Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mungu Hukubali Watu wa Mataifa Yote

Mungu Hukubali Watu wa Mataifa Yote

Mungu Hukubali Watu wa Mataifa Yote

ALIPOSAFIRI nchini Mali kwa mara ya kwanza, John aliguswa moyo na ukarimu alioonyeshwa na Mamadou na familia yake. Alipoketi chini sakafuni akila kutoka sahani moja na mkaribishaji wake, John alijiuliza atampaje mkaribishaji huyo zawadi iliyo kuu kuliko zote—habari njema ya Ufalme kutoka kwa Neno la Mungu, Biblia? Ijapokuwa alijua Kifaransa, lugha inayozungumzwa nchini Mali, John alijiuliza atawasilianaje na familia iliyofuata dini tofauti kabisa na iliyofikiri kwa njia tofauti.

Haishangazi kwamba John alifikiria simulizi la Biblia kuhusu jiji la Babeli. Huko, Mungu alivuruga lugha ya wanadamu waasi. (Mwanzo 11:1-9) Ndiyo sababu leo kuna watu wanaosema lugha tofauti-tofauti, na wanaofuata dini mbalimbali na kufikiri kwa njia tofauti katika sehemu mbalimbali za dunia. Leo, kwa kuwa imekuwa kawaida kusafiri au kuhamia sehemu nyingine, wengi kama vile John hukabili hali ngumu hata mahali wanapoishi: Jinsi ya kuwaeleza watu wa malezi tofauti na yao tumaini lao linalotegemea Biblia.

Kielelezo cha Kale

Kama manabii wengine wa Israeli, Yona alizungumza hasa na Waisraeli. Alitabiri wakati ambapo ufalme wa makabila kumi ulioasi ulifanya waziwazi mambo yenye kumvunjia Mungu heshima. (2 Wafalme 14:23-25) Hebu wazia jinsi Yona alivyohisi alipopokea mgawo huo wa pekee wa kuondoka nchini mwake na kwenda Ashuru kuhubiria wakazi wa Ninewi, waliokuwa na dini na utamaduni tofauti. Yamkini Yona hakujua lugha ya Waninewi na hata kama aliijua, yaelekea hakuizungumza kwa ufasaha. Vyovyote iwavyo, yaonekana Yona aliona mgawo huo kuwa mgumu na hivyo akatoroka.—Yona 1:1-3.

Bila shaka, Yona alipaswa kujua kwamba Yehova Mungu haangalii tu sura bali huchunguza mioyo. (1 Samweli 16:7) Baada ya kumwokoa Yona kimuujiza asife maji, Yehova alimwamuru mara ya pili awahubirie wakazi wa Ninewi. Yona alitii, nao Waninewi wote wakatubu. Hata hivyo, Yona hakuwa na maoni yanayofaa. Kwa kutumia mfano ulioonyesha mambo waziwazi, Yehova alimwonyesha Yona kwamba alipaswa kubadili maoni yake. Yehova alimwuliza Yona hivi: “Je, haikunipasa kuuhurumia Ninawi, mji ule mkubwa; ambamo ndani yake wamo watu zaidi ya mia na ishirini elfu, wasioweza kupambanua katika mkono wao wa kulia na mkono wao wa kushoto?” (Yona 4:5-11) Namna gani sisi leo? Tunaweza kusaidiaje watu wa malezi tofauti?

Kuwapokea Wasamaria na Wasio Wayahudi

Katika karne ya kwanza, Yesu aliwaagiza wafuasi wake wafanye watu wa mataifa yote kuwa wanafunzi. (Mathayo 28:19) Kazi hiyo haikuwa rahisi kwa wanafunzi hao. Wanafunzi wa Yesu walikuwa Wayahudi, na sawa na Yona, walikuwa wamezoea tu kuzungumza na watu wa malezi na utamaduni wa kwao. Bila shaka, wangeathiriwa pia na ubaguzi uliokuwepo wakati huo. Hata hivyo, Yehova alielekeza mambo hivi kwamba watumishi wake walifahamu mapenzi yake hatua kwa hatua.

Hatua ya kwanza ilikuwa kushinda ubaguzi kati ya Wayahudi na Wasamaria. Wayahudi hawakujishughulisha na Wasamaria. Hata hivyo, katika pindi kadhaa Yesu aliwatayarisha Wasamaria ili wapokee habari njema. Alionyesha kwamba hana ubaguzi kwa kuzungumza na mwanamke Msamaria. (Yohana 4:7-26) Katika pindi nyingine, kwa kutumia mfano wa Msamaria mwenye fadhili, alionyesha mwanadini mmoja Myahudi kwamba watu wengine mbali na Wayahudi wangeweza kuonyesha upendo kwa jirani. (Luka 10:25-37) Wakati ulipofika wa Yehova kuwaingiza Wasamaria katika kutaniko la Kikristo, Filipo, Petro, na Yohana waliokuwa Wayahudi, waliwahubiria wakazi wa Samaria. Ujumbe wao ulitokeza shangwe nyingi katika jiji hilo.—Matendo 8:4-8, 14-17.

Ilikuwa vigumu kwa Wakristo Wayahudi kuwapenda Wasamaria, ambao walikuwa watu wao wa ukoo wa mbali. Lazima iwe ilikuwa vigumu hata zaidi kwa Wayahudi kuwaonyesha upendo wa jirani watu wasio Wayahudi, au watu wa Mataifa, waliodharauliwa na kuchukiwa na Wayahudi hao. Hata hivyo, baada ya Yesu kufa, kizuizi kilichokuwa kati ya Wakristo Wayahudi na watu wa Mataifa kingeweza kuondolewa. (Waefeso 2:13, 14) Ili kumsaidia Petro akubali mpango huo mpya, Yehova alimwonyesha maono ambapo Alimwambia ‘akome kuviita kuwa najisi vitu ambavyo Mungu ametakasa.’ Kisha roho ya Yehova ikamwongoza hadi kwa mtu asiye Myahudi aliyeitwa Kornelio. Petro alipoelewa maoni ya Mungu—kwamba asimwite mtu huyo wa mataifa najisi kwa sababu Mungu amemtakasa—alipuliziwa kusema hivi: “Kwa hakika nahisi kwamba Mungu si mwenye ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye humhofu na kutenda uadilifu akubalika kwake.” (Matendo 10:9-35) Petro alishangaa kama nini Mungu alipoonyesha kwamba amemkubali Kornelio na familia yake kwa kuwamwagia roho takatifu!

PauloChombo-Kichaguliwa kwa Mataifa

Tunapofikiria huduma ya Paulo, twaona kielelezo chenye kutokeza cha jinsi Yehova anavyowatayarisha watumishi wake hatua kwa hatua kupenda na kusaidia watu wa aina zote. Wakati Paulo alipogeuzwa imani, Yesu alisema kwamba Paulo angetumikia akiwa chombo-kichaguliwa ili kupeleka jina Lake kwa mataifa. (Matendo 9:15) Kisha Paulo akaenda Arabuni, labda akatafakari kusudi la Mungu la kumtumia kutangaza habari njema kwa mataifa.—Wagalatia 1:15-17.

Katika safari yake ya kwanza ya umishonari, Paulo alionyesha bidii ya kuhubiria watu wasio Wayahudi. (Matendo 13:46-48) Yehova alibariki utendaji wa Paulo, na hilo lilithibitisha kwamba mtume huyo alikuwa akifanya mambo kupatana na mpango wa Yehova. Paulo alionyesha kwamba alielewa kabisa maoni ya Yehova alipomsahihisha Petro kwa ujasiri, ambaye alionyesha ubaguzi kwa kukwepa kushirikiana na ndugu zake wasio Wayahudi.—Wagalatia 2:11-14.

Twapata uthibitisho zaidi kwamba Mungu alikuwa akiongoza jitihada za Paulo kwenye safari yake ya pili ya umishonari wakati roho takatifu ilipomzuia Paulo asihubiri katika mkoa wa Bithinia wa Roma. (Matendo 16:7) Yaonekana huo haukuwa wakati unaofaa kuhubiri huko. Hata hivyo, baadaye baadhi ya Wabithinia wakawa Wakristo. (1 Petro 1:1) Katika maono, mkazi mmoja wa Makedonia alimsihi Paulo hivi: “Vuka uingie Makedonia utusaidie.” Paulo alifikia mkataa kwamba anapaswa kubadili safari yake ili akatangaze habari njema katika mkoa huo wa Roma.—Matendo 16:9, 10.

Paulo alikabili jaribu gumu sana la kubadilikana ili afaane na hali alipowahubiria Waathene. Ilikuwa kinyume cha sheria ya Wagiriki na Waroma kuleta miungu mipya au desturi mpya za kidini. Upendo wa Paulo kwa watu ulimchochea kufikiria kwa makini desturi zao za kidini. Huko Athene aliona madhabahu iliyoandikwa “Kwa Mungu Asiyejulikana.” Alitaja habari hiyo katika kazi yake ya kutoa ushahidi. (Matendo 17:22, 23) Alianza ujumbe wake kwa njia yenye fadhili na ya heshima kama nini!

Lazima Paulo awe alifurahi kama nini alipokumbuka matokeo mazuri ya kazi yake akiwa mtume kwa ajili ya mataifa! Alisaidia kuanzisha makutaniko huko Korintho, Filipi, Thesalonike, na miji kadhaa ya Galatia. Wengi wa Wakristo katika makutaniko hayo hawakuwa Wayahudi. Alisaidia wanaume na wanawake waliokuwa na imani kama vile Damarisi, Dionisio, Sergio Paulo, na Tito. Lilikuwa pendeleo kama nini kuona watu ambao hawakumjua Yehova wala Biblia wakikubali kweli ya Kikristo! Paulo alisema hivi kuhusu daraka lake la kuwasaidia watu wasio Wayahudi waifahamu kweli: “Kwa kweli, katika njia hii, nilifanya iwe shabaha yangu kutotangaza habari njema mahali ambapo Kristo tayari alikuwa amekwisha kutajwa jina, . . . bali, kama vile imeandikwa: ‘Wale ambao hawajatangaziwa juu yake wataona, na wale ambao hawajasikia wataelewa.’” (Waroma 15:20, 21) Je, tunaweza kuwatangazia habari njema watu wa utamaduni tofauti?

Kusaidia Watu Wote wa Dunia

Solomoni alimwomba Yehova kuhusu watu wasio Waisraeli ambao wangekuja kuabudu kwenye hekalu huko Yerusalemu. Aliomba hivi: “Basi, usikie huko mbinguni, makao yako, ukatende kwa kadiri ya yote atakayokuomba mgeni huyo; ili watu wote wa dunia wapate kulijua jina lako.” (1 Wafalme 8:41-43, italiki ni zetu.) Maelfu ya watangazaji wa Ufalme katika nchi nyingi leo wana maoni kama hayo. Wanakutana na watu walio kama Waninewi ambao kwa habari ya mambo ya kiroho ‘hawawezi kupambanua katika mkono wao wa kulia na mkono wao wa kushoto.’ Wahubiri wa Ufalme wana hamu ya kushiriki kutimizwa kwa unabii mbalimbali unaohusu kukusanywa kwa waabudu wa kweli kutoka mataifa mbalimbali.—Isaya 2:2, 3; Mika 4:1-3.

Wafuasi wa dini nyingine sawa na Jumuiya ya Wakristo wanakubali ujumbe wa Biblia. Hilo lapaswa kukuathirije? Jichunguze kwa unyofu. Ukihisi kwamba una ubaguzi, uondoe kwa kusitawisha upendo. * Usikatae watu ambao Mungu yuko tayari kuwakubali.—Yohana 3:16.

Fanya utafiti kabla ya kuzungumza na watu wa dini nyingine. Fahamu imani yao, mambo yanayowahangaisha, na jinsi wanavyofikiri; kisha utafute jambo mnalokubaliana nao. Waonyeshe wengine wema na huruma. Epuka mabishano, uwe mwenye kubadilikana na mwenye kujenga. (Luka 9:52-56) Ukifanya hivyo, utampendeza Yehova, “ambaye mapenzi yake ni kwamba watu wa namna zote waokolewe na kuja kwenye ujuzi sahihi wa kweli.”—1 Timotheo 2:4.

Tunafurahi kama nini kuwa na watu kutoka malezi ya namna mbalimbali katika makutaniko yetu! (Isaya 56:6, 7) Inafurahisha kama nini leo kusikia majina kama vile Mamadou, Jegan, Reza, na Chan mbali na majina kama Mary, John, Stephen, na Tom! Kwa kweli, tumefunguliwa “mlango mkubwa uongozao kwenye utendaji.” (1 Wakorintho 16:9) Na tutumie fursa tulizo nazo kueneza mwaliko unaotolewa na Yehova, Mungu asiye na ubaguzi, na anayekubali watu wa mataifa yote!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 19 Ona gazeti Amkeni!, la Julai 8, 1996, ukurasa wa 5-7, “Vizuizi Vinavyozuia Mawasiliano.”

[Picha katika ukurasa wa 23]

Paulo aliwatangazia watu habari njema kila mahali kwa kuwa mwenye kubadilikana

. . . huko Athene

. . . huko Filipi

. . . akiwa safarini