Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mikutano Inayotuchochea Kwenye Upendo na Kazi Zilizo Bora

Mikutano Inayotuchochea Kwenye Upendo na Kazi Zilizo Bora

“Njoni Kwangu, . . . Nami Hakika Nitawaburudisha Nyinyi”

Mikutano Inayotuchochea Kwenye Upendo na Kazi Zilizo Bora

KUTOKA Toronto hadi Tokyo, kutoka Moscow hadi Montevideo—mara kadhaa kila juma, mamilioni ya Mashahidi wa Yehova pamoja na rafiki zao humiminika kwenye mahali pao pa ibada. Watu hawa hutia ndani wanaume wenye familia na waliochoka baada ya kufanya kazi siku nzima; wake na akina mama wenye bidii wanaoambatana na watoto wao wachanga; vijana wenye uchangamfu ambao wamekuwa shuleni siku nzima; wazee walio wanyonge ambao hutembea polepole kwa sababu ya maumivu; wajane na mayatima wajasiri; na watu walioshuka moyo ambao wanahitaji faraja.

Mashahidi hawa wa Yehova hutumia njia mbalimbali za usafiri—gari-moshi la abiria linaloenda kwa kasi sana, punda, magari-moshi ya chini ya ardhi yanayojaa sana watu na pia malori. Baadhi yao hulazimika kuvuka mito iliyojaa mamba, hali wengine hulazimika kuvumilia misongamano ya magari katika majiji makubwa. Kwa nini watu wote hawa hujitahidi sana hivyo?

Hasa kwa sababu kuhudhuria na kushiriki katika mikutano ya Kikristo ni njia muhimu ya kumwabudu Yehova Mungu. (Waebrania 13:15) Mtume Paulo alirejezea sababu nyingine alipoandika hivi: “Na acheni tufikiriane ili kuchocheana kwenye upendo na kazi zilizo bora, si kuachilia mbali kukusanyika pamoja sisi wenyewe, . . . bali kutiana moyo, na zaidi sana hivyo kwa kadiri mwonavyo siku ikikaribia.” (Waebrania 10:24, 25) Hapa Paulo anakubaliana na maneno ya mtunga-zaburi Daudi, aliyeimba: “Nalifurahi waliponiambia: ‘Na twende nyumbani kwa BWANA.’”—Zaburi 122:1.

Kwa nini Wakristo hufurahi kuhudhuria mikutano yao? Kwa sababu wale wanaohudhuria si watazamaji tu. Bali mikutano hiyo huwapa nafasi ya kujuana. Mikutano hiyo hasa huandaa pindi za kutoa, si kupokea tu, na kuchocheana kuonyesha upendo na kufanya kazi zilizo bora. Hii husaidia kufanya mikutano kuwa pindi zenye kujenga. Kwa kuongezea, mikutano ya Kikristo ni mojawapo ya njia ambazo Yesu hutumia kutimiza ahadi yake: “Njoni kwangu, . . . nami hakika nitawaburudisha nyinyi.”—Mathayo 11:28.

Mahali Ambapo Watu Wanakujali na Kukufariji

Mashahidi wa Yehova wana sababu nzuri za kuona mikutano yao kuwa yenye kuburudisha. Kwanza, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” huandaa chakula cha kiroho kwa wakati ufaao kwenye mikutano. (Mathayo 24:45) Mikutano pia huwasaidia sana watumishi wa Yehova kuwa walimu ustadi na wenye bidii wa Neno la Mungu . Pia katika Jumba la Ufalme, unaweza kupata marafiki wenye upendo, wanaokujali, na walio tayari kusaidia na kufariji wengine wakati wa taabu.—2 Wakorintho 7:5-7.

Mwanamke mmoja mjane anayeitwa Phillis alijionea ukweli wa maneno hayo. Mume wake alipokufa alikuwa na watoto wawili, mmoja mwenye umri wa miaka mitano na mwingine minane. Yeye alieleza hivi kuhusu namna walivyoburudishwa katika mikutano ya Kikristo: “Tulifarijika kwenda kwenye Jumba la Ufalme kwa sababu kila wakati waamini wenzetu walituonyesha upendo na walitujali kwa kutukumbatia, kutuonyesha wazo la Kimaandiko au hata kutushika mikono kwa upendo walipotusalimu. Ni mahali nilipenda kuwa siku zote.”—1 Wathesalonike 5:14.

Baada ya Marie kufanyiwa upasuaji, daktari wake alisema kwamba ingemchukua angalau majuma sita kupona. Majuma kadhaa ya kwanza alipokuwa akipata nafuu, Marie hakuweza kuhudhuria mikutano. Daktari wake aligundua kwamba hakuwa na shangwe kama hapo awali. Alipotambua kwamba Marie hakuwa anahudhuria mikutano, alimtia moyo afanye hivyo. Marie alimwambia kwamba mume wake ambaye hakuwa Shahidi, hangemruhusu kwenda mikutanoni kwa sababu ya afya yake. Basi daktari akaandika maagizo rasmi ya “kuamrisha” Marie kwenda kwenye Jumba la Ufalme ili apate kitia moyo na ushirika wenye kujenga. Marie amalizia hivi: “Nilihisi nafuu baada ya kuhudhuria mkutano mmoja tu. Nilianza kula, nikalala usiku wote, sikuhitaji kutumia dawa za kupunguza maumivu mara nyingi, na nikaanza kuwa na furaha tena!”—Mithali 16:24.

Upendo unaopatikana kwenye mikutano ya Kikristo huonwa na watu wa nje. Mwanafunzi fulani wa chuo kimoja aliamua kuwachunguza Mashahidi wa Yehova ili aandike juu yao katika somo lake la kuchunguza tamaduni mbalimbali. Kuhusiana na amani na utulivu mikutanoni, aliandika hivi: “Nilivutiwa sana na ukaribishaji wenye uchangamfu niliopokea. . . . Shauku ya Mashahidi wa Yehova ilikuwa yenye kutokeza sana nami nahisi kwamba hiyo ilikuwa sehemu ya maana zaidi katika mikutano yao.”—1 Wakorintho 14:25.

Katika ulimwengu huu wenye matatizo, kutaniko la Kikristo ni mahali pa kupata faraja ya kiroho. Ni mahali pa amani na upendo. Kwa kuhudhuria mikutano, utajionea ukweli wa maneno haya ya mtunga-zaburi: “Tazama, jinsi ilivyo vema, na kupendeza, ndugu wakae pamoja, kwa umoja”!—Zaburi 133:1.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 25]

KUTOSHELEZA MAHITAJI YA PEKEE

Wasioweza kusikia wanaweza kufaidikaje na mikutano ya Kikristo? Ulimwenguni pote, Mashahidi wa Yehova wanaanzisha makutaniko yanayotumia lugha za ishara. Kwa kipindi cha miaka 13 iliyopita, makutaniko 27 na vikundi 43 vya lugha za ishara vimeanzishwa huko Marekani. Katika angalau nchi nyingine 40, kuna karibu makutaniko 140 ya lugha za ishara. Vichapo vya Kikristo vimetayarishwa kwa video katika lugha 13 za ishara.

Kutaniko la Kikristo huwaandalia wasioweza kusikia fursa ya kumtukuza Yehova. Mwanamke mmoja huko Ufaransa anayeitwa Odile ambaye alikuwa Mkatoliki hapo awali, alikuwa ameshuka moyo sana na kufikiria kujiua, sasa anashukuru sana kwa elimu ya Biblia aliyopokea katika mikutano ya Kikristo. Yeye asema hivi: “Nilipata nafuu na shangwe ya kuishi. Lakini zaidi ya yote, nilipata ile kweli. Sasa maisha yangu yana kusudi.”