Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Je, hali ya kutokamilika ya msichana bikira Maria iliathiri kutungwa kwa mimba ya Yesu?

Kuhusu “kuzaliwa kwa Yesu,” maandiko yaliyopuliziwa yanasema: “Katika wakati ambao Maria mama yake alikuwa ameposwa na Yosefu, alipatwa kuwa ana mimba kwa roho takatifu kabla ya wao kuungana pamoja.” (Mathayo 1:18) Ni kweli kwamba roho takatifu ya Mungu ilitimiza fungu muhimu sana kuhusiana na mimba hiyo ya Maria.

Hata hivyo, namna gani Maria? Je, yai lake lilitumiwa katika utungaji wa mimba hiyo? Kwa kufikiria ahadi ambazo Mungu alitoa kwa mababu wa Maria—Abrahamu, Isaka, Yakobo, Yuda, na Mfalme Daudi—mtoto ambaye angezaliwa angepaswa kuwa mzao wao halisi. (Mwanzo 22:18; 26:24; 28:10-14; 49:10; 2 Samweli 7:16) La sivyo, mtoto huyo ambaye angezaliwa na Maria hangeweza kuwa mrithi halali wa ahadi hizo za Mungu. Angepaswa kuwa mwana halisi wa Maria.—Luka 3:23-34.

Malaika wa Yehova alimtokea msichana bikira Maria na kusema: “Usiwe na hofu, Maria, kwa maana umepata upendeleo kwa Mungu; na, tazama! utachukua mimba katika tumbo lako la uzazi na kuzaa mwana, nawe itakupasa kumwita jina lake Yesu.” (Luka 1:30, 31) Ili mimba itungike, ni lazima yai liungane na mbegu ya kiume. Yaonekana Yehova Mungu alitungisha mimba hiyo kwa kuhamisha uhai wa Mwanawe mzaliwa wa pekee kutoka makao ya roho hadi duniani, na kuunganisha uhai huo na yai katika tumbo la uzazi la Maria.—Wagalatia 4:4.

Je, mtoto ambaye mimba yake imetungwa kwa kutumia yai la mwanamke asiye mkamilifu, angekuwa bila dhambi? Kanuni za urithi hufanyaje kazi wakati kitu kilicho kikamilifu kinapoungana na kitu kisicho kikamilifu? Kumbuka kwamba roho takatifu ilitumiwa kuhamisha uhai mkamilifu wa Mwana wa Mungu na kutungisha mimba hiyo. Roho hiyo ilibatilisha hali yoyote ya kutokamilika katika yai la Maria, na hivyo kutokeza kiumbe mkamilifu.

Hata mimba hiyo iwe ilitungwa jinsi gani, tunaweza kuwa na uhakika kwamba utendaji wa roho takatifu ya Mungu wakati huo ulihakikisha kwamba kusudi la Mungu lilifaulu. Malaika Gabrieli alikuwa amemweleza Maria hivi: “Roho takatifu itakuja juu yako, na nguvu ya Aliye Juu Zaidi Sana itakufunika kivuli. Kwa sababu hiyo pia kitakachozaliwa kitaitwa kitakatifu, Mwana wa Mungu.” (Luka 1:35) Naam, tangu mimba hiyo itungwe, ni kana kwamba roho takatifu ya Mungu ilikizingira kiinitete hicho na kukilinda kisiathiriwe na hali yoyote ya kutokamilika.

Ni wazi kwamba, Yesu alipata uhai mkamilifu kutoka kwa Baba yake wa mbinguni, wala si kutoka kwa mwanadamu yeyote. Yehova ‘alimtayarishia Yesu mwili,’ na tangu kutungwa kwa mimba yake na kuendelea, Yesu ‘hakutiwa unajisi, alitengwa na watenda-dhambi.’—Waebrania 7:26; 10:5.

[Picha katika ukurasa wa 19]

“Utachukua mimba katika tumbo lako la uzazi na kuzaa mwana”