Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Tufuate Imani Bila Kufikiri?

Je, Tufuate Imani Bila Kufikiri?

Je, Tufuate Imani Bila Kufikiri?

Mkuu wa kitivo cha theolojia katika chuo fulani huko Marekani aliandika: “Kuna watu wengi wanaodai kuwa na imani katika dini, wanaojiunga na dini hasa ili waepuke kutumia nguvu zao za kufikiri.” Kisha aongezea kusema: “Wanataka tu kuamini kila jambo bila kutaka uthibitisho.”

HILI ladokeza kwamba watu wengi wanaodai kwamba wanaamini mafundisho ya dini hawafikirii ni kwa nini wana imani hiyo au kama imani yao ina msingi mzuri. Si ajabu kwamba wengi hawapendi kuzungumza kuhusu dini.

Inasikitisha kwamba, mazoea kama yale ya kutumia mifano ya kidini na sala zinazokaririwa hufanya watu wasifikiri kwa njia ifaayo. Mazoea hayo, pamoja na majengo yenye kuvutia, madirisha ya vioo yenye rangi mbalimbali, na miziki yenye kusisimua, ndiyo mambo tu yapatikanayo katika dini nyingi. Ijapokuwa makanisa mengi yanadai kwamba imani yao ina msingi wa Biblia, ujumbe wao unaosema ‘amini katika Yesu nawe utaokolewa’ hauwachochei watu kujifunza Biblia kwa bidii. Wengine huhubiri gospeli ya kijamii au ya kisiasa. Matokeo yamekuwa nini?

Mwandishi fulani wa dini alisema hivi kuhusu hali za kule Amerika Kaskazini: “Ukristo unaelekea kuwa wa kijuu-juu tu, na waumini hawafunzwi vizuri ile imani.” Msimamizi mmoja wa kura ya maoni alieleza kuwa Marekani ni “taifa la watu wasio na elimu ya Biblia.” Kwa hakika, maoni hayo yahusu pia nchi nyinginezo zinazodai kuwa za Kikristo. Pia dini nyingi zisizo za Kikristo haziwasaidii watu kufikiri badala yake zinatilia mkazo kukariri nyimbo, sala za kidesturi, na kutafakari kwa namna mbalimbali kunakohusisha mafumbo badala ya kufikiri kwa njia ifaayo.

Hata hivyo, watu haohao wasiojali usahihi au ukweli wa imani yao ya kidini, mara nyingi hufikiria mambo mengine kwa makini sana katika maisha yao ya kila siku. Je, si jambo la kusikitisha kwamba mtu anayefanya utafiti mwingi ili anunue tu gari ambalo hatimaye litaharibika na kutupwa aweza kusema hivi kuhusu dini, ‘Ikiwa iliwaridhisha wazazi wangu, itaniridhisha pia.’

Ikiwa kwa kweli twataka kumpendeza Mungu, je, hatupaswi kufikiria kwa uzito usahihi wa yale tunayoamini kumhusu? Mtume Paulo alizungumza kuhusu watu fulani wa kidini wa siku zake ambao walikuwa na “bidii kwa ajili ya Mungu; lakini si kulingana na ujuzi sahihi.” (Waroma 10:2) Watu kama hao waweza kufananishwa na mpaka-rangi anayeajiriwa apake nyumba rangi lakini anatumia rangi zisizofaa kwa sababu hakusikiliza maagizo ya mwajiri wake. Huenda mpaka-rangi akapendezwa na kazi yake, lakini je, itakubaliwa na mwenye nyumba?

Ni nini kinachokubaliwa na Mungu kuhusiana na ibada ya kweli? Biblia yajibu: “Hili ni bora na lenye kukubalika machoni pa Mwokozi wetu, Mungu, ambaye mapenzi yake ni kwamba watu wa namna zote waokolewe na kuja kwenye ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Timotheo 2:3, 4) Huenda wengine wakahisi kwamba haiwezekani kupata ujuzi wa aina hiyo miongoni mwa dini nyingi za siku hizi. Lakini fikiria—ikiwa ni mapenzi ya Mungu kwamba watu waje kwenye ujuzi sahihi wa kweli, je, angeweza kuuficha isivyo haki kutoka kwao? Sivyo kwa kuwa Biblia, inasema: “Ukimtafuta [Mungu], ataonekana nawe.”—1 Mambo ya Nyakati 28:9.

Mungu anawezaje kupatikana kwa wale wanaomtafuta kwa unyofu? Makala ifuatayo itajibu swali hilo.