Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Elekeza Hatua Zako kwa Kufuata Kanuni za Mungu

Elekeza Hatua Zako kwa Kufuata Kanuni za Mungu

Elekeza Hatua Zako kwa Kufuata Kanuni za Mungu

‘Yehova anakufundisha ili upate faida.’—ISAYA 48:17.

1. Muumba huwaongozaje wanadamu?

WANASAYANSI wanapofumbua mambo yasiyojulikana kuhusu ulimwengu, wanashangaa kupata nishati nyingi sana katika ulimwengu unaotuzunguka. Jua letu—ambalo ni nyota yenye ukubwa wa wastani—hutoa nishati inayotoshana na “milipuko ya mabomu bilioni 100 ya haidrojeni kila sekunde.” Muumba anaweza kudhibiti na kuelekeza sayari hizo kubwa kwa nguvu zake zisizo na kifani. (Ayubu 38:32; Isaya 40:26) Namna gani sisi wanadamu ambao tumepewa zawadi ya uhuru wa kuchagua, uwezo wa kupambanua mema na mabaya, uwezo wa kufikiri, na uwezo wa kufahamu mambo ya kiroho? Muumba wetu amechagua kutuongoza vipi? Yeye hutuongoza kwa upendo kupitia sheria zake kamilifu na kanuni zake bora, na dhamiri yetu iliyozoezwa vizuri.—2 Samweli 22:31; Waroma 2:14, 15.

2, 3. Mungu hupendezwa na utii wa aina gani?

2 Mungu hupendezwa na viumbe wenye akili wanaochagua kumtii. (Mithali 27:11) Badala ya kuumbwa tufanye mambo kama roboti bila kufikiri, Yehova alitupatia uhuru wa kuchagua ili tuweze kuamua kufanya yaliyo sawa kwa kutumia ujuzi tulio nao.—Waebrania 5:14.

3 Yesu, ambaye alionyesha kikamili jinsi Babake alivyo, aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Nyinyi ni marafiki wangu ikiwa mwafanya lile ninalowaamuru nyinyi. Siwaiti nyinyi tena watumwa.” (Yohana 15:14, 15) Nyakati za kale, ilikuwa lazima mtumwa atii maagizo ya bwana-mkubwa wake. Kwa upande mwingine, urafiki hufanywa kwa kuonyesha sifa zinazovutia moyo. Tunaweza kuwa marafiki wa Yehova. (Yakobo 2:23) Urafiki huo unaimarishwa na upendo. Yesu alihusianisha utii kwa Mungu na upendo aliposema: “Ikiwa yeyote anipenda mimi, atashika neno langu, na Baba yangu atampenda.” (Yohana 14:23) Yehova anatutia moyo tuishi kupatana na kanuni zake kwa kuwa anatupenda na anataka kutuongoza kwa usalama.

Kanuni za Mungu

4. Kanuni ni nini?

4 Kanuni ni nini? Kanuni inafafanuliwa kuwa ‘kweli, sheria, au fundisho la msingi ambalo mafundisho mengine hutegemea.’ (Webster’s Third New International Dictionary) Uchunguzi wa makini wa Biblia hufunua kwamba Baba yetu wa mbinguni hutoa miongozo ya msingi kuhusu hali mbalimbali maishani. Yeye hufanya hivyo kwa kufikiria jinsi tuwezavyo kufaidika milele. Hilo linapatana na yale ambayo Mfalme Solomoni mwenye hekima aliandika: “Mwanangu, sikiliza, na kuzipokea kauli zangu; na miaka ya maisha yako itakuwa mingi. Nimekufundisha katika njia ya hekima; nimekuongoza katika mapito ya unyofu.” (Mithali 4:10, 11) Kanuni za msingi ambazo Yehova ametoa zinahusu uhusiano wetu pamoja naye na pamoja na wanadamu wenzetu. Zinahusu pia ibada yetu na maisha yetu ya kila siku. (Zaburi 1:1) Na tuchunguze baadhi ya kanuni hizo za msingi.

5. Toa mifano ya kanuni fulani za msingi.

5 Kuhusu uhusiano wetu na Yehova, Yesu alisema: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.” (Mathayo 22:37) Isitoshe, Mungu hutoa kanuni zinazohusu jinsi tunavyowatendea wanadamu wenzetu, kama ile Kanuni Bora: “Kwa hiyo, mambo yote mtakayo watu wawafanyie nyinyi, lazima mwafanyie wao pia hivyohivyo.” (Mathayo 7:12; Wagalatia 6:10; Tito 3:2) Tunashauriwa hivi kuhusiana na ibada: “Acheni tufikiriane ili kuchocheana kwenye upendo na kazi zilizo bora, si kuachilia mbali kukusanyika pamoja sisi wenyewe.” (Waebrania 10:24, 25) Mtume Paulo alisema hivi kuhusu shughuli zetu za kila siku: “Kama mnakula au mnakunywa au mnafanya jambo jingine lolote, fanyeni mambo yote kwa utukufu wa Mungu.” (1 Wakorintho 10:31) Neno la Mungu lina kanuni nyingine nyingi.

6. Kanuni zinatofautianaje na sheria?

6 Kanuni ni kweli za msingi zenye kutumika, nao Wakristo wenye hekima hujifunza kuzipenda. Yehova alimpulizia Solomoni kuandika: “Sikiliza maneno yangu; tega sikio lako, uzisikie kauli zangu. Zisiondoke machoni pako; uzihifadhi ndani ya moyo wako. Maana ni uhai kwa wale wazipatao.” (Mithali 4:20-22) Kanuni hutofautianaje na sheria? Sheria hutungwa kutokana na kanuni. Sheria huhusiana sanasana na mambo hususa na zinaweza kutumika kwa muda fulani au katika hali fulani hususa, lakini kanuni hutumika wakati wote. (Zaburi 119:111) Kanuni za Mungu hazipitwi na wakati wala haziachi kutumika. Maneno haya yaliyopuliziwa ya nabii Isaya yanathibitika kuwa kweli: “Majani yakauka, ua lanyauka; bali neno la Mungu wetu litasimama milele.”—Isaya 40:8.

Fikiri na Kutenda kwa Kutegemea Kanuni

7. Neno la Mungu linatutiaje moyo tufikiri na kutenda kwa kutegemea kanuni?

7 Mara nyingi, “neno la Mungu wetu” hututia moyo tufikiri na kutenda kwa kutegemea kanuni. Yesu alipoombwa atoe muhtasari wa Sheria, alitoa taarifa mbili fupi zilizo wazi—moja ilikazia upendo kwa Yehova, na nyingine ikakazia upendo kwa wanadamu wenzetu. (Mathayo 22:37-40) Yesu alifanya hivyo kwa kunukuu sehemu fulani ya muhtasari mfupi uliokuwa umetolewa awali kuhusu kanuni za msingi za Sheria ya Musa, ambazo zimetajwa kwenye Kumbukumbu la Torati 6:4, 5: “BWANA, Mungu wetu, BWANA ndiye mmoja. Nawe mpende BWANA, Mungu wako, kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa nguvu zako zote.” Yaonekana kwamba Yesu pia alikuwa anakumbuka agizo la Mungu katika Mambo ya Walawi 19:18. Mfalme Solomoni anamalizia kitabu cha Mhubiri kwa maneno mafupi, yaliyo wazi, na yenye nguvu ambayo yanajumlisha sheria nyingi sana za Mungu: “Hii ndiyo jumla ya maneno; yote yamekwisha sikiwa; mche Mungu, nawe uzishike amri zake, maana kwa jumla ndiyo impasayo mtu. Kwa maana Mungu ataleta hukumuni kila kazi, pamoja na kila neno la siri, likiwa jema au likiwa baya.”—Mhubiri 12:13, 14; Mika 6:8.

8. Kwa nini ni ulinzi kuzifahamu vizuri kanuni za msingi za Biblia?

8 Kufahamu vizuri kanuni hizo za msingi kunaweza kutusaidia kuelewa na kufuata maagizo yanayotaja mambo hususa. Zaidi ya hayo, ikiwa hatuelewi vizuri na hatukubali kanuni za msingi, huenda tusiweze kufanya maamuzi ya hekima na imani yetu inaweza kutikiswa kwa urahisi. (Waefeso 4:14) Tukikazia kanuni hizo akilini na moyoni, tutakuwa tayari kuzitumia tunapofanya maamuzi. Tutafanikiwa tukizitumia kwa uelewevu.—Yoshua 1:8; Mithali 4:1-9.

9. Kwa nini si rahisi sikuzote kutambua na kufuata kanuni za Biblia?

9 Kutambua na kufuata kanuni za Biblia si rahisi kama kufuata sheria fulani zilizoandikwa. Tukiwa wanadamu wasio wakamilifu, huenda tusitake kutumia akili ili kufanya maamuzi yanayotegemea kanuni. Huenda tukapendelea sheria fulani hususa tunapokabili maamuzi au hali fulani ngumu. Huenda nyakati nyingine tukatafuta ushauri kutoka kwa Mkristo fulani mkomavu—labda mzee wa kutaniko—tukitarajia kupata sheria fulani hususa kuhusiana na hali yetu. Hata hivyo, huenda Biblia au vichapo vinavyotegemea Biblia visiwe na sheria hususa, na hata ikiwa tutapewa sheria hiyo, huenda isiweze kutumika nyakati zote na katika hali zote. Huenda unakumbuka kwamba mwanamume fulani alimwomba Yesu hivi: “Mwalimu, mwambie ndugu yangu anigawie urithi.” Badala ya kumpa sheria inayohusiana na kutatua migogoro kati ya ndugu, Yesu alimpa kanuni inayohusisha mambo mengi zaidi: “Fulizeni kufungua macho yenu na mlinde dhidi ya kila namna ya tamaa.” Hivyo, Yesu akampa mwongozo uliotumika wakati huo na unaotumika hata sasa.—Luka 12:13-15.

10. Kutenda kupatana na kanuni huonyeshaje nia ya moyo wetu?

10 Labda umeona watu ambao hutii sheria shingo upande, wakiogopa tu kuadhibiwa. Ikiwa tunaheshimu kanuni, hatutakuwa na maoni kama hayo. Kanuni huchochea watu wanaoongozwa nazo watii kutoka moyoni. Ni kweli kwamba, kanuni nyingi hazihusishi adhabu ya papo hapo kwa wale wanaozivunja. Jambo hilo hutuwezesha kuonyesha ni kwa nini tunamtii Yehova, na nia yetu ni nini. Yosefu alituwekea mfano mzuri alipokataa kutongozwa na mke wa Potifa. Ingawa Yehova hakuwa ametoa sheria iliyoandikwa kuhusu uzinzi wala kuonyesha ni adhabu gani mtu angepewa kwa kufanya mapenzi na mke wa mtu mwingine, Yosefu alijua kanuni za Mungu kuhusu uaminifu katika ndoa. (Mwanzo 2:24; 12:18-20) Jibu lake linatuonyesha kwamba alishikilia sana kanuni hizo: “Nifanyeje ubaya huu mkubwa nikamkose Mungu?”—Mwanzo 39:9.

11. Wakristo wangependa kuongozwa na kanuni za Yehova katika mambo gani?

11 Leo, Wakristo wangependa kuongozwa na kanuni za Yehova katika mambo ya kibinafsi, kama vile kuchagua marafiki, vitumbuizo, muziki, na habari wanazosoma. (1 Wakorintho 15:33; Wafilipi 4:8) Tunapoongeza ujuzi wetu, uelewevu, na uthamini wetu kwa Yehova na viwango vyake, dhamiri, yaani, hisia inayotuwezesha kupambanua mema na mabaya, itatusaidia kufuata kanuni za Mungu chini ya hali yoyote tunayokabili, hata katika mambo ya kibinafsi. Tukiongozwa na kanuni za Biblia, hatutatafuta njia ya kukwepa sheria za Mungu wala hatutawaiga wale ambao hujaribu kuona ni kwa kadiri gani wanaweza kujiingiza katika jambo fulani bila hasa kuvunja sheria fulani. Tunatambua kwamba kufikiri kwa aina hiyo huleta madhara.—Yakobo 1:22-25.

12. Kuna sababu gani kuu ya kuongozwa na kanuni za Mungu?

12 Wakristo wakomavu wanatambua kwamba sababu kuu inayofanya wafuate kanuni za Mungu ni kutaka kujua jinsi Yehova anavyoona mambo. “Enyi mmpendao BWANA, uchukieni uovu,” anahimiza mtunga-zaburi. (Zaburi 97:10) Likitaja baadhi ya mambo ambayo Mungu huona kuwa mabaya, andiko la Mithali 6:16-19 linasema hivi: “Kuna vitu sita anavyovichukia BWANA; naam, viko saba vilivyo chukizo kwake. Macho ya kiburi, ulimi wa uongo, na mikono imwagayo damu isiyo na hatia; moyo uwazao mawazo mabaya; miguu iliyo myepesi kukimbilia maovu; shahidi wa uongo asemaye uongo; naye apandaye mbegu za fitina kati ya ndugu.” Tunapoongozwa na tamaa ya kuona mambo hayo ya msingi kama vile Yehova anavyoyaona, daima tutaishi kupatana na kanuni zake.—Yeremia 22:16.

Tunahitaji Kuwa na Nia Nzuri

13. Yesu alikazia kufikiri kwa aina gani katika Mahubiri yake ya Mlimani?

13 Kujua na kufuata kanuni hutulinda na mtego wa ibada ya kidesturi, isiyo na maana. Kuna tofauti ya kufuata kanuni na kutii sheria tu bila kufikiri. Yesu alieleza jambo hilo vizuri katika Mahubiri yake ya Mlimani. (Mathayo 5:17-48) Kumbuka kwamba wasikilizaji wa Yesu walikuwa Wayahudi, kwa hiyo walipaswa kuongozwa na Sheria ya Musa. Lakini ukweli ni kwamba hawakuielewa Sheria vizuri. Walikazia tu ufuataji wa sheria kama zilivyoandikwa badala ya kukazia kusudi la sheria hizo. Nao walikazia mapokeo yao, wakiyachukua kuwa ya maana kuliko mafundisho ya Mungu. (Mathayo 12:9-12; 15:1-9) Kwa sababu hiyo watu kwa ujumla hawakufundishwa kufikiri kupatana na kanuni.

14. Yesu aliwasaidiaje wasikilizaji wake wafikiri kwa kutegemea kanuni?

14 Kinyume cha hilo, katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alitaja mambo haya matano kuhusu maadili: hasira, ndoa na talaka, ahadi, kulipiza kisasi, na upendo na chuki. Kuhusiana na kila mojawapo ya mambo hayo, Yesu alionyesha faida ya kufuata kanuni. Hivyo, Yesu aliwapa wafuasi wake maadili ya kiwango cha juu sana. Kwa mfano, kuhusiana na uzinzi, alitupatia kanuni ambayo hulinda matendo, mawazo, na tamaa zetu: “Kila mtu ambaye hufuliza kumtazama mwanamke ili kuwa na harara kwa ajili yake tayari amefanya uzinzi pamoja naye moyoni mwake.”—Mathayo 5:28.

15. Tunaweza kuepukaje mwelekeo wowote wa kufuata sheria tu bila kufikiri?

15 Mfano huo unaonyesha kwamba hatupaswi kusahau lengo au kusudi la kanuni za Yehova. Hatupaswi kamwe kujaribu kupata kibali cha Mungu kwa kufanya mambo kidesturi tu. Yesu alifunua kosa la kuwa na maoni kama hayo kwa kuonyesha kwamba Mungu ni mwenye rehema na upendo. (Mathayo 12:7; Luka 6:1-11) Kwa kufuata kanuni za Biblia, tutaepuka kujaribu kuishi (au kuwataka wengine waishi) kwa kufuata sheria nyingi na ngumu ambazo haziko katika Biblia. Tutazingatia zaidi kanuni za upendo na utii kwa Mungu badala ya kuzingatia tu jinsi ibada yetu inavyoonekana kwa nje.—Luka 11:42.

Matokeo Yenye Kufurahisha

16. Toa mifano ya kanuni ambazo ndio msingi wa sheria fulani za Biblia?

16 Tunapojitahidi kumtii Yehova, ni muhimu kutambua kwamba sheria zake zinategemea kanuni za msingi. Kwa mfano, Wakristo wanapaswa kuepuka ibada ya sanamu, mwenendo mchafu kingono, na matumizi mabaya ya damu. (Matendo 15:28, 29) Msimamo wa Wakristo kuhusiana na masuala hayo unategemea nini? Kumpa Mungu ujitoaji usiohusisha wengine; kuwa waaminifu kwa mwenzi wetu wa ndoa; na kujua kwamba Yehova ndiye Mpaji-Uhai. (Mwanzo 2:24; Kutoka 20:5; Zaburi 36:9) Kufahamu kanuni hizi za msingi hufanya iwe rahisi kukubali na kufuata sheria zinazohusiana na kanuni hizo.

17. Tunapata matokeo gani mazuri kwa kufahamu na kufuata kanuni za Biblia?

17 Tunapofahamu kanuni za msingi na kuzifuata, tunatambua kwamba zinatufaidi. Faida za kiroho zinazofurahiwa na watu wa Mungu mara nyingi huambatana na faida za kimwili. Kwa mfano, wale wanaoepuka kuvuta sigara, wanaoishi maisha mazuri kiadili, na kuheshimu utakatifu wa damu, huepuka magonjwa fulani. Vivyo hivyo, kuishi kupatana na kweli ya Mungu kwaweza kutufaidi kifedha, kijamii, au katika maisha ya familia. Faida kama hizo za kimwili zinathibitisha kwamba viwango vya Mungu vinafaa na vinaweza kutumika. Lakini hatufuati kanuni za Mungu kusudi tu tupate faida hizo. Wakristo wa kweli humtii Yehova kwa sababu wanampenda, anastahili kuabudiwa, na kwa sababu jambo hilo linafaa.—Ufunuo 4:11.

18. Ikiwa tunataka kuwa Wakristo wenye mafanikio, ni nini kinachopasa kuongoza maisha yetu?

18 Tunapoacha kanuni za Biblia zituongoze, maisha yetu yanakuwa bora na jambo hilo linaweza kuwafanya wengine wafuate njia ya Mungu. La muhimu hata zaidi ni kwamba maisha yetu humtukuza Yehova. Tunatambua kwamba Yehova kwa kweli ni Mungu mwenye upendo anayetutakia mema. Tunapofanya maamuzi kupatana na kanuni za Biblia na kuona jinsi Yehova anavyotubariki, tunahisi tukiwa karibu hata zaidi naye. Naam, tunasitawisha uhusiano wenye upendo pamoja na Baba yetu wa mbinguni.

Je, Unakumbuka?

• Kanuni ni nini?

• Kanuni zinatofautianaje na sheria?

• Kwa nini inafaa kutenda kwa kutegemea kanuni?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku katika ukurasa wa 20]

Wilson, Mkristo kutoka Ghana, alijulishwa kwamba angefutwa kazi baada ya siku chache. Siku yake ya mwisho kazini, aliagizwa aoshe gari la mkurugenzi mkuu wa kampuni. Wilson alipata kiasi fulani cha pesa ndani ya gari hilo. Mkubwa wake alimwambia kwamba Mungu alimtumia pesa hizo kwa sababu Wilson alikuwa afutwe kazi siku hiyo. Hata hivyo, Wilson alitumia kanuni ya Biblia kuhusu unyofu na kumrudishia mkurugenzi pesa hizo. Kwa kuvutiwa na kushangazwa na kitendo hicho, mkurugenzi huyo alimpa Wilson kazi ya kudumu mara moja na kumpandisha cheo kuwa mfanyikazi mwenye madaraka makubwa katika kampuni hiyo.—Waefeso 4:28.

[Sanduku katika ukurasa wa 21]

Rukia ni mwanamke kutoka Albania mwenye umri wa miaka 60 hivi. Kwa sababu ya mgogoro katika familia, Rukia hakuzungumza na ndugu yake kwa zaidi ya miaka 17. Alianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova na kujua kwamba Wakristo wa kweli wanapaswa kuishi kwa amani na watu wengine, bila kuweka kinyongo. Alisali usiku kucha, na huku moyo ukimdunda, akaenda nyumbani kwa ndugu yake. Binti ya ndugu yake alifungua mlango na kwa mshangao akamwuliza Rukia hivi: “Ni nani amekufa? Unafanya nini hapa?” Rukia alimwambia alitaka kuona ndugu yake. Alimweleza ndugu yake kwa utulivu kwamba baada ya kujifunza juu ya Yehova na kanuni za Biblia, amechochewa afanye amani naye. Walilia, wakakumbatiana, kisha wakasherehekea muungano huo wa pekee!—Waroma 12:17, 18.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Mathayo 5:27, 28

[Picha katika ukurasa wa 23]

Mathayo 5:3

[Picha katika ukurasa wa 23]

Mathayo 5:24

[Picha katika ukurasa wa 23]

“Alipouona umati alipanda kwenda katika mlima; na baada ya yeye kuketi wanafunzi wake wakamjia; naye akafungua kinywa chake na kuanza kuwafundisha.”MATHAYO 5:1, 2