Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wakumbuka?

Je, Wakumbuka?

Je, Wakumbuka?

Je, umefurahia kusoma matoleo ya hivi karibuni ya Mnara wa Mlinzi? Ona kama unaweza kujibu maswali yafuatayo:

Ni ratiba gani ya kibinafsi inayohusu Mahubiri ya Mlimani unayoweza kutumia ili kupunguza mkazo?

Kila siku, unaweza kusoma mojawapo ya mafundisho ya msingi ya Yesu yanayopatikana katika mahubiri hayo, au kwingineko katika Gospeli. Kwa kutafakari fundisho hilo na kujitahidi kulitumia, huenda ukapata furaha zaidi na kupunguza mkazo.—12/15, ukurasa wa 12-14.

Ni sababu zipi tatu zinazofanya wazee wa kutaniko wawazoeze watumishi wa huduma kuchukua madaraka zaidi?

Kwa sababu ya kuongezeka kwa idadi ya Mashahidi wa Yehova, wanaume zaidi wanahitajiwa kuchukua madaraka ili kusaidia wapya waliobatizwa wafanye maendeleo. Wazee ambao wametumikia kwa muda mrefu sasa hawawezi kufanya mengi kwa sababu ya uzee au matatizo ya afya. Na wazee fulani wenye uwezo wana madaraka zaidi mbali na yale ya kutaniko lao, kwa hiyo huenda wasiweze kufanya mengi katika kutaniko lao kama zamani.—1/1, ukurasa wa 29.

Watu hutumaini miungu isiyo halisi jinsi gani?

Watu wengi huabudu miungu ya dini zao, lakini miungu hiyo haina uhai na haiwezi kuokoa sawa na vile Baali aliyeabudiwa siku za Eliya hangeweza kuokoa. (1 Wafalme 18:26, 29; Zaburi 135:15-17) Wengine hutukuza watumbuizaji mashuhuri au wanamichezo, ambao hawawezi kuwapa tumaini lolote la wakati ujao. Tofauti na miungu hiyo, kwa kweli Yehova yuko, naye hutimiza makusudi yake.—1/15, ukurasa wa 3-5.

Tunaweza kujifunza nini kutokana na jinsi Kaini alivyoitikia onyo la Mungu?

Mungu ametupatia uhuru wa kuchagua, na tunaweza kuchagua kufanya mambo yafaayo badala ya kuacha kutenda mema kama Kaini. Pia, simulizi hilo la Biblia laonyesha kwamba Yehova huwahukumu wasiotubu.—1/15, ukurasa wa 22-23.

Kwa nini usafi ni muhimu sana hasa sasa?

Kwa kuwa maisha ya jamii yanazidi kubadilika, watu wengi hutumia muda mfupi kusafisha nyumba zao kuliko hapo awali. Kupuuza usafi wa chakula na maji kwaweza kuhatarisha afya. Mbali na usafi wa kimwili, Biblia hukazia usafi wa kiroho, kiadili, na kiakili.—2/1, ukurasa wa 3-6.

Kuhusu Mashahidi walioishi kabla ya Ukristo, Paulo alisema kwamba ‘hawangefanywa wakamilifu bila sisi.’ Jinsi gani? (Waebrania 11:40)

Wakati wa Milenia, Kristo na ndugu zake watiwa-mafuta wakiwa mbinguni, watatumikia wakiwa wafalme na makuhani na kuleta manufaa za fidia kwa waliofufuliwa. Hivyo waaminifu hao kama wale wanaotajwa katika Waebrania sura ya 11 ‘watafanywa wakamilifu.’—2/1, ukurasa wa 23.

Paulo alimaanisha nini alipowaambia Waebrania: “Bado hamjakinza kamwe hadi damu”? (Waebrania 12:4)

Alimaanisha kukinza hadi kifo. Kulikuwa na mifano ya watu waliokuwa waaminifu hadi kifo. Ingawa Waebrania ambao Paulo aliwaandikia maneno hayo hawakuwa wamejaribiwa hadi kifo, walihitaji kufanya maendeleo hadi kufikia ukomavu, na kujenga imani yao ili kuvumilia jaribu lolote ambalo lingetokea.—2/15, ukurasa wa 29.

Je, inafaa Mkristo akubali mwili wa mpendwa wake aliyekufa uhifadhiwe kwa kupakwa dawa?

Kupaka maiti dawa ni njia ya kuhifadhi mwili. Watu fulani wa zamani walifanya hivyo kwa sababu za kidini. Sivyo ilivyo na waabudu wa kweli. (Mhubiri 9:5; Matendo 24:15) Kupaka maiti dawa ni kuchelewesha tu jambo lisiloweza kuepukika, mwili kurudi mavumbini. (Mwanzo 3:19) Lakini hakuna haja ya kuhangaika iwapo sheria inaamuru mwili uhifadhiwe kwa kupakwa dawa, washiriki fulani wa familia wanaunga mkono jambo hilo, au kwa sababu wengine watalazimika kusafiri kutoka mbali ili kuhudhuria maziko.—3/15, ukurasa wa 29-31.

Ni mifano gani ya Biblia inayotufundisha kwamba Mungu hukubali watu wa mataifa yote?

Yehova alimtuma nabii Yona awaonye Waninewi, naye Mungu akamsihi Yona akubali toba yao. Kwa maneno na matendo, Yesu aliwatia watu moyo wawaonyeshe Wasamaria upendo. Mtume Petro na Paulo walikuwa na daraka la kupeleka habari njema kwa watu wasio Wayahudi. Kutokana na mifano hiyo, twaweza kuona kwamba tunahitaji kusaidia watu wa kila malezi.—4/1, ukurasa wa 21-24.