Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mahali pa Kujificha na Upepo

Mahali pa Kujificha na Upepo

Mahali pa Kujificha na Upepo

UKIWA juu ya milima ya Alps ya Ulaya, utaona vichaka imara vya mawaridi ya Alps. Mawaridi haya mafupi aina ya rhododendron mara nyingi humea yakiwa yamesongamana pamoja kwenye ardhi ili kujilinda kutokana na upepo mkali wa nyanda za juu. Upepo huo mkali usiotulia huhatarisha mimea hii ya milimani kwa kupunguza halijoto yake, kukausha hewa na udongo, na kung’oa mizizi.

Mawaridi ya Alps mara nyingi huepuka kuharibiwa na upepo kwa kumea katika mianya iliyo katika miamba. Ijapokuwa udongo katika sehemu hizo si mwingi, mianya hiyo huilinda mimea dhidi ya upepo na kuiwezesha kuhifadhi maji. Yajapokuwa hayaonekani sana kwa karibu mwaka mzima, mawaridi hayo hurembesha milima hiyo kwa maua yenye rangi nyekundu nyangavu wakati wa kiangazi.

Nabii Isaya alieleza kwamba “wakuu” wangechaguliwa na Mungu na kila mmoja angekuwa kama “mahali pa kujificha na upepo.” (Isaya 32:1, 2) Chini ya mwelekezo wa Mfalme Yesu Kristo, wakuu hawa wa kiroho, au waangalizi wangekuwa kama miamba imara, isiyoondoleka wakati wa mikazo au magumu. Wangeandaa kimbilio linalotegemeka wakati wa hatari na kuwasaidia wenye uhitaji kuhifadhi akiba yao ya maji ya kiroho kutoka kwa Neno la Mungu.

Kama upepo mkali, minyanyaso, kuvunjika moyo, au magonjwa yanaweza kumpiga-piga Mkristo na kufanya imani yake idhoofike iwapo hana ulinzi. Wazee Wakristo wanaweza kuandaa ulinzi kwa kusikiliza kwa makini matatizo yake, kutoa ushauri wa Biblia na kutoa kitia moyo au msaada halisi. Kama Kristo Yesu, Mfalme wao aliyetawazwa, wao wanataka kuwasaidia wale ‘waliotupwa huku na huku.’ (Mathayo 9:36) Nao hutamani kuwasaidia wale walioathiriwa na pepo za mafundisho yasiyo ya kweli. (Waefeso 4:14) Huenda msaada huo ukawa wa maana zaidi iwapo utatolewa kwa wakati unaofaa.

“Nilifadhaika sana wakati marafiki wangu wa karibu walipoliacha kutaniko na wakati huohuo baba yangu akapatwa na ugonjwa wa kuvuja damu katika ubongo,” aeleza Miriam. “Nilishuka moyo sana na ili kushinda hali hiyo nilianza urafiki na mvulana mmoja mlimwengu. Muda mfupi baadaye, nilihisi kuwa sifai kitu hivyo nikawajulisha wazee wa kutaniko kwamba nilikuwa nimeamua kuacha kweli kwa sababu nilikuwa na uhakika kwamba Yehova hangenipenda.

“Katika kipindi hicho cha matatizo, mzee mmoja mwenye kujali alinikumbusha miaka ambayo nilikuwa nimetumikia nikiwa painia wa kawaida. Aliniambia kwamba alivutiwa sana na uaminifu wangu, na akanisihi niwaruhusu wazee wanisaidie na kunihakikishia kwamba Yehova ananipenda. Upendo wao wakati huo wa matatizo ulikuwa kama ‘mahali pa kujificha’ na dhoruba kali ya kiroho iliyokuwa imenizunguka. Kwa kipindi cha mwezi mmoja nilivunja uhusiano wangu na mvulana yule na tangu wakati huo nimeendelea kutembea katika njia ya kweli.”

Wazee hufurahi sana wanapoona Wakristo wenzao wakifanya maendeleo ya kiroho kwa sababu ya ulinzi wanaopata kwa wakati ufaao. Nao wazee hao walio kama “mahali pa kujificha” hutupa mwonjo wa misaada mingi ya kiroho tutakayofurahia wakati wa kipindi cha Miaka Elfu ya Utawala wa Kristo.