Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Walikabiliana na Miiba Katika Miili Yao

Walikabiliana na Miiba Katika Miili Yao

Walikabiliana na Miiba Katika Miili Yao

“Nilipewa mwiba katika mwili, malaika wa Shetani, afulize kunipiga kofi.”—2 WAKORINTHO 12:7.

1. Ni matatizo gani yanayokabili watu leo?

JE, UNAPAMBANA na jaribu lenye kuendelea? Ikiwa ndivyo, si wewe tu unayepambana na jaribu kama hilo. Katika ‘nyakati hizi za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,’ Wakristo waaminifu wanakabiliana na mnyanyaso mkali, matatizo ya kifamilia, magonjwa, mahangaiko ya kifedha, maumivu ya kihisia-moyo, kufiwa na wapendwa, na magumu mengine. (2 Timotheo 3:1-5) Katika nchi fulani, njaa na vita vinatisha maisha ya watu wengi.

2, 3. Ni mtazamo upi usiofaa unaoweza kutokezwa na matatizo yaliyo kama miiba ambayo tunakabili, na kwa nini huenda jambo hilo likawa hatari?

2 Matatizo hayo yanaweza kumfanya mtu ajihisi hoi kabisa, hasa ikiwa atapatwa na matatizo kadhaa kwa wakati mmoja. Ona vile lisemavyo andiko la Mithali 24:10: “Ukizimia [“ukivunjika moyo,” NW] siku ya taabu, nguvu zako ni chache.” Naam, kuvunjika moyo kwa sababu ya majaribu kunaweza kufanya tukose nguvu tunazohitaji sana na kunaweza pia kudhoofisha azimio letu la kuvumilia hadi mwisho. Jinsi gani?

3 Huenda kuvunjika moyo kukatufanya tukose usawaziko. Kwa mfano, ni rahisi sana kutilia chumvi matatizo yetu na kuanza kujihurumia. Huenda wengine hata wakamlilia Mungu, “Kwa nini unaruhusu jambo hili linipate?” Mtu akiruhusu mtazamo kama huo usiofaa usitawi moyoni mwake, basi utamkosesha furaha na uhakika. Mtumishi wa Mungu anaweza kuvunjika moyo sana hivi kwamba huenda hata akaacha kupigana “pigano bora la imani.”—1 Timotheo 6:12.

4, 5. Katika hali fulani, Shetani anahusikaje na matatizo yetu, lakini tunaweza kuwa na uhakika gani?

4 Bila shaka, Yehova Mungu hasababishi majaribu ambayo hutupata. (Yakobo 1:13) Matatizo mengine hutupata kwa sababu tu tunajitahidi kuwa waaminifu kwake. Kwa kweli, wote wanaomtumikia Yehova hushambuliwa na Shetani Ibilisi, adui yake mkubwa. Katika wakati wake mfupi unaosalia, ‘mungu huyo mwovu wa huu mfumo wa mambo’ anajaribu kufanya yeyote anayempenda Yehova aache kufanya mapenzi Yake. (2 Wakorintho 4:4) Shetani hutesa kadiri awezavyo ushirika mzima wa ndugu zetu ulimwenguni pote. (1 Petro 5:9) Ni kweli kwamba matatizo yetu yote hayasababishwi moja kwa moja na Shetani, lakini anaweza kutumia isivyofaa matatizo tunayokabili, akitaka kutudhoofisha zaidi.

5 Hata Shetani au silaha zake ziwe zenye nguvu kadiri gani, tunaweza kumshinda! Tunawezaje kuwa na uhakika huo? Kwa sababu Yehova Mungu hutupigania. Mungu amehakikisha kwamba watumishi wake wanafahamu mbinu za Shetani. (2 Wakorintho 2:11) Kwa kweli, Neno la Mungu hutueleza mengi kuhusu majaribu ambayo huwasumbua Wakristo wa kweli. Kwa habari ya mtume Paulo, Biblia inatumia usemi “mwiba katika mwili.” Kwa nini? Na tuchunguze jinsi ambavyo Neno la Mungu hufafanua usemi huo. Kisha tutaona kwamba si sisi tu tunaohitaji msaada wa Yehova ili kushinda majaribu.

Kwa Nini Majaribu Ni Kama Miiba?

6. Paulo alimaanisha nini kwa usemi “mwiba katika mwili,” na huenda mwiba huo ulikuwa nini?

6 Baada ya kujaribiwa vikali, Paulo alipuliziwa kuandika: “Nilipewa mwiba katika mwili, malaika wa Shetani, afulize kunipiga kofi, ili nisipate kukwezwa kupita kiasi.” (2 Wakorintho 12:7) Mwiba huo uliokuwa katika mwili wa Paulo ni nini? Bila shaka, mwiba ambao umepenya sana kwenye ngozi unasababisha maumivu. Kwa hiyo mfano huo wa mwiba unadokeza kitu ambacho kilimletea Paulo maumivu—yawe ya kimwili, ya kihisia-moyo, au yote mawili. Huenda ikawa Paulo alisumbuliwa na ugonjwa wa macho au ugonjwa mwingine. Au huenda mwiba huo ulimaanisha watu waliopinga kustahili kwake kuwa mtume na kutilia shaka thamani ya kazi yake ya kuhubiri na kufundisha. (2 Wakorintho 10:10-12; 11:5, 6, 13) Hata huo mwiba uwe ulikuwa nini, ulibaki palepale na haungeweza kuondolewa.

7, 8. (a) Usemi ‘kufuliza kupiga kofi’ unamaanisha nini? (b) Kwa nini ni muhimu kukabiliana na miiba yoyote inayotusumbua leo?

7 Ona kwamba mwiba huo ulifuliza kumpiga Paulo kofi. Ona pia kwamba kitenzi cha Kigiriki ambacho Paulo alitumia hapa kinatokana na neno linalotafsiriwa “konzi za vidole.” Neno hilo linatumiwa kihalisi kwenye Mathayo 26:67 na kwa njia ya mfano kwenye 1 Wakorintho 4:11. Katika mistari hiyo, neno hilo lina maana ya kupigwa ngumi. Kwa kuwa Shetani anamchukia sana Yehova na watumishi Wake, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Ibilisi alifurahi kwamba mwiba fulani ulifuliza kumpiga Paulo kofi. Leo, Shetani hufurahi tunapotaabishwa vilevile na mwiba fulani katika mwili.

8 Kwa hiyo, kama Paulo, tunahitaji kujua jinsi ya kukabiliana na miiba hiyo. Hilo ni jambo la kufa na kupona! Kumbuka kwamba Yehova anataka kutupatia uhai wa milele katika ulimwengu mpya, ambako hatutapatwa kamwe na matatizo yaliyo kama miiba. Ili kutusaidia kupata zawadi hiyo nzuri, Mungu ametupatia mifano mingi katika Neno lake takatifu, Biblia, ambayo inaonyesha kwamba watumishi wake waaminifu walifanikiwa kukabiliana na miiba katika miili yao. Hao walikuwa watu wa kawaida, wasio wakamilifu kama vile sisi. Huenda kufikiria watu fulani miongoni mwa ‘wingu hilo kubwa la Mashahidi’ kukatusaidia “tukimbie kwa uvumilivu shindano la mbio lililowekwa mbele yetu.” (Waebrania 12:1) Kutafakari juu ya mambo waliyovumilia kunaweza kuimarisha uhakika wetu kwamba tunaweza kukabiliana na miiba yoyote ambayo Shetani anaweza kutumia dhidi yetu.

Miiba Iliyomsumbua Mefiboshethi

9, 10. (a) Mefiboshethi alipataje kuwa na mwiba katika mwili wake? (b) Mfalme Daudi alimwonyeshaje fadhili Mefiboshethi, nasi tunawezaje kumwiga Daudi?

9 Mfikirie Mefiboshethi, mwana wa Yonathani aliyekuwa rafiki ya Daudi. Mefiboshethi alipokuwa na umri wa miaka mitano, habari zilifika kwamba babake, Yonathani, na babu yake Mfalme Sauli, walikuwa wameuawa. Kwa kushtuka, yaya wa Mefiboshethi ‘alimchukua na ikawa, alipokimbia kwa haraka, huyo mtoto alianguka, akawa kilema.’ (2 Samweli 4:4) Ni lazima ulemavu huo ulikuwa mwiba kwelikweli ambao Mefiboshethi alivumilia alipokuwa akikua.

10 Miaka kadhaa baadaye, Mfalme Daudi alimwonyesha Mefiboshethi fadhili-upendo. Alifanya hivyo kwa sababu alimpenda sana Yonathani baba ya Mefiboshethi. Daudi alimpa Mefiboshethi shamba lote la Sauli na kumweka Siba mtumishi wa Sauli alitunze. Daudi pia alimwambia Mefiboshethi hivi: ‘Utakula chakula mezani pangu daima.’ (2 Samweli 9:6-10) Yaelekea fadhili-upendo za Daudi zilimfariji Mefiboshethi na zilimpunguzia mateso yaliyotokana na ulemavu wake. Ni somo zuri kama nini! Sisi pia tunapaswa kuwaonyesha fadhili wale wanaopambana na mwiba katika mwili.

11. Siba alidai nini kuhusu Mefiboshethi, na tunajuaje kwamba dai lake lilikuwa la uwongo? (Ona kielezi-chini.)

11 Baadaye Mefiboshethi alilazimika kupambana na mwiba mwingine katika mwili wake. Mtumishi wake Siba alimchongea mbele ya Mfalme Daudi, ambaye alikuwa akikimbia Yerusalemu kwa sababu ya uasi wa Absalomu, mwana wa Daudi. Siba alisema kwamba Mefiboshethi si mwaminifu na alikuwa amebaki Yerusalemu akitumaini kujitwalia utawala. * Daudi aliamini uchongezi wa Siba na kumpa mwongo huyo shamba lote la Mefiboshethi!—2 Samweli 16:1-4.

12. Mefiboshethi alitendaje kuhusu mambo yaliyompata, naye anatuwekea mfano gani mzuri?

12 Hata hivyo, Mefiboshethi alipokutana na Daudi hatimaye, alimweleza mfalme huyo yale yaliyotokea. Mefiboshethi alikuwa akijitayarisha kujiunga na Daudi wakati Siba alipojitolea kwenda kwa niaba yake. Je, Daudi alirekebisha mambo? Si kabisa. Aligawanya lile shamba kati ya wanaume hao wawili. Jambo hilo lingeweza kuwa mwiba mwingine katika mwili wa Mefiboshethi. Je, alivunjika moyo sana? Je, alipinga uamuzi wa Daudi akilalamika kwamba haukuwa wa haki? La, alikubali kwa unyenyekevu uamuzi wa mfalme. Alizingatia mambo yafaayo, akifurahi kwamba mfalme aliyestahili kutawala Israeli alikuwa amerudi salama. Bila shaka, Mefiboshethi aliweka mfano bora sana kwa kuvumilia ulemavu, uchongezi, na kivunja-moyo.—2 Samweli 19:24-30.

Nehemia Alikabiliana na Majaribu Yake

13, 14. Nehemia alilazimika kuvumilia miiba gani aliporudi kujenga upya kuta za Yerusalemu?

13 Fikiria miiba ya mfano ambayo Nehemia alivumilia aliporudi katika jiji la Yerusalemu lisilokuwa na kuta mnamo karne ya tano K.W.K. Alikuta jiji hilo likiwa bila ulinzi wowote, nao Wayahudi waliorudishwa walikuwa hawana utaratibu, wamevunjika moyo, na wasio safi mbele za Yehova. Baada ya muda mfupi, Nehemia alitambua kwamba hata ingawa Mfalme Artashasta alimruhusu kujenga upya kuta za Yerusalemu, ujenzi huo uliwachukiza magavana wa nchi jirani. Magavana hao ‘walihuzunika sana, kwa kuwa amekuja mtu kuwatakia heri wana wa Israeli.’—Nehemia 2:10.

14 Wapinzani hao wa kigeni walifanya yote wawezayo kusimamisha kazi ya Nehemia. Lazima vitisho, uwongo, na uchongezi wao—kutia ndani wapelelezi waliotumwa kumvunja moyo—ulikuwa kama miiba yenye kudumu katika mwili wake. Je, mbinu za adui hao zilimshinda? La! Alimtumaini Mungu kabisa na kusimama imara. Hivyo, Nehemia alipomaliza kujenga upya kuta za Yerusalemu, kuta hizo zilitoa ushuhuda wenye kudumu kwamba Yehova alimwunga mkono kwa upendo.—Nehemia 4:1-12; 6:1-19.

15. Ni matatizo gani ya Wayahudi yaliyomsumbua sana Nehemia?

15 Akiwa gavana, Nehemia alilazimika kupambana na matatizo mengi miongoni mwa watu wa Mungu. Matatizo hayo yalikuwa kama miiba iliyomsumbua sana kwa sababu yaliathiri uhusiano wao na Yehova. Matajiri walikuwa wanatoza riba ya juu sana, nao ndugu zao maskini walilazimika kuacha mashamba yao yachukuliwe na wengine na hata kuwauza watoto wao kuwa watumwa ili kulipa madeni na pia kulipa kodi kwa Waajemi. (Nehemia 5:1-10) Wayahudi wengi walivunja Sabato na hawakuwategemeza Walawi wala hekalu. Pia, wengine walioa wake “wa Ashdodi, na Amoni, na Moabu.” Jambo hilo lilimwumiza Nehemia kama nini! Lakini miiba hiyo haikumfanya aache kazi yake. Akiwa mtetezi mwenye bidii wa sheria za uadilifu za Mungu, Nehemia alikabiliana na hali hiyo kikamilifu. Kama Nehemia, na tusiruhusu mwenendo mbaya wa wengine utuzuie kumtumikia Yehova kwa uaminifu-mshikamanifu.—Nehemia 13:10-13, 23-27.

Waaminifu Wengine Wengi Walikabiliana na Miiba Katika Mwili

16-18. Isaka na Rebeka, Hana, Daudi, na Hosea walipatwa na matatizo gani ya kifamilia?

16 Biblia ina mifano mingine mingi ya watu waliokabiliana na hali zenye kutaabisha zilizokuwa kama miiba. Matatizo ya kifamilia ndiyo sanasana yaliyosababisha miiba hiyo. Wake wawili wa Esau “waliyafanya maisha ya Isaka na Rebeka [wazazi wa Esau] kuwa machungu.” Rebeka hata alisema kwamba alichukia maisha yake kwa sababu ya wake hao. (Mwanzo 26:34, 35; 27:46, Biblia Habari Njema) Fikiria pia Hana na jinsi mke mwenza Penina ‘alivyomchokoza sana’ kwa sababu Hana alikuwa tasa. Labda hata alimchokoza mara nyingi wakiwa nyumbani. Penina pia alimchokoza hadharani—yaelekea mbele ya watu wa ukoo na marafiki—wakati familia hiyo ilipohudhuria msherehekeo huko Shilo. Uchokozi huo ulikuwa kama kushindilia mwiba katika mwili wa Hana.—1 Samweli 1:4-7.

17 Hebu fikiria yale ambayo Daudi alivumilia kwa sababu ya wivu wa kipumbavu wa Mfalme Sauli, baba mkwe wake. Ili kuokoa uhai wake, ilimbidi Daudi aishi mapangoni katika nyika ya En-gedi, ambako alilazimika kupanda miamba hatari yenye miinuko mikali. Lazima ukosefu huo wa haki uwe ulimtia uchungu mwingi kwa kuwa hakuwa amemkosea Sauli. Hata hivyo, ilimbidi Daudi aishi maisha ya utoro kwa sababu ya wivu wa Sauli.—1 Samweli 24:14, 15; Mithali 27:4.

18 Wazia matatizo ya kifamilia yaliyompata nabii Hosea. Mke wake alikuwa mzinzi. Ni lazima uzinzi huo ulikuwa kama miiba katika moyo wa Hosea. Na ni lazima awe aliumia kama nini mke wake alipozaa watoto wawili haramu kutokana na uasherati wake!—Hosea 1:2-9.

19. Ni mnyanyaso gani uliompata nabii Mikaya?

19 Mnyanyaso ni mwiba mwingine katika mwili. Fikiria yaliyompata nabii Mikaya. Ni lazima Mikaya mwadilifu awe aliumia sana kuona kwamba Mfalme Ahabu aliamini uwongo wa wazi wa manabii wasio wa kweli waliomzunguka. Naye kiongozi wa wadanganyifu hao alifanya nini wakati Mikaya alipomwambia Ahabu kwamba manabii hao wote walikuwa wakizungumza kwa “pepo wa uongo”? “Alimpiga Mikaya kofi la shavu”! Jambo baya hata zaidi ni jinsi Ahabu alivyotenda alipoonywa na Yehova kwamba vita vyake vya kutwaa tena Ramoth-Gileadi havingefanikiwa. Ahabu aliagiza Mikaya atiwe gerezani na apewe posho lililopunguzwa. (1 Wafalme 22:6, 9, 15-17, 23-28) Kumbuka pia Yeremia na jinsi alivyotendewa na wanyanyasi wake wakatili.—Yeremia 20:1-9.

20. Naomi alilazimika kuvumilia miiba gani, naye alithawabishwaje?

20 Kufiwa na wapendwa pia ni hali nyingine yenye kuumiza ambayo inaweza kuwa kama mwiba katika mwili. Naomi alilazimika kuvumilia kifo cha mumewe na cha wanawe wawili kilichomwumiza sana. Vifo hivyo vilikuwa vingali vinamwumiza aliporudi Bethlehemu. Aliwaambia marafiki wake wasimwite Naomi bali wamwite Mara, jina lililoonyesha uchungu aliokuwa nao kwa sababu ya mambo yaliyompata. Hata hivyo, kwa sababu ya uvumilivu wake, hatimaye Yehova alimthawabisha kwa kumpa mjukuu wa kiume ambaye alikuja kuwa mmoja wa mababu wa Mesiya.—Ruthu 1:3-5, 19-21; 4:13-17; Mathayo 1:1, 5.

21, 22. Yobu alipoteza nini, naye alitendaje?

21 Fikiria jinsi Yobu alivyoshtuka alipopata habari za vifo vya ghafula na vya ukatili vya watoto wake kumi wapendwa pamoja na kupoteza mifugo na watumishi wake wote. Ghafula, maisha yake yalionekana kana kwamba yamefikia mwisho! Kisha, hata kabla Yobu hajapata nguvu kutokana na mapigo hayo, Shetani akampiga kwa ugonjwa. Huenda Yobu alifikiria kwamba ugonjwa huo mbaya ungemwua. Maumivu yake yalikuwa makali sana hivi kwamba aliona kwamba kifo kingemletea kitulizo.—Ayubu 1:13-20; 2:7, 8.

22 Na kana kwamba Yobu hakuwa ameteseka vya kutosha, mke wake alimjia akiwa mwenye huzuni na uchungu na kumwambia: “Umkufuru Mungu, ukafe!” Huo ulikuwa mwiba ulioje katika mwili wake wenye maumivu! Kisha, marafiki watatu wa Yobu wakamshambulia kwa hoja zao za uwongo badala ya kumfariji, wakimshutumu kwamba amefanya dhambi kisiri na kusema kwamba dhambi hiyo ndiyo iliyofanya apatwe na magumu hayo. Ni kana kwamba hoja zao zenye makosa zilishindilia miiba katika mwili wake. Kumbuka pia kwamba Yobu hakujua ni kwa nini mambo hayo mabaya yalikuwa yakimpata; wala hakujua kama angenusurika. Lakini, “katika mambo hayo yote Ayubu [“Yobu,” NW] hakufanya dhambi, wala hakumwazia Mungu kwa upumbavu.” (Ayubu 1:22; 2:9, 10; 3:3; 14:13; 30:17) Ingawa alisumbuliwa na miiba mingi kwa wakati mmoja, aliendelea kuwa mwaminifu. Hicho ni kitia-moyo kilichoje!

23. Ni nini kilichowawezesha watu waaminifu ambao tumezungumzia, wavumilie miiba mbalimbali katika mwili?

23 Bila shaka, Biblia ina mifano mingine mingi kama hiyo ambayo imetajwa. Watumishi wote hao waaminifu walilazimika kupambana na miiba yao ya mfano. Nao walikuwa na matatizo ya aina nyingi. Hata hivyo, kuna jambo moja ambalo wote walizingatia. Wote waliendelea kumtumikia Yehova. Licha ya majaribu yao yenye kutaabisha, walimshinda Shetani kwa nguvu za Yehova. Jinsi gani? Makala ifuatayo itajibu swali hilo na kutuonyesha jinsi sisi pia tunavyoweza kukabiliana na jambo lolote lililo kama mwiba katika mwili wetu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Haielekei kwamba mtu aliyekuwa mwenye shukrani na mnyenyekevu kama Mefiboshethi angepanga njama kama hiyo kwa kujitakia makuu. Inaelekea alijua sifa ya uaminifu ya babake Yonathani. Ingawa alikuwa mtoto wa Mfalme Sauli, Yonathani alitambua kwa unyenyekevu kwamba Daudi alikuwa amechaguliwa na Yehova kuwa mfalme wa Israeli. (1 Samweli 20:12-17) Yonathani hangemfunza mwanawe mchanga kutamani mamlaka ya kifalme kwa kuwa alikuwa mzazi aliyemhofu Mungu na rafiki mwaminifu-mshikamanifu wa Daudi.

Ungejibuje?

• Kwa nini matatizo tunayokabili yanaweza kufananishwa na miiba katika mwili?

• Mefiboshethi na Nehemia walilazimika kuvumilia miiba gani?

• Kati ya mifano ya Kimaandiko ya wanaume na wanawake ambao walivumilia miiba mbalimbali katika mwili, ni mfano gani ulioona kuwa wenye kuchochea zaidi, na kwa nini?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 15]

Mefiboshethi alilazimika kukabiliana na ulemavu, uchongezi, na kivunja-moyo

[Picha katika ukurasa wa 16]

Nehemia alistahimili licha ya upinzani