni mwa mwaka wa 1952. Hata hivyo, baada ya miezi michache, Eleni akawa mgonjwa sana. Madaktari waligundua kwamba alikuwa na uvimbe kwenye ubongo, na kwamba hali yake ilikuwa mbaya sana. Ilibidi afanyiwe upasuaji mara moja. Baada ya jitihada nyingi za kutafuta daktari, tuliweza kupata mmoja huko Athens ambaye, licha ya kuwa na vifaa vichache wakati huo, alikubali kumfanyia upasuaji bila damu kupatana na imani yetu ya kidini. (Mambo ya Walawi 17:10-14; Matendo 15:28, 29) Baada ya upasuaji huo, madaktari hawakuwa na hakika kabisa kwamba mchumba wangu angepatwa na kansa hiyo tena.

Ningefanyaje katika hali hiyo? Kwa kuwa hali zilikuwa zimebadilika, je, ningevunja uchumba huo ili niwe huru? La! Tulipoanza uchumba nilikuwa nimetoa ahadi, na nilitaka ndiyo yangu imaanishe ndiyo. (Mathayo 5:37) Sikufikiria kamwe kubadili uamuzi wangu. Eleni alitunzwa na dadake mkubwa na baada ya kupata nafuu kwa kiasi fulani tukaoana mnamo Desemba mwaka wa 1954.

Miaka mitatu baadaye, Eleni alirudiwa na kansa, na daktari yuleyule akamfanyia upasuaji mwingine. Wakati huu alipasua ndani zaidi kwenye ubongo ili kuuondoa uvimbe wote. Kwa sababu hiyo mke wangu alilemaa kwa kadiri fulani na hangeweza kuzungumza vizuri. Sote wawili tulikabili magumu mengi mapya. Haikuwa rahisi kwa mke wangu kufanya hata zile kazi ndogo-ndogo. Hali yake ilizidi kuwa mbaya na tukalazimika kufanya mabadiliko makubwa katika shughuli zetu za kila siku. Zaidi ya yote, hali hiyo ilihitaji tuwe na uvumilivu na ustahimilivu mkubwa.

Sasa yale mazoezi niliyopata kutoka kwa mamangu yalinisaidia sana. Nilitayarisha vitu vyote vilivyohitajika kwa upishi mapema kila asubuhi naye Eleni alipika. Tulialika wageni mara nyingi, ambao walitia ndani wahudumu wa wakati wote, watu tuliojifunza nao Biblia, na Wakristo wenzetu wenye uhitaji katika kutaniko. Wote walisema kwamba milo hiyo ilikuwa mitamu sana! Mimi na Eleni tulisaidiana kufanya kazi nyingine za nyumbani na nyumba yetu ilikuwa safi na nadhifu. Hali hiyo ngumu sana iliendelea kwa miaka 30.

Bidii Licha ya Ulemavu

Mimi na wengine tulichochewa sana kuona kwamba hakuna chochote kingeweza kupunguza upendo wa mke wangu kwa Yehova na bidii yake katika kumtumikia. Baada ya kujitahidi sana kwa muda fulani, Eleni aliweza kusema maneno machache. Alipenda kuwafikia watu barabarani na kuwahubiria habari njema kutoka katika Biblia. Nilikuwa nikiandamana naye katika safari zangu za kikazi na kuegesha gari karibu na njia ya miguu. Alikuwa akifungua dirisha la gari na kuwakaribisha wapita njia waje wachukue nakala za Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Wakati mmoja, aliwapatia watu magazeti 80 katika muda wa saa mbili. Mara nyingi alichukua na kuwaachia watu magazeti yote ya zamani yaliyokuwa kutanikoni. Eleni pia alishiriki kwa ukawaida mahubiri ya aina nyingine.

Sikuzote mke wangu aliandamana nami kwenye mikutano katika miaka yote ya ulemavu wake. Hakukosa mkusanyiko au kusanyiko, hata tulipohitajika kusafiri nje ya nchi kwa sababu Mashahidi wa Yehova walinyanyaswa nchini Ugiriki. Licha ya ulemavu wake, alihudhuria makusanyiko huko Austria, Ujerumani, Saiprasi, na nchi nyinginezo. Eleni hakulalamika kamwe wala kuwa mwenye kudai mno, hata wakati majukumu yangu yaliyoongezeka katika utumishi wa Yehova yalipofanya mambo yasiwe rahisi kwake.

Hali hiyo ilinifunza kuvumilia na kustahimili. Yehova alinisaidia mara nyingi. Ndugu na dada walijitoa kadiri wawezavyo ili kutusaidia, nao madaktari walitusaidia kwa fadhili. Wakati wa miaka hiyo migumu, hatukukosa vitu vya lazima maishani, ingawa sikuweza kufanya kazi wakati wote kwa sababu ya hali yetu ngumu. Sikuzote tulitanguliza masilahi ya Yehova na utumishi wake.—Mathayo 6:33.

Wengi wametaka kujua kilichotutegemeza wakati huo wa magumu. Ninapokumbuka yaliyopita, ninaona kwamba funzo la Biblia la kibinafsi, kusali kwa Mungu kutoka moyoni, kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida, na kushiriki kwa bidii kazi ya kuhubiri kulitusaidia kuvumilia na kustahimili. Sikuzote tulikumbuka maneno yenye kutia moyo kwenye Zaburi 37:3-5: “Umtumaini BWANA ukatende mema . . . Nawe utajifurahisha kwa BWANA . . . Umkabidhi BWANA njia yako, pia umtumaini, naye atafanya.” Andiko lingine lililokuwa muhimu kwetu ni Zaburi 55:22: “Umtwike BWANA mzigo wako naye atakutegemeza, hatamwacha mwenye haki aondoshwe milele.” Kama mtoto anayemtumaini babake kabisa, tulimtwika Yehova mizigo yetu na kumwachia.—Yakobo 1:6.

Katika Aprili 12, 1987, mke wangu alipokuwa akihubiri mbele ya nyumba yetu, mlango mkubwa wa chuma ulijifunga kwa kishindo nyuma yake, nao ukamrusha na kumwangusha kwenye njia ya miguu. Alijeruhiwa vibaya na kwa sababu hiyo akapoteza fahamu kwa miaka mitatu. Alikufa mapema mwaka wa 1990.

Kumtumikia Yehova Kadiri Niwezavyo

Niliwekwa rasmi kutumikia nikiwa mtumishi wa kutaniko huko Nikaia, Piraiévs, mwaka wa 1960. Tangu wakati huo nimepata pendeleo la kutumikia katika makutaniko kadhaa huko Piraiévs. Ingawa sikupata watoto, nimefurahia kuwasaidia watoto wengi wa kiroho wawe imara katika kweli. Baadhi yao sasa wanatumikia wakiwa wazee wa kutaniko, watumishi wa huduma, wahudumu mapainia, na Wanabetheli.

Baada ya demokrasia kurudishwa Ugiriki mwaka wa 1975, Mashahidi wa Yehova waliweza kufanya makusanyiko yao kwa uhuru, pasipo kujificha misituni. Mazoezi ambayo baadhi yetu tulipata tulipotayarisha makusanyiko katika nchi nyingine, yalitusaidia sana. Kwa hiyo, nilifurahia pendeleo la kutumika katika halmashauri mbalimbali za makusanyiko kwa miaka mingi.

Kisha mnamo mwaka wa 1979, mipango ilifanywa kujenga Jumba la Kusanyiko nchini Ugiriki, kwenye vitongoji vya Athens. Nilipewa mgawo wa kusaidia kupanga na kujenga jumba hilo kubwa. Ujenzi huo pia ulihitaji uvumilivu na ustahimilivu mwingi. Kufanya kazi kwa miaka mitatu pamoja na mamia ya akina ndugu na dada wenye kujitoa, kulifanya tuwe na upendo thabiti na umoja kati yetu. Sitasahau kamwe ujenzi huo.

Kutosheleza Mahitaji ya Kiroho ya Wafungwa

Miaka michache baadaye, nilipata pendeleo jingine. Karibu na eneo ambalo kutaniko langu limegawiwa kuhubiri, huko Korydallos, kuna mojawapo ya magereza makubwa zaidi nchini Ugiriki. Tangu Aprili mwaka wa 1991, nilipewa mgawo wa kutembelea gereza hilo kila juma nikiwa mhudumu wa Mashahidi wa Yehova. Nimeruhusiwa kuongoza mafunzo ya Biblia na kufanya mikutano ya Kikristo pamoja na wafungwa wenye kupendezwa kwenye gereza hilo. Wengi wao wamefanya mabadiliko makubwa yanayothibitisha kwamba Neno la Mungu lina nguvu nyingi. (Waebrania 4:12) Jambo hilo limewavutia wafanyakazi wa gereza na wafungwa pia. Baadhi ya wafungwa ambao nimejifunza nao Biblia wameachiliwa na sasa ni wahubiri wa habari njema.

Kwa muda fulani nilijifunza na wafungwa watatu waliokuwa wauzaji sugu wa dawa za kulevya. Walipofanya maendeleo ya kiroho, walianza kuhudhuria funzo lao la Biblia wakiwa wamenyoa ndevu, wamechana nywele vizuri, na wamevaa shati na tai katikati ya mwezi wa Agosti—mmojawapo ya miezi yenye joto jingi sana nchini Ugiriki! Mkurugenzi wa gereza hilo, msimamizi mkuu, na wafanyakazi kadhaa walitoka mbio ofisini mwao kuwatazama wafungwa hao. Hawakuamini macho yao!

Jambo jingine lenye kutia moyo lilitukia katika sehemu ya gereza ya wafungwa wanawake. Funzo la Biblia lilianzishwa na mwanamke aliyekuwa akitumikia kifungo cha maisha kwa kuua. Alikuwa mkaidi sana. Lakini baada ya muda mfupi, akaanza kufanya mabadiliko makubwa kwa sababu ya kweli ya Biblia aliyokuwa anajifunza. Wengi walisema kwamba alikuwa simba aliyekuwa anageuka kuwa kondoo! (Isaya 11:6, 7) Punde si punde mkurugenzi wa gereza hilo akaanza kumheshimu na kumwamini. Nilifurahi kuona akifanya maendeleo ya kiroho na kufikia hatua ya kujiweka wakfu kwa Yehova.

Kuwasaidia Wagonjwa na Wazee

Baada ya kuona jinsi mke wangu alivyopambana na ugonjwa kwa muda mrefu, nimekuwa mwenye kujali sana mahitaji ya walio wagonjwa na wazee miongoni mwetu. Nilipendezwa sana na makala katika vichapo vyetu zilizotutia moyo tujitahidi kuwasaidia kwa upendo wagonjwa na wazee. Nilithamini sana makala hizo na kuzikusanya. Baada ya miaka kadhaa nilitengeneza kijitabu chenye kurasa zaidi ya mia moja. Makala ya kwanza kwenye kijitabu hicho ilikuwa “Consideration for Older Persons and Afflicted Ones” (“Kuwafikiria Wazee na Walio na Shida”) kutoka katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Julai 15, 1962 la Kiingereza. Nyingi za makala hizo zilionyesha kwamba inafaa kwa kila kutaniko kuwasaidia wagonjwa na wazee.—1 Yohana 3:17, 18.

Wazee walianzisha kikundi cha akina ndugu na dada waliojitoa kushughulikia mahitaji ya wagonjwa na wazee kutanikoni mwetu. Tuliwagawanya wajitoleaji hao katika vikundi mbalimbali. Baadhi yao waliweza kusaidia mchana, wengine usiku, wengine kushughulikia usafiri, na wengine ambao wangeweza kuitwa kusaidia wakati wowote wa dharura, iwe usiku au mchana.

Matokeo ya jitihada hizo yamekuwa yenye kutia moyo. Kwa mfano, dada mmoja mgonjwa aliyekuwa akiishi peke yake alikutwa sakafuni akiwa amepoteza fahamu wakati wa mojawapo ya ziara alizokuwa akifanyiwa kila siku. Tulimjulisha dada mmoja mwenye gari aliyekuwa akiishi karibu. Dada huyo alimpeleka haraka kwenye hospitali iliyokuwa karibu. Ilimchukua dakika kumi kufika kwenye hospitali hiyo—hajawahi kuendesha gari kwa kasi hivyo! Madaktari walisema kwamba kufikishwa hospitalini haraka kuliokoa maisha yake.

Shukrani kutoka kwa wagonjwa na wazee huwaridhisha sana washiriki wa kikundi hicho. Wao hutiwa moyo na tumaini kwamba wataishi na ndugu na dada hao katika mfumo mpya wa Mungu chini ya hali tofauti. Nao huthawabishwa pia na kule kujua kwamba msaada waliotoa uliwasaidia wagonjwa na wazee hao kuvumilia wakati wa shida.

Ustahimilivu Umeleta Thawabu

Sasa ninatumikia nikiwa mzee katika mojawapo ya makutaniko huko Piraiévs. Licha ya uzee na matatizo ya afya, nina furaha kwamba ninaweza kushiriki utendaji mbalimbali wa kutaniko.

Katika miaka iliyopita, nimehitaji kuwa na nguvu na ustahimilivu usio wa kawaida kwa sababu ya hali ngumu, matatizo, na matukio yasiyotazamiwa. Hata hivyo, sikuzote Yehova amenipa nguvu ninazohitaji ili kushinda matatizo hayo. Mara nyingi maneno haya ya mtunga-zaburi yametimizwa kwangu: “Niliposema, mguu wangu unateleza; Ee BWANA, fadhili zako zilinitegemeza. Katika wingi wa mawazo ya moyoni mwangu, faraja zako zaifurahisha roho yangu.”—Zaburi 94:18, 19.

[Picha katika ukurasa wa 25]

Nikiwa na mke wangu, Eleni, baada ya yeye kufanyiwa upasuaji wa pili, mwaka wa 1957

[Picha katika ukurasa wa 26]

Kwenye mkusanyiko huko Nuremberg, Ujerumani, mwaka wa 1969

[Picha katika ukurasa wa 28]

Kikundi cha akina ndugu waliowasaidia wagonjwa na wazee