Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Hisia-Mwenzi—Hutusaidia Kudhihirisha Fadhili na Huruma

Hisia-Mwenzi—Hutusaidia Kudhihirisha Fadhili na Huruma

Hisia-Mwenzi—Hutusaidia Kudhihirisha Fadhili na Huruma

“MAISHA si bure maadamu unaweza kutuliza maumivu ya mtu mwingine,” akaandika Helen Keller. Bila shaka Keller alifahamu maumivu ya kihisia-moyo. Alipokuwa na umri wa miezi 19, alipatwa na ugonjwa uliofanya asiweze kuona wala kusikia kabisa. Lakini mwalimu mwenye huruma alimfunza Helen kusoma na kuandika katika Braille, na baadaye akamfunza kuzungumza.

Mwalimu wa Keller, Ann Sullivan, alifahamu kabisa jinsi inavyofadhaisha kukabiliana na ulemavu. Yeye mwenyewe karibu apoteze uwezo wa kuona. Lakini Ann alibuni njia ya kuwasiliana na Helen kwa kuandika herufi mojamoja katika mkono wa Helen. Kwa kuchochewa na hisia-mwenzi za mwalimu wake, Helen aliamua kujitolea ili awasaidie watu wasioona wala kusikia. Baada ya kujitahidi sana alishinda ulemavu wake, na aliwahurumia na kuwaonyesha hisia-mwenzi wale waliokuwa na hali kama zake. Alitaka kuwasaidia.

Labda umeona kwamba katika ulimwengu huu wenye ubinafsi, ni rahisi ‘kufunga mlango wa huruma nyororo’ na kupuuza mahitaji ya wengine. (1 Yohana 3:17) Hata hivyo, Wakristo wanaamuriwa wapende jirani zao na wawe na upendo mwingi wao kwa wao. (Mathayo 22:39; 1 Petro 4:8) Lakini huenda unafahamu ukweli huu: Ijapokuwa sisi tunataka sana kupendana, mara nyingi tunapuuza fursa za kuwatuliza wengine. Hiyo huenda ikawa ni kwa sababu hatujui mahitaji yao. Kuwa na hisia-mwenzi kwaweza kutusaidia kuonyesha fadhili na huruma.

Hisia-Mwenzi Ni Nini?

Kamusi moja inasema kwamba hisia-mwenzi ni “kutambua na kuelewa hali ya mtu mwingine, hisia zake, na nia yake.” Pia hisia-mwenzi imefafanuliwa kuwa uwezo wa kujiweka katika hali ya mtu mwingine. Kwa hiyo kuonyesha hisia-mwenzi kwanza kwataka tuelewe hali za mtu mwingine, na pili tuelewe jinsi anavyohisi kutokana na hali hizo. Naam, kuwa na hisia-mwenzi kwahusisha kuhisi maumivu ya mtu mwingine katika moyo wetu.

Maandiko hueleza kwa njia mbalimbali sifa tunayozungumzia hapa. Mtume Petro aliwashauri Wakristo waonyeshe ‘hisia-mwenzi, shauku ya kidugu, na huruma.’ (1 Petro 3:8) Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “hisia-mwenzi” kihalisi linamaanisha “kuteseka na mtu mwingine” au “kuwa na huruma.” Mtume Paulo alikuwa na maoni hayohayo alipowahimiza Wakristo wenzake ‘washangilie pamoja na watu washangiliao; watoe machozi pamoja na watu watoao machozi.’ Paulo aliongeza kusema: “Iweni na nia ya jinsi ileile kuelekea wengine kama ilivyo kwenu wenyewe.” (Waroma 12:15, 16) Je, hukubali kwamba ni vigumu kumpenda jirani yako usipojiweka katika hali yake?

Karibu kila mtu anaweza kudhihirisha hisia-mwenzi. Ni jambo la kawaida kuhuzunika unapoona watoto wakifa njaa au wakimbizi wakihangaika. Ni mama yupi anayeweza kupuuza kilio cha mtoto wake? Lakini kuna kuteseka kwingine kusikoonekana wazi. Ni vigumu sana kuelewa hisia za mtu aliyeshuka moyo, mtu mwenye kasoro ya kimwili isiyoonekana waziwazi, au mtu mwenye matatizo ya kula—ikiwa hatujawahi kupatwa na matatizo hayo! Hata hivyo, Maandiko huonyesha kwamba tunaweza na tunapaswa kuwaonyesha hisia-mwenzi watu ambao hali yao ni tofauti na yetu.

Mifano ya Kimaandiko ya Watu Walio na Hisia-Mwenzi

Yehova ndiye kielelezo bora zaidi katika kuonyesha hisia-mwenzi. Ingawa yeye ni mkamilifu, hatarajii tuwe wakamilifu, “kwa maana yeye anatujua umbo letu, na kukumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi.” (Zaburi 103:14; Waroma 5:12) Isitoshe, kwa kuwa anafahamu udhaifu wetu, ‘haachi tushawishwe kupita vile tuwezavyo kuhimili.’ (1 Wakorintho 10:13) Kupitia watumishi wake na roho yake, anatusaidia kupata suluhisho.—Yeremia 25:4, 5; Matendo 5:32.

Yehova huhisi uchungu watu wake wanapoteseka. Aliwaambia hivi Wayahudi waliorudi kutoka Babiloni: ‘Yeye awagusaye ninyi aigusa mboni ya jicho langu.’ (Zekaria 2:8) Akifahamu kabisa hisia-mwenzi za Mungu, mwandikaji wa Biblia Daudi alisema hivi: “Uyatie machozi yangu katika chupa yako, je! hayamo katika kitabu chako?” (Zaburi 56:8) Inafariji kama nini kujua kwamba Yehova anakumbuka—kana kwamba yameandikwa katika kitabu—machozi ambayo watumishi wake waaminifu wanatoa wanapojitahidi kudumisha uaminifu-maadili!

Kama Baba yake wa kimbingu, Yesu Kristo hujali hisia za wengine. Alipomponya kiziwi mmoja, alimchukua kando, yaelekea ili kuponywa kwake kimuujiza kusimwaibishe au kumshtua. (Marko 7:32-35) Katika pindi nyingine, Yesu alimwona mjane aliyekuwa akienda kumzika mwana wake wa pekee. Alihisi uchungu aliokuwa nao mjane huyo, na mara moja akakaribia msafara wa maziko, na kumfufua mwanamume huyo kijana.—Luka 7:11-16.

Baada ya kufufuliwa, Yesu alimtokea Sauli aliyekuwa njiani kuelekea Damasko na kumjulisha jinsi alivyohisi kwa sababu ya kuwanyanyasa kikatili wanafunzi wake. Alimwambia, “Mimi ni Yesu, ambaye wewe unanyanyasa.” (Matendo 9:3-5) Yesu alihisi maumivu waliyopata wanafunzi wake, kama vile mama huhisi uchungu mtoto wake anapokuwa mgonjwa. Vivyo hivyo, Yesu, Kuhani wetu wa kimbingu wa Cheo cha Juu, ‘hushiriki hisia za udhaifu wetu,’ au kulingana na tafsiri ya Rotherham, ana “hisia-mwenzi kuelekea udhaifu wetu.”—Waebrania 4:15.

Mtume Paulo alijifunza kuwa mwenye kujali hisia za wengine na kuteseka kwao. “Ni nani aliye dhaifu, nami si dhaifu? Ni nani amekwazika, nami siwaki hasira?” akauliza. (2 Wakorintho 11:29) Malaika alipowaachilia kimuujiza Paulo na Sila kutoka gereza moja huko Filipi, Paulo aliona ni afadhali amwambie mlinzi wa jela mara moja kwamba hakuna mtu ambaye ametoroka. Alimhurumia mlinzi wa gereza kwa kuwa alihisi kwamba huenda angejiua. Paulo alijua kwamba kulingana na desturi ya Waroma, mlinzi wa gereza angeadhibiwa vikali iwapo mfungwa angetoroka—hasa iwapo alikuwa ameagizwa amlinde asitoroke. (Matendo 16:24-28) Tendo hilo la fadhili la Paulo lililookoa uhai wa mlinzi huyo wa gereza lilimvutia sana, naye pamoja na familia yake wakachukua hatua ya kuwa Wakristo.—Matendo 16:30-34.

Jinsi ya Kusitawisha Hisia-Mwenzi

Maandiko hututia moyo tena na tena tumwige Baba yetu wa kimbingu na Mwana wake, Yesu Kristo, kwa hiyo twapaswa kusitawisha hisia-mwenzi. Tunaweza kusitawishaje sifa hiyo? Kuna njia tatu kuu ambazo sisi tunaweza kuonyesha kwamba tunajali hisia na mahitaji ya wengine: kwa kusikiliza, kuwa macho, na kwa kuwaza.

Sikiliza. Kwa kusikiliza kwa makini tunapata kujua matatizo ambayo wengine wanakabili. Tukiwasikiliza kwa makini yaelekea watafunua yote yaliyo moyoni mwao na jinsi wanavyohisi. “Ninaweza kuzungumza na mzee iwapo nina uhakika kwamba atanisikiliza,” asema Miriam. “Nataka kujua kwamba kweli anaelewa tatizo langu. Mimi huwa na uhakika zaidi naye anaponiuliza maswali ya kindani ambayo yanaonyesha kwamba alikuwa akisikiliza kwa makini mambo niliyomwambia.”

Kuwa macho. Si kila mtu atakayetuambia waziwazi jinsi anavyohisi au mambo anayokabili. Hata hivyo, mtu aliye macho atajua wakati Mkristo mwenzake anapoonekana kuwa ameshuka moyo, tineja anapoacha kuzungumza na watu, au mhudumu mwenye bidii anapokosa shauku. Uwezo huo wa kutambua tatizo mapema ni muhimu kwa wazazi. “Kwa njia fulani, mama yangu hujua jinsi ninavyohisi hata kabla sijazungumza naye, kwa hiyo ni rahisi kumweleza waziwazi matatizo yangu,” asema Marie.

Jaribu kuwazia mambo. Njia yenye matokeo zaidi ya kusitawisha hisia-mwenzi ni kujiuliza hivi: ‘Ikiwa ningekuwa katika hali hii, ningehisije? Ningetendaje? Ningehitaji nini?’ Wafariji bandia watatu wa Yobu hawakuweza kujiweka katika hali yake. Kwa hiyo walimlaumu kwa dhambi walizodhani ametenda.

Mara nyingi wanadamu wasio wakamilifu huona ni rahisi kuchambua watu kwa sababu ya makosa yao badala ya kuelewa hisia zao. Hata hivyo, tukijitahidi sana kuwazia jinsi ambavyo mtu mwenye taabu husononeka, tutaweza kumwonyesha hisia-mwenzi badala ya kumshutumu. “Mimi hutoa shauri bora zaidi ninaposikiliza kwa makini na kujitahidi kuelewa mambo yote yanayohusika kabla sijaanza kutoa madokezo,” akasema Juan, mzee mwenye uzoefu.

Vichapo vinavyogawanywa na Mashahidi wa Yehova vimewasaidia wengi kudhihirisha sifa hiyo. Magazeti Mnara wa Mlinzi na Amkeni! yamezungumzia matatizo makubwa kama vile mshuko-moyo na kutenda watoto vibaya. Habari hiyo ya wakati unaofaa husaidia wasomaji wajali zaidi hisia za wale wanaoteseka. Hali kadhalika, kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi kimewasaidia wazazi wengi waelewe matatizo ya watoto wao.

Hisia-Mwenzi Husaidia Katika Utendaji wa Kikristo

Ni watu wachache sana kati yetu wangempuuza mtoto mwenye njaa ikiwa wana chakula cha kumpa. Tukiwa na hisia-mwenzi, tutatambua pia hali ya kiroho ya wengine. Biblia husema hivi kumhusu Yesu: “Alipouona umati alihisi sikitiko kwa ajili yao, kwa sababu ulikuwa umechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.” (Mathayo 9:36) Mamilioni ya watu leo wako katika hali hiyo ya kiroho, nao wanahitaji msaada.

Kama ilivyokuwa katika siku za Yesu, huenda tukalazimika kushinda ubaguzi au desturi tuliyoshikilia sana ili tuweze kufikia mioyo ya watu. Ili ujumbe wake uvutie zaidi, mhudumu mwenye hisia-mwenzi hujitahidi kutafuta jambo ambalo anakubaliana na watu au huzungumza kuhusu habari ambayo watu wanaifikiria. (Matendo 17:22, 23; 1 Wakorintho 9:20-23) Matendo ya fadhili yanayochochewa na hisia-mwenzi yanaweza kufanya wasikilizaji wetu wakubali ujumbe wa Ufalme, kama yule mlinzi wa gereza huko Filipi.

Hisia-mwenzi hutusaidia kupuuza makosa ya wengine kutanikoni. Tukijitahidi kufahamu hisia za ndugu aliyetukosea, bila shaka itakuwa rahisi kumsamehe. Labda tungetenda vivyo hivyo kama tungekuwa katika hali hiyo. Hisia-mwenzi huchochea Yehova ‘kukumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi.’ Kwa hiyo, je, hatupaswi kuchochewa na hisia-mwenzi kufikiria hali za kutokamilika za wengine na ‘kuwasamehe kwa hiari’?—Zaburi 103:14; Wakolosai 3:13.

Tukilazimika kutoa shauri, labda tutalitoa kwa fadhili zaidi iwapo tunaelewa hisia za mtu aliyekosea. Mzee Mkristo mwenye hisia-mwenzi hujikumbusha hivi: ‘Mimi pia ningeweza kufanya kosa hilo. Ningeweza kuwa katika hali yake.’ Kwa hiyo Paulo atoa pendekezo hili: “Jaribuni kumrekebisha upya mtu wa namna hiyo katika roho ya upole, huku kila mmoja wenu akifuliza kujiangalia mwenyewe, kwa kuhofu wewe pia usipate kushawishwa.”—Wagalatia 6:1.

Pia hisia-mwenzi yaweza kutuchochea kutoa msaada iwapo tuna uwezo wa kufanya hivyo, hata ingawa huenda Mkristo mwenzetu akasita kuomba msaada. Mtume Yohana aandika hivi: “Yeyote yule aliye na njia ya ulimwengu huu ya kutegemeza maisha na amwona ndugu yake akiwa na uhitaji na bado amfungia mlango wa huruma zake nyororo, ni katika njia gani kumpenda Mungu hukaa katika yeye? . . . Acheni tupende, si katika neno wala kwa ulimi, bali katika kitendo na kweli.”—1 Yohana 3:17, 18.

Ili tupende “katika kitendo na kweli,” lazima kwanza tutambue mahitaji hususa ya ndugu yetu. Je, sisi huwa macho kuona mahitaji ya wengine tukiwa na nia ya kuwasaidia? Kufanya hivyo ni kudhihirisha hisia-mwenzi.

Sitawisha Hisia-Mwenzi

Huenda si jambo la kawaida kwetu kuonyesha hisia-mwenzi, lakini tunaweza kusitawisha sifa hiyo. Tukisikiliza kwa makini zaidi, tuwe macho zaidi na tujiweke katika hali za mtu mwingine, tutakuwa wenye hisia-mwenzi. Kwa kufanya hivyo, tutachochewa kuonyesha upendo, fadhili, na huruma kwa watoto wetu, Wakristo wengine, na majirani wetu.

Usiruhusu ubinafsi ukuzuie kuonyesha hisia-mwenzi. Paulo aliandika hivi: “Yeyote kati yenu asifikirie tu masilahi yake, bali afikirie masilahi ya watu wengine pia. (Wafilipi 2:4; Phillips) Wakati wetu ujao wa milele unategemea hisia-mwenzi ya Yehova na ya Kuhani wake wa Cheo cha Juu, Yesu Kristo. Kwa hiyo tuna daraka la kusitawisha sifa hiyo. Hisia-mwenzi itatupatia nguvu za kuwa wahudumu bora na wazazi bora. Zaidi ya yote, hisia-mwenzi itatusaidia kutambua kwamba “kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko kulivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35.

[Picha katika ukurasa wa 25]

Hisia-mwenzi inahusisha kuwa macho sana kuona mahitaji ya wengine tukiwa na nia ya kuwasaidia

[Picha katika ukurasa wa 26]

Je, tutajifunza kuonyesha hisia-mwenzi ambayo mama mwenye upendo humwonyesha mtoto wake?