Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uongozi—Bora Tatizo la Ulimwenguni Pote

Uongozi—Bora Tatizo la Ulimwenguni Pote

Uongozi—Bora Tatizo la Ulimwenguni Pote

Mwanamume huyo alikuwa mwandishi na mshairi. Alikuwa na matumaini makubwa ya wakati ujao. Miaka 90 hivi iliyopita, aliwazia mahali ‘pasipo na woga ambapo mtu angejivunia hali yake ya maisha, mahali ambapo ujuzi ungepatikana bila malipo, mahali pasipo na mipaka ya kitaifa, mahali ambapo watu wanasema kweli, na ambapo watu wanajitahidi sana kufikia ukamilifu.’

KISHA mwandishi huyo akasema kwamba anatumainia siku watu ulimwenguni pote, kutia ndani watu wa nchi yake, wataishi mahali kama hapo. Iwapo mshairi huyo aliyekuwa mshindi wa Tuzo la Nobeli angalikuwa hai leo, angalisikitika sana. Licha ya mafanikio yaliyopo, ulimwengu umegawanyika sana leo kuliko wakati mwingine wowote. Na mwanadamu kwa ujumla hana matumaini yoyote ya wakati ujao.

Alipoulizwa ni kwa nini jeuri ilitokea kwa ghafla kati ya vikundi fulani katika nchi yake, mkulima mmoja alitaja kile alichoona kuwa mojawapo ya visababishi vya jeuri hiyo. “Ni kwa sababu ya viongozi wafisadi,” akasema. Mwanahistoria Jonathan Glover ana maoni kama hayo anaposema hivi katika kitabu chake Humanity—A Moral History of the Twentieth Century: “Mauaji ya kikabila [katika nchi hiyo] hayakutokana na chuki ya kikabila iliyotokea kwa ghafula tu bali yalipangwa na watu waliotaka mamlaka.”

Wakati vita vilipoanza kati ya jamhuri mbili za iliyokuwa nchi ya Yugoslavia mwanzoni mwa miaka ya 1990, mwandishi mmoja wa habari aliandika hivi: “Tuliishi pamoja kwa furaha kwa miaka mingi na sasa tumeanza kuuana. Kwa nini tunauana?”

Mshairi aliyetajwa mwanzoni alizaliwa India, nchi iliyoko maelfu ya kilometa kutoka Ulaya. Katika hotuba yenye kichwa “Je, India Yaweza Kuokoka Ikiwa Taifa Moja?,” mwandishi Pranay Gupte alisema: ‘Asilimia 70 ya idadi kubwa ya watu wa India wako chini ya umri wa miaka 30, hata hivyo hakuna viongozi wanaowawekea mfano bora wa kuiga.’

Katika nchi fulani, viongozi wamelazimika kujiuzulu kwa sababu ya mashtaka ya ufisadi. Kwa sababu mbalimbali basi, inaonekana kwamba ulimwengu una tatizo la uongozi. Hali zilizopo zinathibitisha maneno ya nabii aliyeishi miaka 2,600 hivi iliyopita. Alisema: “Njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.”—Yeremia 10:23.

Je, kuna suluhisho la matatizo yaliyopo ulimwenguni sasa? Ni nani awezaye kuongoza wanadamu kuingia katika ulimwengu ambapo jamii ya kibinadamu haitakuwa na vita wala woga, mahali ambapo ujuzi wa kweli utakuwa mwingi na bila malipo, na mahali ambapo wanadamu watafikia ukamilifu?

[Maelezo ya Picha katika ukurasa wa 3 zimeandaliwa na]

Fatmir Boshnjaku