Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Nilitaka Kumtumikia Mungu”

“Nilitaka Kumtumikia Mungu”

Ripoti ya Watangazaji wa Ufalme

“Nilitaka Kumtumikia Mungu”

“TOKENI kwake, watu wangu.” Huo ulikuwa wito wa malaika uliosikiwa na mtume Yohana katika karne ya kwanza W.K. Katika siku zetu mamilioni ya watu walio wanyofu wameitikia wito huo na kutoka katika “Babiloni Mkubwa,” milki ya ulimwengu ya dini isiyo ya kweli. (Ufunuo 18:1-4) Miongoni mwao ni Wilner kutoka Haiti anayesimulia yaliyompata.

“Nilizaliwa katika familia ya Wakatoliki wenye kumcha Mungu katika mji mdogo wa St. Marc, Haiti, mnamo mwaka wa 1956. Wazia furaha ya familia yangu wakati mimi pamoja na wengine wawili kutoka mji wetu tulipochaguliwa kwenda seminari huko St. Michel de l’Atalaye, Haiti. Kisha katika mwaka wa 1980, tukapelekwa kwa mafunzo zaidi huko Stavelot, Ubelgiji. Tukiwa huko tulipata mafunzo pia katika chuo kikuu kimoja cha Katoliki.

“Mwanzoni nilifurahia sana kuwa kasisi. Siku moja tukiwa kwenye chumba cha kulia chakula cha mchana, kasisi aliyesimamia kikundi chetu aliniambia nibaki kwa dakika chache kwani alitaka kuniambia jambo fulani. Nilipigwa na butaa aliponiambia waziwazi kwamba alipendezwa nami kingono. Nilikataa utongozaji wake lakini nilivunjika moyo sana. Niliwaandikia familia yangu barua kuwaeleza kuhusu jambo hilo na ijapokuwa hawakufurahia uamuzi wangu, niliondoka katika seminari hiyo miezi michache baadaye. Nilipata mahali pa kukaa kijijini na nikaanza kusomea kazi nyingine.

“Niliporudi St. Marc, sikuwa na imani yoyote katika Kanisa Katoliki. Hata hivyo, nilitaka kumtumikia Mungu lakini sikujua la kufanya. Nilienda katika kanisa la Wasabato, Wabaptisti wa Haiti, na Wamormoni. Sikuwa na mwongozo wowote wa kiroho.

“Kisha nikakumbuka kwamba nilipokuwa katika seminari huko Ubelgiji, nilizoea kusoma Biblia ya Crampon. Ndani yake niligundua kwamba Mungu ana jina. Kwa kutumia jina lake, nilisali kwa bidii ili anisaidie kupata dini ya kweli.

“Muda mfupi baadaye, Mashahidi wa Yehova wawili wakaja kuishi karibu na mahali nilipoishi. Walikuwa watulivu na wenye kuheshimika. Nilipendezwa sana na mwenendo wao. Siku moja, mmoja wao alinialika kuhudhuria Ukumbusho wa kila mwaka wa kifo cha Kristo. Nilifurahia sana mkutano huo na nikakubali kujifunza Biblia kwa ukawaida na Mashahidi. Kwa kipindi cha miezi sita hivi, nilisadikishwa kwamba nilikuwa nimeipata njia ya kweli ya kumtumikia Mungu. Nilijiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa Novemba 20, 1988.”

Baadaye, Wilner akaanza utumishi wa wakati wote. Sasa, anatumikia akiwa mzee wa kutaniko. Yeye na mke wake pamoja na watoto wao wawili wanatumikia kwa furaha kutanikoni.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Kwa kusoma Biblia, Wilner aligundua kwamba jina la Mungu ni Yehova