Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuhisi Usalama Sasa na Kuwa Salama Milele

Kuhisi Usalama Sasa na Kuwa Salama Milele

Kuhisi Usalama Sasa na Kuwa Salama Milele

KWA nini si rahisi kupata usalama, na unapopatikana, kwa nini haudumu? Je, inawezekana kwamba tunahisi tukiwa salama kwa sababu ya kuwazia mambo tunayotazamia kupata badala ya yale tunayoweza kupata? Tunaweza kusema kufanya hivyo ni sawa na kuishi katika ulimwengu wa ndoto.

Mtu anayewaza hivyo haoni maisha na ukosefu wa usalama kwa njia halisi badala yake mtu huyo huwazia hali nzuri yenye utulivu, huku akipuuza chochote kinachoweza kuharibu ndoto yake. Hata hivyo, mara nyingi matatizo ya maisha hupenyeza kwenye ulimwengu huo wa ndoto na kuondoa hisi ya usalama kisha mwotaji huamka na kuona hali ikiwa kama ilivyo kihalisi.

Njia moja ambayo watu hutafuta usalama ni kwa kuhamia mahali fulani hususa. Kwa mfano, jiji kubwa huenda likafanya mtu awe na matarajio makubwa kama vile maisha ya raha, mshahara mnono, na nyumba nzuri. Ni kweli kuhamia jijini kwaweza kuonekana kuwa suluhisho liletalo usalama uliongojewa kwa muda mrefu. Lakini je, ndivyo ilivyo kihalisi?

Je, Jiji Kubwa Linaleta Usalama au Ni Ndoto Kubwa?

Katika mataifa yanayositawi, matangazo ya biashara yanavuta watu kwenye majiji makubwa na huenda wengine wakadanganyika. Mashirika yanayotoa matangazo hayo yanafanya hivyo si ili yakupatie usalama, bali ili yauze bidhaa zao. Mashirika hayo hayaonyeshi matatizo yaliyopo bali huonyesha picha za watu waliofanikiwa maishani na wenye usalama. Hivyo, mashirika hayo huonyesha kwamba ili uwe na usalama, lazima uhamie jijini na uwe na bidhaa wanazotangaza.

Fikiria mfano ufuatao. Maafisa katika jiji moja la Afrika Magharibi walisimamisha vibao vya matangazo vilivyoonyesha waziwazi kwamba kuvuta sigara ni sawa na kutumia vibaya pesa zilizochumwa kwa jasho. Hiyo ilikuwa sehemu ya kampeni ya kuwaonya wananchi wa huko wasivute sigara. Mashirika yanayotengeneza sigara nayo yaliweka vibao vilivyochorwa picha zenye kuvutia za wavutaji sigara walioonekana kuwa wenye furaha na mafanikio. Zaidi ya hayo, kampuni moja ya sigara iliwapeleka baadhi ya wafanyakazi wake barabarani wakiwa wamevalia nguo na kofia zenye kuvutia ili kugawanya sigara kwa vijana huku wakihimiza kila mmoja wao “aijaribu.” Ilikuwa rahisi kwa wengi wa vijana hao waliotoka vijijini kudanganywa na matangazo hayo yenye ujanja. Wengi wa vijana hao walikuwa wametoka kijijini hivyo hawakujua mbinu ambazo mashirika ya kibiashara hutumia. Hivyo, wengi walishawishiwa na wakawa wavutaji-sigara sugu. Vijana hao walikuwa wamekuja jijini kutafuta usalama ili kuruzuku familia zao ama kufanikisha maisha yao. Badala yake, walitumia vibaya pesa ambazo wangetumia kufanya mambo yafaayo.

Matangazo ya biashara yanayoonyesha kwamba maisha yanakuwa mazuri katika majiji makubwa hayatokani sikuzote na wafanya-biashara. Huenda matangazo hayo yakaenezwa na wale waliohamia jijini lakini sasa wanaona haya kurudi nyumbani. Ili wasionekane ni kana kwamba wameshindwa na maisha ya mjini, wao hujivunia utajiri na mafanikio ya uongo. Hata hivyo, ukichunguza maisha yao sasa, utaona kwamba si bora kuliko yalivyokuwa walipokuwa kijijini, na hata wanang’ang’ana kama wakazi wengine wengi wa majiji.

Wapya wanapokuja kutafuta usalama katika majiji makubwa ndipo hasa huangukia katika mitego ya walaghai. Hii ni kwa sababu wako mbali na nyumbani na hawajapata marafiki wa karibu. Kwa hiyo hawana watu wa kuwashauri kuhusu mitego ya kufuatia vitu vya kimwili.

Josué hakuingia kamwe katika mtego wa kuvuta sigara. Zaidi ya hayo, alikuja kutambua kwamba hangeweza kufaulu kukabiliana na magumu ya jijini. Alichopata jijini ni matarajio makubwa tu. Alitambua kuwa hangepata usalama wa kweli jijini, hivyo, maisha ya huko hayakumfaa. Mawazo ya kujihisi kuwa hafai, kutojiamini na kushindwa yalimsonga, na mwishowe aliamua kujinyenyekeza na kurudi kijijini.

Alikuwa akihofia kuwa angechekwa. Badala yake, familia yao na marafiki wake wa kweli walimkaribisha nyumbani kwa furaha. Kwa sababu ya uchangamfu huu wa familia yake na mazingira ya kijijini aliyozoea, pamoja na upendo alioonyeshwa na marafiki wake katika kutaniko la Kikristo, punde alihisi akiwa salama zaidi ya alivyokuwa katika lile jiji kubwa, ambapo ndoto za wengi zinakosa kutimia. Alishangaa kuona kuwa pesa alizopata kwa kufanya kazi pamoja na babake shambani zilikuwa nyingi kuliko mshahara ambao angepata katika jiji.

Pesa—Tatizo Ni Nini?

Je, pesa zinaleta hisia ya usalama? Liz, kutoka Kanada anasema hivi: “Nilipokuwa mdogo niliamini kwamba pesa huondoa wasiwasi.” Yeye alikutana na mwanamume mmoja tajiri na wakapendana. Baada ya muda mfupi walioana. Je, alihisi akiwa salama? Yeye anaendelea kueleza hivi: “Wakati tulipooana, tulikuwa na nyumba nzuri na magari mawili, na tulikuwa na pesa za kutosha kununua chochote tulichotaka, kusafiri, kuwa na starehe. Kwa kushangaza, bado nilikuwa na wasiwasi kuhusu pesa.” Anaeleza sababu: “Tulikuwa na vitu vingi sana na tulihofu tungeweza kuvipoteza vyote. Ni kana kwamba kadiri ulivyo na nyingi, ndivyo unavyohisi kukosa usalama zaidi. Pesa hazikuondoa wasiwasi au hangaiko.”

Iwapo unahisi kwamba huna pesa za kutosha kuwa salama, jiulize, ‘tatizo ni nini? Ni kukosa pesa au ni kutozitumia vizuri? Liz anasema hivi kuhusu yale yaliyompata akiwa mchanga: “Sasa ninatambua kwamba chanzo cha matatizo katika familia yetu nilipokuwa mchanga kilikuwa matumizi mabaya ya pesa. Tulikuwa na madeni sikuzote kwa sababu ya kununua vitu kwa mkopo. Hilo lilifanya tuwe na wasiwasi.”

Leo, Liz na mume wake wanahisi wakiwa salama zaidi ingawa pato lao ni dogo kuliko hapo zamani. Walipojifunza Neno la Mungu, waliacha kukazia fikira vishawishi vya kupata pesa zaidi na wakaanza kusikiliza hekima ya Mungu kutia ndani maneno haya: “Bali kila anisikilizaye atakaa salama, naye atatulia bila kuogopa mabaya.” (Mithali 1:33) Walitaka maisha yenye maana kuliko yale ambayo pesa zingeweza kuwapa. Sasa wakiwa mishonari katika nchi ya mbali, Liz na mumewe wanafundisha matajiri kwa maskini kwamba hivi karibuni Yehova Mungu ataleta usalama wa kweli ulimwenguni pote. Kazi hii huleta uradhi mwingi na uthabiti ambao, hautokani na pesa, lakini hutokana na kuwa na kusudi na maadili bora.

Kumbuka ukweli huu wa maana: Kuwa tajiri kuelekea Mungu ni muhimu zaidi ya kuwa na utajiri wa kimwili. Kotekote katika Maandiko Matakatifu, lile ambalo limekaziwa zaidi si kuwa na vitu vingi vya kimwili, bali ni kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Yehova, uhusiano ambao tunaweza kuudumisha kwa kuendelea kufanya mapenzi ya Mungu kwa imani. Yesu Kristo alituhimiza tuwe ‘matajiri kuelekea Mungu,’ na kuweka ‘hazina katika mbingu.’— Luka 12:21, 33.

Cheo—Utapanda hadi Wapi?

Ikiwa unashawishiwa kuona kwamba cheo cha juu katika jamii ni njia ya kupata usalama, jiulize hivi: ‘Ni nani aliye katika daraja la usalama halisi? Ni cheo gani ninachopaswa kufikia ili niwe salama? Kazi nzuri yaweza kukupatia hisia ya usalama isiyo ya kweli, na hilo linaweza kufanya ukate tamaa, na jambo baya hata zaidi, mambo hayo yanaweza kusababisha anguko.’

Mambo halisi yaliyoonwa yanadhihirisha kwamba jina jema pamoja na Mungu linatoa usalama kuliko kusifiwa na watu. Ni Yehova pekee anayeweza kuwapa wanadamu zawadi ya uhai wa milele. Hilo latia ndani kuandika jina letu si katika orodha za watu mashuhuri katika jamii bali katika kitabu cha uhai cha Mungu.—Kutoka 32:32; Ufunuo 3:5.

Unapotazama mambo kihalisi, unaonaje hali yako ya sasa na unaweza kutazamia nini wakati ujao? Hakuna aliye na vitu vyote. Ni kama tu vile Mkristo mmoja mwenye hekima alivyosema: ‘Nilijifunza kwamba huwezi kupata kila kitu maishani, ni lazima uchague.’ Tua kidogo na usome sanduku lenye kichwa “Imesimuliwa Nchini Benin.”

Sasa jibu maswali haya: Ninataka nini maishani? Je ninaweza kukipata kwa njia ya moja kwa moja? Je huenda ninatumia njia isiyo salama na labda kitu ninachotaka chaweza kupatikana kwa njia rahisi?

Baada ya kuonyesha jinsi vitu vya kimwili vilivyo na thamani ndogo vikilinganishwa na mambo ya kiroho, Yesu alisema tudumishe jicho “sahili.” (Mathayo 6:22) Alisema wazi kuwa mambo makuu maishani ni maadili na miradi ya kiroho yanayokazia jina la Mungu na Ufalme wake. (Mathayo 6:9, 10) Mambo mengine yana umuhimu mdogo au, hayapaswi kuzingatiwa kwa uzito ule ule.

Kamera nyingi leo hupiga picha vitu vilivyo mbali na vilivyo karibu. Je, wewe ni kama kamera hizo? Je, mambo yote unayoona ni muhimu kwako, unayatamani yote na unawaza kwamba unaweza kuyafikia? Ikiwa ndivyo unavyoona mambo, basi jambo kuu kwa Wakristo yaani Ufalme, laweza kupotelea kwa urahisi miongoni mwa mambo mengi ambayo yanataka uangalifu wako. Yesu alihimiza hivi: “Basi, fulizeni kutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, na vitu vingine vyote hivi mtaongezewa.”—Mathayo 6:33.

Salama Sasa na Milele

Tunaweza kuwa na matazamio mazuri kwa ajili yetu na wapendwa wetu. Hata hivyo, kwa kuwa sisi si wakamilifu, tunaishi katika ulimwengu usio mkamilifu, na maisha ni mafupi, tunalazimika kupunguza mambo tunayotarajia kutimiza kihalisi. Mwandikaji mmoja wa Biblia aliandika hivi maelfu ya miaka iliyopita: “Nikarudi, na kuona chini ya jua, ya kwamba si wenye mbio washindao katika michezo, wala si walio hodari washindao vitani, wala si wenye hekima wapatao chakula, wala si watu wa ufahamu wapatao mali, wala wenye ustadi wapatao upendeleo; lakini wakati na bahati [“tukio lisilotazamiwa,” NW] huwapata wote.”—Mhubiri 9:11.

Wakati mwingine sisi hujiingiza sana katika shughuli za kila siku na kusahau kuangalia mambo yenye maana zaidi, yaani, sisi ni nani na tunachohitaji ili tuhisi tukiwa salama kikweli. Fikiria maneno haya ya kale yenye hekima: “Apendaye fedha hatatosheka na fedha, wala atamaniye mali hata akiipata hatatosheka. Hilo nalo ni bure kabisa. Usingizi wa kibarua ni mtamu, awe ameshiba au amekula kidogo tu. Lakini usingizi wa tajiri ni wa wasiwasi daima, maana ziada ya mali yake humsumbua usiku kucha.” (Mhubiri 5:10, 12, Bibia Habari Njema) Naam, usalama wako unategemea nini?

Ikiwa una ndoto isiyoweza kutimia kama ile ya Josué, je, unaweza kubadili mipango yako? Wale wanaokupenda kikweli watakuunga mkono, kama vile familia na marafiki katika kutaniko la Kikristo walivyomsaidia Josué. Unaweza kupata usalama mwingi zaidi katika mazingira ya hali ya chini pamoja na wale wanaokupenda kuliko katika jiji miongoni mwa watu wanaojaribu kukutumia kwa faida zao wenyewe.

Ikiwa tayari una mali nyingi, kama Liz na mumewe, je, unaweza kurekebisha maisha yako ili utumie wakati na nguvu zaidi katika kusaidia watu, matajiri au maskini, kujifunza kuhusu Ufalme ambao utaleta usalama wa kweli?

Iwapo umekuwa ukitafuta cheo katika jamii, unaweza kujiuliza kwa moyo mweupe ni nini kinachokuchochea kufanya hivyo. Kwa hakika, kutumia uwezo fulani ulio nao kwaweza kuongeza furaha yako. Lakini, je, kufanya hivyo kutakuwezesha kuweka Ufalme—ambao ni njia ya kweli ya kupata usalama wa kudumu katika mahali pa kwanza? Kumbuka maneno ya Yesu: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko kulivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35) Ukishiriki utendaji mbalimbali katika kutaniko la Kikristo, utapata usalama wenye kuthawabisha.

Wale wanaomtumaini Yehova na Ufalme wake kikamili wanapata usalama wenye kuchangamsha moyo sasa na wanakuwa na tumaini la kupata usalama kamili wakati ujao. Mtunga-zaburi alisema hivi: “Nimeweka BWANA mbele yangu daima; kwa sababu yeye ni kwa mukono wangu wa kuume, sitaondoshwa. Kwa hivi moyo wangu unafurahi na utukufu wangu unashangilia; mwili wangu vilevile utakaa salama.”—Zaburi 16:8, 9, Zaire Swahili Bible.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6]

Imesimuliwa Nchini Benin

Hadithi ifuatayo imesimuliwa nchini Benin mara nyingi kwa njia tofauti-tofauti. Hivi majuzi, mkazi mmoja ambaye ameishi kijijini kwa miaka mingi huko Benin, Afrika Magharibi aliisimulia hivi kwa vijana fulani.

Mvuvi alirudi nyumbani akiwa ndani ya mtumbwi wake na kukutana na mtaalamu mmoja wa mambo ya kibiashara kutoka nchi ya kigeni aliyekuwa akifanya kazi katika nchi hiyo inayositawi. Mtaalamu huyo anamuuliza mvuvi kwa nini amerudi mapema hivyo. Yeye anamjibu kuwa angekaa kidogo lakini alikuwa amevua samaki wa kutosha kulisha jamaa yake.

“Na sasa, wewe hutumiaje wakati wako?” yule mtaalamu anamuuliza.

Mvuvi anajibu: “Mimi huvua kidogo, hucheza na watoto wangu na sote hupumzika kidogo jua linapokuwa kali. Jioni, sisi hula mlo pamoja. Baadaye, mimi hukutana na rafiki zangu ili kusikiliza muziki, na kadhalika.”

Mtaalamu huyo anamkatiza na kusema: “Mimi nina shahada ya chuo kikuu na nimesomea mambo hayo. Ninataka kukusaidia. Unapaswa kuvua samaki kwa muda mrefu zaidi ili upate pesa zaidi. Hizo zitakuwezesha kununua mashua kubwa zaidi kuliko mtumbwi huu. Ukiwa na mashua hiyo kubwa, utapata pesa nyingi zaidi na utaweza kununua mashua nyingi za kuvulia samaki.”

“Halafu?” mvuvi anauliza.

“Halafu, badala ya kuwauzia wachuuzi samaki, ungeweza kuwapeleka moja kwa moja kwenye kiwanda ama hata uanzishe kiwanda chako mwenyewe cha samaki. Ungeweza kusafiri hadi Cotonou, au Paris, au New York na kuendeleza biashara yako ukiwa huko. Labda hata ungefikiria kuweka biashara yako katika soko la hisa na kupata utajiri mwingi.”

“Hayo yote yatachukua muda gani?” yule mvuvi anauliza.

“Labda miaka 15 hadi 20,” mtaalamu anajibu.

“Halafu?” mvuvi anaendelea kuuliza.

“Kisha unaanza kufurahia maisha,” yule mtaalamu anaelezea. “Kisha unaweza kustaafu na kuhamia kwenye kijiji kilicho mbali na pilikapilika za jijini.”

“Halafu itakuwaje?” mvuvi anauliza.

“Kisha utapata wakati wa kuvua kidogo, kucheza na watoto wako, kupumzika kunapokuwa na jua kali, kula mlo wa jioni pamoja na jamaa, na kukutana na marafiki ili kusikiliza muziki.”

[Picha katika ukurasa wa 7]

Je, kupandishwa cheo huleta usalama?

[Picha katika ukurasa wa 8]

Wakristo wenzako wanapendezwa kikweli na usalama wako