Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Uongozi wa Kristo Ni Halisi Kwako?

Je, Uongozi wa Kristo Ni Halisi Kwako?

Je, Uongozi wa Kristo Ni Halisi Kwako?

“Wala msiitwe ‘viongozi,’ kwa maana Kiongozi wenu ni mmoja, Kristo.”—MATHAYO 23:10.

1. Ni nani pekee aliye Kiongozi wa Wakristo wa kweli?

ILIKUWA Jumanne, Nisani 11. Siku tatu baadaye, Yesu Kristo angeuawa. Hii ilikuwa ziara yake ya mwisho hekaluni. Siku hii, Yesu aliwafundisha wanafunzi wake na umati mkubwa uliokuwa umekusanyika hapo jambo fulani muhimu. Alisema: “Msiitwe Rabi, kwa maana mmoja ni mwalimu wenu, lakini nyinyi nyote ni akina ndugu. Zaidi ya hayo, msiite yeyote baba yenu duniani, kwa maana mmoja ni Baba yenu, Aliye wa kimbingu. Wala msiitwe ‘viongozi,’ kwa maana Kiongozi wenu ni mmoja, Kristo.” (Mathayo 23:8-10) Ni wazi kwamba Yesu Kristo ndiye Kiongozi wa Wakristo wa kweli.

2, 3. Kumsikiliza Yehova na kukubali Kiongozi aliyemweka rasmi kuna matokeo gani maishani mwetu?

2 Tunapata manufaa yaliyoje maishani tunapokubali kuongozwa na Yesu! Yehova Mungu alitangaza hivi alipotabiri kuja kwa Kiongozi huyo kupitia nabii Isaya: “Haya, kila aonaye kiu, njoni majini, naye asiye na fedha; njoni, nunueni mle; naam, njoni, nunueni divai na maziwa, bila fedha na bila thamani. . . . Nisikilizeni kwa bidii, mle kilicho chema, na kujifurahisha nafsi zenu kwa unono. . . . Angalieni, nimemweka kuwa shahidi kwa kabila za watu; kuwa kiongozi na jemadari kwa kabila za watu.”—Isaya 55:1-4.

3 Isaya alitumia vitu vya kawaida kama vile maji, maziwa, na divai kama mifano ya jinsi maisha yetu yanavyokuwa tunapomsikiliza Yehova na kufuata Kiongozi na Jemadari aliyetupatia. Matokeo yanakuwa yenye kuburudisha. Ni kama vile kunywa glasi ya maji baridi katika siku yenye joto. Tunakata kiu yetu ya ile kweli na uadilifu. Kama vile maziwa huwatia nguvu watoto wachanga na kuwasaidia wakue, ‘maziwa ya lile neno’ hututia nguvu na kutusaidia tukue kiroho katika uhusiano wetu na Mungu. (1 Petro 2:1-3) Hapana shaka kwamba divai huleta furaha wakati wa sherehe. Vivyo hivyo, kumwabudu Mungu wa kweli na kufuata hatua za Kiongozi aliyemweka rasmi hufanya ‘tufurahie maisha kabisa.’ (Kumbukumbu la Torati 16:15) Hivyo basi, ni muhimu kwamba sote—vijana kwa wazee, wanaume kwa wanawake—tuonyeshe kwamba uongozi wa Kristo ni halisi kwetu. Hata hivyo, tunawezaje kuonyesha katika maisha yetu kwamba Mesiya ndiye Kiongozi wetu?

Vijana—Fulizeni “Kufanya Maendeleo Katika Hekima”

4. (a) Ni nini kilichotukia wakati Yesu mwenye umri wa miaka 12 alipozuru Yerusalemu wakati wa Sikukuu ya Kupitwa? (b) Yesu alikuwa na ufahamu kadiri gani alipokuwa na umri wa miaka 12 tu?

4 Fikiria mfano ambao Kiongozi wetu aliwawekea vijana. Japo si mambo mengi yanayojulikana kuhusu maisha ya utotoni ya Yesu, kuna tukio moja linalotufahamisha mengi. Yesu alipokuwa na umri wa miaka 12, wazazi wake waliandamana naye katika ziara yao ya kila mwaka kwenda Yerusalemu kwa ajili ya Sikukuu ya Kupitwa. Pindi hiyo Yesu alizama katika mazungumzo ya Kimaandiko, na watu wa familia yake wakamwacha bila kujua. Siku tatu baadaye, wazazi wake wenye wasiwasi, Yosefu na Maria, walimpata hekaluni, “ameketi katikati ya walimu na akiwasikiliza na kuwauliza maswali.” Isitoshe, “wote wale waliokuwa wakimsikiliza walikuwa katika mshangao wa daima juu ya uelewevu wake na majibu yake.” Hebu wazia, Yesu alikuwa na umri wa miaka 12 tu na angeweza kuuliza maswali yenye kuamsha fikira kuhusu mambo ya kiroho na pia kutoa majibu ya kiakili! Bila shaka mafundisho aliyopata kutoka kwa wazazi wake yalimsaidia.—Luka 2:41-50.

5. Vijana wanawezaje kuchanganua maoni yao kuelekea funzo la Biblia la familia?

5 Huenda wewe ni kijana. Ikiwa wazazi wako ni watumishi wa Mungu waliojitoa, yaelekea nyumbani mna ratiba ya kujifunza Biblia kwa ukawaida mkiwa familia. Unalionaje funzo hilo la familia? Kwa nini usitafakari maswali yafuatayo: ‘Je, mimi ninaunga mkono kwa moyo wote ratiba ya funzo la Biblia la familia? Je, ninajaribu kuifuata bila kufanya chochote kinachoweza kuivuruga?’ (Wafilipi 3:16) ‘Je, mimi hushiriki kwa uchangamfu katika funzo hilo? Inapofaa, je, mimi huuliza maswali kuhusu habari inayozungumziwa na kutoa maelezo kuhusu vile habari hiyo inavyoweza kutumiwa? Ninapofanya maendeleo ya kiroho, je, ninasitawisha hamu ya “chakula kigumu cha watu wakomavu”?’—Waebrania 5:13, 14.

6, 7. Usomaji wa Biblia kila siku ni muhimu kadiri gani kwa vijana?

6 Ratiba ya usomaji wa Biblia kila siku pia ni muhimu. Mtunga-zaburi aliimba: “Heri mtu yule asiyekwenda katika shauri la wasio haki; . . . bali sheria ya BWANA ndiyo impendezayo, na sheria yake huitafakari mchana na usiku.” (Zaburi 1:1, 2) Yoshua, aliyechukua uongozi baada ya Musa, ‘aliyatafakari maneno ya kitabu cha torati mchana na usiku.’ Jambo hilo lilimwezesha kutenda kwa hekima na kufanikiwa kutimiza mgawo aliopewa na Mungu. (Yoshua 1:8) Kiongozi wetu Yesu Kristo alisema: “Imeandikwa, ‘Binadamu lazima aishi, si kwa mkate pekee, bali kwa kila tamko linalokuja kupitia kinywa cha Yehova.’” (Mathayo 4:4) Ikiwa tunahitaji chakula cha kimwili kila siku, bila shaka tunahitaji hata zaidi chakula cha kiroho kwa ukawaida!

7 Alipotambua uhitaji wake wa kiroho, Nicole mwenye umri wa miaka 13 alianza kusoma Biblia kila siku. * Sasa Nicole ana umri wa miaka 16 na amemaliza kusoma Biblia nzima. Sasa anaisoma kwa mara ya pili na amefika katikati. Ratiba yake ni sahili. Yeye anasema, “Ninahakikisha kwamba nimesoma angalau sura moja kila siku.” Usomaji wake wa Biblia wa kila siku umemsaidiaje? Anajibu: “Leo kuna uvutano mwingi mbaya. Kila siku mimi hukabili mikazo shuleni na kwingineko ambayo hujaribu imani yangu. Kusoma Biblia kila siku hunisaidia kukumbuka haraka amri na kanuni za Biblia ambazo hunitia moyo nisimame imara dhidi ya mikazo hiyo. Kwa sababu hiyo, ninahisi nikiwa karibu zaidi na Yehova na Yesu.”

8. Yesu alikuwa na desturi gani alipoenda kwenye sinagogi, na vijana wanaweza kumwigaje?

8 Yesu alikuwa na desturi ya kusikiliza na kushiriki usomaji wa Maandiko katika sinagogi. (Luka 4:16; Matendo 15:21) Ni jambo lenye manufaa kama nini kwa vijana kufuata kielelezo hicho kwa kuhudhuria kwa ukawaida mikutano ya Kikristo, ambapo wahudhuriaji husoma na kujifunza Biblia! Akionyesha shukrani kwa mikutano hiyo, Richard mwenye umri wa miaka 14 anasema: “Mikutano ni muhimu sana kwangu. Kwenye mikutano ninakumbushwa daima mambo yaliyo mema na mabaya, mambo yaliyo ya adili na yasiyo ya adili, mwenendo ulio kama wa Kristo na usio kama wa Kristo. Si lazima nipate magumu ili nijifunze mambo hayo.” Naam, “Ushuhuda [“kumbusho,” NW] wa BWANA ni amini, humtia mjinga hekima.” (Zaburi 19:7) Nicole pia huhakikisha kwamba anahudhuria mikutano yote mitano ya kutaniko kila juma. Pia yeye hutumia muda wa saa mbili au tatu akitayarisha mikutano hiyo.—Waefeso 5:15, 16.

9. Vijana wanawezaje kufuliza “kufanya maendeleo katika hekima”?

9 Ujana ni wakati mzuri wa kupata ‘ujuzi juu ya Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule aliyemtuma, Yesu Kristo.’ (Yohana 17:3) Huenda unajua vijana fulani ambao hutumia wakati mwingi wakisoma vitabu vya katuni, wakitazama televisheni, wakicheza michezo ya video, au kutazama Internet. Usifuate mfano wa vijana hao bali fuata mfano wa Kiongozi wetu. Akiwa kijana mdogo, alifurahia kujifunza juu ya Yehova. Na matokeo yalikuwa nini? Kwa kuwa alipenda mambo ya kiroho, ‘Yesu alifuliza kufanya maendeleo katika hekima.’ (Luka 2:52) Wewe pia unaweza kufanya hivyo.

“Iweni Katika Ujitiisho Kuelekea Mmoja na Mwenzake”

10. Ni nini kitakachochangia amani na furaha katika maisha ya familia?

10 Nyumbani panaweza kuwa mahali salama penye amani na uradhi au mahali pa mabishano na ugomvi. (Mithali 21:19; 26:21) Kukubali kuongozwa na Kristo huchangia amani na furaha katika familia. Kwa kweli, mfano wa Yesu unastahili kuigwa katika mahusiano ya familia. Maandiko yanasema: “Iweni katika ujitiisho kuelekea mmoja na mwenzake katika hofu ya Kristo. Acheni wake wawe katika ujitiisho kwa waume zao kama kwa Bwana, kwa sababu mume ni kichwa cha mke wake kama vile Kristo pia alivyo kichwa cha kutaniko, yeye akiwa mwokozi wa mwili huu. . . . Waume, endeleeni kuwapenda wake zenu, kama vile Kristo pia alivyolipenda kutaniko na kujikabidhi mwenyewe kwa ajili yalo.” (Waefeso 5:21-25) Mtume Paulo aliliandikia hivi kutaniko la Kolosai: “Nyinyi watoto, iweni watiifu kwa wazazi wenu katika kila jambo, kwa maana hilo ni lenye kupendeza vema katika Bwana.”—Wakolosai 3:18-20.

11. Mume anaweza kuonyeshaje kwamba uongozi wa Kristo ni halisi kwake?

11 Kufuata ushauri huo kunamaanisha kwamba mume atachukua uongozi katika familia, mke atamwunga mkono kwa uaminifu-mshikamanifu, nao watoto watatii wazazi wao. Hata hivyo, ukichwa wa mwanamume huleta furaha tu unapotumiwa ifaavyo. Mume mwenye hekima anapaswa kujifunza jinsi ya kutumia ukichwa kwa kumwiga Kichwa na Kiongozi wake, Kristo Yesu. (1 Wakorintho 11:3) Ingawa baadaye Yesu alikuwa “kichwa juu ya vitu vyote kwa kutaniko,” alikuja duniani, “si kuhudumiwa, bali kuhudumu.” (Waefeso 1:22; Mathayo 20:28) Kwa njia hiyohiyo, mume Mkristo hatumii ukichwa wake kujinufaisha mwenyewe, bali kwa manufaa ya mke na watoto—naam, familia nzima. (1 Wakorintho 13:4, 5) Yeye hujitahidi kuiga sifa za kimungu za Yesu Kristo, aliye kichwa chake. Kama Yesu, yeye ni mwenye tabia-pole na wa hali ya chini moyoni. (Mathayo 11:28-30) Anapokosea hataona ugumu wa kusema, “Ninaomba msamaha” au “ulisema kweli.” Mfano wake mzuri hufanya iwe rahisi zaidi kwa mke wake kuwa “msaidizi,” “kikamilisho,” na ‘mwenzi,’ akijifunza kutoka kwake na kufanya kazi naye bega kwa bega.—Mwanzo 2:20, NW; Malaki 2:14.

12. Ni nini kitakachomsaidia mke afuate kanuni ya ukichwa?

12 Mke naye anapaswa kujitiisha kwa mume wake. Hata hivyo, huenda mke asipendezwe na wazo la kujitiisha kwa mwanamume ikiwa ameathiriwa na roho ya ulimwengu na huenda akaanza kudharau kanuni ya ukichwa. Maandiko hayasemi kwamba mwanamume anapaswa kuwa mwenye kukandamiza, lakini huwataka wake wajitiishe kwa waume zao. (Waefeso 5:24) Biblia pia humtaka mume au baba azingatie daraka lake katika familia, na ushauri wa Biblia unapofuatwa, kunakuwa na amani na utaratibu katika familia.—Wafilipi 2:5.

13. Yesu amewawekea watoto kielelezo gani cha ujitiisho?

13 Watoto wanapaswa kuwatii wazazi wao. Kwa habari hiyo, Yesu aliweka kielelezo bora. Baada ya tukio ambapo Yesu mwenye umri wa miaka 12 aliachwa hekaluni kwa siku tatu, yeye ‘aliteremka kwenda pamoja na wazazi wake akaja hadi Nazareti, naye akaendelea kuwa mwenye kujitiisha kwao.’ (Luka 2:51) Ujitiisho wa watoto kwa wazazi wao huchangia amani na upatano katika familia. Familia inakuwa yenye furaha ikiwa kila mmoja anajitiisha kwa uongozi wa Kristo.

14, 15. Ni nini kitakachotusaidia tufanikiwe tunapokabili hali ngumu nyumbani? Toa mfano.

14 Hata matatizo yanapotokea nyumbani, yanaweza kutatuliwa kwa mafanikio kwa kumwiga Yesu na kukubali mwongozo wake. Kwa mfano, Jerry mwenye umri wa miaka 35 alipomwoa Lana, ambaye alikuwa na binti tineja, walipata matatizo ambayo wote wawili hawakutazamia. Jerry anaeleza: “Nilijua kwamba ili nifanikiwe nikiwa kichwa cha familia, nilihitaji kutumia kanuni za Biblia ambazo familia nyingine zimetumia na kufanikiwa. Lakini muda si muda, nikatambua kwamba nilihitaji kuzitumia kwa hekima na kwa utambuzi zaidi.” Binti yake wa kambo alimwona kama mtu aliyemtenganisha na mamake na kumchukia sana. Jerry alihitaji utambuzi ili kuona kwamba maoni hayo yaliathiri yale msichana huyo aliyosema na kutenda. Alishughulikaje na hali hiyo? Jerry anajibu: “Mimi na Lana tulikubaliana kwamba angalau kwa wakati huo, yeye angechukua daraka la kumtia nidhamu huku mimi nikizingatia kusitawisha uhusiano mzuri na binti yangu wa kambo. Baada ya muda tulifanikiwa.”

15 Tunapokabili hali ngumu nyumbani, tunahitaji utambuzi ili kujua ni kwa nini watu wa familia wanazungumza na kutenda kwa njia fulani. Tunahitaji pia hekima ili kutumia kanuni za Mungu ifaavyo. Kwa mfano, Yesu alitambua sababu iliyomfanya mwanamke aliyekuwa akitokwa na damu amguse, na akamtendea kwa hekima na huruma. (Mambo ya Walawi 15:25-27; Marko 5:30-34) Kiongozi wetu ana sifa za hekima na utambuzi. (Mithali 8:12) Tunapata furaha tukitenda jinsi ambavyo angetenda.

‘Fuliza Kutafuta Kwanza Ufalme’

16. Ni nini tunachopaswa kutanguliza maishani mwetu, naye Yesu alituwekea mfano gani kuhusiana na jambo hilo?

16 Yesu alionyesha wazi kile ambacho wale wanaokubali uongozi wake wangepaswa kutanguliza. Alisema: “Fulizeni kutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake [wa Mungu].” (Mathayo 6:33) Naye mwenyewe alituonyesha jinsi ya kufanya hivyo. Baada ya kipindi cha siku 40 cha kufunga, kutafakari, na kusali kufuatia ubatizo wake, Yesu alijaribiwa. Shetani Ibilisi alimtolea “falme zote za ulimwengu.” Hebu wazia Yesu angaliishi maisha ya aina gani kama angalikubali toleo hilo la Ibilisi! Lakini Kristo alikazia fikira kufanya mapenzi ya Babake. Pia alitambua kwamba maisha kama hayo katika ulimwengu wa Shetani yangekuwa mafupi. Hivyo, akakataa toleo la Shetani mara moja na kusema: “Imeandikwa, ‘Ni Yehova Mungu wako ambaye lazima uabudu, na ni kwake peke yake lazima utoe utumishi mtakatifu.’” Muda mfupi baadaye, Yesu “alianza kuhubiri na kusema: ‘Tubuni, nyinyi watu, kwa maana ufalme wa mbingu umekaribia.’” (Mathayo 4:2, 8-10, 17) Muda wote uliosalia wa maisha yake duniani, Kristo alikuwa mhubiri wa wakati wote wa Ufalme wa Mungu.

17. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunatanguliza masilahi ya Ufalme maishani mwetu?

17 Tunapaswa kumwiga Kiongozi wetu na kutoruhusu ulimwengu wa Shetani utushawishi kuifanya kazi yenye mshahara mnono, au kazi-maisha iwe mradi wetu mkuu maishani. (Marko 1:17-21) Lingekuwa jambo la kipumbavu kama nini kujishughulisha sana na mambo ya ulimwengu hivi kwamba masilahi ya ufalme yanachukua nafasi ya pili! Yesu ametupatia kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Ndiyo, huenda tukawa na familia au madaraka mengine ya kushughulikia, lakini tutafurahi kutumia jioni na miisho-juma kutimiza daraka letu la Kikristo la kuhubiri na kufundisha. Inatia moyo kama nini kwamba katika mwaka wa utumishi wa 2001, watu wapatao 780,000 walitumikia wakiwa mapainia au wahudumu wa wakati wote!

18. Ni nini ambacho hutusaidia tupate furaha katika huduma?

18 Masimulizi ya vitabu vya Injili yanamwonyesha Yesu kuwa mtu wa vitendo na pia mtu mwenye hisia nyororo. Alipoona mahitaji ya kiroho ya watu waliokuwa karibu naye, aliwahurumia na akajitolea kwa hamu kuwasaidia. (Marko 6:31-34) Tunafurahia huduma yetu tunapoifanya kwa sababu tunawapenda wengine na tunatamani sana kuwasaidia. Lakini tunawezaje kusitawisha tamaa hiyo? “Nilipokuwa tineja, sikufurahia sana huduma,” anasema mwanamume kijana aitwaye Jayson. Ni nini kilichomsaidia asitawishe upendo kwa kazi hiyo? Jayson anajibu: “Familia yetu ilishiriki utumishi wa shambani kila Jumamosi asubuhi. Jambo hilo lilinisaidia kwa kuwa kadiri nilivyoshiriki katika huduma, ndivyo nilivyozidi kuona manufaa yake na kuifurahia zaidi.” Sisi pia tunapaswa kushiriki katika huduma kwa ukawaida na kwa bidii.

19. Tunapaswa kuazimia kufanya nini kuhusiana na uongozi wa Kristo?

19 Kwa kweli inaburudisha na kuthawabisha kukubali uongozi wa Kristo. Tunapofanya hivyo, ujana unakuwa wakati wa kujipatia ujuzi na hekima zaidi. Maisha ya familia yanakuwa yenye amani na furaha, nayo huduma inaleta shangwe na uradhi. Hivyo basi, na tujitahidi kabisa kuonyesha katika maisha yetu ya kila siku na katika maamuzi tunayofanya kwamba uongozi wa Kristo ni halisi kwetu. (Wakolosai 3:23, 24) Hata hivyo, Yesu Kristo ametuongoza kupitia njia nyingine—kutaniko la Kikristo. Makala ifuatayo itazungumzia jinsi tunavyoweza kunufaika na mpango huo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

Je, Unakumbuka?

• Kufuata Kiongozi aliyewekwa rasmi na Mungu kunatunufaishaje?

• Vijana wanaweza kuonyeshaje kwamba wanataka kufuata uongozi wa Yesu?

• Uongozi wa Kristo una matokeo gani kwa maisha ya familia ya wale wanaojitiisha kwake?

• Huduma yetu inaweza kuonyeshaje kwamba uongozi wa Kristo ni halisi kwetu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 9]

Ujana ni wakati mzuri wa kujipatia ujuzi juu ya Mungu na Kiongozi wetu aliyewekwa rasmi

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kujitiisha kwa uongozi wa Kristo huchangia furaha katika familia

[Picha katika ukurasa wa 12]

Yesu alitafuta kwanza Ufalme. Unafanya hivyo?