Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tunaweza Kupata Wapi Uongozi Bora?

Tunaweza Kupata Wapi Uongozi Bora?

Tunaweza Kupata Wapi Uongozi Bora?

“KILA nyumba imejengwa na mtu fulani,” yasema Biblia, “lakini yeye aliyejenga vitu vyote ni Mungu.” (Waebrania 3:4; Ufunuo 4:11) Kwa sababu Mungu wa kweli Yehova, ndiye Muumba wetu, “anatujua umbo letu.” (Zaburi 103:14) Anajua kabisa udhaifu na mahitaji yetu. Na kwa sababu yeye ni Mungu mwenye upendo, anataka kututimizia mahitaji hayo. (Zaburi 145:16; 1 Yohana 4:8) Hii yatia ndani uhitaji wetu wa uongozi bora.

Kupitia nabii Isaya, Yehova alitangaza: “Angalieni, nimemweka kuwa shahidi kwa kabila za watu; kuwa kiongozi na jemadari kwa kabila za watu.” (Isaya 55:4) Suluhisho la tatizo la siku hizi la uongozi latia ndani kumtambua Kiongozi huyo—aliyewekwa rasmi na Mweza Yote mwenyewe—na kukubali uongozi wake. Basi Kiongozi na Jemadari huyo aliyetabiriwa ni nani? Ni sifa zipi zinazomfanya astahili kuwa kiongozi? Atatuongoza kwenda wapi? Tunapaswa kufanya nini ili tufaidike na uongozi wake?

Kiongozi Aliyeahidiwa Awasili

Miaka 2,500 iliyopita, malaika Gabrieli alimtokea nabii Danieli na kumwambia hivi: “Basi ujue na kufahamu, ya kuwa tangu kuwekwa amri ya kutengeneza na kuujenga upya Yerusalemu hata zamani zake masihi aliye mkuu [“Mesiya aliye Kiongozi,” NW]; kutakuwa na majuma saba; na katika majuma sitini na mawili utajengwa tena pamoja na njia kuu zake na handaki, naam, katika nyakati za taabu”—Danieli 9:25.

Ni wazi kwamba malaika alimfahamisha Danieli wakati hususa wa kuja kwa Kiongozi aliyechaguliwa na Yehova. “Mesiya aliye Kiongozi” angetokea mwishoni mwa majuma 69 au miaka 483, tukihesabu kuanzia mwaka wa 455 K.W.K., tangu kutolewa kwa amri ya kujengwa upya Yerusalemu. * (Nehemia 2:1-8) Ni nini kilichotendeka mwishoni mwa kipindi hicho? Luka, mwandishi wa Gospeli aeleza: “Mwaka wa kumi na tano wa kumiliki kwa Tiberio Kaisari, Pontio Pilato alipokuwa gavana wa Yudea, na Herode alipokuwa mtawala wa wilaya ya Galilaya [29 W.K.], . . . tangazo la Mungu likamjia Yohana mwana wa Zekaria nyikani. Basi akaja kuingia katika nchi yote kuzunguka Yordani, akihubiri ubatizo katika ufananisho wa toba kwa msamaha wa dhambi.” Wakati huo, “watu walikuwa wakitarajia” Mesiya aliye Kiongozi. (Luka 3:1-3, 15) Ijapokuwa wengi walimwendea Yohana, yeye hakuwa huyo Kiongozi.

Kisha karibu Oktoba 29 W.K., Yesu wa Nazareti akamwendea Yohana ili abatizwe. Naye Yohana akatoa ushahidi, akisema: “Mimi nilitazama roho ikiteremka kama njiwa kutoka mbinguni, nayo ikakaa juu yake. Hata mimi sikumjua yeye, bali Yuleyule aliyenituma mimi nibatize katika maji aliniambia, ‘Yeyote yule ambaye waona roho ikiteremka na kukaa juu yake, huyo ndiye ambaye hubatiza katika roho takatifu.’ Nami nimeona, na nimetoa ushahidi kwamba huyo ndiye Mwana wa Mungu.” (Yohana 1:32-34) Alipobatizwa, Yesu akawa Kiongozi mtiwa-mafuta—Mesiya, au Kristo.

Naam, Yesu Kristo akathibitika kuwa “kiongozi na jemadari aliyeahidiwa kwa kabila za watu.” Tuchunguzapo sifa zake akiwa kiongozi, tunatambua kwamba uongozi wake unapita matakwa yote yanayohitajiwa kwa kiongozi bora wa kisasa.

Mesiya—Kiongozi Bora

Kiongozi bora hutoa mwongozo unaofaa na kusaidia watu anaoongoza wapate nguvu na uwezo wa kutatua matatizo kwa mafanikio. ‘Hilo ni takwa la kiongozi mwenye mafanikio wa karne ya 21,’ chasema kitabu 21st Century Leadership: Dialogues With 100 Top Leaders. Yesu aliwatayarisha wasikilizaji wake vizuri kama nini ili kukabiliana na hali za kila siku! Ebu fikiria mahubiri yake maarufu sana—Mahubiri ya Mlimani. Maneno yaliyoandikwa katika Mathayo sura za 5 hadi 7 yamejaa mashauri yenye busara.

Kwa mfano, fikiria shauri la Yesu linalohusu kutatua tofauti za kibinafsi. Alisema: “Basi, ikiwa wewe unaleta zawadi yako kwenye madhabahu na huko wakumbuka kwamba ndugu yako ana jambo fulani dhidi yako, acha zawadi yako hapo mbele ya madhabahu, na uende zako; kwanza fanya amani yako na ndugu yako, na ndipo, ukiisha kurudi, toa zawadi yako.” (Mathayo 5:23, 24) Tunapaswa kwanza kufanya amani na wengine hata kabla ya kutimiza wajibu wa kidini, kama vile kutoa zawadi kwenye madhabahu ya hekalu huko Yerusalemu kama ilivyotakiwa katika Sheria ya Musa. Tusipofanya hivyo, ibada haitakubaliwa na Mungu. Shauri la Yesu linatumika leo kama lilivyotumika karne nyingi zilizopita.

Yesu pia aliwasaidia wasikilizaji wake kujiepusha na mtego wa ukosefu wa maadili. Yeye aliwaonya: “Nyinyi mlisikia kwamba ilisemwa, ‘Lazima usifanye uzinzi.’ Lakini mimi nawaambia nyinyi kwamba kila mtu ambaye hufuliza kumtazama mwanamke ili kuwa na harara kwa ajili yake tayari amefanya uzinzi pamoja naye moyoni mwake.” (Mathayo 5:27, 28) Onyo hilo linafaa kama nini! Kwa nini hata tushawishwe kufanya uzinzi kwa kuwaziawazia juu yake? Yesu alisema kwamba uzinzi na uasherati huanzia moyoni. (Mathayo 15:18, 19) Ni mwendo wa hekima kulinda moyo wetu.—Mithali 4:23.

Mahubiri ya Mlimani pia yana mashauri mazuri sana kuhusu kuwapenda maadui, kuonyesha ukarimu, kuwa na mtazamo unaofaa kuelekea mambo ya kimwili na ya kiroho, na mengineyo. (Mathayo 5:43-47; 6:1-4, 19-21, 24-34) Yesu hata aliwafundisha wasikilizaji wake jinsi ya kusali ili wapate msaada wa Mungu. (Mathayo 6:9-13) Mesiya aliye Kiongozi aliwaimarisha na kuwatayarisha wafuasi wake kushughulikia matatizo yaliyo ya kawaida kwa wanadamu.

Mara sita katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu anaanzisha mazungumzo yake kwa maneno “nyinyi mlisikia kwamba ilisemwa” au “zaidi ya hayo ilisemwa,” halafu analeta wazo lingine, akisema “hata hivyo, mimi nawaambia nyinyi.” (Mathayo 5:21, 22, 27, 28, 31-34, 38, 39, 43, 44) Hilo laonyesha kwamba wasikilizaji wake walizoea kutenda mambo kwa njia fulani, kulingana na mapokeo waliyofundishwa na Mafarisayo. Lakini Yesu sasa aliwaonyesha njia tofauti—njia iliyoonyesha maana halisi ya Sheria ya Musa. Kwa hivyo Yesu alikuwa anaanzisha mabadiliko, naye alifanya hivyo katika njia iliyokuwa rahisi kwa wafuasi wake kuikubali. Naam, Yesu aliwachochea watu kufanya mabadiliko ya kiroho na ya kiadili maishani mwao. Hilo linamtambulisha kiongozi wa kweli.

Kitabu fulani kinachozungumza kuhusu usimamizi, kinaonyesha jinsi ilivyo vigumu kuleta badiliko la namna hiyo. Chasema: “Kiongozi awezaye kuleta badiliko apaswa kuwa na huruma ya mfanyakazi anayehudumia jamii, utambuzi wa mwanasaikolojia, bidii ya mkimbiaji wa masafa marefu, mwenye kujitegemea kama mtu aishiye peke yake, na mwenye subira kama ya mtakatifu. Na licha ya sifa zote hizo, hana uhakika kwamba atafanikiwa.”

“Viongozi wanapaswa kutenda kama vile wangependa wafuasi wao watende,” ikasema makala fulani yenye kichwa: “Je, Mwenendo ni wa Maana Katika Uongozi?” Bila shaka, kiongozi bora hutenda kulingana na yale anayosema. Yesu alitenda hivyo! Naam, aliwafunza waliokuwa naye somo la unyenyekevu kwa kuwaosha miguu. (Yohana 13:5-15) Hakuwatuma tu wanafunzi wake wakahubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu, bali pia alifanya kazi hiyo kwa bidii. (Mathayo 4:18-25; Luka 8:1-3; 9:1-6; 10:1-24; Yohana 10:40-42) Yesu aliweka kielelezo kizuri cha uongozi, aliposema hivi kujihusu, “Mwana hawezi kufanya hata kitu kimoja kwa uanzisho wake mwenyewe, ila tu kile atazamacho Baba akifanya.”—Yohana 5:19.

Baada ya kuchunguza mambo ambayo Yesu alisema na kutenda, ni wazi kwamba yeye ndiye Kiongozi bora. Kwa hakika sifa zake zinapita viwango vyote vya uongozi bora wa wanadamu. Yesu ni mkamilifu. Baada ya kufa na kufufuliwa, alipata mwili usioweza kuharibiwa, na anaishi milele. (1 Petro 3:18; Ufunuo 1:13-18) Ni kiongozi yupi wa kibinadamu awezaye kuwa na sifa kama hizo?

Tunapaswa Kufanya Nini?

Akiwa Mfalme anayetawala wa Ufalme wa Mungu, “Mesiya aliye Kiongozi” atawaletea wanadamu watiifu baraka tele. Kuhusiana na hilo Maandiko yanaahidi: “Dunia itajawa na kumjua BWANA, kama vile maji yanavyoifunika bahari.” (Isaya 11:9) “Wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani.” (Zaburi 37:11) “Wataketi kila mtu chini ya mzabibu wake, na chini ya mtini wake; wala hapana mtu atakayewatia hofu.” (Mika 4:4) “Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”—Ufunuo 21:3, 4.

Ulimwengu leo umekosa uongozi bora. Lakini Yesu Kristo anaongoza wapole kwenye ulimwengu mpya wenye amani, ambapo wanadamu watiifu wataungana katika ibada ya Yehova Mungu na kuendelea kusonga mbele hadi ukamilifu. Jinsi lilivyo jambo la maana kutafuta wakati ili kupata kumjua Mungu wa kweli na Kiongozi aliyemweka rasmi na kutenda kulingana na ujuzi huo!—Yohana 17:3.

Njia bora zaidi ya kumsifu mtu ni kwa kumwiga. Je, haitupasi kumwiga Kiongozi mkuu zaidi katika historia ya binadamu—Yesu Kristo? Tunaweza kufanya hivyo jinsi gani? Kukubali uongozi wake kutakuwa na matokeo gani maishani mwetu? Maswali haya na mengineyo yatazungumziwa katika makala mbili zifuatazo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Ona kurasa 186-192 za kitabu Sikiliza Unabii wa Danieli!, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Danieli alitabiri kuja kwa Kiongozi aliyechaguliwa na Mungu

[Picha katika ukurasa wa 7]

Mafundisho ya Yesu yaliwatayarisha watu kushughulikia matatizo maishani

[Picha katika ukurasa wa 7]

Yesu atawaongoza wanadamu watiifu kwenye ulimwengu mpya wenye amani