Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unaweza Kuushinda Upweke

Unaweza Kuushinda Upweke

Unaweza Kuushinda Upweke

NI NANI awezaye kudai kwamba hajapata maumivu yaletwayo na upweke? Kuna mambo mengi yanayoweza kutufanya tuhisi upweke. Upweke ulio mbaya zaidi hasa, ni ule wa wanawake ambao bado hawajaolewa, wajane au waliotalikiwa.

Kwa mfano, kijana mwanamke Mkristo aitwaye Frances asema: “Nilipokuwa mwenye umri wa miaka 23, ilionekana kwamba marafiki wangu wote walikuwa wameolewa, nami nilibaki mpweke.” * Hisia za kutengwa na wengine huongezeka kadiri miaka inavyozidi na matumaini ya kuolewa yanapozidi kupungua. “Sikukusudia kubaki mseja, na ikiwezekana ningependa kuolewa,” akiri Sandra, ambaye sasa umri wake unakaribia miaka 50. Angela aliye katika miaka yake ya 50 asema: “Sikuazimia kubaki mseja, lakini hivyo ndivyo hali ilivyo. Kulikuwa na ndugu waseja wachache sana katika eneo nililogawiwa nikiwa painia wa pekee.”

Wanawake wengi Wakristo wastahili kusifiwa kwa kuamua kutoolewa kwa sababu wanatii kwa unyofu shauri la Yehova la kuolewa “katika Bwana tu.” (1 Wakorintho 7:39) Wengine huzoea maisha ya useja, lakini kwa wengine tamaa ya kuolewa na kuwa na watoto huongezeka kadiri miaka ipitavyo. Sandra akiri hivi: “Utupu wa kihisia-moyo unaotokana na kukosa mwenzi wa ndoa hunisumbua daima.”

Mambo mengine, kama vile kutunza wazazi wazee, huenda yakaongeza hisia za upweke. “Kwa sababu sijaolewa, familia yetu ilitazamia nitunze wazazi wetu wazee,” asema Sandra. “Kwa miaka 20 nilichukua sehemu kubwa ya daraka hilo, ijapokuwa mimi ni mmoja kati ya watoto sita katika familia yetu. Maisha yangekuwa rahisi zaidi kama ningalikuwa na mume ambaye angeniunga mkono.”

Frances ataja jambo lingine lililozidisha upweke wake. Yeye aeleza: “Wakati mwingine watu huniuliza hivi moja kwa moja, ‘Mbona hujaolewa?’ Maneno kama hayo hunifanya nihisi kwamba kuwa mseja ni kosa langu. Kila arusi nihudhuriayo, mtu fulani huniuliza swali ninaloogopa sana, ‘Nawe utaolewa lini?’ Kisha ninaanza kuwaza, ‘Kwa sababu ndugu wa kiroho hawapendezwi nami, basi labda sina sifa za Kikristo zinazohitajiwa au labda mimi sivutii.’”

Hisia za kutengwa na wengine na za upweke zaweza kushindwaje? Je, wengine waweza kusaidia?

Mtegemee Yehova

Mtunga-zaburi aliimba: “Umtwike BWANA mzigo wako naye atakutegemeza, hatamwacha mwenye haki aondoshwe milele.” (Zaburi 55:22) Neno “mzigo” katika maandishi ya Kiebrania humaanisha kihalisi “fungu,” na hurejezea huzuni au mahangaiko ambayo huenda yakatupata kwa sababu ya fungu letu maishani. Yehova anaelewa mizigo hii kuliko mtu mwingine yeyote na anaweza kutupatia nguvu za kukabiliana nayo. Kumtegemea Yehova kumemsaidia Angela kukabiliana na upweke. Anapofikiria huduma yake ya wakati wote, yeye akumbuka: “Nilipoanza upainia, mimi na dada painia mwenzangu tuliishi mbali na kutaniko. Tulijifunza kumtegemea Yehova kabisa, jambo ambalo limenisaidia katika maisha yangu yote. Ninapokuwa na mawazo yasiyofaa, mimi husali kwa Yehova naye hunisaidia. Zaburi ya 23 imenifariji sana, nami huisoma mara nyingi.”

Mtume Paulo alibeba mzigo mzito. Katika pindi tatu hivi ‘alimsihi sana Bwana ili mwiba katika mwili wake upate kumwondoka.’ Paulo hakusaidiwa kimuujiza, bali aliahidiwa kwamba fadhili ya Mungu isiyostahiliwa ingemtegemeza. (2 Wakorintho 12:7-9) Paulo pia alitambua siri ya kutosheka. Baadaye aliandika: “Katika kila jambo na katika hali zote nimejifunza siri ya jinsi ya kushiba na pia jinsi ya kuwa na njaa, jinsi ya kuwa na wingi na pia jinsi ya kupatwa na uhitaji. Kwa mambo yote ninayo nguvu kwa njia ya yeye anipaye nguvu.”—Wafilipi 4:12, 13.

Mtu anawezaje kupata nguvu ya Mungu ikiwa anahisi amevunjika moyo au ni mpweke? Paulo aliandika: “Msihangaikie kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na utoaji-shukrani acheni maombi yenu ya bidii yajulishwe kwa Mungu; na amani ya Mungu izidiyo fikira yote kwa ubora italinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.” (Wafilipi 4:6, 7) Sandra hutumia shauri hilo. Yeye aeleza: “Kwa kuwa mimi ni mseja, mara nyingi ninakuwa peke yangu. Hiyo hunipa nafasi ya kutosha kusali kwa Yehova. Mimi hujihisi nikiwa karibu sana naye na ninaweza kuongea naye kuhusu matatizo na shangwe yangu.” Naye Frances asema hivi: “Kupigana dhidi ya mawazo yasiyofaa nikiwa peke yangu ni pambano gumu sana. Lakini ninapomwambia Yehova hisia zangu bila kuficha ninapata msaada mkubwa sana. Nina hakika kwamba Yehova anapendezwa na chochote kiwezacho kuathiri hali yangu ya kiroho na kihisia-moyo.”—1 Timotheo 5:5.

“Endeleeni Kuchukuliana Mizigo Yenye Kulemea”

Miongoni mwa udugu wa Kikristo, hakuna anayepaswa kubeba mizigo yenye kulemea peke yake. Mtume Paulo alihimiza hivi: “Endeleeni kuchukuliana mizigo yenye kulemea, na hivyo kutimiza sheria ya Kristo.” (Wagalatia 6:2) Tukishirikiana na Wakristo wenzetu, tutapata “neno jema” la kitia moyo ambalo laweza kufanya mzigo wa upweke uwe mwepesi.—Mithali 12:25.

Fikiria pia vile Maandiko yasemavyo kuhusu binti Yeftha, Mwamuzi wa Israeli. Kabla ya ushindi wake dhidi ya majeshi ya Waamoni, Yeftha aliweka nadhiri kwa Yehova kwamba yeyote wa nyumbani mwake ambaye angekuwa wa kwanza kutoka ili kumlaki angemtoa kwake. Bintiye akawa wa kwanza kumlaki. (Waamuzi 11:30, 31, 34-36) Ijapokuwa hiyo ilimaanisha kwamba binti Yeftha angebaki mseja na kuacha tamaa yake ya kawaida ya kuwa na familia, yeye alijitiisha chini ya nadhiri hiyo kwa hiari na akatumikia katika hekalu huko Shilo muda wote wa maisha yake. Je, kujidhabihu kwake kulipuuzwa? Hata kidogo. ‘Binti za Israeli walienda mwaka baada ya mwaka ili kumkumbuka [“kumpongeza,” NW] huyo mwana wa Yeftha, Mgileadi, siku nne katika mwaka.’ (Waamuzi 11:40) Naam, pongezi yaweza kuwatia moyo wanaoipokea. Kwa hivyo, tusikose kuwapongeza wanaostahili kupongezwa.

Ni vizuri pia tukifikiria mfano wa Yesu. Ijapokuwa haikuwa desturi ya Wayahudi wanaume kuzungumza na wanawake, Yesu alitumia wakati pamoja na Maria na Martha. Yaelekea walikuwa ama wajane au wanawake ambao hawakuwa wameolewa. Yesu alitaka wote wawili wafurahie faida za kiroho kutokana na urafiki wake. (Luka 10:38-42) Tunaweza kumwiga Yesu kwa kuwashirikisha dada zetu wa kiroho ambao hawajaolewa katika shughuli za kawaida na kupanga kuandamana pamoja nao katika kazi ya kuhubiri. (Waroma 12:13) Je, wao huthamini tunapowajali? Dada mmoja alisema: “Ninajua kwamba ndugu wananipenda na kunithamini, lakini ninathamini zaidi wanapopendezwa nami.”

Sandra aeleza, “Kwa sababu hatuna familia, tuna uhitaji mkubwa sana wa kuonyeshwa upendo, kuhisi kuwa sisi ni sehemu ya familia ya akina ndugu na dada wa kiroho.” Bila shaka Yehova anawajali watu kama hao, nasi tunashirikiana naye tunapowafanya wajihisi wanahitajiwa na kupendwa. (1 Petro 5:6, 7) Hangaiko hilo halitapuuzwa, kwa sababu yeye “amhurumiaye maskini humkopesha BWANA, naye atamlipa kwa tendo lake jema.”—Mithali 19:17.

“Kila Mmoja Atachukua Mzigo Wake Mwenyewe”

Ijapokuwa wengine wanaweza kusaidia, na msaada wao waweza kuwa wenye kutia moyo, “kila mmoja atachukua mzigo wake mwenyewe.” (Wagalatia 6:5) Hata hivyo, tunapochukua mzigo wa upweke tunapaswa kutahadhari kwani kuna hatari fulani. Kwa mfano, upweke unaweza kutushinda tukiamua kujinyamazia tu. Kwa upande mwingine, tunaweza kushinda upweke tukiwa na upendo. (1 Wakorintho 13:7, 8) Kutoa na kushiriki vitu na wengine ndiyo njia bora ya kupata furaha—hata hali zetu ziweje. (Matendo 20:35) “Sina wakati mwingi wa kufikiria juu ya upweke,” asema dada mmoja aliye painia mwenye bidii. “Ninapohisi kwamba ninathaminiwa na ninapokuwa na shughuli, sihisi upweke.”

Tunapaswa pia kuwa waangalifu tusiruhusu upweke utufanye tuingie katika uhusiano wa kimapenzi usiofaa. Kwa mfano, litakuwa jambo lenye kuhuzunisha kama nini iwapo tutaruhusu tamaa ya kutaka kuolewa ituzuie kuona matatizo yaletwayo na kuolewa na mtu asiye mwamini na hasa kutuzuia kuona hekima ya shauri la Kimaandiko la kuepuka nira kama hiyo! (2 Wakorintho 6:14) Mwanamke Mkristo aliyetalikiwa alisema: “Kitu kilicho kibaya zaidi kuliko kuwa mseja ni kuolewa na mtu asiyefaa.”

Tatizo lisiloweza kutatuliwa litahitaji kuvumiliwa angalau kwa wakati huu. Kwa msaada wa Mungu, hisia za upweke zaweza kuvumiliwa. Tunapoendelea kumtumikia Yehova, na tuwe na hakika kwamba siku moja mahitaji yetu yote yatatimizwa kwa njia bora zaidi iwezekanayo.—Zaburi 145:16.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Majina ya wanawake waliotajwa yamebadilishwa.

[Picha katika ukurasa wa 28]

Unaweza kushinda upweke kwa kutoa na kushiriki vitu pamoja na wengine