Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Upendo Wetu Umeongezeka’

‘Upendo Wetu Umeongezeka’

‘Upendo Wetu Umeongezeka’

MNAMO Ijumaa, Machi 31, 2000, Mlima Usu huko Hokkaido, Japani, ulilipuka baada ya kukaa miaka 23 bila kulipuka. Watu wengi walilazimika kukimbia eneo hilo hatari. Wengi walipoteza makao na kazi zao, lakini hakuna mtu aliyekufa. Mashahidi wa Yehova 46 walikuwa miongoni mwa watu hao waliolazimika kukimbia lakini hawakuachwa bila msaada.

Siku ambayo mlima huo ulilipuka, mhudumu Mkristo asafiriye aliyetumikia katika eneo hilo alisaidia kuanzisha mpango wa kutoa misaada. Baada ya muda mfupi, makutaniko ya karibu yakaanza kuleta misaada. Chini ya usimamizi wa ofisi ya tawi ya Japani, halmashauri ya kutoa misaada ilianzishwa mara moja, na Mashahidi wa Yehova kutoka kote nchini Japani wakachanga kwa wingi. Ili kushughulikia utendaji wa kiroho, wahudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova walitumwa kwenye kutaniko lililoathiriwa sana, naye mwangalizi wa mzunguko akatembelea eneo hilo mara nyingi ili kutoa msaada wa kihisia-moyo na kiroho.

Katika kipindi hicho chenye magumu, Mashahidi kutoka maeneo yaliyoathirika waliendelea kufanya mikutano yao ya Kikristo katika nyumba za watu binafsi kwenye maeneo yaliyokuwa salama zaidi. Wakati watu waliporuhusiwa kurudi kwenye eneo ambapo Jumba la Ufalme lilikuwa, ndugu walipata Jumba hilo likiwa limeinama na kuta zake zilikuwa zimepasuka-pasuka. Karibu na Jumba la Ufalme, shimo lililotokezwa na mlipuko huo lilikuwa bado linatoa moshi mzito. Mashahidi waliwaza, ‘Je, ni jambo la hekima kuendelea kufanya mikutano katika eneo hili? Je, Jumba la Ufalme linaweza kurekebishwa?’

Uamuzi ulifikiwa wa kujenga Jumba jipya la Ufalme katika eneo la karibu lililokuwa salama zaidi. Halmashauri ya Ujenzi ya Mkoa iliwapa msaada waliohitaji. Pesa zilizochangwa na Mashahidi kote nchini zilitumiwa katika ujenzi huo. Muda si muda walipata mahali pa kujenga na kwa msaada wa maelfu ya wajitoleaji, Jumba hilo jipya la Ufalme likamalizwa upesi sana. Siku ya Jumapili, Julai 23, 2000 watu 75 walihudhuria mkutano wa kwanza uliofanywa katika hilo Jumba la Ufalme jipya. Wengi waliohudhuria walitokwa na machozi ya furaha. Wakati Jumba hilo la Ufalme lilipowekwa wakfu mnamo Oktoba mwaka huohuo, mzee mmoja wa kutaniko hilo alichochewa kusema: “Mlipuko huo ulisababisha magumu na mateso. Hata hivyo, ujenzi huu umebadili hofu yetu ikawa furaha. Upendo wetu kwa Yehova na kwa ndugu zetu Wakristo umeongezeka sana.”

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 19]

Kulipuka kwa Mlima Usu: AP Photo/Koji Sasahara