Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kristo Analiongoza Kutaniko Lake

Kristo Analiongoza Kutaniko Lake

Kristo Analiongoza Kutaniko Lake

“Tazameni! mimi nipo pamoja nanyi siku zote hadi umalizio wa mfumo wa mambo.”—MATHAYO 28:20.

1, 2. (a) Yesu aliyefufuliwa aliwaahidi wafuasi wake nini alipotoa amri ya kufanya wanafunzi? (b) Yesu aliliongozaje kutaniko la Kikristo la mapema?

KABLA ya kupaa mbinguni, Yesu Kristo, Kiongozi wetu aliyefufuliwa aliwatokea wanafunzi wake na kusema: “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na juu ya dunia. Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo mimi nimewaamuru nyinyi. Na, tazameni! mimi nipo pamoja nanyi siku zote hadi umalizio wa mfumo wa mambo.”—Mathayo 23:10; 28:18-20.

2 Yesu aliwapa mitume wake kazi yenye kuokoa uhai ya kufanya wanafunzi na pia akawaahidi kwamba angekuwa pamoja nao. Historia ya Ukristo wa mapema kama ilivyoandikwa katika kitabu cha Biblia cha Matendo, yaonyesha pasipo shaka kwamba Kristo alitumia mamlaka aliyopewa kuliongoza kutaniko lililokuwa limeanzishwa karibuni. Alituma “msaidiaji” aliyeahidi—roho takatifu—ili kuwatia nguvu wafuasi wake na kuongoza jitihada zao. (Yohana 16:7; Matendo 2:4, 33; 13:2-4; 16:6-10) Yesu alitumia pia malaika walio chini ya amri yake kuwategemeza wanafunzi wake. (Matendo 5:19; 8:26; 10:3-8, 22; 12:7-11; 27:23, 24; 1 Petro 3:22) Isitoshe, Kiongozi wetu alitoa mwongozo katika kutaniko kwa kupanga kuwe na wanaume wanaostahili ili watumikie wakiwa baraza linaloongoza.—Matendo 1:20, 24-26; 6:1-6; 8:5, 14-17.

3. Ni maswali gani yatakayozungumziwa katika makala hii?

3 Hata hivyo, namna gani kuhusu wakati wetu ambao ni “umalizio wa mfumo wa mambo”? Yesu Kristo analiongozaje kutaniko la Kikristo leo? Na tunaweza kuonyeshaje kwamba tunakubali uongozi huo?

Bwana-Mkubwa Ana Mtumwa Mwaminifu

4. (a) Ni nani wanaofanyiza “mtumwa mwaminifu na mwenye busara”? (b) Bwana-mkubwa amemweka mtumwa huyo ashughulikie nini?

4 Alipotoa unabii kuhusu ishara ya kuwapo kwake, Yesu alisema: “Ni nani kwa kweli aliye mtumwa mwaminifu na mwenye busara ambaye bwana-mkubwa wake alimweka rasmi juu ya watumishi wake wa nyumbani, kuwapa chakula chao kwa wakati ufaao? Mwenye furaha ni mtumwa huyo ikiwa bwana-mkubwa wake anapowasili amkuta akifanya hivyo! Kwa kweli nawaambia nyinyi, Atamweka yeye rasmi juu ya mali zake zote.” (Mathayo 24:45-47) “Bwana-mkubwa,” Yesu Kristo, ndiye Kiongozi wetu naye amemweka rasmi “mtumwa mwaminifu na mwenye busara”—jamii ya Wakristo watiwa-mafuta duniani—kushughulikia masilahi yake yote duniani.

5, 6. (a) Katika maono ambayo mtume Yohana aliona, “vinara saba vya taa vya dhahabu” na “zile nyota saba” zinafananisha nini? (b) Ni nini kinachoonyeshwa na kuwepo kwa “zile nyota saba” katika mkono wa kuume wa Yesu?

5 Kitabu cha Biblia cha Ufunuo chaonyesha kwamba mtumwa mwaminifu na mwenye busara anaongozwa moja kwa moja na Yesu Kristo. Katika maono juu ya “siku ya Bwana,” mtume Yohana aliona “vinara saba vya taa vya dhahabu, na katikati ya vinara vya taa mtu fulani kama mwana wa binadamu” ambaye “katika mkono wake wa kuume alikuwa na nyota saba.” Yesu alisema hivi alipomweleza Yohana maono hayo: “Kwa habari ya siri takatifu ya zile nyota saba ulizoona juu ya mkono wangu wa kuume, na ya vile vinara saba vya taa vya dhahabu: Zile nyota saba zamaanisha wale malaika wa makutaniko saba, na vile vinara saba vya taa vyamaanisha makutaniko saba.”—Ufunuo 1:1, 10-20.

6 Vile “vinara saba vya taa vya dhahabu” vinafananisha makutaniko yote ya Wakristo wa kweli yaliyopo katika “siku ya Bwana,” iliyoanza mwaka wa 1914. Namna gani “zile nyota saba?” Mwanzoni, zilifananisha waangalizi wote watiwa-mafuta, waliozaliwa kwa roho, ambao walisimamia makutaniko ya karne ya kwanza. * Waangalizi hao walikuwa katika mkono wa kuume wa Yesu—chini ya uthibiti na mwongozo wake. Naam, Kristo Yesu aliongoza jamii ya mtumwa. Hata hivyo, leo waangalizi watiwa-mafuta ni wachache. Kristo anayaongozaje makutaniko zaidi ya 93,000 ya Mashahidi wa Yehova ulimwenguni?

7. (a) Yesu hulitumiaje Baraza Linaloongoza kutoa uongozi katika makutaniko duniani pote? (b) Kwa nini inaweza kusemwa kwamba waangalizi Wakristo wanawekwa rasmi na roho takatifu?

7 Kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, sasa kikundi kidogo cha wanaume wanaostahili ambao wanateuliwa kutoka miongoni mwa waangalizi waliotiwa mafuta wanatumikia wakiwa Baraza Linaloongoza. Baraza hilo linawakilisha jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara. Kiongozi wetu hutumia Baraza hilo Linaloongoza kuweka rasmi wanaume wanaostahili—wawe watiwa-mafuta kwa roho au la—kuwa wazee katika makutaniko ya kwao. Kuhusiana na hilo, roho takatifu, ambayo Yehova amempa Yesu mamlaka ya kuitumia, inatimiza jukumu muhimu sana. (Matendo 2:32, 33) Kwanza kabisa, lazima waangalizi hao watimize matakwa yanayoonyeshwa katika Neno la Mungu lililopuliziwa kwa roho takatifu. (1 Timotheo 3:1-7; Tito 1:5-9; 2 Petro 1:20, 21) Kupendekezwa na kuwekwa rasmi hufanywa baada ya sala na chini ya uongozi wa roho takatifu. Isitoshe, watu waliowekwa rasmi wanadhihirisha matunda ya roho hiyo. (Wagalatia 5:22, 23) Hivyo, ushauri huu wa Paulo unawahusu wazee wote, wawe watiwa-mafuta au la: “Kazieni uangalifu kwa nyinyi wenyewe na kundi lote, ambalo miongoni mwalo roho takatifu imewaweka nyinyi rasmi kuwa waangalizi.” (Matendo 20:28) Wanaume hao waliowekwa rasmi hupokea mwongozo kutoka kwa Baraza Linaloongoza, nao hulichunga kutaniko kwa moyo wa kupenda. Kwa njia hiyo, Kristo yuko pamoja nasi sasa na analiongoza kutaniko.

8. Yesu hutumiaje malaika kuongoza wafuasi wake?

8 Yesu pia huwatumia malaika halisi kuongoza wafuasi wake leo. Kulingana na mfano wa ngano na magugu, wakati wa mavuno ungefika kwenye “umalizio wa mfumo wa mambo.” Bwana-mkubwa angetumia nani kuvuna? “Wavunaji ni malaika,” akasema Kristo. Aliongeza kusema hivi: “Mwana wa binadamu atatuma malaika zake, nao watakusanya kutoka katika ufalme wake vitu vyote ambavyo husababisha kukwazika na watu wanaofanya uasi-sheria.” (Mathayo 13:37-41) Isitoshe, kama vile malaika alivyomwongoza Filipo kumpata yule towashi Mwethiopia, leo kuna uthibitisho wa kutosha kwamba Kristo hutumia malaika kuongoza kazi ya Wakristo wa kweli ya kutafuta watu wenye mioyo minyofu.—Matendo 8:26, 27; Ufunuo 14:6.

9. (a) Kristo analiongoza kutaniko la Kikristo leo kupitia njia gani? (b) Tunapaswa kufikiria swali gani iwapo tunataka kunufaika na uongozi wa Kristo?

9 Inatia moyo kama nini kujua kwamba Yesu Kristo anaongoza wanafunzi wake leo kupitia Baraza Linaloongoza, roho takatifu, na malaika! Hata kama baadhi ya waabudu wa Yehova wangetengwa kwa muda na Baraza Linaloongoza kwa sababu ya mnyanyaso au kwa sababu nyingine kama hizo, bado Kristo angeendelea kutoa uongozi kupitia roho takatifu na utegemezo wa malaika. Hata hivyo, tunanufaika tu na uongozi wake tunapoukubali. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunakubali uongozi wa Kristo?

“Iweni Watiifu . . . Wenye Kunyenyekea”

10. Tunawezaje kuonyesha heshima kwa wazee waliowekwa rasmi kutanikoni?

10 Kiongozi wetu ameyapa makutaniko “zawadi [zikiwa] wanadamu”—‘wengine kuwa mitume, wengine kuwa manabii, wengine kuwa waeneza-evanjeli, wengine kuwa wachungaji na walimu.’ (Waefeso 4:8, 11, 12) Mtazamo na matendo yetu kuwaelekea huonyesha wazi kabisa kama tunakubali uongozi wa Kristo. Inafaa ‘tujionyeshe wenyewe kuwa wenye shukrani’ kwa ajili ya wanaume wenye kustahili kiroho ambao Kristo ametoa. (Wakolosai 3:15) Tunapaswa kuwaheshimu pia. “Acha wanaume wazee wasimamiao katika njia bora wahesabiwe kustahili heshima maradufu,” akaandika mtume Paulo. (1 Timotheo 5:17) Tunawezaje kuonyesha shukrani na heshima kwa wanaume wazee, yaani, wazee au waangalizi wa kutaniko? Paulo anajibu: “Iweni watiifu kwa wale ambao wanaongoza miongoni mwenu na kuwa wenye kunyenyekea.” (Waebrania 13:17) Naam, tunapaswa kuwatii na kuwanyenyekea.

11. Kwa nini kuheshimu mpango wa kuwa na wazee kunahusiana na kuishi kupatana na ubatizo wetu?

11 Kiongozi wetu ni mkamilifu. Wanaume ambao ametoa wakiwa zawadi si wakamilifu. Kwa hiyo, wanaweza kukosea mara kwa mara. Hata hivyo, ni muhimu kwamba tuendelee kuwa waaminifu-washikamanifu kwa mpango wa Kristo. Bila shaka, kuishi kulingana na wakfu na ubatizo wetu kunamaanisha kwamba tunatambua uhalali wa mamlaka yaliyowekwa rasmi kutanikoni kupitia roho, na tunakuwa tayari kujitiisha kwa mamlaka hayo. Ubatizo wetu ‘katika jina la roho takatifu’ ni tangazo la hadharani kwamba tunatambua roho takatifu na kukubali jukumu inayotimiza katika makusudi ya Yehova. (Mathayo 28:19) Ubatizo huo unamaanisha kwamba tunashirikiana na roho na tunaepuka kufanya chochote kinachoweza kuzuia roho hiyo isitende kazi miongoni mwa wafuasi wa Kristo. Kwa kuwa roho takatifu inatimiza jukumu muhimu katika kupendekezwa na kuwekwa rasmi kwa wazee, hatuwezi kuwa waaminifu kwa wakfu wetu ikiwa hatuungi mkono mpango wa kuwa na wazee kutanikoni.

12. Yuda anataja mifano gani kuhusu kutoheshimu mamlaka, nayo inatufundisha nini?

12 Maandiko yana mifano inayotufundisha umuhimu wa kutii na kunyenyekea. Akirejezea wale waliosema kwa maneno yenye kuudhi kuhusu wanaume waliowekwa rasmi kutanikoni, mwanafunzi Yuda alitaja mifano mitatu yenye kuonya, akisema: “Ole wao, kwa sababu wamekwenda katika pito la Kaini, na wametimua mbio kali kuingia katika mwendo wenye kosa wa Balaamu kwa ajili ya thawabu, nao wameangamia katika maongezi ya uasi ya Kora!” (Yuda 11) Kaini alipuuza ushauri wenye upendo wa Yehova na kwa makusudi akasitawisha chuki iliyomwongoza kuua kimakusudi. (Mwanzo 4:4-8) Ingawa Balaamu alionywa na Mungu mara nyingi, yeye alijaribu kuwalaani watu wa Mungu ili apate zawadi ya kifedha. (Hesabu 22:5-28, 32-34; Kumbukumbu la Torati 23:5) Kora alikuwa na cheo chenye heshima katika Israeli, lakini hakutosheka nacho. Alichochea uasi dhidi ya mtumishi wa Mungu Musa, aliyekuwa mnyenyekevu zaidi duniani. (Hesabu 12:3; 16:1-3, 32, 33) Kaini, Balaamu, na Kora walipatwa na msiba. Mifano hiyo inatufundisha kwa njia iliyo wazi kusikiliza ushauri wa wale ambao Yehova hutumia katika nyadhifa za madaraka na pia kuwaheshimu.

13. Nabii Isaya alitabiri baraka gani kwa wale wanaonyenyekea mpango wa kuwa na wazee?

13 Ni nani ambaye hangetaka kunufaika na mpango mzuri wa uangalizi ambao Kiongozi wetu ameanzisha katika kutaniko la Kikristo? Nabii Isaya alitabiri baraka ambazo zingetokana na mpango huo aliposema: “Tazama, mfalme atamiliki kwa haki, na wakuu watatawala kwa hukumu. Na mwanadamu atakuwa kama mahali pa kujificha na upepo, na mahali pa kujisitiri na dhoruba; kama mito ya maji mahali pakavu, kama kivuli cha mwamba mkubwa katika nchi yenye uchovu.” (Isaya 32:1, 2) Kila mmoja wa wazee hao anapaswa kuwa “mahali” pa ulinzi na usalama. Hata ikiwa si rahisi kwetu kunyenyekea mamlaka, na tusali ili kupata msaada tunapojitahidi kutii na kunyenyekea mamlaka ambayo Mungu ameweka kutanikoni.

Jinsi Wazee Wanavyonyenyekea Uongozi wa Kristo

14, 15. Wale wanaoongoza kutanikoni wanaonyeshaje kwamba wananyenyekea uongozi wa Kristo?

14 Wakristo wote, na hasa wazee, wanapaswa kutii uongozi wa Kristo. Waangalizi, au wazee, wana mamlaka ya kiasi fulani kutanikoni. Lakini hawatafuti kuwa ‘mabwana-wakubwa juu ya imani ya waamini wenzao’ kwa kujaribu kudhibiti maisha yao. (2 Wakorintho 1:24) Wazee hutii maneno haya ya Yesu: “Mwajua kwamba watawala wa mataifa hupiga ubwana juu yao na watu wakubwa hutumia mamlaka juu yao. Hivyo sivyo ilivyo miongoni mwenu.” (Mathayo 20:25-27) Wanapotimiza daraka lao, wazee hujitahidi kuwatumikia wengine kwa unyofu.

15 Wakristo wanahimizwa: “Kumbukeni wale ambao wanaongoza miongoni mwenu, . . . nanyi mfikiriapo jinsi mwisho wa mwenendo wao upatavyo kuwa, igeni imani yao.” (Waebrania 13:7) Wakristo hawahimizwi waige imani ya wazee eti tu kwa sababu wao wamewekwa kuwa viongozi. Yesu alisema: “Kiongozi wenu ni mmoja, Kristo.” (Mathayo 23:10) Kile kinachopaswa kuigwa ni imani ya wazee kwa sababu wao humwiga Kristo, Kiongozi wetu halisi. (1 Wakorintho 11:1) Fikiria njia fulani ambazo wazee hujitahidi kuwa kama Kristo katika uhusiano wao na wengine kutanikoni.

16. Licha ya mamlaka aliyokuwa nayo, Yesu aliwatendeaje wafuasi wake?

16 Ingawa Yesu alikuwa mkuu sana kuliko wanadamu wasio wakamilifu na alikuwa na mamlaka yasiyo na kifani kutoka kwa Babake, yeye alikuwa na kiasi aliposhughulika na wanafunzi wake. Hakutumia ujuzi wake kuwaaibisha na kujionyesha kwa wasikilizaji wake. Yesu aliwahurumia wafuasi wake na alijali mahitaji yao ya kimwili. (Mathayo 15:32; 26:40, 41; Marko 6:31) Hakudai wanafunzi wake watimize mengi kuliko uwezo wao, wala hakuwapa madaraka yaliyozidi uwezo wao. (Yohana 16:12) Yesu alikuwa “mwenye tabia-pole na wa hali ya chini moyoni.” Kwa hiyo, haishangazi kwamba wengi walimwona kuwa mtu mwenye kuburudisha.—Mathayo 11:28-30.

17. Wazee wanapaswa kuonyeshaje kiasi kama Kristo katika uhusiano wao na wengine kutanikoni?

17 Ikiwa Kristo aliye Kiongozi alionyesha kiasi, basi wanaoongoza kutanikoni wanapaswa kuonyesha sifa hiyo kwa kadiri kubwa hata zaidi. Naam, wanakuwa waangalifu wasitumie vibaya mamlaka yoyote waliyopewa. Na ‘hawaji wakiwa na usemi wenye kupita kiasi,’ wakijaribu kujionyesha kwa wengine. (1 Wakorintho 2:1, 2) Badala yake, wanajitahidi kusema kweli ya Kimaandiko kwa njia inayoeleweka na ya unyofu. Isitoshe, wazee wanajitahidi kufikiria mahitaji ya wengine na kuwa wenye kiasi kuhusiana na wanayotarajia kutoka kwao. (Wafilipi 4:5) Kwa kuwa wazee wanajua kwamba kila mtu ana udhaifu, kwa upendo wanafikiria udhaifu huo wanaposhughulika na ndugu zao. (1 Petro 4:8) Wazee wanyenyekevu na wenye tabia ya upole wanaburudisha kwelikweli.

18. Wazee wanaweza kujifunza nini kutokana na jinsi Yesu alivyowatendea watoto?

18 Watu wote, hata wale wa hali ya chini walijihisi huru kumfikia Yesu. Ona vile Yesu alivyotenda wakati wanafunzi wake walipowakemea watu kwa “kumletea watoto wachanga.” Alisema: “Waacheni watoto wachanga waje kwangu; msijaribu kuwakomesha.” Kisha “akachukua watoto akawakumbatia na kuanza kuwabariki, akiweka mikono yake juu yao.” (Marko 10:13-16) Yesu alikuwa mchangamfu, mwenye fadhili, na aliwavutia wengine. Watu hawakumwogopa. Hata watoto walihisi wamestarehe wakiwa pamoja naye. Watu hujihisi huru kuwafikia wazee, na wazee wanapoonyesha upendo mchangamfu na fadhili, wengine—hata watoto—huhisi wamestarehe wakiwa pamoja nao.

19. Inamaanisha nini kuwa na “akili ya Kristo,” na jambo hilo linahitaji tufanye jitihada gani?

19 Wazee wanaweza kumwiga Kristo Yesu ikiwa tu wanamjua vizuri. Paulo aliuliza, “Ni nani amekuja kuijua akili ya Yehova, kwamba apate kumfundisha?” Kisha akaongeza: “Lakini sisi tunayo akili ya Kristo.” (1 Wakorintho 2:16) Kuwa na akili ya Kristo kunamaanisha kujua jinsi anavyofikiri na kuelewa utu wake kabisa ili tujue namna tuwezavyo kutenda katika hali fulani hususa. Hebu wazia kupata kumjua Kiongozi wetu vizuri hivyo! Naam, jambo hilo linahitaji tuzingatie kwa makini masimulizi ya vitabu vya Injili na kujifunza kwa ukawaida maisha na kielelezo cha Yesu. Wazee wanapojitahidi kutii uongozi wa Kristo kwa kadiri hiyo, inakuwa rahisi zaidi kwa wale walio kutanikoni kuiga imani yao. Nao wazee wanafurahi kuona wengine wakifuata hatua za Kiongozi wao kwa shangwe.

Endelea Chini ya Uongozi wa Kristo

20, 21. Tutazamapo mbele kwenye ulimwengu mpya ulioahidiwa, tunapaswa kuazimia kufanya nini?

20 Ni muhimu kwamba sote tuendelee kunyenyekea uongozi wa Kristo. Tukaribiapo mwisho wa mfumo huu wa mambo, hali yetu inaweza kulinganishwa na ya Waisraeli kwenye Nyanda za Moabu mwaka wa 1473 K.W.K. Walikuwa karibu sana kuingia katika Bara Lililoahidiwa, na kupitia nabii Musa, Mungu alitangaza hivi: “Wewe [Yoshua] utawaongoza watu hawa kwenda kuimiliki nchi ambayo Mwenyezi-Mungu aliwaahidi babu zao; nawe utawakabidhi waimiliki.” (Kumbukumbu la Torati 31:7, 8, Biblia Habari Njema) Yoshua ndiye aliyewekwa rasmi awe kiongozi wao. Waisraeli walipaswa kunyenyekea uongozi wa Yoshua ili kuingia katika Bara Lililoahidiwa.

21 Biblia hutuambia hivi: “Kiongozi wenu ni mmoja, Kristo.” Kristo pekee ndiye atakayetuongoza kuingia katika ulimwengu mpya ulioahidiwa ambapo uadilifu utakaa. (2 Petro 3:13) Hivyo basi, na tuazimie kunyenyekea uongozi wake katika sehemu zote za maisha.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Hapa “nyota” hazifananishi malaika halisi. Yesu hangetumia mwanadamu kuandika habari kwa ajili ya viumbe wa roho wasioonekana. Kwa hiyo, lazima “nyota” hizi ziwe zinafananisha waangalizi wa kibinadamu au wazee katika makutaniko, wanaoonwa kuwa wajumbe wa Yesu. Nyota hizo ni saba, idadi inayoonyesha ukamilifu kupatana na kiwango cha Mungu.

Je, Unakumbuka?

• Kristo aliliongozaje kutaniko la mapema?

• Kristo huliongozaje kutaniko lake leo?

• Kwa nini tuwanyenyekee wale wanaoongoza kutanikoni?

• Wazee wanaweza kuonyesha kwa njia zipi kwamba Kristo ndiye Kiongozi wao?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 15]

Kristo analiongoza kutaniko lake naye amewashika waangalizi katika mkono wake wa kuume

[Picha katika ukurasa wa 16]

“Iweni watiifu kwa wale ambao wanaongoza miongoni mwenu na kuwa wenye kunyenyekea”

[Picha katika ukurasa wa 18]

Yesu alikuwa mchangamfu na watu walijihisi huru kumfikia. Wazee Wakristo hujitahidi kumwiga