Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kaeni Macho, Songeni Mbele kwa Ujasiri!

Kaeni Macho, Songeni Mbele kwa Ujasiri!

Kaeni Macho, Songeni Mbele kwa Ujasiri!

Ripoti Kuhusu Mikutano ya Pekee

KWA hakika tunaishi katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” Tukiwa Mashahidi wa Yehova tunapatwa na mikazo ya kuishi katika “siku za mwisho.” (2 Timotheo 3:1-5) Lakini tunatambua kwamba watu wanahitaji msaada. Hawaelewi maana ya matukio ya ulimwengu. Wanahitaji faraja na tumaini. Tuna daraka gani hasa tunapowasaidia wanadamu wenzetu?

Tumeamriwa na Mungu kuhubiri habari njema za Ufalme wake unaotawala. (Mathayo 24:14) Watu wanapaswa kujua kwamba tumaini pekee la wanadamu ni Ufalme wa mbinguni. Hata hivyo, si watu wengi wanaoitikia ujumbe wetu. Katika sehemu fulani, kazi yetu imepigwa marufuku na ndugu zetu wananyanyaswa. Na bado tunaendelea kuhubiri. Tumeazimia kukaa macho na kuendelea kusonga mbele kwa ujasiri, tukihubiri habari njema bila kuacha huku tukimtumaini Yehova kabisa.—Matendo 5:42.

Azimio hilo imara lilionekana wazi kwenye mikutano ya pekee iliyofanywa mnamo Oktoba 2001. Mkutano wa kila mwaka wa Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania ulifanywa siku ya Jumamosi, Oktoba 6, katika Jumba la Kusanyiko la Mashahidi wa Yehova huko Jersey City, New Jersey, Marekani. * Siku iliyofuata mikutano ya ziada ilifanywa katika sehemu nne, mitatu huko Marekani na mmoja huko Kanada. *

Samuel F. Herd, mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, alianza mkutano wa kila mwaka kwa kurejezea andiko la Zaburi 92:1, 4, kisha akasema: “Tunataka kuwa wenye shukrani.” Ripoti tano zilizotolewa kutoka sehemu mbalimbali za ulimwengu zilionyesha ni kwa nini tunapaswa kuwa wenye shukrani.

Ripoti Kutoka Sehemu Zote

Ndugu Alfred Kwakye alitoa ripoti ya maendeleo ya kazi ya kuhubiri huko Ghana, nchi ambayo hapo zamani iliitwa Gold Coast. Kazi yetu ilipigwa marufuku kwa miaka kadhaa katika nchi hiyo. Watu walituuliza: “Mbona mmepigwa marufuku? Kwani mlifanya nini?” Maswali hayo yalitoa fursa ya kutoa ushahidi, akaeleza Ndugu Kwakye. Marufuku ilipoondolewa katika mwaka wa 1991, kulikuwa na Mashahidi wa Yehova 34,421 nchini Ghana. Katika Agosti mwaka wa 2001, kulikuwa na jumla ya wahubiri 68,152, kukiwa na ongezeko la asilimia 98. Mipango inafanywa ili kujenga Jumba la Kusanyiko linaloweza kutoshea watu 10,000. Bila shaka ndugu zetu huko Ghana wanatumia vizuri uhuru wao wa kidini.

Kujapokuwa msukosuko wa kisiasa, ndugu zetu huko Ireland wanahubiri kwa bidii, na wanaheshimiwa kwa sababu ya msimamo wao wa kutokuwamo katika siasa. Peter Andrews, mratibu wa Halmashauri ya Ofisi ya Tawi alisema kwamba kuna makutaniko 115 na mizunguko 6 huko Ireland. Ndugu Andrews alisimulia kuhusu Liam, mvulana mwenye umri wa miaka kumi ambaye anahubiri kwa ujasiri shuleni. Liam aliwaachia wanadarasa wenzake 25 pamoja na mwalimu wake Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Liam alitaka kubatizwa, lakini mtu fulani akamwuliza kama alikuwa bado mchanga mno. Liam akajibu: “Jambo linalopasa kuamua si umri wangu bali upendo wangu kwa Yehova. Ubatizo wangu utaonyesha kadiri ninavyompenda.” Liam ana mradi wa kuwa mishonari.

Katika mwaka wa 1968, kulikuwa na wahubiri wa habari njema 5,400 huko Venezuela. Lakini sasa kuna zaidi ya wahubiri 88,000 akasema Stefan Johansson, mratibu wa Halmashauri ya Ofisi ya Tawi. Na kuna uwezekano wa ongezeko kwani zaidi ya watu 296,000 walihudhuria Ukumbusho mwaka wa 2001. Mnamo Desemba 1999, mvua nyingi ilisababisha maporomoko ya ardhi yaliyoua watu wapatao 50,000 kutia ndani Mashahidi kadhaa. Jumba moja la Ufalme lilijaa matope. Wakati mtu fulani alipopendekeza kwamba jengo hilo liache kutumiwa, ndugu walisema: “La hasha! Hili ni Jumba letu la Ufalme, na hatutaki kuliacha wakati huu.” Walianza kazi ya kuondoa matope, mawe na vifusi vingine. Jengo hilo lilirekebishwa, na akina ndugu wanasema kwamba sasa linavutia kuliko lilivyokuwa kabla ya msiba!

Kuna lugha 87 zinazozungumzwa huko Filipino, akasema Ndugu Denton Hopkinson, mratibu wa Halmashauri ya Ofisi ya Tawi. Katika mwaka wa utumishi uliopita, Biblia nzima ya New World Translation of the Holy Scriptures ilitolewa katika lugha tatu kuu nchini humo—Cebuano, Iloko, na Tagalog. Ndugu Hopkinson alisimulia kuhusu mvulana mmoja mwenye umri wa miaka tisa ambaye alisoma kitabu Good News—To Make You Happy, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Alisoma vichapo vingine pia alivyopata kutoka kwa ofisi ya tawi, lakini alipingwa na washiriki wa familia yake. Miaka kadhaa baadaye akiwa katika chuo cha kusomea tiba, aliwasiliana na ofisi ya tawi na akaomba funzo la Biblia. Alibatizwa katika mwaka wa 1996 na kuanza utumishi wa wakati wote. Sasa yeye na mkewe wanatumikia katika ofisi ya tawi.

Mratibu wa Halmashauri ya Ofisi ya Tawi, Ronald Parkin alisema kwamba Mashahidi wengi wa Puerto Riko huhamia nchi nyinginezo. Idadi ya wahubiri katika kisiwa hicho ni 25,000 na haijaongezeka kwa miaka mingi. Kwa nini? Inakadiriwa kwamba kila mwaka, karibu wahubiri 1,000 kutoka Puerto Riko huhamia Marekani, wengi wao kwa sababu za kiuchumi. Ndugu Parkin alisimulia kuhusu uamuzi muhimu uliofikiwa mahakamani kuhusu Luis, kijana Shahidi mwenye umri wa miaka 17 aliyeugua ugonjwa wa lukemia. Luis alishtakiwa mahakamani kwa kukataa kutiwa damu. Hakimu alitaka kuongea naye, kwa hiyo akamtembelea hospitalini. Luis alimwambia hivi: “Kama ningefanya tendo baya la uhalifu, ungenihukumu kama mtu mzima, lakini sasa ninapotaka kumtii Mungu, unanitendea kama mtoto, kwa nini?” Hakimu akasadikishwa kwamba Luis alikuwa mtu mzima kulingana na sheria na hivyo angeweza kufanya uamuzi.

Baada ya ripoti hizo kutoka nchi za mbali, Harold Corkern mshiriki wa Halmashauri ya Ofisi ya Tawi ya Marekani, aliwahoji wahudumu wanne ambao wamemtumikia Yehova kwa muda mrefu. Arthur Bonno amekuwa katika utumishi wa wakati wote kwa miaka 51 na sasa anatumikia katika Halmashauri ya Ofisi ya Tawi ya Ekuado. Angelo Catanzaro amekuwa katika utumishi wa wakati wote kwa miaka 59, mingi ya miaka hiyo akiwa mwangalizi wa mzunguko. Richard Abrahamson alifuzu kutoka Shule ya Gileadi mnamo mwaka wa 1953, na akawa na pendeleo la kusimamia kazi ya kuhubiri huko Denmark kwa miaka 26 kabla ya kurudi Betheli ya Brooklyn. Hatimaye, wote walifurahi kumsikiliza Carey W. Barber mwenye umri wa miaka 96. Ndugu Barber alibatizwa mwaka wa 1921, naye amekuwa katika utumishi wa wakati wote kwa miaka 78. Ametumikia akiwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza tangu mwaka wa 1978.

Hotuba Zenye Kusisimua

Mkutano wa kila mwaka ulitia ndani hotuba zenye kuamsha fikira. Ndugu Robert W. Wallen alitoa hotuba yenye kichwa “Watu kwa Ajili ya Jina Lake.” Sisi tunaitwa kwa jina la Mungu na tunapatikana katika nchi zaidi ya 230. Yehova ametupatia “wakati ujao na tumaini.” (Yeremia 29:11, NW) Ni lazima tuendelee kutangaza Ufalme wa Mungu, na kuwaeleza wengine ujumbe mzuri wenye kufariji. (Isaya 61:1) Ndugu Wallen alimalizia kwa kusema: “Na tuendelee kila siku kuishi kulingana na jina letu, Mashahidi wa Yehova.”—Isaya 43:10.

Sehemu ya mwisho ya programu ilikuwa na mfululizo uliotolewa na washiriki watatu wa Baraza Linaloongoza. Mfululizo huo ulikuwa na kichwa “Huu Ndio Wakati wa Kukaa Macho, Kusimama Imara, na Kukua Katika Uweza.”—1 Wakorintho 16:13.

Kwanza, Ndugu Stephen Lett alizungumzia kichwa “Kaeni Macho Wakati Huu wa Mwisho.” Ndugu Lett alieleza kwamba usingizi ni zawadi. Huo hutupatia nguvu. Hata hivyo, usingizi wa kiroho hauna faida yoyote. (1 Wathesalonike 5:6) Basi, tunawezaje kuendelea kuwa macho kiroho? Ndugu Lett alizungumzia “vidonge” vitatu vya kiroho: (1) Kuwa na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana. (1 Wakorintho 15:58) (2) Ona uhitaji wako wa kiroho. (Mathayo 5:3) (3) Kubali shauri la Biblia ili utende kwa hekima.—Mithali 13:20.

Ndugu Theodore Jaracz alitoa hotuba yenye kusisimua yenye kichwa “Simama Imara Chini ya Jaribu.” Akirejezea andiko la Ufunuo 3:10, Ndugu Jaracz aliuliza: “Ni nini ‘ile saa ya jaribu’?” Jaribu hilo linakuja “katika siku ya Bwana,” wakati huu tunamoishi. (Ufunuo 1:10) Jaribu hilo linahusu suala hili muhimu—je, tunatetea Ufalme wa Mungu unaotawala au tunatetea mfumo mwovu wa mambo wa Shetani? Kabla ya ile saa ya jaribu kumalizika, tutapatwa na majaribu au magumu. Je, tutabaki tukiwa waaminifu-washikamanifu kwa Yehova na tengenezo lake? ‘Ni lazima kila mmoja wetu aonyeshe uaminifu-mshikamanifu,’ akasema Ndugu Jaracz.

Kwa kumalizia, Ndugu John E. Barr alitoa hotuba yenye kichwa “Kua Katika Uweza Ukiwa Mtu wa Kiroho.” Akirejezea andiko la Luka 13:23-25, alisema kwamba ni lazima tujikakamue ‘ili tuingie ndani kupitia mlango mwembamba.’ Wengi wanashindwa kwa sababu hawajitahidi kukua katika uweza. Ili tuwe Wakristo walio watu wazima, ni lazima tujifunze kutumia kanuni za Biblia katika kila sehemu ya maisha yetu. Ndugu Barr alihimiza hivi: “Nina hakika mtakubaliana nami kwamba huu ni wakati wa (1) kumtanguliza Yehova; (2) kukua katika uweza, na (3) kujikakamua kufanya mapenzi ya Yehova.” Kwa njia hiyo tutaweza kupitia mlango mwembamba unaoongoza kwenye maisha mazuri yasiyo na mwisho.”

Mkutano wa kila mwaka ulipokaribia kumalizika, kuna swali moja ambalo halikuwa limejibiwa: Andiko la mwaka wa utumishi wa 2002 ni lipi? Swali hilo lilijibiwa siku iliyofuata.

Mkutano wa Ziada

Mengi yalitarajiwa siku ya Jumapili asubuhi wakati mkutano wa ziada ulipoanza. Programu ilianza kwa muhtasari wa Mnara wa Mlinzi wa juma hilo, ukifuatiwa na mambo makuu ya mkutano wa kila mwaka. Kisha wote walifurahi kusikiliza hotuba iliyotegemea andiko la mwaka wa 2002: “Njoni kwangu, . . . nami hakika nitawaburudisha nyinyi.” (Mathayo 11:28) Msingi wa hotuba hiyo ulikuwa makala ya funzo la Mnara wa Mlinzi ambayo baadaye ilichapishwa kwenye toleo la Desemba 15, 2001.

Baadaye, baadhi ya wajumbe waliohudhuria Makusanyiko ya pekee ya “Walimu wa Neno la Mungu” huko Ufaransa na Italia mnamo Agosti 2001 walitoa masimulizi yao. * Hatimaye, programu ya siku hiyo ilifikia kilele kwa hotuba mbili za mwisho zilizotolewa na wasemaji waliozuru kutoka Betheli ya Brooklyn.

Hotuba ya kwanza ilikuwa na kichwa “Kumtumaini Yehova kwa Ujasiri Wakati Huu wa Hatari.” Msemaji alizungumzia mambo makuu yafuatayo: (1) Sikuzote watu wa Mungu wameona umuhimu wa kumtumaini Yehova kwa ujasiri. Biblia ina mifano mingi ya watu walioonyesha ujasiri na imani wajapokabiliana na upinzani. (Waebrania 11:1–12:3) (2) Yehova hutuandalia msingi imara wa kumtumaini kabisa. Kazi zake na Neno lake hutuhakikishia kwamba anawajali watumishi wake na kwamba hatawasahau kamwe. (Waebrania 6:10) (3) Ujasiri na imani yahitajiwa hasa wakati huu. Sisi ni “vitu vya kuchukiwa,” kama Yesu alivyotabiri. (Mathayo 24:9) Ili tuvumilie, tunahitaji kutegemea Neno la Mungu, tukiwa na uhakika kwamba roho yake iko pamoja nasi tunapoendelea kutangaza habari njema kwa ujasiri. (4) Mifano iliyopo inaonyesha kwamba tunakabiliana na upinzani sasa. Wasikilizaji waliguswa moyo waliposikia msemaji akisimulia mambo ambayo ndugu zetu wamevumilia huko Armenia, Georgia, Kazakhstan, Turkmenistan, Ufaransa, na Urusi. Bila shaka huu ndio wakati wa kuonyesha ujasiri na kumtumaini Yehova!

Msemaji wa mwisho alizungumzia hotuba yenye kichwa “Kusonga Mbele kwa Umoja Pamoja na Tengenezo la Yehova.” Hotuba hiyo ilizungumzia mambo kadhaa kwa wakati ufaao. (1) Ongezeko la watu wa Yehova linaonekana kila mahali. Kazi yetu ya kuhubiri na makusanyiko yetu huwavutia wengi. (2) Yehova amefanyiza tengenezo lenye umoja. Yesu alitiwa mafuta kwa roho takatifu katika mwaka wa 29 W.K., ili ‘akusanye vitu vyote’—wale walio na tumaini la kuishi mbinguni na walio na tumaini la kuishi duniani—kwa familia ya Mungu yenye umoja. (Waefeso 1:8-10) (3) Makusanyiko ni njia ya pekee ya kuonyesha umoja wetu wa kimataifa. Haya yalionekana wazi katika makusanyiko ya pekee yaliyofanywa huko Ufaransa na Italia mwezi wa Agosti mwaka jana. (4) Azimio lenye kusisimua lilikubaliwa huko Ufaransa na Italia. Msemaji alisimulia mambo machache kutoka kwa azimio hilo lenye kusisimua.

Mwishoni mwa hotuba ya kumalizia, msemaji alisoma tangazo lenye kugusa moyo kutoka kwa Baraza Linaloongoza. Tangazo hilo lilisema hivi kwa sehemu: “Sasa ndio wakati wa kukaa macho na kuendelea kulinda, tutambuapo jinsi matukio ya ulimwengu yanavyotimizwa. . . . Tungependa kuwajulisha kwamba Baraza Linaloongoza linawahangaikia nyinyi na watu wote wa Mungu kwa upendo. Yehova na awabariki sana mwendeleapo kufanya mapenzi yake kwa moyo wote.” Kila mahali watu wa Yehova wameazimia kukaa macho katika nyakati hizi za hatari na kuendelea kusonga mbele kijasiri pamoja na tengenezo la Yehova lenye umoja.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Programu ya mkutano wa kila mwaka ilisikilizwa kupitia simu katika sehemu kadhaa, kukiwa na jumla ya wahudhuriaji 13,757.

^ fu. 5 Mikutano ya ziada ilifanywa huko Long Beach, California; Pontiac, Michigan; Uniondale, New York; na Hamilton, Ontario. Watu 117,885 walihudhuria, kutia ndani waliosikiliza katika sehemu nyingine kupitia simu.

^ fu. 23 Makusanyiko matatu ya pekee yalifanywa Ufaransa—huko Paris, Bordeaux, na Lyons. Huko Italia, wajumbe kutoka Marekani walihudhuria kusanyiko huko Rome na Milan, ijapokuwa kulikuwa na jumla ya makusanyiko tisa yaliyofanywa wakati huohuo.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 29-31]

Azimio

Mnamo Agosti mwaka wa 2001, Makusanyiko ya pekee ya “Walimu wa Neno la Mungu” yalifanywa huko Ufaransa na Italia. Azimio lenye kusisimua lilipitishwa katika makusanyiko hayo. Yafuatayo ni maneno ya azimio hilo.

“SOTE tuliokusanyika hapa, tukiwa Mashahidi wa Yehova, kwenye Kusanyiko la ‘Walimu wa Neno la Mungu,’ tumefundishwa kwa njia yenye kunufaisha sana. Twajua chanzo cha fundisho hilo. Si cha kibinadamu. Fundisho hilo linatoka kwa Yule anayetajwa na nabii Isaya kuwa ‘Mfunzi wetu Mtukufu.’ (Isaya 30:20, NW) Ona kikumbusho cha Yehova katika Isaya 48:17: ‘Mimi ni BWANA, Mungu wako, nikufundishaye ili upate faida, nikuongozaye kwa njia ikupasayo kuifuata.’ Yeye anatimizaje hilo? Njia kuu zaidi ni kupitia Biblia, kitabu kinachotafsiriwa na kusambazwa sana ulimwenguni, kinachotuambia waziwazi hivi: ‘Andiko lote limepuliziwa na Mungu na ni lenye manufaa.’—2 Timotheo 3:16.

“Wakati huu wanadamu wanahitaji sana fundisho hilo lenye kunufaisha. Kwa nini twasema hivyo? Watu wenye utambuzi huitikiaje wanapoona mambo yanayobadilika-badilika na yenye kutatanisha ya ulimwengu huu? Ijapokuwa watu wengi wamefundishwa katika shule za kilimwengu, kuna hali yenye kusikitisha ya ukosefu wa kanuni bora na kukosa kutofautisha mema na mabaya. (Isaya 5:20, 21) Watu wamekosa kuijua Biblia. Wajapoandaliwa habari nyingi kupitia kompyuta, je, wanadamu wamepata majibu kwa maswali kama vile, Ni nini kusudi la uhai? Tuyaeleweje matukio ya wakati wetu? Je, kuna sababu ya msingi ya kuwa na tumaini la wakati ujao? Je, inawezekana kuwa na amani na usalama wa kweli? Zaidi ya hayo, katika maktaba nyingi kuna vitabu vingi sana vya marejeo vinavyozungumzia jitihada mbalimbali za wanadamu. Hata hivyo, wanadamu bado wanarudia makosa yaleyale ya wakati uliopita. Uhalifu unazidi kuongezeka. Magonjwa yaliyodhaniwa kuwa yalimalizwa, yanarudi tena, na mengine kama UKIMWI yanaenea sana kwa njia yenye kutisha. Familia nyingi sana zinavunjika. Mazingira yanaharibiwa na uchafuzi wa hewa. Ugaidi pamoja na silaha zenye kusababisha uharibifu mkubwa sana zinatisha amani na usalama. Matatizo yasiyoweza kutatuliwa yanazidi kurundamana. Tuna daraka gani la kuwasaidia wanadamu wenzetu katika siku hizi zenye hatari? Je, kuna fundisho linaloonyesha kwa nini wanadamu wana matatizo, jinsi ya kuwa na maisha bora sasa na pia linaloandaa tumaini zuri hakika la wakati ujao?

“Maandiko yanatuamuru hivi, ‘Nendeni mkafanye wanafunzi kwa watu wa mataifa yote, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo Kristo aliamuru.’ (Mathayo 28:19, 20) Kazi hiyo iliamriwa na Yesu Kristo baada ya kufa na kufufuliwa, alipopokea mamlaka yote mbinguni na duniani. Kazi hii inapita kazi zote zinazofanywa na wanadamu. Kulingana na maoni ya Mungu, tunapaswa kutanguliza kazi hii ambayo inakazia mahitaji ya kiroho ya watu wanaoona njaa ya uadilifu. Tuna sababu nzuri za Kimaandiko zinazofanya tuchukue kazi hii kwa uzito.

“Hiyo inataka tutangulize kazi hii maishani. Tukiwa na baraka na msaada wa Mungu, tutafanya kazi hii kujapokuwa vikengeusha fikira vingi, vizuizi na upinzani kutoka kwa matengenezo ya kidini na kisiasa yanayokusudia kuzuia kazi hii ya ufundishaji inayofanywa ulimwenguni pote. Tuna uhakika na tunaamini kwamba kazi hii itaendelea kufanikiwa hata kufikia upeo wake mtukufu. Kwa nini tuna uhakika huo? Kwa sababu Bwana Yesu Kristo aliahidi kwamba atakuwa pamoja nasi katika huduma hii tuliyopewa na Mungu hadi umalizio wa mfumo wa mambo.

“Kuteseka kwa wanadamu kunakaribia kwisha. Kazi tuliyo nayo sasa lazima itimizwe kabla ya mwisho kuja. Kwa hivyo, tukiwa Mashahidi wa Yehova tunaazimia kwamba:

“Kwanza: Tukiwa wahudumu waliojiweka wakfu, tumeazimia kutanguliza masilahi ya Ufalme katika maisha yetu na kuendelea kukua kiroho. Kwa hiyo, sala yetu inapatana na maneno ya Zaburi 143:10: ‘Unifundishe kuyatenda mapenzi yako, kwa maana ndiwe Mungu wangu.’ Ili kufundishwa naye, tunahitaji kuwa wanafunzi wenye bidii, tukijitahidi kusoma Biblia kila siku, kuwa na funzo la binafsi na kufanya utafiti. Ili maendeleo yetu yaonekane kwa watu wote, tutajitahidi sana kutayarisha na kufaidika kabisa kutokana na elimu ya kitheokrasi inayoandaliwa kwenye mikutano ya kutaniko, makusanyiko ya mzunguko, wilaya, kitaifa, na kimataifa.—1 Timotheo 4:15; Waebrania 10:23-25.

“Pili: Ili tufundishwe na Mungu, tutakula tu katika meza yake na kutii kwa makini maonyo ya Biblia kuhusiana na mafundisho ya roho waovu yenye kupotosha. (1 Wakorintho 10:21; 1 Timotheo 4:1) Tutakuwa waangalifu ili kuepuka mambo yanayodhuru yanayotia ndani uwongo wa kidini, mawazo yenye ubatili, mwenendo wenye kuaibisha kingono, ponografia iliyoenea sana, vitumbuizo vyenye kushusha heshima na mambo yote ‘yasiyokubaliana na maneno yenye afya.’ (Waroma 1:26, 27; 1 Wakorintho 3:20; 1 Timotheo 6:3; 2 Timotheo 1:13) Kwa kuheshimu ‘zawadi katika wanaume,’ wanaostahili kufundisha lililo jema, tutathamini kabisa jitihada zao na kushirikiana nao kwa moyo wote katika kudumisha viwango safi, vya adili, na vya kiroho vya Neno la Mungu.—Waefeso 4:7, 8, 11, 12; 1 Wathesalonike 5:12, 13; Tito 1:9.

“Tatu: Tukiwa wazazi Wakristo, tutajitahidi kwa moyo wote kuwafundisha watoto wetu si katika neno tu bali pia kwa kielelezo. Hangaiko letu kuu ni kuwasaidia tangu utotoni ‘wajifunze maandishi matakatifu ili wawe wenye hekima kwa ajili ya wokovu.’ (2 Timotheo 3:15) Tutakumbuka kwamba tukiwalea katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova watakuwa na fursa ya kufurahia ahadi ya Mungu kwamba ‘itakuwa vema kwao nao watapata kudumu muda mrefu juu ya dunia.’—Waefeso 6:1-4.

“Nne: Iwapo tutapatwa na mahangaiko au matatizo yoyote, kwanza kabisa, ‘tutamjulisha Mungu maombi yetu ya bidii,’ tukiwa na uhakika kwamba ‘amani ya Mungu izidiyo fikira yote ya binadamu kwa ubora,’ itatulinda. (Wafilipi 4:6, 7) Kwa kuwa tuko chini ya nira ya Kristo, tutaburudishwa. Hatutasita kumtupia Mungu mahangaiko yetu, kwani twajua anatujali.—Mathayo 11:28-30; 1 Petro 5:6, 7.

“Tano: Ili kuonyesha shukrani zetu kwa Yehova kwa pendeleo la kuwa walimu wa Neno lake, tutajitahidi sana ili ‘tulitumie sawasawa neno la ile kweli’ na ‘kutimiza kikamili huduma yetu.’ (2 Timotheo 2:15; 4:5) Kwa sababu tunajua yanayohusika, tamaa yetu ya kutoka moyoni ni kutafuta wale wanaostahili na kupalilia mbegu iliyopandwa ndani yao. Zaidi ya hayo, tutaboresha ufundishaji wetu kwa kuongoza mafunzo ya Biblia ya nyumbani kwa mafanikio zaidi. Kufanya hivyo kutatupatanisha na mapenzi ya Mungu kwamba ‘watu wa namna zote waokolewe na kuja kwenye ujuzi sahihi wa kweli.’—1 Timotheo 2:3, 4.

“Sita: Mashahidi wa Yehova wamekabiliana na aina mbalimbali ya minyanyaso na upinzani katika nchi nyingi katika karne iliyopita na karne hii. Lakini Yehova amethibitika kuwa pamoja nasi. (Waroma 8:31) Neno lake lenye kutegemeka latuhakikishia kwamba hakuna ‘silaha itakayofanyika juu yetu’ ambayo itafanikiwa kutuzuia, kuturudisha nyuma, au kutufanya tuache kazi yetu ya kuhubiri na kufundisha kuhusu Ufalme. (Isaya 54:17) Iwe ni wakati ufaao au usiofaa, hatuwezi kamwe kuacha kusema ile kweli. Azimio letu ni kufanya kazi yetu ya kuhubiri na kufundisha kwa uharaka. (2 Timotheo 4:1, 2) Lengo letu ni kuwahubiria kikamili iwezekanavyo watu wa mataifa yote habari njema za Ufalme wa Mungu. Hivyo, wataendelea kujifunza mambo wanayohitaji kufanya ili kupata uhai wa milele katika ulimwengu mpya wenye uadilifu. Tukiwa umati wenye umoja wa walimu wa Neno la Mungu, azimio letu ni kuendelea kufuata kielelezo cha Mwalimu wetu Mkuu, Yesu Kristo, na kuiga sifa zake za kimungu. Tukifanya hivyo, tutamletea heshima na utukufu Mfunzi wetu Mtukufu na Mpaji-Uhai wetu, Yehova Mungu.

“Wote walio katika kusanyiko hili wanaokubaliana na azimio hili, tafadhali semeni NDIYO!”

Wakati wahudhuriaji 160,000 katika makusanyiko matatu huko Ufaransa na 289,000 katika sehemu tisa huko Italia walipoulizwa swali la mwisho la azimio hilo, walijibu kwa sauti kubwa “Ndiyo” katika lugha nyingi zilizowakilishwa na wajumbe wa kusanyiko hilo.