Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Ubatizwe?

Kwa Nini Ubatizwe?

Kwa Nini Ubatizwe?

“Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza.”—MATHAYO 28:19.

1, 2. (a) Ubatizo fulani umefanywa chini ya hali gani? (b) Ni maswali gani yanayozuka kuhusu ubatizo?

CHARLEMAGNE, Mfalme wa kabila la Frank aliwalazimisha Wasaxon wote walioshindwa wabatizwe katika mwaka wa 775-777 W.K. “Aliwalazimisha wabadili imani yao na kuwa Wakristo wa jina tu,” akaandika mwanahistoria John Lord. Vivyo hivyo, baada ya kumwoa binti-mfalme wa Kanisa la Othodoksi la Ugiriki mnamo mwaka wa 987 W.K. kiongozi wa Urusi Vladimir wa Kwanza aliamua raia zake wawe “Wakristo.” Aliamuru raia zake wabatizwe, akitisha kuwaua wale ambao wangekataa!

2 Je, ubatizo huo ulifaa? Una maana yoyote? Je, mtu yeyote tu anapaswa kubatizwa?

Ubatizo—Jinsi Gani?

3, 4. Kwa nini kunyunyizia watu maji au kuwamwagia maji kichwani si ubatizo unaofaa wa Kikristo?

3 Mfalme Charlemagne na Vladimir wa Kwanza walitenda kinyume cha Neno la Mungu walipowalazimisha watu wabatizwe. Kwa kweli, haifai kuwabatiza watu kwa kuwanyunyizia maji, kuwamwagia maji kichwani, au hata kuwazamisha ikiwa watu hao hawajafundishwa kweli za Biblia.

4 Fikiria kilichotukia wakati Yesu wa Nazareti alipomfikia Yohana Mbatizaji katika mwaka wa 29 W.K. Yohana alikuwa akibatiza watu katika Mto Yordani. Walikuwa wamejitolea kubatizwa. Je, aliwasimamisha katika Mto Yordani na kuwamwagia maji kidogo vichwani au kuwanyunyizia maji tu? Ni nini kilichotokea Yohana alipombatiza Yesu? Mathayo aripoti kwamba baada ya kubatizwa ‘mara Yesu alipanda kutoka katika maji.’ (Mathayo 3:16) Alikuwa chini ya maji, baada ya kuzamishwa katika Mto Yordani. Hali kadhalika, towashi Mwethiopia alibatizwa katika “maji fulani.” Maji hayo yalihitajiwa kwa kuwa Yesu na wanafunzi wake walibatizwa kwa kuzamishwa kabisa katika maji.—Matendo 8:36.

5. Wakristo wa mapema walibatiza watu jinsi gani?

5 Maneno ya Kigiriki yanayotafsiriwa “batiza,” “ubatizo,” na kadhalika, hurejezea kuzamisha au kutumbukiza ndani ya maji. Kichapo Smith’s Bible Dictionary chasema: “Kwa kufaa na kihalisi, ubatizo humaanisha kuzamisha.” Kwa hiyo, tafsiri fulani za Biblia humwita “Yohana Mzamishaji” au “Yohana mtumbukizaji.” (Mathayo 3:1, Rotherham; Diaglott, yenye tafsiri katikati ya mistari) Kichapo cha Augustus Neander, History of the Christian Religion and Church, During the Three First Centuries chasema: “Hapo awali ubatizo ulifanywa kwa kuzamisha watu katika maji.” Kichapo maarufu cha Kifaransa Larousse du XXe Siècle (Paris, 1928) chasema: “Wakristo wa mapema walibatizwa kwa kuzamishwa katika maji mahali popote palipokuwa na maji.” Nacho kichapo New Catholic Encyclopedia chasema: “Ni wazi kwamba Ubatizo uliofanywa katika Kanisa la mapema ulikuwa wa kuzamisha watu katika maji.” (1967, Buku la pili, ukurasa wa 56) Kwa hiyo leo, watu hubatizwa kwa kuzamishwa kabisa katika maji na kuwa Mashahidi wa Yehova kwa hiari yao wenyewe.

Sababu Mpya ya Kubatizwa

6, 7. (a) Yohana alibatiza watu kwa kusudi gani? (b) Ubatizo wa wafuasi wa Yesu ulihusisha hatua gani mpya?

6 Ubatizo uliofanywa na Yohana ulikuwa na kusudi tofauti na ubatizo uliofanywa na wafuasi wa Yesu. (Yohana 4:1, 2) Yohana alibatiza watu waliotaka kuonyesha wazi kwamba wametubu dhambi walizotenda dhidi ya Sheria. * (Luka 3:3) Lakini ubatizo wa wafuasi wa Yesu ulihusisha jambo fulani jipya. Katika Pentekoste 33 W.K., mtume Petro aliwahimiza hivi wasikilizaji wake: “Tubuni, na acheni kila mmoja wenu abatizwe katika jina la Yesu Kristo kwa msamaha wa dhambi zenu.” (Matendo 2:37-41) Ingawa alikuwa akizungumza na Wayahudi na wageuzwa-imani, Petro hakuwa akizungumza kuhusu ubatizo wa kuonyesha toba ya dhambi zilizofanywa dhidi ya Sheria; wala hakumaanisha kwamba kubatizwa katika jina la Yesu kunaonyesha kuondolea mbali dhambi.—Matendo 2:10.

7 Wakati huo, Petro alitumia ‘ufunguo wa kwanza wa ufalme.’ Kwa kusudi gani? Ili kuwajulisha wasikilizaji wake kwamba walikuwa na fursa ya kuingia katika Ufalme wa mbinguni. (Mathayo 16:19) Kwa kuwa Wayahudi walikuwa wamemkataa Yesu kuwa Mesiya, walihitaji kutubu na kuonyesha imani katika Yesu. Hatua hiyo mpya na muhimu ilihitajika ili waweze kupokea msamaha wa Mungu. Wangeweza kudhihirisha imani hiyo hadharani kwa kuzamishwa katika maji katika jina la Yesu Kristo. Kwa kufanya hivyo wangeonyesha wakfu wao kwa Mungu kupitia Kristo. Wote wanaotaka kupata kibali cha Mungu leo lazima wadhihirishe imani kama hiyo, wajiweke wakfu kwa Yehova Mungu, na kubatizwa ubatizo wa Kikristo ili kuonyesha kwamba wamejiweka wakfu kwa Mungu Aliye Juu Zaidi kwa hiari.

Ujuzi Sahihi Ni Muhimu

8. Kwa nini si kila mtu anayestahili ubatizo wa Kikristo?

8 Si kila mtu anayestahili ubatizo wa Kikristo. Yesu aliwaamuru wafuasi wake hivi: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, kuwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, kuwafundisha kushika mambo yote ambayo mimi nimewaamuru nyinyi.” (Mathayo 28:19, 20) Kabla ya kubatizwa, watu wanapaswa ‘kufundishwa kushika mambo yote ambayo Yesu aliwaamuru wanafunzi wake.’ Kwa hiyo, haifai kulazimisha watu wasio na imani inayotegemea ujuzi sahihi wa Neno la Mungu wabatizwe na pia ni kinyume cha maagizo ambayo Yesu aliwapa wafuasi wake wa kweli.—Waebrania 11:6.

9. Inamaanisha nini kubatizwa “katika jina la Baba”?

9 Inamaanisha nini kubatizwa “katika jina la Baba”? Inamaanisha kwamba mtu anayetaka kubatizwa anatambua cheo na mamlaka ya Baba yetu wa kimbingu. Kwa hiyo, anamtambua Yehova Mungu kuwa Muumba wetu, ‘Aliye juu, juu ya nchi yote,’ na Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu.—Zaburi 83:18; Isaya 40:28; Matendo 4:24.

10. Inamaanisha nini kubatizwa ‘katika jina la Mwana’?

10 Kubatizwa ‘katika jina la Mwana’ kunamaanisha kutambua cheo na mamlaka ya Yesu ambaye ni Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu. (1 Yohana 4:9) Wale wanaostahili kubatizwa humkubali Yesu kuwa yule ambaye kupitia kwake Mungu ameandaa “fidia katika kubadilishana kwa ajili ya wengi.” (Mathayo 20:28; 1 Timotheo 2:5, 6) Pia wanaotaka kubatizwa lazima watambue “cheo cha juu zaidi” ambacho Mungu amempa Mwanaye.—Wafilipi 2:8-11; Ufunuo 19:16.

11. Ni nini kinachomaanishwa na kubatizwa ‘katika jina la roho takatifu’?

11 Kubatizwa ‘katika jina la roho takatifu’ kunamaanisha nini? Kunamaanisha kwamba wanaotaka kubatizwa wanatambua kwamba roho takatifu ni nguvu ya utendaji ya Yehova, inayotumiwa kwa njia mbalimbali kupatana na kusudi lake. (Mwanzo 1:2; 2 Samweli 23:1, 2; 2 Petro 1:21) Wale wanaostahili kubatizwa hutambua kwamba roho takatifu huwasaidia kuelewa “mambo yenye kina kirefu ya Mungu,” kuendelea na kazi ya kuhubiri juu ya Ufalme, na kudhihirisha matunda ya roho ambayo ni “upendo, shangwe, amani, ustahimilivu, fadhili, wema, imani, upole, kujidhibiti.”—1 Wakorintho 2:10; Wagalatia 5:22, 23; Yoeli 2:28, 29.

Umuhimu wa Toba na Kugeuka

12. Ubatizo wa Kikristo unahusianaje na toba?

12 Isipokuwa kisa cha Yesu ambaye hakuwa na dhambi, ubatizo ni ishara ya peupe inayokubaliwa na Mungu kuonyesha kwamba mtu ametubu. Tunapotubu, tunajuta sana kuhusu jambo fulani tulilofanya au tulilokosa kufanya. Wayahudi wa karne ya kwanza waliotaka kumpendeza Mungu walilazimika kutubu dhambi zao dhidi ya Kristo. (Matendo 3:11-19) Waumini fulani wasio Wayahudi huko Korintho walitubu dhambi ya uasherati, ibada ya sanamu, wizi, na dhambi nyingine nzito. Kwa sababu ya toba yao, ‘walioshwa wakawa safi’ katika damu ya Yesu; ‘wakatakaswa,’ au kutengwa kwa ajili ya utumishi wa Mungu; na ‘kutangazwa kuwa waadilifu’ katika jina la Kristo na roho ya Mungu. (1 Wakorintho 6:9-11) Toba ni hatua muhimu ya kupata dhamiri safi na kitulizo kutoka kwa Mungu kutokana na hatia ya dhambi.—1 Petro 3:21.

13. Kugeuka kunahusianaje na ubatizo?

13 Lazima tugeuke kwanza kabla ya kubatizwa na kuwa Mashahidi wa Yehova. Kugeuka ni hatua ya hiari inayofanywa na mtu ambaye ameamua kwa moyo wote kuwa mfuasi wa Kristo Yesu. Watu hao huacha mwenendo wao mbaya wa zamani na kuazimia kufanya mambo yanayofaa machoni pa Mungu. Katika Maandiko, kitenzi cha Kiebrania na Kigiriki kinachohusiana na neno kugeuka humaanisha kurejea. Hatua hiyo yahusisha kumgeukia Mungu na kuacha njia isiyofaa. (1 Wafalme 8:33, 34) Kugeuka kwataka “kazi zinazofaa toba.” (Matendo 26:20) Kwataka tuache ibada isiyo ya kweli, tuishi kupatana na amri za Mungu, na kumpa Yehova ujitoaji usiohusisha wengine. (Kumbukumbu la Torati 30:2, 8-10; 1 Samweli 7:3) Kugeuka hutokeza mabadiliko katika kufikiri kwetu, miradi yetu, na nyutu zetu. (Ezekieli 18:31) ‘Tunageuka kabisa’ kwa kuacha mwenendo mwovu na kuvaa utu mpya.—Matendo 3:19; Waefeso 4:20-24; Wakolosai 3:5-14.

Ni Muhimu Kujitoa kwa Moyo Wote

14. Wakfu wa wafuasi wa Yesu humaanisha nini?

14 Kabla mfuasi wa Yesu hajabatizwa lazima ajiweke wakfu kwa moyo wote kwa Mungu. Kuweka wakfu humaanisha kutenga kitu kwa kusudi takatifu. Hatua hii ni muhimu sana hivi kwamba tunapaswa kusali kwa Yehova na kumweleza uamuzi wetu wa kumpa ujitoaji usiohusisha wengine milele. (Kumbukumbu la Torati 5:9) Bila shaka, hatujiweki wakfu kwa mwanadamu au kwa ajili ya kazi fulani, bali sisi hujiweka wakfu kwa Mungu.

15. Kwa nini wanaotaka kubatizwa huzamishwa katika maji?

15 Tunapojiweka wakfu kwa Mungu kupitia Kristo, tunadhihirisha azimio letu la kutumia maisha yetu kufanya mapenzi ya Mungu kama yanavyoonyeshwa katika Maandiko. Wanaotaka kubatizwa huonyesha wakfu wao kwa kubatizwa katika maji, kama vile Yesu alivyobatizwa katika Mto Yordani kuonyesha kwamba amejitoa kwa Mungu. (Mathayo 3:13) Twapasa kutambua kwamba Yesu alikuwa akisali wakati huo muhimu.—Luka 3:21, 22.

16. Tunaweza kuonyeshaje shangwe yetu kwa njia inayofaa tunapoona watu wakibatizwa?

16 Mbali na kuwa tukio muhimu sana, ubatizo wa Yesu ulileta shangwe nyingi. Ndivyo ilivyo na ubatizo wa Kikristo leo. Tunapoona watu wakionyesha wakfu wao kwa Mungu, twaweza kuonyesha shangwe yetu kwa kupiga makofi na kutoa pongezi changamfu kwa heshima. Lakini hatushangilii kwa vigelegele au kupiga mbinja, kwa kuwa tunaheshimu tukio hilo takatifu la kudhihirisha imani. Tunaonyesha shangwe yetu kwa njia ya heshima.

17, 18. Ni nini kinachosaidia kuamua kama mtu anastahili kubatizwa?

17 Tofauti na watu ambao huwanyunyizia maji watoto wachanga, au kulazimisha watu wasio na ujuzi wa Biblia wabatizwe, Mashahidi wa Yehova hawalazimishi mtu yeyote kamwe abatizwe. Hata hawabatizi watu wasiostahili kiroho. Hata kabla mtu hajawa mhubiri asiyebatizwa wa habari njema, wazee Wakristo huhakikisha kwamba anaelewa mafundisho ya msingi ya Biblia, anaishi kupatana nayo, naye hujibu ndiyo kwa swali kama vile, “Je, kwa kweli unataka kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova?”

18 Mara nyingi, watu ambao wameshiriki vya kutosha kuhubiri kuhusu Ufalme wanaposema kwamba wanataka kubatizwa, wazee Wakristo huwa na mazungumzo pamoja nao ili kuhakikisha kwamba wao ni waamini ambao wamejiweka wakfu kwa Yehova na wanatimiza matakwa yake kuhusu ubatizo. (Matendo 4:4; 18:8) Majibu wanayotoa kwa maswali 100 kuhusu mafundisho ya Biblia husaidia wazee kujua iwapo wale wanaojibu wanatimiza matakwa ya Kimaandiko kuhusu ubatizo. Wengine hukosa kustahili na hivyo hawakubaliwi kubatizwa wawe Wakristo.

Je, Kuna Jambo Linalokuzuia?

19. Kwa kuzingatia andiko la Yohana 6:44, ni nani watakaotawala pamoja na Yesu?

19 Watu wengi waliolazimishwa kubatizwa huenda waliambiwa kwamba wakifa wataenda mbinguni. Lakini akirejezea wafuasi wake, Yesu alisema: “Hakuna mtu awezaye kuja kwangu isipokuwa Baba, aliyenituma, amvute yeye.” (Yohana 6:44) Yehova amevuta kwa Kristo watu 144,000 watakaotawala pamoja na Yesu katika Ufalme wa mbinguni. Ubatizo wa kulazimishwa haujawahi kumtakasa mtu yeyote kuwa mshiriki wa mpango huo mtukufu wa Mungu.—Waroma 8:14-17; 2 Wathesalonike 2:13; Ufunuo 14:1.

20. Ni nini kinachoweza kuwasaidia watu fulani ambao bado hawajabatizwa?

20 Tangu katikati ya miaka ya 1930 hasa, umati wa watu wanaotumaini kuokoka “dhiki kubwa” na kuishi duniani milele wamejiunga na “kondoo wengine” wa Yesu. (Ufunuo 7:9, 14; Yohana 10:16) Wanastahili kubatizwa kwa sababu wanaishi kupatana na Neno la Mungu na wanampenda kwa ‘moyo wao wote, nafsi, nguvu, na akili.’ (Luka 10:25-28) Ingawa watu fulani wanatambua kwamba Mashahidi wa Yehova ‘huabudu Mungu katika roho na kweli,’ bado hawafuati kielelezo cha Yesu kwa kuonyesha hadharani upendo wao wa kweli na kumpa Yehova ujitoaji usiohusisha wengine kwa kubatizwa. (Yohana 4:23, 24; Kumbukumbu la Torati 4:24; Marko 1:9-11) Kusali kwa bidii na kutaja mambo waziwazi kuhusu hatua hii muhimu kwaweza kuwapa kichocheo na ujasiri wa kujipatanisha kabisa na Neno la Mungu, na kujiweka wakfu kwa Yehova Mungu kwa hiari na kubatizwa.

21, 22. Kwa nini wengine husitasita kujiweka wakfu na kubatizwa?

21 Watu fulani husitasita kujiweka wakfu na kubatizwa kwa sababu wanajihusisha sana na mambo ya ulimwengu au kufuatia mali hivi kwamba hawana wakati wa kutosha kwa ajili ya mambo ya kiroho. (Mathayo 13:22; 1 Yohana 2:15-17) Wangepata furaha iliyoje iwapo wangebadili maoni na miradi yao! Kumkaribia Yehova kutawatajirisha kiroho, kutawasaidia wasiwe na mahangaiko mengi sana, na kuwapa amani na uradhi unaotokana na kufanya mapenzi ya Mungu.—Zaburi 16:11; 40:8; Mithali 10:22; Wafilipi 4:6, 7.

22 Wengine husema kwamba wanampenda Yehova lakini hawataki kujiweka wakfu na kubatizwa kwa sababu wanafikiri kwamba kwa kutobatizwa hawatatoa hesabu kwa Mungu. Lakini kila mmoja wetu lazima atoe hesabu kwa Mungu. Tunawajibika tunapolisikia neno la Yehova. (Ezekieli 33:7-9; Waroma 14:12) Wakiwa ‘watu waliochaguliwa,’ Waisraeli wa kale walizaliwa katika taifa lililokuwa wakfu kwa Yehova, na kwa hiyo walikuwa na daraka la kumtumikia kwa uaminifu kulingana na maagizo yake. (Kumbukumbu la Torati 7:6, 11) Hakuna mtu anayezaliwa katika taifa kama hilo leo, lakini ikiwa tumepokea mafundisho sahihi ya Kimaandiko, twapaswa kutenda kwa imani.

23, 24. Ni hofu gani isiyopaswa kuzuia watu wasibatizwe?

23 Huenda wengine wakasita kubatizwa kwa sababu ya kuhofu kwamba hawana ujuzi wa kutosha. Hata hivyo, sote tuna mambo mengi ya kujifunza kwa sababu ‘mwanadamu hawezi kuvumbua kazi ya Mungu anayoifanya, tangu mwanzo hata mwisho.’ (Mhubiri 3:11) Fikiria towashi Mwethiopia. Akiwa mgeuzwa-imani, alifahamu Maandiko kwa kadiri fulani, lakini hakufahamu mambo yote kuhusu kusudi la Mungu. Hata hivyo, baada ya kujifunza mpango wa Yehova wa wokovu kupitia dhabihu ya ukombozi ya Yesu, towashi huyo alibatizwa katika maji.—Matendo 8:26-38.

24 Wengine husitasita kujiweka wakfu kwa Mungu kwa sababu wanahofu kwamba hawataweza kuishi kupatana na wakfu wao. Monique, mwenye umri wa miaka 17 asema: “Nimekuwa nikisitasita kubatizwa kwa sababu ya kuhofu kwamba sitaweza kuishi kupatana na wakfu wangu.” Hata hivyo, tukimtumaini Yehova kwa moyo wetu wote, ‘atanyosha mapito yetu.’ Atatusaidia ‘tuendelee kutembea katika kweli’ tukiwa watumishi wake waaminifu waliojiweka wakfu.—Mithali 3:5, 6; 3 Yohana 4.

25. Inafaa tuchunguze swali gani?

25 Kwa sababu ya kumtumaini Yehova kabisa na kumpenda kwa moyo wote, kila mwaka maelfu huchochewa kujiweka wakfu na kubatizwa. Kwa kweli watumishi wote wa Mungu waliojiweka wakfu wanataka kuwa waaminifu kwake. Hata hivyo, tunaishi katika nyakati za hatari, na tunakabili majaribu mbalimbali ya imani. (2 Timotheo 3:1-5) Tunaweza kufanya nini ili kuishi kupatana na wakfu wetu kwa Yehova? Tutachunguza swali hilo katika makala ifuatayo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Kwa kuwa Yesu hakuwa na dhambi, hakubatizwa ili kuonyesha toba. Ubatizo wake ulionyesha kwamba alikuwa amejitoa kwa Mungu kufanya mapenzi ya Baba yake.—Waebrania 7:26; 10:5-10.

Je, Unakumbuka?

• Ubatizo wa Kikristo hufanywaje?

• Mtu anahitaji kuwa na ujuzi gani ili abatizwe?

• Ni hatua gani ambazo huongoza kwenye ubatizo wa Wakristo wa kweli?

• Kwa nini wengine husitasita kubatizwa, lakini wanaweza kusaidiwaje?

[Maswali ya Funzo]

[Maelezo ya Picha katika ukurasa wa 14]

Unajua inamaanisha nini kubatizwa ‘katika jina la Baba, la Mwana, na la roho takatifu’?